Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 125

Yesu Anapelekwa kwa Anasi, Kisha kwa Kayafa

Yesu Anapelekwa kwa Anasi, Kisha kwa Kayafa

MATAYO 26:57-68 MARKO 14:53-65 LUKA 22:54, 63-65 YOHANA 18:13, 14, 19-24

  • YESU ANAPELEKWA KWA ANASI MWENYE ZAMANI ALIKUWA KUHANI MUKUBWA

  • SANHEDRINI INAFANYA HUKUMU YENYE HAIPATANE NA SHERIA

Kisha Yesu kufungwa kama mutu mwenye alifanya makosa makubwa, anapelekwa kwa Anasi, mwenye alikuwa kuhani mukubwa wakati kijana Yesu alishangaza walimu kwenye hekalu. (Luka 2:42, 47) Kisha, watoto fulani wa Anasi walitumikia cheo cha kuhani mukubwa, na sasa ni Kayafa, mukwe wake, ndiye kuhani mukubwa.

Wakati Yesu iko kwenye nyumba ya Anasi, Kayafa anakusanya watu wote wenye kufanyiza Sanhedrini. Sanhedrini hiyo inafanyizwa na watu 71 kutia ndani kuhani mukubwa na wengine wenye walikuwa wametumikia cheo hicho zamani.

Anasi anauliza Yesu “juu ya wanafunzi wake na juu ya mafundisho yake.” Yesu anajibu kwa kifupi hivi: “Nimesema na ulimwengu waziwazi. Sikuzote nilifundisha katika sinagogi na katika hekalu, mahali penye Wayahudi wote wanakusanyika, na sikusema jambo lolote kwa siri. Sababu gani unaniuliza? Uliza wale wenye walisikia kile niliwaambia.”—Yohana 18:19-21.

Mumoja wa walinzi mwenye alikuwa anasimama pale anamupiga Yesu kofi kwenye uso na kusema hivi kwa ukali: “Je, ni vile unajibu mukubwa wa makuhani?” Lakini kwa sababu Yesu alijua kuwa hakufanya jambo fulani la mubaya, anajibu hivi: “Kama nimesema mubaya, shuhudia ubaya huo; lakini kama yale nilisema yako sawa, sababu gani unanipiga?” (Yohana 18:22, 23) Kisha Anasi anaomba Yesu apelekwe kwa Kayafa, mukwe wake.

Sasa wale wote wenye kufanyiza Sanhedrini, ni kusema, kuhani mukubwa wa sasa, wazee wa watu, na waandishi, wamekusanyika. Wanakusanyika kwenye nyumba ya Kayafa. Sheria inakataza kusambisha mutu katika usiku wa Pasaka, lakini hilo haliwazuie kuendelea na kusudi lao la mubaya.

Kwa kweli, Kikundi hicho hakitende kwa haki hata kidogo. Kisha Yesu kumufufua Lazaro, Sanhedrini iliamua kuwa Yesu anapaswa kufa. (Yohana 11:47-53) Na siku fulani zenye zilikuwa zimepita viongozi wa dini walipanga njama ya kumukamata Yesu na kumuua. (Matayo 26:3, 4) Kwa kweli, hata mbele ya kusambishwa, tayari Yesu amekwisha kuhukumiwa kifo!

Zaidi ya kufanya mukutano wenye haukubaliwe na sheria, wakubwa wa makuhani na wengine wenye kufanyiza Sanhedrini wanajaribu kutafuta mashahidi wa uwongo ili wapate mambo ya kumushitaki Yesu. Wanapata mashahidi wengi, lakini ushuhuda wao ni wenye kupingana. Mwishowe, mashahidi wawili wanakuja na kusema hivi: “Tulimusikia akisema, ‘Nitabomoa hekalu hili lenye lilifanywa kwa mikono, na kwa siku tatu (3) nitajenga lingine lenye halikufanywa kwa mikono.’” (Marko 14:58) Hata hivyo, wanaume hao hawakubaliane kabisa-kabisa.

Kayafa anauliza Yesu: “Haujibu hata neno moja? Watu hawa wanashuhudia nini juu yako?” (Marko 14:60) Yesu anabakia kimya juu ya mashitaka hayo ya uongo yenye kusemwa na mashahidi wenye ushuhuda wao haupatane. Kwa hiyo, Kayafa, Kuhani Mukubwa, anatumikisha ufundi mwingine.

Kayafa anajua kuwa Wayahudi wanachukia mutu yeyote mwenye kujiita kuwa Mwana wa Mungu. Mbele ya hapo, wakati Yesu alimuita Mungu Baba yake, Wayahudi walipenda kumuua kwa sababu walisema “anajifanya kuwa sawa na Mungu.” (Yohana 5:17, 18; 10:31-39) Kwa sababu anajua jambo hilo, Kayafa anamuuliza Yesu kwa ujanja hivi: “Ninakuapisha mbele ya Mungu mwenye kuishi utuambie kama wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu!” (Matayo 26:63) Kwa kweli, Yesu amesema waziwazi kuwa yeye ni Mwana wa Mungu. (Yohana 3:18; 5:25; 11:4) Ikiwa hafanye hivyo sasa, hilo linaweza kuonyesha kuwa anakataa kuwa yeye ni Mwana wa Mungu na kuwa yeye ni Kristo. Yesu anasema hivi: “Mimi ndiye; na mutaona Mwana wa binadamu akiwa amekaa kwenye mukono wa kuume wa nguvu na akikuja pamoja na mawingu ya mbinguni.”—Marko 14:62.

Wakati Kayafa anasikia jambo hilo, anapasua nguo zake na kusema hivi: “Amemutukana Mungu! Je, tuko na lazima ya mashahidi wengine? Muone! Sasa mumesikia matukano juu ya Mungu. Munafikiri nini?” Watu wa Sanhedrini wanafanya hukumu yenye kukosa haki, wanasema hivi: “Anastahili kufa.”—Matayo 26:65, 66.

Kisha wanaanza kumuchekelea Yesu na kumupiga ngumi. Wengine wanamupiga makofi kwenye sura na kumutemea mate. Kisha kufunika sura yake yote na kumupiga makofi, wanamuchekelea kwa kusema hivi: “Toa unabii! Ni nani alikupiga?” (Luka 22:64) Ni hivyo Mwana wa Mungu anatendewa mubaya wakati hasambishwe kulingana na sheria!