Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA INE

Alijifunza Kuwa Mwenye Rehema

Alijifunza Kuwa Mwenye Rehema

1. Ni safari ya namna gani ambayo Yona anapaswa kufanya, na anajisikia namna gani kuhusu mahali anapoenda?

YONA ana wakati wa kutosha ili kufikiri. Anapaswa kufanya safari ya kilometre zaidi ya 800; atatembea kwa miguu mwezi mumoja hivi, ao hata muda murefu zaidi. Kwanza anapaswa kuchagua ikiwa atapitia njia fupi ao njia ndefu zilizokuwa na usalama. Kisha anaamua kufunga safari kupitia mabonde na milima mingi sana. Anapaswa kupita kandokando ya Jangwa Kubwa la Siria, kuvuka mito kama vile muto mukubwa Efrati, na kuomba watu asiowajua mahali pa kulala katika miji na vijiji vya Siria, Mesopotamia na Asiria. Kadiri siku zinavyopita anakaribia muji wa Ninawi, muji ambao anaogopa sana.

2. Namna gani Yona alijifunza kwamba hapaswe kukimbia mugao wake?

2 Hata hivyo, Yona anajua hakika jambo hili: Hawezi kurudi nyuma na kukimbia mugao wake. Alikwisha kujaribu kufanya hivyo. Kama tulivyoona katika Sura ya 13, kwa uvumilivu Yehova alimufundisha Yona kupitia zoruba yenye upepo mukali na kwa kumuokoa kwa muujiza kutoka katika tumbo la samaki mukubwa. Kisha siku tatu, samaki huyo alimutapika kwenye inchi kavu; Yona aliingiwa na woga sana kwa sababu ya mambo hayo yaliyomupata na akawa mutu mutiifu zaidi.—Yona, sura ya 1, na ya 2.

3. Yehova alimuonyesha Yona sifa gani, na ni ulizo gani tunaweza kujiuliza?

3 Wakati Yehova anamuamuru Yona mara ya pili kuenda Ninawi, nabii huyo anatii na anafunga safari hiyo ndefu kuelekea upande wa mashariki. (Soma Yona 3:1-3.) Lakini, kisha Yehova kumuadibisha, je, Yona alibadilisha kabisa namna yake ya kuona mambo? Yehova alimuonyesha rehema wakati alimuokoa, asife katika maji, hakumuazibu kwa sababu ya kukosa kuwa mutiifu, na sasa anamupatia tena nafasi ya kutimiza mugao wake. Kisha mambo hayo yote, je, Yona amejifunza kuonyesha wengine rehema? Mara nyingi kwa wanadamu wasio wakamilifu, kufanya hivyo si vyepesi. Basi acha tuone kile magumu ya Yona yanaweza kutufundisha.

Ujumbe wa Hukumu na Badiliko Lisilotazamiwa

4, 5. Sababu gani Yehova alisema kwamba muji wa Ninawi ni ‘muji mukubwa,’ na hilo linatufundisha nini kumuhusu Yehova?

4 Mawazo ya Yona na ya Yehova juu ya muji wa Ninawi yanatofautiana. Tunasoma hivi: ‘Basi Ninawi ulikuwa muji mukubwa sana kwa Mungu.’ (Yona 3:3) Mara tatu katika habari ya Yona, Yehova anatumia usemi ‘Ninawi ule muji mukubwa sana.’ (Yona 1:2; 3:2; 4:11) Sababu gani Yehova anauona muji huo kuwa mukubwa sana, ao wa lazima?

5 Ninawi ni moja ya miji ya kwanza ya zamani sana ambayo Nimrodi alijenga kisha Garika. Lilikuwa eneo kubwa lenye miji mingi, kwa hiyo, ilimuomba mutu atembee mwendo wa siku tatu kutoka upande mumoja mupaka upande mwengine. (Mwa. 10:11; Yona 3:3) Ninawi ulikuwa muji wenye kuvutia sana, ulikuwa na hekalu kubwakubwa, kuta zenye nguvu, na majengo mengine yenye kupendeza. Lakini si mambo hayo ndio yanafanya muji huo uwe wa lazima kwa Yehova Mungu. Jambo la lazima sana kwake ni watu. Wakati huo muji wa Ninawi ulikuwa na watu wengi sana kuliko miji mingine. Hata ikiwa walikuwa wanafanya mambo mabaya, Yehova aliwahangaikia. Yeye anaona uzima wa mwanadamu kuwa wa bei sana na anataka kila mumoja atubu na pia ajifunze kufanya mambo mazuri.

Yona aliingia katika muji wa Ninawi; muji mukubwa sana na unaojaa watu wenye kutenda mabaya

6. (a) Sababu gani labda Yona aliogopeshwa na muji wa Ninawi? (Soma pia maelezo yaliyo chini.) (b) Kwa kuwa Yona alitimiza mugao wake wa kuhubiri, jambo hilo linatufundisha nini juu ya Yona?

6 Mwishowe, Yona anafika Ninawi. Labda anaogopeshwa hata zaidi kwa sababu muji huo una watu zaidi ya 120 000. * Anatembea kwa siku moja, anaingia ndani kabisa ya muji huo, labda anatafuta mahali panapofaa ili kuanza kutangaza ujumbe aliopewa. Anahubiria watu hao katika luga gani? Je, amejifunza luga ya Waasiria? Ao, je, Yehova anamupatia uwezo wa kuzungumuza luga hiyo kimuujiza? Hatujue. Inawezekana Yona anatoa ujumbe wake katika Kiebrania na anatumia mutafsiri fulani ili kuwaelezea watu wa Ninawi. Iwe alitumia luga gani, ujumbe wake haukuwa na mambo mengi na haungefanya apendwe na watu. Ujumbe anaotangazia watu ni huu: ‘Bado siku 40 tu, na muji wa Ninawi utaangamizwa.’ (Yona 3:4) Anasema hivyo kwa ujasiri na anarudilia ujumbe huo tena na tena. Kwa kufanya hivyo, anaonyesha uhodari na imani kubwa, sifa ambazo ni za lazima sana kwa Wakristo leo, kuliko wakati mwengine wowote.

Ujumbe wa Yona haukuwa na mambo mengi na haungefanya apendwe na watu

7, 8. (a) Watu wa Ninawi wanafanya nini wanaposikia ujumbe wa Yona? (b) Naye mufalme wa Ninawi anafanya nini?

7 Watu wa Ninawi wanasikiliza ujumbe wa Yona. Bila shaka, kwa sababu ni wenye jeuri na wakali, alifikiri kwamba hawatasikiliza. Lakini mambo ni tofauti kabisa. Watu wanasikiliza na kutii! Maneno yake yanaenea kwa haraka mahali pote. Kwa muda kidogo tu, watu wote wa muji wanazungumuzia unabii wa Yona kuhusu hukumu ya Mungu. (Soma Yona 3:5.) Iwe masikini ao tajiri, mutu mwenye nguvu ao muzaifu, kijana ao muzee, wote wanatubu. Wanafunga kula chakula. Bila kukawia, tayari mufalme anapata habari kwamba watu ni wenye kutubu.

Yona alipaswa kuwa na ujasiri na imani ili kuhubiri katika muji wa Ninawi

8 Mufalme pia anaposikia ujumbe huo wa Yona, anatubu. Anaanza kumuogopa Mungu, anaondoka kwenye kiti chake cha ufalme, anavua mavazi yake ya kifalme, anavaa magunia kama watu wake, na hata ‘anaketi katika majivu.’ Yeye na watu wake “wakubwa,” ao watu wenye vyeo, wanatoa sheria kwamba kufunga kula chakula inakuwa sheria, hata ikiwa watu walikuwa tayari wamekwisha kufanya hivyo. Anaamuru kwamba watu wote, na hata wanyama wa kufugwa, wavae magunia. * Anakubali kwa unyenyekevu kwamba watu wake wanakosa kwa sababu wamefanya mambo mabaya na mambo ya uuaji ao jeuri. Kwa kuwa mufalme huyo anatumaini kwamba toba yao itamufanya Mungu wa kweli awasikilie huruma; anasema hivi: ‘Labda Mungu ataacha hasira yake inayowaka, tusije tukaangamia.’—Yona 3:6-9.

9. Watu wenye kuchambua Biblia wamesema nini kuhusu watu wa Ninawi, na namna gani tunajua kwamba wamedanganyika?

9 Watu wengine wenye kuchambua Biblia wanasema kwamba watu wa Ninawi hawangeweza kubadilika haraka hivyo. Lakini, watu wenye elimu ya Biblia wamesema kwamba wakati wa zamani, watu walioamini sana mambo ya uchawi na wageugeu katika mazoea yao walikuwa wanabadilisha maoni yao haraka. Tena, jambo lenye kuonyesha kwamba wachambuzi hao wanadanganyika ni kwamba kisha miaka mingi, hata Yesu Kristo alizungumuzia kutubu kwa watu wa Ninawi. (Soma Mathayo 12:41.) Yesu alijua vizuri sana mambo yaliyofanyika Ninawi, kwa sababu wakati huo alikuwa mbinguni na alijionea mambo hayo. (Yoh. 8:57, 58) Jambo tunalojifunza ni hili: hata ikiwa watu wanaonekana kuwa wabaya namna gani, hatupaswe kuamua mara moja kwamba hawawezi kuacha matendo yao mabaya. Ni Yehova tu ndiye anaweza kusoma kile kilicho katika moyo wa mwanadamu.

Tofauti Kati ya Moyo wa Huruma wa Mungu na Moyo Mugumu wa Mwanadamu

10, 11. (a) Yehova anafanya nini wakati watu wa Ninawi wanatubu? (b) Sababu gani tunaweza kuwa hakika kwamba Yehova hakukosea kuhusu hukumu yake?

10 Yehova anafanya nini wakati watu wa Ninawi wanatubu? Yona aliandika hivi baadaye: ‘Naye Mungu wa kweli akaona matendo yao, kwamba walikuwa wamegeuka kutoka katika njia yao mbaya; naye Mungu wa kweli akajuta juu ya musiba ambao alikuwa amesema ataleta juu yao; naye hakuuleta.’—Yona 3:10.

11 Je, hilo linamaanisha kwamba Yehova alikosea kuhusu hukumu aliyosema juu ya Ninawi? Hapana. Biblia inasema kama hukumu ya Yehova ni kamilifu. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:4.) Kwa hiyo, Yehova aliacha tu kuwakasirikia watu wa Ninawi. Aliona kama wamebadilika na kwamba azabu ambayo alikuwa amekusudia juu yao haikuwa tena ya lazima. Basi Mungu alikuwa na sababu ya kuwaonyesha rehema yake ao kuwahurumia.

12, 13. (a) Namna gani Yehova anajionyesha kuwa Mungu asiyengangania, Mungu mwenye huruma na anayetenda kulingana na hali? (b) Sababu gani hatuwezi kusema kwamba unabii wa Yona ulikuwa unabii wa uongo?

12 Yehova si Mungu mwenye moyo mugumu, asiyehangaikia watu, wala si mukali kama mafundisho ya viongozi wa kidini yanavyofanya watu wafikiri. Tofauti na hilo, yeye ni Mungu asiyengangania, ni Mungu mwenye rehema, na anayetenda kulingana na hali. Anapoamua kuazibu waovu, yeye anatuma kwanza watumishi wake ili kuwaonya watu, kwa sababu anatamani sana kuona waovu wanatubu na kubadilisha maisha yao, kama vile watu wa Ninawi walivyofanya. (Eze. 33:11) Yehova alimuambia nabii wake Yeremia hivi: ‘Wakati wowote nikisema juu ya taifa na juu ya ufalme ili kuung’oa na kuubomoa na kuuharibu, na kwa kweli taifa lile ligeuke kutoka katika ubaya wake ambao nilisema juu yake, mimi pia nitajuta juu ya ule musiba niliokuwa nimefikiria kuutimiza juu yake.’—Yer. 18:7, 8.

Mungu anatamani sana kuona waovu wanatubu na kubadilisha maisha yao, kama vile watu wa Ninawi walivyofanya

13 Je, tunaweza kusema kwamba unabii wa Yona ulikuwa unabii wa uongo? Hapana; kwa sababu ulitimiza kusudi lake la kuwaonya watu. Onyo hilo lilitolewa kwa sababu ya mwenendo mubaya wa watu wa Ninawi, lakini sasa walikuwa wamebadilika. Ikiwa watu wa Ninawi wangerudilia njia zao mbaya, Mungu angewaazibu. Na ni hivyo ndivyo Mungu alifanya baadaye.—Sef. 2:13-15.

14. Yona anajisikia namna gani kwa kuwa Yehova anahurumia watu wa Ninawi?

14 Yona anajisikia namna gani kwa sababu uharibifu haukuje kwa wakati aliotazamia? Tunasoma hivi: ‘Jambo hilo halikumupendeza Yona hata kidogo, naye akawaka hasira.’ (Yona 4:1) Yona anafikia hata kusali, lakini sala yake ni kama mutu anayemufokea Mungu! Anasema kwamba afazali angebakia nyumbani, katika inchi yao. Anajitetea kuwa alijua kwamba Yehova hangewaharibu watu wa Ninawi, na hata anatumia wazo hilo ili kuonyesha kwamba alikuwa na haki ya kukimbilia Tarshishi ao Tarsisi wakati Mungu alimutuma mara ya kwanza. Kisha anaomba akufe, anasema kwamba ingekuwa afazali kufa kuliko kuishi.—Soma Yona 4:2, 3.

15. (a) Ni nini labda inamufanya Yona awe mwenye uchungu ao kuvunjika moyo? (b) Yehova anamutendea namna gani Yona, nabii wake mwenye kuvunjika moyo?

15 Ni nini kabisa iliyokuwa inamuhangaisha Yona? Hatujue kabisa nini alikuwa anafikiri, lakini kile tunajua ni kwamba Yona alitangazia watu wote kwamba muji wa Ninawi utaangamizwa. Na watu walimuaminia. Na sasa, hakuna jambo linalofanyika. Je, Yona anaogopa kuchekwa ao kuitwa nabii wa uongo? Hata ikiwa anafikiri nini, inaonekana kwamba Yona hafurahi kuona watu wametubu, wala namna Yehova amewaonyesha rehema ao amewahurumia. Yeye ni mwenye uchungu zaidi na zaidi, anajisikitikia sana, na anaona kwamba sifa yake imeharibiwa. Hata hivyo, ni wazi kwamba Mungu mwenye rehema bado anaona sifa nzuri katika moyo wa Yona, nabii huyo mwenye kuvunjika moyo. Yehova hamuazibu Yona kwa sababu anamukosea heshima, kuliko kufanya hivyo, anamuuliza Yona kwa upole ulizo hili lenye kumufanya ajichunguze: “Je, umewaka hasira kwa haki?” (Yona 4:4) Je, Yona alijibu ulizo hilo? Biblia haiseme kitu.

16. Namna gani mawazo ya watu fulani yanaweza kutofautiana na mawazo ya Mungu, na mufano wa Yona unaweza kutufundisha nini?

16 Labda tunaweza kumuhukumu Yona haraka​-haraka, lakini tusisahau kwamba mara nyingi mawazo ya mwanadamu asiye mukamilifu hayapatane na mawazo ya Mungu. Kwa mufano, kunapotokea musiba fulani, watu wengine wanasema Mungu angepaswa kuzuia musiba huo ao wanajiuliza kwa nini hawahukumu watu waovu haraka ao kwa nini anakawia kuleta mwisho wa dunia hii mbovu. Mufano wa Yona unatukumbusha kwamba wakati mawazo yetu yanatofautiana na yale ya Yehova Mungu, tujue kwamba sikuzote ni sisi tunapaswa kubadilisha mawazo yetu, wala si Mungu.

Yehova Anamufundisha Yona Kuwa Mwenye Rehema

17, 18. (a) Yona anapotoka Ninawi anaenda wapi? (b) Ni miujiza gani Yehova anafanya kuhusu mumea wa mutango, na Yona anajisikia namna gani?

17 Nabii huyo anayevunjika moyo anaondoka Ninawi, lakini kuliko kurudi nyumbani, anajielekeza upande wa mashariki, kwenye milima fulani yenye kuinuka, mahali mutu anaweza kuona vizuri eneo lote la Ninawi. Hapo anajenga kibanda kidogo, anakaa humo na anangojea kuona jambo litakaloupata muji wa Ninawi. Labda anaendelea kutumainia kwamba ataona kuharibiwa kwa muji huo. Yehova anafanya nini ili kumufundisha mutu huyo mwenye moyo mugumu kwamba anapaswa kuwa mwenye rehema?

18 Usiku, Yehova anaotesha mumea unaoitwa mutango. Yona anapoamuka, anaona mumea huo wenye kuchipuka vizuri, majani yake yanamupa kivuli kizuri sana kuliko kivuli cha kibanda chake kisichokaza. Yona anajisikia vizuri sana. “Yona akaanza kushangilia sana” kwa sababu ya mumea huo; labda anaona mumea huo uliotokea kimuujiza kuwa ni alama ya baraka na kukubaliwa na Mungu. Lakini, Yehova hakutaka tu kumulinda Yona asiteseke kwa joto ao kutuliza hasira yake isiyo na musingi. Anataka kugusa moyo wa Yona. Kwa hiyo, Mungu anafanya tena miujiza. Anatuma mududu uharibu kabisa mumea huo. Kisha anafanya “upepo wenye kukausha wa mashariki” uvume mupaka Yona anaanza ‘kuzimia’ kwa sababu ya joto. Mwanaume huyo anavunjika tena moyo na anaomba akufe.—Yona 4:6-8.

19, 20. Namna gani Yehova anamusaidia Yona kufikiri kupitia mumea wa mutango?

19 Tena Yehova anamuuliza Yona ikiwa ana haki kabisa ya kukasirika, hasa kwa sababu mumea wa mutango umeharibika. Kuliko kutubu, Yona anaanza kujitetea, anasema hivi: ‘Ni kwa haki mimi nimewaka hasira, kiasi cha kufa.’ Sasa hali ilikuwa yenye kufaa ili Yehova amufundishe Yona jambo fulani.—Yona 4:9.

Mungu alitumia mumea wa mutango ili kumufundisha Yona namna ya kuwa mwenye rehema ao huruma

20 Mungu anaanza kumusaidia Yona afikiri. Anamuambia nabii huyo kwamba mumea ambao anasikitikia ambao ulikomaa usiku mumoja tu, si Yona aliyeupanda wala kuufanya ukomae. Kisha Mungu anamalizia kwa kusema hivi: ‘Na mimi, kwa upande wangu, je, sipaswe kusikitikia Ninawi ule muji mukubwa, ambao una watu zaidi ya 120 000 wasiojua hata kidogo tofauti kati ya mukono wao wa kuume na wa kushoto, na tena wanyama wengi wa kufugwa?’​—Yona 4:10, 11. *

21. (a) Yehova alitumia mufano gani ili kumufundisha Yona? (b) Namna gani habari ya Yona inaweza kutusaidia tujichunguze vizuri namna tulivyo kabisa?

21 Je, unaelewa kabisa jambo Yehova alipenda kumufundisha Yona kupitia mufano huo? Yona hakufanya jambo lolote ili mumea huo uote na kukomaa. Kwa upande mwengine, ni Yehova aliyekuwa amewapa watu wa Ninawi uzima, na kuwapa vitu vyote vinavyoendeleza uzima huo kama anavyofanya kwa viumbe vyote vyenye uzima hapa duniani. Namna gani Yona anaweza kuona mumea kuwa wa lazima sana kuliko uzima wa watu zaidi ya 120 000, pamoja na wanyama wao wote wa kufugwa? Ikiwa Yona anasikitikia mumea wa mutango, ni kwa sababu ya faida zake mwenyewe, sivyo? Bila shaka, ni kwa sababu unamufaidi yeye. Tena, ikiwa anakasirika kwa sababu ya Ninawi, ni kwa sababu hasira hiyo inatokana na mawazo yake ya uchoyo, sivyo? Tamaa ya kupenda aheshimiwe, aonekane kuwa si muongo. Habari ya Yona inaweza kutusaidia tujichunguze vizuri namna tulivyo kabisa. Ni nani kati yetu anayeweza kusema kwamba hana mawazo kama hayo ya uchoyo? Tunapaswa kuwa wenye shukrani kwa sababu Yehova ametuvumilia sana na anaendelea kutufundisha kuwafikiria wengine zaidi, kujitia mahali pa wengine na kuwa wenye rehema ao huruma zaidi, kama yeye!

22. (a) Ni nini inayoonyesha kwamba mafundisho ya Yehova yenye kujaa hekima kuhusu rehema ao huruma yaligusa moyo wa Yona? (b) Ni nini ambayo sisi wote tunapaswa kujifunza?

22 Sasa ulizo ni hili, je, jambo hilo lililomupata Yona katika maisha lilimufundisha kabisa? Kitabu cha Yona mwenyewe kinamalizika na ulizo la Yehova ambalo halikujibiwa. Watu wanaoichambua Biblia wanasikitika kwamba Yona hakujibu ulizo hilo. Lakini, kwa kweli alijibia kwa sababu aliandika kitabu cha Biblia cha Yona. Ushuhuda mbalimbali unaonyesha kwamba ni Yona ndiye aliyeandika kitabu hicho. Wazia nabii huyo anaporudi katika inchi yake, anaanza kuandika habari yake. Katika akili yako unaweza kuona picha ya mwanaume huyo muzee kabisa, mwenye hekima sana, munyenyekevu kabisa, anatikisa kichwa ili kuonyesha sikitiko lake kadiri anavyozungumuzia makosa yake, uasi wake, na jinsi alivyojionyesha kuwa mwenye moyo mugumu kwa kukataa kuonyesha rehema. Ni wazi kabisa, Yehova kupitia mafundisho yake yenye kujaa hekima, alimufundisha Yona namna ya kuwa mwenye rehema. Je, sisi pia tutaonyesha sifa hiyo?—Soma Mathayo 5:7.

^ fu. 6 Inafikiriwa kwamba wakati wa Yona muji wa Samaria, muji mukubwa wa makabila kumi ya ufalme wa Waisraeli, ulikuwa na wakaaji 20 000 mupaka 30 000 hivi. Hesabu hiyo ni ndogo mara ine ikilinganishwa na hesabu ya wakaaji wa Ninawi. Wakati muji wa Ninawi ulikuwa wenye kuendelea sana kuliko inchi zingine, inaonekana kama huo ndio ulikuwa muji mukubwa kuliko miji mingine duniani kote.

^ fu. 8 Kusema kwamba wanyama wa kufugwa pia walihusika kunaweza kushangaza, lakini wakati wa zamani jambo hilo lilikuwa linafanyika. Mwanahistoria Mugiriki Herodote alisema kwamba hapo zamani wakati jenerali wa Perse mwenye kupendwa sana alikufa, watu walimuomboleza kwa kuhusisha wanyama wa kufugwa katika desturi zao.

^ fu. 20 Mungu anaposema kwamba watu wa Ninawi hawajue tofauti kati ya mukono wao wa kuume na wa kushoto, hilo linamaanisha kwamba watu hao wako kama watoto wadogo wasiojua sheria za Mungu.