Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA INE

Yesu Kristo Ni Nani?

Yesu Kristo Ni Nani?
  • Yesu ana daraka gani la pekee?

  • Alitoka wapi?

  • Alikuwa mutu wa namna gani?

1, 2. (a) Kwa nini kujua tu jina la mutu fulani anayejulikana sana hakumaanishi kama unamujua vizuri? (b) Watu wana mawazo gani mbalimbali juu ya Yesu?

HAPA duniani kuna watu wenye kujulikana sana. Wamoja wanajulikana sana katika muji wao ao katika inchi yao. Wengine wanajulikana duniani pote. Lakini, kujua tu jina la mutu fulani anayejulikana sana, haimaanishi kama unamujua vizuri. Haimaanishi kama unajua kila jambo juu ya namna alivyokomaa na juu ya sifa zake.

2 Mahali pote duniani watu wamekwisha kusikia habari juu ya Yesu Kristo, hata ikiwa aliishi duniani kumekwisha kupita miaka 2 000 hivi. Hata hivyo, wengi hawajui vizuri ikiwa Yesu alikuwa nani. Wamoja wanasema yeye alikuwa tu mutu muzuri. Wengine wanasema alikuwa tu nabii. Tena kuna wengine wanaoamini kama Yesu ni Mungu na hivyo anapaswa kuabudiwa. Anapaswa kweli kuabudiwa?

3. Sababu gani ni lazima ujue mambo ambayo Biblia inafundisha juu ya Yesu?

3 Ni jambo la lazima ujue yale ambayo Biblia inafundisha juu ya Yesu. Kwa sababu gani? Biblia inasema hivi: ‘Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemutuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Ndiyo, kumujua Yehova Mungu na Yesu Kristo kunaweza kumufanya mutu apate uzima wa milele katika paradiso hapa duniani. (Yohana 14:6) Tena, Yesu ndiye aliyetuonyesha vizuri zaidi namna tunapaswa kujiendesha na namna tunapaswa kuwatendea wengine. (Yohana 13:34, 35) Katika sura ya 1 tulijifunza mambo ambayo Biblia inafundisha juu ya Mungu. Sasa acha tujifunze yale inayosema juu ya Yesu Kristo.

YESU NDIYE MASIYA ALIYEAHIDIWA

4. Majina “Masiya” na “Kristo” yanamaanisha nini?

4 Zamani sana mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Biblia ilisema Mungu atatuma mutu fulani ili aje kuwa Masiya, ao Kristo. Majina “Masiya” (neno la Kiebrania) na “Kristo” (neno la Kigiriki) yanamaanisha “Mutiwa-Mafuta.” Masiya huyo alipaswa kutiwa mafuta, maana yake, Mungu alipaswa kumuchagua ili kumupa daraka fulani la pekee. Katika sura za mwisho tutajifunza mengi juu ya daraka kubwa la Masiya katika utimizo wa ahadi za Mungu. Tena tutajifunza mambo mazuri ambayo Yesu anaweza kutufanyia hata sasa. Lakini, mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, watu wengi walikuwa wakijiuliza, ‘Ni nani atakayekuwa Masiya?’

5. Wanafunzi wa Yesu waliamini kabisa kama yeye ni nani?

5 Wanafunzi wa Yesu wa Nazareti waliamini kabisa kama yeye ndiye Masiya aliyeahidiwa. (Yohana 1:41) Simoni Petro, mumoja kati yao, alimuambia Yesu bila kusita: “Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” (Mathayo 16:16) Basi, ni nini iliyowasaidia waamini kama Yesu kabisa ndiye Masiya aliyeahidiwa? Ni nini inayoweza kutusaidia sisi pia?

6. Toa mufano unaoonyesha namna Yehova amewasaidia watu waaminifu wamutambue Masiya.

6 Manabii wa Mungu walioishi mbele ya kuja kwa Yesu walitabiri mambo mengi juu ya Masiya, mambo ambayo yangemutambulisha. Kwa mufano: Tuseme wanakuomba uende kumupokea mutu usiyemujua mahali palipo na watu wengi, kama vile sokoni. Ikiwa wanakupatia alama fulani ya kumutambua mutu huyo, hilo linaweza kukusaidia, sivyo? Vilevile, kupitia manabii, Yehova ametuelezea mambo mengi ambayo Masiya angefanya na yale ambayo yangemupata katika maisha. Kutimia kwa unabii huo kungesaidia watu waaminifu wamutambue Masiya vizuri.

7. Ni mambo gani mawili yaliyotabiriwa juu ya Yesu na yalitimia?

7 Tuchukue mifano miwili ya unabii ambao ungesaidia watu. Mufano wa kwanza: Miaka zaidi ya 700 mbele ya kuzaliwa kwa Masiya, nabii Mika alitabiri kama Masiya atazaliwa Bethlehemu, muji mudogo katika Yuda. (Mika 5:2) Sasa, Yesu alizaliwa wapi? Ajabu, alizaliwa tu katika muji huo! (Mathayo 2:1, 3-9) Mufano wa pili: Miaka mingi mbele, unabii wa Danieli 9:25 ulionyesha mwaka ambao Masiya atatokea, yaani, mwaka wa 29. * Kutimia kwa unabii huo na unabii mwingine mbalimbali kunaonyesha kama Yesu ndiye Masiya aliyeahidiwa.

Wakati Yesu alibatizwa, ndio wakati alikuwa sasa Masiya, ao Kristo

8, 9. Siku Yesu alipobatizwa, ni nini iliyoonyesha wazi kama yeye ndiye Masiya?

8 Jambo lingine lililoonyesha kama Yesu ndiye Masiya lilionekana wazi karibu na mwisho wa mwaka wa 29. Mwaka huo, Yesu alimuendea Yohana Mubatizaji kwenye Muto Yordani, ili abatizwe. Yehova alikuwa amemuahidi Yohana kama ataona alama itakayomusaidia kumutambua Masiya. Aliiona alama hiyo alipomubatiza Yesu. Biblia inasema hivi: ‘Baada ya kubatizwa Yesu akapanda mara moja kutoka katika maji; na, tazama! mbingu zikafunguliwa, naye akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa, ikija juu yake. Tazama! Kulikuwa pia na sauti kutoka mbinguni iliyosema: Huyu ni Mwanangu, mupendwa, ambaye nimemukubali.’ (Mathayo 3:16, 17) Kisha kuona na kusikia, Yohana aliamini kabisa kama Yesu alitumwa na Mungu. (Yohana 1:32-34) Siku hiyo, wakati roho ya Mungu, ao nguvu yake ya utendaji, ilipomwangwa juu ya Yesu, ndipo akawa Masiya, ao Kristo, aliyechaguliwa na Mungu ili kuwa Kiongozi na Mufalme.​—Isaya 55:4.

9 Kutimia kwa unabii wa Biblia na sauti ya Mungu mwenyewe vinaonyesha wazi kama Yesu ndiye Masiya aliyeahidiwa. Lakini Biblia inajibu maulizo mengine mawili ya lazima juu ya Yesu Kristo: Alitoka wapi? Na alikuwa mutu wa namna gani?

YESU ALITOKA WAPI?

10. Biblia inafundisha nini juu ya maisha ya Yesu mbele ya kuzaliwa kwake duniani?

10 Biblia inafundisha kama Yesu aliishi mbinguni mbele ya kuja hapa duniani. Nabii Mika alitabiri kuwa Masiya alipaswa kuzaliwa Bethlehemu na kama asili Yake “ni kutoka nyakati za kale.” (Mika 5:2) Mara nyingi, Yesu mwenyewe alikuwa akisema kama aliishi mbinguni mbele ya kuzaliwa mwanadamu. (Yohana 3:13; 6:38, 62; 17:4, 5) Alipokuwa kiumbe cha kiroho huko mbinguni, Yesu alikuwa na uhusiano wa kipekee sana pamoja na Yehova.

11. Kwa sababu gani Yesu ndiye mwana ambaye Yehova anapenda sana?

11 Yesu ndiye mwana ambaye Yehova anapenda sana. Kuna sababu! Yesu anaitwa ‘muzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,’ maana yake yeye ndiye kiumbe cha kwanza cha Mungu. * (Wakolosai 1:15) Kuna jambo lingine linalomutofautisha Yesu na viumbe vingine. Yeye ni ‘Mwana muzaliwa wa pekee.’ (Yohana 3:16) Maana yake ni Yesu pekee yake ndiye aliyeumbwa moja kwa moja na Mungu. Kisha, Mungu alimutumia ili kuumba viumbe vingine vyote. (Wakolosai 1:16) Yesu pia anaitwa “Neno.” (Yohana 1:14) Maana yake alikuwa musemaji wa Mungu; alikuwa akiwapelekea wana wengine wa Mungu, yaani, malaika na wanadamu, habari na maagizo kutoka kwa Baba yao.

12. Namna gani tunajua kama Yesu halingani na Mungu?

12 Je, Mwana huyo muzaliwa wa kwanza analingana na Mungu kama wengine wanavyoamini? Biblia haifundishi hivyo. Fungu la 11 linaonyesha kama Mwana huyo aliumbwa na Mungu. Kwa hiyo, Yesu ana mwanzo, lakini Yehova Mungu hana mwanzo wala mwisho. (Zaburi 90:2) Mwana huyo muzaliwa wa pekee hajawaza hata siku moja kujilinganisha na Baba yake. Biblia inafundisha waziwazi kama Baba ni mukubwa kuliko Mwana. (Yohana 14:28; 1 Wakorintho 11:3) Yehova tu ndiye “Mungu Mweza-Yote.” (Mwanzo 17:1) Kwa hiyo, hakuna mutu anayeweza kujilinganisha naye. *

13. Biblia inasema Yesu ni ‘mufano wa Mungu asiyeonekana,’ maana yake nini?

13 Yehova aliishi pamoja na mwana wake wa kwanza mamilioni ya miaka, mbele ya kuumba mbingu zenye kujaa nyota na pia dunia. Kwa kweli, walipendana sana! (Yohana 3:35; 14:31) Mwana huyo aliyependwa sana alifanana kabisa Baba yake. Ndiyo sababu Biblia inasema kama Mwana huyo ni ‘mufano wa Mungu asiyeonekana.’ (Wakolosai 1:15) Kama vile tu mwana anavyoweza kumufanana baba yake sana katika mambo mbalimbali, Mwana huyo wa Mungu alionyesha sifa mbalimbali za Baba yake.

14. Namna gani Mwana muzaliwa wa pekee wa Yehova alizaliwa mwanadamu?

14 Mwana muzaliwa wa pekee wa Yehova alikubali kuacha makao yake mbinguni na kuja duniani, kuwa mwanadamu. Labda unaweza kujiuliza, ‘Namna gani kiumbe cha kiroho anaweza kuzaliwa mwanadamu?’ Ili jambo hilo lifanyike, Yehova alifanya muujiza. Alihamisha uzima wa Mwana wake muzaliwa wa kwanza na kuutia katika tumbo la uzazi la Maria, aliyekuwa bado bikira. Mimba ya Maria haikuwa ya mwanaume yeyote. Ndiyo sababu mwana ambaye Maria alizaa alikuwa mukamilifu na akamuita Yesu.​—Luka 1:30-35.

YESU ALIKUWA MUTU WA NAMNA GANI?

15. Kwa nini kupitia Yesu tunaweza kumujua Yehova vizuri zaidi?

15 Mambo ambayo Yesu alisema na kufanya yanatusaidia kumujua vizuri. Tena, kupitia Yesu tunaweza kumujua Yehova vizuri zaidi. Sababu gani? Kumbuka kama Mwana huyo ni mufano kabisa wa Baba yake. Ndiyo sababu Yesu alimuambia mwanafunzi wake mumoja hivi: ‘Yule ambaye ameniona mimi amemuona Baba pia.’ (Yohana 14:9) Vitabu ine vya Biblia vinavyoitwa Injili (Mathayo, Marko, Luka, na Yohana) vinatuelezea mambo mengi juu ya maisha, kazi na sifa mbalimbali za Yesu Kristo.

16. Yesu alikuwa akifundisha habari gani, na habari hiyo ilikuwa ya nani?

16 Yesu alijulikana sana kuwa “Mwalimu.” (Yohana 1:38; 13:13) Alikuwa akifundisha nini? Alikuwa akifundisha zaidi sana “habari njema ya ufalme,” yaani, Ufalme wa Mungu, serikali ya mbinguni itakayoitawala dunia nzima na kuwaletea wanadamu watiifu baraka za milele. (Mathayo 4:23) Habari hiyo ilikuwa ya nani? Yesu mwenyewe alisema: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma,” yaani, Yehova. (Yohana 7:16) Yesu alijua kama Baba yake anapenda watu wasikie ile habari njema ya Ufalme. Katika sura ya 8, tutajifunza mambo mengi juu ya Ufalme wa Mungu na mambo ambayo utatimiza.

17. Yesu alikuwa akifundisha wapi, na sababu gani alikuwa akijikaza sana kuwafundisha watu?

17 Yesu alikuwa akifundisha wapi? Kila mahali alipokuta watu: nyumbani kwao, mashambani, katika vijiji, katika miji, na sokoni. Yesu hakuwa anangojea watu wamutafute; yeye ndiye aliyekuwa akiwatafuta. (Marko 6:56; Luka 19:5, 6) Sababu gani Yesu alikuwa akijikaza hivyo na kutumia wakati mwingi katika kuhubiri na kufundisha? Kwa sababu Mungu alipenda afanye hivyo. Sikuzote Yesu alikuwa anafanya mapenzi ya Baba yake. (Yohana 8:28, 29) Lakini kulikuwa sababu nyingine iliyomuchochea kuhubiri. Alikuwa akiwasikilia huruma watu waliomukaribia. (Mathayo 9:35, 36) Viongozi wao wa kidini hawakuwahangaikia. Yesu alijua kama watu hao walipenda kusikia habari ya Ufalme.

18. Ni sifa gani za Yesu zinazokuvutia sana?

18 Yesu alikuwa muchangamufu, alikuwa mutu mwema, na alikuwa akiwahangaikia watu. Kwa hiyo, watu walimukaribia bila magumu. Hata watoto wadogo walifurahia kumukaribia. (Marko 10:13-16) Yesu hakuwa na ubaguzi. Alikuwa akichukia mambo mabaya na ukosefu wa haki. (Mathayo 21:12, 13) Alikuwa akiwaheshimu wanawake ingawa wakati huo walikuwa wakionewa na kuimwa haki zao. (Yohana 4:9, 27) Yesu alikuwa munyenyekevu kabisa. Siku fulani, aliwanawisha mitume wake miguu; kazi ambayo ilifanywa kwa kawaida na mutumishi wa hali ya chini.

Yesu alikuwa anahubiria watu kila mahali alipowakuta

19. Ni mufano gani unaoonyesha kama Yesu alikuwa akijitia pa nafasi ya watu wengine?

19 Yesu alikuwa akijitia pa nafasi ya watu wengine. Hilo lilionekana wazi alipokuwa akiwaponya watu kwa miujiza, kwa nguvu ya roho ya Mungu. (Mathayo 14:14) Kwa mufano, mutu fulani mwenye ukoma alimukaribia Yesu na kusema: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Yesu alijisikia kama vile ni yeye aliyekuwa akiteseka. Alimusikilia huruma, akanyoosha mukono na kumugusa mutu huyo, akamuambia: “Ninataka. Takasika.” Na mara moja mutu huyo akapona! (Marko 1:40-42) Unawaza mutu huyo alijisikia namna gani?

YESU ALIBAKI MWAMINIFU MUPAKA KUFA

20, 21. Namna gani Yesu alituwekea mufano muzuri kabisa wa kumutii Mungu kwa uaminifu?

20 Yesu alimutii Mungu kwa uaminifu, alituwekea mufano muzuri kabisa. Alibaki mwaminifu kwa Baba yake wa mbinguni katika hali zote na hata mbele ya upinzani na mateso. Yesu alipinga kabisa vishawishi vya Shetani. (Mathayo 4:1-11) Wakati fulani, wengine kati ya ndugu zake hawakumuamini, hata walisema kama alikuwa “amerukwa na akili.” (Marko 3:21) Hata hivyo, Yesu hakuwafuata; aliendelea kufanya kazi ya Mungu. Ijapokuwa alitukanwa na kutendewa vibaya, Yesu alijizuia, hata siku moja hakulipiza wapinzani wake kisasi.​—1 Petro 2:21-23.

21 Yesu alibaki mwaminifu mupaka kufa; maadui wake walimutesa sana na kumuua bila huruma. (Wafilipi 2:8) Wazia kwanza mambo aliyovumilia usiku wa mwisho wa maisha yake hapa duniani. Alikamatwa, alishitakiwa na mashahidi wa uongo, alihukumiwa na waamuzi waovu, alichekewa kwa zarau, aliteswa na maaskari. Akiwa mwenye kupigwa misumari na kutundikwa kwenye muti wa mateso, mbele ya kufa, alipaza sauti: “Imetimizwa!” (Yohana 19:30) Hata hivyo, siku ya tatu kisha kufa kwake, Baba yake wa mbinguni alimufufua na alimufanya tena kuwa kiumbe cha kiroho. (1 Petro 3:18) Kisha majuma machache, Yesu alirudia mbinguni. Huko, ‘aliketi kwenye mukono wa kuume wa Mungu’ akingojea kupokea mamlaka ya kifalme.​—Waebrania 10:12, 13.

22. Yesu alitimiza jambo gani kwa kubaki mwaminifu mupaka kufa?

22 Yesu alitimiza jambo gani kwa kubaki mwaminifu mupaka kufa? Kifo cha Yesu kimetufungulia njia ya kupata uzima wa milele katika paradiso hapa duniani, kama vile Yehova alivyokusudia hapo mwanzo. Namna gani? Sura inayofuata itazungumuzia jambo hilo.

^ fu. 7 Unaweza kupata maelezo zaidi ya unabii wa Danieli uliotimia juu ya Yesu katika Nyongeza, ukurasa 197-199.

^ fu. 11 Ikiwa Yehova anaitwa Baba ni kwa sababu yeye ndiye Muumbaji. (Isaya 64:8) Yesu anaitwa Mwana wa Mungu, kwa sababu Mungu ndiye aliyemuumba. Hiyo ndiyo sababu malaika wengine na hata Adamu wanaitwa wana wa Mungu.​—Ayubu 1:6; Luka 3:38.

^ fu. 12 Unaweza kupata maelezo mengine yanayoonyesha kama Yesu halingani na Mungu katika Nyongeza, ukurasa wa 201-204.