Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA SABA

Namna ya Kumukaribia Mungu Katika Sala

Namna ya Kumukaribia Mungu Katika Sala
  • Sababu gani tunapaswa kusali kwa Mungu?

  • Tunapaswa kufanya nini ili Mungu asikilize sala zetu?

  • Namna gani Mungu anajibu sala zetu?

[Picha kwenye ukurasa wa 171]Watu wanasali katika hali mbalimbali

Mungu anaweza kusikiliza sala zako wakati wowote na mahali popote ulipo

1, 2. Sababu gani tunapaswa kuiona sala kuwa pendeleo la ajabu, na sababu gani kujua yale Biblia inafundisha juu ya sala ni kwa lazima sana?

TUKILINGANISHA dunia na nyota nyingi zilizo angani, utaona kama dunia ni kitu kidogo sana. Kwa kweli, Yehova, “[Muumbaji] wa mbingu na dunia,” anaona mataifa yote kuwa kama tone dogo la maji katika ndoo ao mbegeti. (Zaburi 115:15; Isaya 40:15) Hata hivyo, Biblia inasema: ‘Yehova yuko karibu na wote wanaomuitia, wote wanaomuitia yeye katika ukweli. Atawatimizia wale wanaomuogopa tamaa yao, naye atakisikia kilio chao cha kuomba musaada.’ (Zaburi 145:18, 19) Hilo ni jambo la ajabu kabisa! Muumbaji mweza-yote yuko karibu yetu naye atatusikiliza ‘tukimuitia yeye katika ukweli.’ Kusali kwa Mungu ni pendeleo la ajabu kabisa!

2 Hata hivyo, ikiwa tunapenda Yehova asikilize sala zetu, tunapaswa kusali namna anavyopenda. Ili kufanya hivyo, tunapaswa kwanza kujua mambo ambayo Biblia inafundisha juu ya sala, sivyo? Kujua yale Biblia inasema juu ya sala ni kwa lazima sana; sala inaweza kutusaidia tuwe na uhusiano muzuri sana na Yehova.

SABABU GANI TUNAPASWA KUSALI KWA YEHOVA?

3. Taja sababu moja kubwa inayotufanya tusali kwa Yehova?

3 Sababu moja kubwa inayotufanya tusali kwa Yehova ni hii: Yeye anataka tufanye hivyo. Neno lake linatuambia hivi: ‘Musihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.’ (Wafilipi 4:6, 7) Hakika, hatupaswi kupuuza mupango huo wenye upendo ambao Mutawala Mukubwa wa ulimwengu amechukua kwa ajili yetu!

4. Namna gani kusali kwa Yehova kwa ukawaida kunafanya uhusiano wetu naye uwe nguvu?

4 Sababu nyingine ni hii: Tunaposali kwa Yehova kwa ukawaida, uhusiano wetu na yeye unakuwa nguvu. Marafiki wa kweli hawazungumuzi tu wakati mumoja ana lazima ya kitu fulani. Marafiki wazuri wanahangaikiana, na urafiki wao unakuwa nguvu wakati kila mumoja anaelezea mwenzake bila woga mawazo yake, mahangaiko yake na namna anavyojisikia. Tunaweza kusema kama uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu uko hivyo. Kitabu hiki kimekusaidia kujua mambo mengi ambayo Biblia inafundisha juu ya Yehova, sifa zake, na makusudi yake. Umejifunza kama yeye ni mutu anayeishi ambaye unaweza kufanya naye urafiki. Kupitia sala, unaweza kumuelezea mawazo yako na namna unavyojisikia kabisa. Unapofanya hivyo uhusiano wako na Yehova unakuwa muzuri kabisa.​—Yakobo 4:8.

MAMBO ANAYOTUOMBA TUTIMIZE

5. Ni nini inayoonyesha kama Mungu hasikilizi sala yoyote?

5 Je, Yehova anasikiliza kila sala? Sikia vile alivyowaambia Waisraeli waasi katika siku za nabii Isaya: ‘Hata munapotoa sala nyingi, mimi sisikilizi; mikono yenu imejaa umwangaji wa damu.’ (Isaya 1:15) Kwa hiyo, kuna matendo fulani yanayoweza kuzuia sala zetu. Basi, ili Mungu asikilize sala zetu na kuzifurahia, tunapaswa kutimiza mambo anayotuomba.

6. Ni jambo gani la maana Mungu anatuomba ili asikilize sala zetu, na ni nini inayoonyesha hilo?

6 Jambo moja la maana analotuomba ni kuwa na imani. (Marko 11:24) Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Bila imani haiwezekani kamwe kumupendeza [Mungu] vema, kwa maana yule anayemukaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa musawabishaji wa wale wanaomutafuta kwa bidii.’ (Waebrania 11:6) Imani ya kweli haimaanishi tu kujua kama Mungu yuko na kama anasikiliza na kujibu sala zetu. Matendo ndio yanayoonyesha kama mutu ana imani. Maisha yetu ya kila siku yanapaswa kuonyesha kama tuna imani.​—Yakobo 2:26.

7. (a) Sababu gani tunapaswa kuonyesha heshima tunapomukaribia Yehova katika sala? (b) Namna gani tunaweza kuonyesha unyenyekevu na moyo usio na unafiki tunaposali?

7 Tena Yehova anaomba wale wanaomukaribia katika sala wafanye hivyo kwa unyenyekevu na moyo usio na unafiki. Wewe hauoni kama inatuomba kabisa kuwa wanyenyekevu tunapozungumuza na Yehova? Kwa mufano, wakati watu wanapopata nafasi ya kuzungumuza na mufalme ao raisi, kwa kawaida wanafanya hivyo kwa heshima ili kuonyesha kama wanaheshimu cheo ao mamlaka yake. Basi, tunapaswa kumuheshimu Yehova hata zaidi tunapozungumuza naye, sivyo? (Zaburi 138:6) Usisahau kama yeye ni “Mungu Mweza-Yote.” (Mwanzo 17:1) Tunaposali hali yetu inapaswa kuonyesha kama tunatambua kwa unyenyekevu kuwa sisi ni wadogo mbele yake. Unyenyekevu huo utatusukuma kusali kwa moyo wote na bila unafiki wowote, na kuepuka sala za kidesturi, za kurudilia mambo yaleyale.​—Mathayo 6:7, 8.

8. Namna gani tunaweza kutenda kulingana na sala zetu?

8 Jambo lingine Mungu anatuomba ili asikilize sala zetu ni kutenda kulingana na sala zetu. Yehova anataka tujikaze ili tutende kulingana na sala zetu. Kwa mufano, tukisali ‘atupatie leo mukate wetu kwa ajili ya siku hii,’ ni lazima tutumike kwa bidii kazi yoyote ile tunayoweza kupata na ile tunayoweza kufanya. (Mathayo 6:11; 2 Wathesalonike 3:10) Tukisali atusaidie kushinda uzaifu wetu fulani wa kimwili, tunapaswa pia kuwa waangalifu ili kuepuka mambo ao hali zinazoweza kutuingiza katika vishawishi. (Wakolosai 3:5) Zaidi ya mambo hayo anayotuomba, kuna maulizo fulani juu ya sala na tutapenda kupata majibu ya maulizo hayo.

MAJIBU YA MAULIZO FULANI JUU YA SALA

9. Tunapaswa kumutolea nani sala zetu, na tutatoa sala kupitia nani?

9 Tunapaswa kumutolea nani sala zetu? Yesu alifundisha wanafunzi wake kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni.” (Mathayo 6:9) Kwa hiyo, ni Yehova Mungu tu ndiye tunapaswa kutolea sala zetu. Lakini, Yehova anataka tutambue cheo cha Mwana wake muzaliwa wa pekee, Yesu Kristo. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 5, Yesu alitumwa duniani ili awe zabihu ya kutukomboa kutoka katika zambi na kifo. (Yohana 3:16; Waroma 5:12) Yeye ndiye Kuhani Mukubwa na Muamuzi aliyechaguliwa na Mungu. (Yohana 5:22; Waebrania 6:20) Kwa hiyo, Maandiko yanatuomba tusali kupitia Yesu. Yeye mwenyewe alisema hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Basi, ili Mungu asikilize sala zetu, ni lazima tusali kwa Yehova tu kupitia Mwana wake.

10. Sababu gani hatulazimishwi kabisakabisa kuwa katika hali fulani wakati tunaposali?

10 Je, tunapaswa kusimama, kukaa, kupiga magoti ao kuwa katika hali fulani wakati tunaposali? Hapana. Yehova haombi kabisakabisa tuwe katika hali fulani. Biblia inafundisha kama mutu anaweza kusimama, kukaa, kuinama ao kupiga magoti anaposali. (1 Mambo ya Nyakati 17:16; Nehemia 8:6; Danieli 6:10; Marko 11:25) Jambo la maana si namna watu wanavyotuona katika hali fulani, lakini namna Mungu anavyoona moyo wetu. Kwa hiyo, iwe wakati tunapofanya kazi yetu ya kila siku ao tunapokutana na hali fulani inayoomba kutenda kwa haraka, tunaweza kusali kimyakimya katika moyo mahali popote tulipo. Yehova anasikiliza sala kama hizo hata ikiwa watu walio pembeni yetu hawaoni kama sisi tunasali.​—Nehemia 2:1-6.

11. Ni mambo gani ya kipekee tunayoweza kuongea na Mungu katika sala?

11 Tunaweza kuomba nini katika sala zetu? Biblia inasema hivi: ‘Hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye [Yehova] anatusikia.’ (1 Yohana 5:14) Kwa hiyo, katika sala zetu tunaweza kuomba kila jambo, lakini hilo linapaswa kupatana na mapenzi ya Mungu. Je, Yehova anapenda tuzungumuze naye katika sala juu ya kila jambo linalotusumbua? Ndiyo! Tunaweza kuzungumuza naye katika sala kama vile mutu anavyozungumuza na rafiki yake wa kufa na kupona; bila kumuficha jambo lolote, ‘tukimimina moyo wetu’ mbele zake. (Zaburi 62:8) Ni vizuri pia tumuombe roho takatifu, kwa sababu itatusaidia kufanya mambo yanayofaa. (Luka 11:13) Tena tunaweza kumuomba Mungu atuongoze tunapochukua maamuzi ili yawe ya hekima na atupatie nguvu ya kushindana na magumu mbalimbali. (Yakobo 1:5) Tunapofanya zambi, tunapaswa kumuomba Mungu atusamehe kupitia zabihu ya Kristo. (Waefeso 1:3, 7) Ni kweli, tunapaswa kuongea na Mungu juu ya mambo yetu ya kipekee, lakini hatupaswi kusali tu juu ya mambo yetu. Tunapaswa pia kusali kwa ajili ya watu wengine kama vile watu wa familia yetu na ndugu na dada zetu Wakristo.​—Matendo 12:5; Wakolosai 4:12.

12. Katika sala zetu namna gani tunaweza kutia pa nafasi ya kwanza mambo ya Baba yetu wa mbinguni?

12 Katika sala zetu, mambo ya Yehova Mungu ndio yanapaswa kutiwa pa nafasi ya kwanza. Tunapaswa kumusifu na kumushukuru kutoka moyoni kwa sababu ya wema wake wote. (1 Mambo ya Nyakati 29:10-13) Katika sala ya mufano inayopatikana katika andiko la Mathayo 6:9-13, Yesu alitufundisha tusali jina la Mungu litakaswe, yaani, tulione kuwa kitu kitakatifu. Kisha akasema tusali Ufalme wa Mungu uje na mapenzi yake yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni. Ni kisha kuzungumuzia mambo hayo ya lazima ya Yehova ndipo Yesu alitaja mambo ya kipekee ya mutu. Sisi pia tunapomutanguliza Mungu katika sala zetu, tunaonyesha kama hatuhangaikii tu mambo yetu wenyewe.

13. Biblia inasema nini juu ya urefu wa sala zinazokubaliwa?

13 Sala zetu zinapaswa kuwa na urefu gani? Biblia haisemi ikiwa sala ambayo mutu anafanya akiwa peke yake ao mbele ya wengine inapaswa kuwa na urefu gani. Tunaweza kutoa sala fupi mbele ya kula ao sala ndefu tunapomuelezea Yehova mambo yaliyo katika moyo wetu kwa kipekee. (1 Samweli 1:12, 15) Hata hivyo, Yesu aliwalaumu watu waliokuwa wakijiona kuwa wenye haki, waliokuwa wakitoa sala ndefu ili waonekane na watu. (Luka 20:46, 47) Sala kama hizo hazimuambii Yehova kitu. Jambo la lazima ni kuongea na Yehova yale yaliyo katika moyo. Kwa hiyo, Mungu anaweza kukubali sala iwe ndefu ao fupi, itategemea hali na mahitaji ya mutu.

14. Biblia inamaanisha nini inapotuomba ‘tusali siku zote,’ na sababu gani hilo ni jambo lenye kufurahisha kabisa?

14 Tunapaswa kusali mara ngapi? Biblia inatutia moyo ‘tusali sikuzote,’ ‘tudumu katika sala,’ na ‘tusali bila kuacha.’ (Mathayo 26:41; Waroma 12:12; 1 Wathesalonike 5:17) Maandiko hayo hayamaanishi kama hatutafanya tena jambo lingine isipokuwa kusali tu kwa Yehova. Lakini, yanamaanisha kama tunapaswa kusali kwa ukawaida na tusiache kumushukuru Yehova kwa sababu ya wema anaotuonyesha, na kila mara tumuombe atuongoze, atufariji, na kututia nguvu. Ni jambo lenye kufurahisha kabisa kujua kama Yehova hatie sheria juu ya urefu wa sala ao hasemi ni mara ngapi tunaweza kumukaribia katika sala, sivyo? Ikiwa tunapendezwa kabisa na pendeleo la kuongea na Mungu katika sala, hatutakosa wakati wa kuzungumuza na Baba yetu wa mbinguni.

15. Sababu gani ni vizuri mutu kusema “Amina” mwisho wa sala, iwe ya kipekee ao wakati mutu fulani anaposali mbele ya watu wengi?

15 Sababu gani tunapaswa kusema “Amina” mwisho wa sala? Neno “amina” linamaanisha “hakika” ao “iwe hivyo.” Mifano iliyo katika Biblia inaonyesha kama ni vizuri kusema “Amina” mwisho wa sala, iwe ni sala yako mwenyewe ao unaposali mbele ya watu wengi. (1 Mambo ya Nyakati 16:36; Zaburi 41:13) Mutu anaposema “Amina” mwisho wa sala yake ya kipekee, anaonyesha kama maneno yake yanatoka katika moyo. Tunaposema “Amina” kimyakimya ao kwa sauti kisha mutu fulani kutoa sala mbele ya watu wengi, tunaonyesha kama tunakubali yale aliyosema katika sala.​—1 Wakorintho 14:16.

NAMNA MUNGU ANAVYOJIBU SALA ZETU

16. Tunaweza kuwa na uhakika gani juu ya sala zetu?

16 Je, kweli Yehova anajibu sala? Ndiyo! Kwa kuwa Yeye ni ‘Musikiaji wa sala’ tuko hakika kama anajibu sala zinazotolewa na mamilioni ya wanadamu walio na mioyo mizuri. (Zaburi 65:2) Yehova anaweza kujibu sala zetu kwa njia mbalimbali.

17. Sababu gani tunaweza kusema kama Mungu anatumia malaika zake na watumishi wake duniani ili kujibu sala zetu?

17 Yehova anatumia malaika zake na watumishi wake duniani ili kujibu sala zetu. (Waebrania 1:13, 14) Kuna watu wengi ambao walisali kwa Mungu ili kumuomba musaada wa kuelewa Biblia na kisha tu kusali walitembelewa na watumishi wa Yehova. Mambo kama hayo yanaonyesha kama malaika wanaongoza kazi ya kuhubiri Ufalme. (Ufunuo 14:6) Yehova anaweza kumusukuma Mukristo mwenzetu atusaidie tunaposali juu ya shida fulani.​—Methali 12:25; Yakobo 2:16.

18. Namna gani Yehova anatumia roho yake takatifu na Neno lake ili kujibu sala zetu?

18 Tena, Yehova anatumia roho yake takatifu na Neno lake, Biblia, ili kujibu sala za watumishi wake. Tunapoomba musaada wa kushindana na majaribu, Yehova anaweza kujibu sala yetu kwa kutuongoza na kututia nguvu kupitia roho yake takatifu. (2 Wakorintho 4:7) Mara nyingi Mungu anatujibu kupitia Biblia tunapomuomba uongozi fulani. Kupitia Biblia Yehova anatusaidia tujue namna ya kuchukua maamuzi ya hekima. Tunapojifunza Biblia kipekee na tunaposoma vichapo vinavyofasiria Biblia, kama kitabu hiki, tunaweza kupata maandiko yanayoweza kutusaidia. Ikiwa tuna lazima ya shauri fulani, yale yanayosemwa kwenye mikutano ya Kikristo kupitia Maandiko ao mashauri ya muzee fulani anayetuhangaikia yanaweza kuwa ndilo jibu tunalohitaji.​—Wagalatia 6:1.

19. Tunapaswa kukumbuka nini ikiwa wakati fulani inaonekana kama sala zetu hazijibiwi?

19 Ikiwa wakati fulani inaonekana kama Yehova anakawia kujibu sala zetu, hilo halimaanishi kama yeye ameshindwa kujibu. Kumbuka, Yehova anajibu sala zetu kupatana na mapenzi yake na kwa wakati wake. Yeye anajua vizuri sana mahitaji yetu kuliko sisi wenyewe na namna ya kuyatimiza. Mara nyingi anatuacha ‘tuendelee kuomba, kutafuta, na kupiga hodi.’ (Luka 11:5-10) Tunapofanya hivyo, Mungu anaona kama tuna lazima kabisa ya jambo tunalomuomba na tuna imani ya kweli. Tena, jua kama Yehova anaweza kujibu sala zetu kwa njia tusiyowazia. Kwa mufano, anaweza kujibu sala yetu juu ya jaribu fulani tunalopambana nalo, kwa kutupatia nguvu ya kuvumilia jaribu hilo kuliko kuliondoa.​—Wafilipi 4:13.

20. Sala ni pendeleo nzuri sana, kwa hiyo, sababu gani tunapaswa kusali kwa ukawaida?

20 Sisi ni wenye furaha sana kuona kama Muumbaji wa ulimwengu wote yuko karibu ya wote wanaomukaribia namna inavyofaa kupitia sala! (Zaburi 145:18) Kwa hiyo, tunapaswa kuzungumuza na Yehova kwa ukawaida kupitia sala kwa kuwa hilo ni pendeleo nzuri sana. Tukifanya hivyo, tutakuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova, ambaye ni Musikiaji wa sala.