Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Usiruhusu Kitu Chochote Kikutenganishe na Yehova

Usiruhusu Kitu Chochote Kikutenganishe na Yehova

‘Mujichagulie leo yule mutakayemutumikia.’​—YOS. 24:15.

1-3. (a) Namna gani mufano wa Yoshua unaweza kutusaidia tufanye uamuzi muzuri katika maisha yetu? (b) Hatupaswe kusahau nini tunapojikuta mbele ya maamuzi mawili ao zaidi?

 “KUCHAGUA,” hilo ni neno nzito kabisa. Maamuzi ya mutu yanaweza kuonyesha namna anavyotaka kutumia maisha yake. Tuchukue mufano: Wazia mutu fulani anatembea katika barabara na mara moja anafika mahali ambapo barabara hiyo inagawanyika na kuwa njia mbili zinazoelekea mahali tofauti. Mutu huyo atachagua njia gani? Ikiwa anajua mahali anapoenda, atachagua njia ambayo itamufikisha mahali amapoenda na kuacha ile inayoweza kumupoteza ao kumupeleka mbali na kusudi lake.

2 Biblia ina mifano ya watu wengi waliojikuta katika hali kama hiyo. Kwa mufano, Kaini alipaswa kuamua ikiwa atatenda kwa hasira ao ikiwa ataizuia hasira yake. (Mwa. 4:6, 7) Yoshua alipaswa kuamua kama atatumikia Mungu wa kweli ao miungu ya uongo. (Yos. 24:15) Kwa kuwa muradi wa Yoshua ulikuwa kumukaribia Yehova; yeye alichagua njia iliyomusaidia kufanya hivyo. Kaini hakuwa na muradi kama huo, kwa hiyo alichagua njia iliyomutenganisha na Yehova.

3 Wakati fulani, tunaweza kujikuta mbele ya maamuzi mawili ao zaidi. Ikiwa tunajikuta katika hali hiyo, tusisahau mahali tunapoenda, ao muradi wetu maishani, ni kusema, kumutukuza Mungu katika mambo yote tunayofanya na kuepuka kitu chochote kinachoweza kututenganisha naye. (Soma Waebrania 3:12.) Katika habari hii na ile inayofuata, tutaona mambo saba yanayoweza kututenganisha na Yehova.

KAZI

4. Kwa nini kazi ya kimwili ni ya maana katika maisha?

4 Wakristo wanapaswa kutosheleza mahitaji yao na ya familia zao. Biblia inaonyesha kama mutu asiyetaka kuwatimizia watu wa familia yake mahitaji yao, ni mubaya sana kuliko hata mupagani. (2 Thes. 3:10; 1 Tim. 5:8) Bila shaka, kazi ya kimwili ni ya maana katika maisha, lakini ikiwa sisi si waangalifu, inaweza kututenganisha na Yehova. Namna gani?

5. Ni mambo gani ya lazima tunapaswa kufikiria tunapotafuta kazi?

5 Wazia kwamba unatafuta kazi. Ikiwa unaishi katika inchi ambamo kupata kazi ni vigumu, unaweza kujaribiwa kuitika kazi yoyote inayojitokeza kwa mara ya kwanza. Lakini, namna gani ikiwa kazi hiyo inapingana na kanuni za Biblia? Namna gani ikiwa kazi hiyo itakuzuia kufanya mambo ya kiroho ao itakupeleka mbali na familia yako? Je, unapaswa tu kuikubali, ukifikiri kama ni afazali kuwa na kazi hata isiyofaa kuliko kubaki bila kazi? Kumbuka kwamba, kuchagua njia mbaya inaweza kukufanya uende mbali na Yehova. (Ebr. 2:1) Iwe unatafuta kazi ao unachunguza kazi uliyo nayo sasa ili kuona kama inafaa kwa Mukristo, namna gani unaweza kufanya maamuzi mazuri?

6, 7. (a) Mutu anaweza kuwa na miradi gani kuhusu kazi ya kimwili? (b) Ni muradi gani unaoweza kukusaidia umukaribie zaidi Yehova, na sababu gani?

6 Kama tulivyosema mwanzoni, usisahau mahali unapoenda, ao muradi wako. Jiulize hivi: ‘Ninataka kazi hii inifikishe wapi?’ Ukiona kazi ya kimwili kuwa tu ni njia ya kukutegemeza na kutegemeza familia yako ili kufanya mapenzi ya Yehova, basi, Yehova atakubariki. (Mt. 6:33) Yehova anajua namna anavyoweza kukusaidia wakati unapoteza kazi ao wakati unapatwa bila kutazamia na matatizo ya feza. (Isa. 59:1) Yeye “anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.”​—2 Pet. 2:9.

7 Lakini, namna gani ikiwa muradi wako ni kutaka tu kuwa na mali? Labda unaweza kufanikiwa. Lakini, usisahau kwamba “mafanikio” hayo hayatakosa kukuletea matatizo mengi. (Soma 1 Timotheo 6:9, 10.) Kufuatilia sana mali na kazi kutakutenganisha kabisa na Yehova.

8, 9. Wazazi wanapaswa kujiuliza nini kuhusu kazi yao ya kimwili? Eleza.

8 Ikiwa wewe ni muzazi, jiulize ikiwa unawapa watoto wako mufano muzuri. Ni mambo gani wanayoona ukitia pa nafasi ya kwanza katika maisha? Je, ni kazi yako ao urafiki wako pamoja na Yehova? Ikiwa wanaona kwamba unahangaikia sana cheo, sifa, na mali, je, hawatakufuata katika njia hiyo yenye hatari? je, jambo hilo haliweze kupunguza heshima yao kwako? Binti mumoja Mukristo mwenye miaka 17 alisema hivi: “Ninakumbuka kama zamani baba yangu alihangaikia sana kazi yake. Mwanzoni, ilionekana kama alitumika sana sababu alitaka tuwe na maisha mazuri kabisa; alitaka kuitunza familia yake vizuri. Lakini katika miaka ya hivi karibuni, mambo fulani yamebadilika. Yeye ni kazi tu, na analeta nyumbani vitu vya bei kali ambavyo hatuhitaji kabisa. Sasa watu wanatuwazia kuwa familia yenye feza nyingi, kuliko kujulikana kuwa familia inayowatia wengine moyo wafuatilie mambo ya kiroho. Ningependelea baba yangu atumike sana ili kuisaidia familia yake imukaribie zaidi Yehova kuliko kutafuta feza sana.”

9 Wazazi, musijitenge na Yehova kwa kuhangaikia sana kazi. Muwaonyeshe watoto wenu kupitia mufano wenu muzuri kwamba munaamini kwelikweli kama mambo ya kiroho ndio utajiri mukubwa zaidi ambao mutu anaweza kuwa nao, na si vitu vya kimwili.​—Mat. 5:3.

10. Kijana anapaswa kujiuliza nini anapotafuta kazi?

10 Ikiwa wewe ni kijana anayetafuta kazi, namna gani unaweza kufanya maamuzi mazuri? Kama tulivyosema mwanzoni, ni vizuri kujua mahali unapoenda, nikusema, muradi wako katika maisha. Ikiwa unajifunza kazi fulani, je, mazoezi hayo na kazi hiyo itakuruhusu kutia mambo ya Ufalme pa nafasi ya kwanza, ao itakutenganisha na Yehova? (2 Tim. 4:10) Je, unataka kuwaiga watu ambao furaha yao inategemea tu feza zao? Ao utachagua kuwa mwenye tumaini kama Daudi ambaye aliandika: ‘Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, Na bado sijamuona mutu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mukate.’ (Zab. 37:25) Kumbuka kwamba kuna njia mbili: moja ni ile inayokutenganisha na Yehova, na nyingine ni ile inayokupeleka kwenye maisha mazuri ya milele. (Soma Methali 10:22; Malaki 3:10.) Wewe utachagua njia gani? *

MAMBO YA KUJIFURAHISHA

11. Biblia inafundisha nini kuhusu kujifurahisha, lakini tunapaswa kuwa waangalifu na nini?

11 Biblia haikataze kujiburudisha ao kujifurahisha, wala haiseme kama kufanya hivyo ni kupoteza wakati. Mutume Paulo alimuandikia Timotheo hivi: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo.” (1 Tim. 4:8) Biblia inasema pia kama kuna “wakati wa kucheka” na “wakati wa kurukaruka,” na inatutia moyo tupumuzike kwa kiasi fulani ili tuwe na afya nzuri. (Mhu. 3:4; 4:6) Hata hivyo, ikiwa hatuko waangalifu, kujifurahisha huko kunaweza kututenganisha na Yehova. Namna gani? Kujifurahisha kunaweza kutokeza hatari mbili: namna ya kujifurahisha na wakati tunaopitisha kwa kujifurahisha.

Kujifurahisha kwa njia nzuri na kwa kiasi kunapumuzisha kabisa

12. Mutu anapaswa kujiuliza nini kuhusu mambo anayotazama ili kujifurahisha?

12 Kwanza, tuzungumuzie namna mbalimbali za kujifurahisha. Uwe hakika kwamba kuna namna mbalimbali za kujifurahisha nzuri. Lakini, jua kwamba namna nyingi ya kujifurahisha leo inahusu mambo ambayo Mungu anachukia sana: mambo ya kuuana, mambo ya kushirikiana na roho waovu, na mambo ya uasherati. Kwa hiyo, tunapaswa kuchunguza sana yale tunayotazama kwa kujifurahisha. Ujiulize hivi: Mambo ninayotazama kwa kujifurahisha yatakuwa na matokeo gani juu yangu? Je, yananichochea kuwa na roho isiyo na huruma, roho ya mashindano, ao roho ya mutu kujivunia sana inchi yake? (Met. 3:31) Je, kujifurahisha huko kunanichukua feza nyingi? Je, kunawakwaza wengine? (Rom. 14:21) Ninajifurahisha na watu wa aina gani? (Met. 13:20) Je, mambo ninayoona ninapojifurahisha yanaamusha ndani ya moyo wangu tamaa ya kufanya mambo mabaya?​—Yak. 1:14, 15.

13, 14. Unapaswa kujiuliza nini kuhusu wakati unaopitisha katika kujifurahisha?

13 Acheni tuzungumuzie pia wakati tunaopitisha katika kujifurahisha. Ujiulize hivi: ‘Je, ninapitisha wakati mwingi katika mambo ya kujifurahisha hivi kwamba ninabaki na wakati mudogo tu kwa ajili ya mambo ya kiroho?’ Ikiwa unachagua kupitisha wakati mwingi katika kujifurahisha, utaona kwamba kuliko kukupumuzisha mambo hayo yatakuchokesha kabisa. Ni kweli, wale wasiopitisha kipimo wanafurahia kabisa kujifurahisha kwao. Sababu gani? Kwa sababu wanajua kwamba wametimiza kwanza “mambo yaliyo ya maana zaidi,” kwa hiyo, wanapojifurahisha zamiri haiwasumbue.​—Soma Wafilipi 1:10, 11.

14 Hata ikiwa mutu anaweza kushawishiwa apitishe wakati mwingi katika mambo ya kujifurahisha, tusisahau kwamba njia hiyo inaweza kututenganisha na Yehova. Dada Kim aliye na miaka 20 alijionea jambo hilo. Yeye anasema hivi: “Nilienda kila mahali nilipoalikwa ili kujifurahisha. Kila mwisho wa juma, ni kusema Siku ya Tano, Siku ya Posho, na Siku ya Yenga, kulikuwa na karamu. Lakini sasa, ninaona kwamba kuna mambo mengi sana ya maana ambayo ninapaswa kufanya. Kwa mufano, kwa kuwa mimi ni painia, ninaamuka saa 12 ya asubui ili niende katika mahubiri, kwa hiyo siweze tena kubaki na marafiki mupaka saa saba ao saa munane ya usiku. Ninajua kwamba karamu zote si mbaya, lakini zinaweza kukengeusha sana. Kama vile katika kila jambo, hatupaswe kupitisha kiasi.”

15. Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao wajifurahishe kwa njia inayofaa?

15 Wazazi wanapaswa kutimiza mahitaji yao na ya watoto wao ya kimwili, ya kiroho, na kuhusu mambo ya kujifurahisha. Hiyo inamaanisha inafaa wawe na wakati wa kujifurahisha na watoto wao. Ikiwa wewe ni muzazi, usiwafanye watoto wako wajisikie kama wafungwa kwa kuwakataza wasijifurahishe hata kidogo. Lakini, uwe mwangalifu kuhusu mambo ya kujifurahisha yasiyo mazuri. (1 Kor. 5:6) Kufikiri vizuri mbele ya wakati, kunaweza kukusaidia upate mambo mazuri ya kujifurahisha yatakayomufanya kila mutu katika familia yako ajisikie vizuri. * Ukifanya hivyo, wewe na familia yako mutakuwa mumechagua njia nzuri ambayo itawafanya mumukaribie Yehova zaidi.

UPENDO WA KIFAMILIA

16, 17. Wazazi wengi wamepatwa na jambo gani lenye kuhuzunisha, na tunajua namna gani kama Yehova anaelewa uchungu wao?

16 Upendo ulio kati ya muzazi na mutoto wake ni wenye nguvu sana hivi kwamba Mungu aliutumia ili kuonyesha namna anavyowapenda watu wake. (Isa. 49:15) Kwa hiyo, ni jambo la kawaida kuhuzunika sana wakati mutu wa familia yetu anatengwa na kutaniko. Dada mumoja ambaye binti yake alitengwa, alisema hivi: “Nilihuzunika sana. Nilijiuliza, ‘Kwa nini binti yangu amemuacha Yehova?’ Nilifikiri kama kosa ni langu, na nilijilaumu.”

17 Yehova anaelewa uchungu wako. Yeye pia ‘aliumia moyoni mwake’ wakati mwana wake wa kwanza wa kibinadamu alimuasi, na baadaye, wakati watu wengi walioishi mbele ya Garika, walipomuasi pia. (Mwa. 6:5, 6) Labda wale ambao mutu wa familia yao hajatengwa hawaweze kuelewa kabisa namna uchungu huo unavyomukoseha mutu usingizi. Hata hivyo, usiruhusu mwenendo mubaya wa mutengwa katika familia yenu ukutenganishe na Yehova. Kwa hiyo, namna gani unaweza kuvumilia huzuni inayotokana na kutengwa kwa mutu fulani wa familia yenu?

18. Sababu gani wazazi hawapaswe kujilaumu wakati mutoto wao anatengwa na ushirika?

18 Usijilaumu wakati jambo hilo linatokea. Yehova amemuachia kila mutu uhuru wa kuchagua, na kila mutu wa familia yetu ambaye amejitoa katika sala kwa Yehova na kubatizwa anapaswa ‘kubeba muzigo wake mwenyewe.’ (Gal. 6:5) Kwa vyovyote, Yehova anamuona yule aliyechagua kufanya zambi kuwa ndiye mwenye kosa, wala si wewe. (Eze. 18:20) Tena, usiwalaumu wengine. Heshimu mupango ambao Yehova anatumia ili kuwanyoosha watu wake. Umupinge Shetani, kuliko kuwapinga wazee wanaolinda kutaniko.​—1 Pet. 5:8, 9.

Si vibaya kutumaini kama siku fulani mutu tunayemupenda atamurudilia Yehova

19, 20. (a) Wazazi walio na watoto waliotengwa wanaweza kufanya nini ili kuvumilia huzuni yao? (b) Wazazi hao wanaendelea kuwa na tumaini gani?

19 Kwa upande mwengine, ukichagua kumuwekea Yehova kinyongo ao kumukasirikia, hilo linaweza kukufanya ujitenge naye. Kwa kweli, jambo ambalo mutu huyo wa familia unayemupenda anahitaji, ni kuona kwamba upendo wako kwa Yehova ndilo jambo la maana zaidi kwako kuliko hata kifungo chenu cha familia. Kwa hiyo, ili uvumilie hali hiyo, unapaswa kuchunga hali yako mwenyewe ya kiroho. Usijitenge na ndugu na dada zako waaminifu. (Met. 18:1) Katika sala, umuambie Yehova namna unavyojisikia. (Zab. 62:7, 8) Usijipatie visababu na kuanza kushirikiana na mutu wa familia aliyetengwa; kwa mufano, kwa kuanza kuandikiana naye kupitia Internete. (1 Kor. 5:11) Uwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana. (1 Kor. 15:58) Dada tuliyezungumuzia hapo juu anaendelea kusema hivi: “Ninajua kwamba ninapaswa kuendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Yehova, na kufanya hali yangu ya kiroho iwe nguvu, ili niweze kumusaidia binti yangu wakati atakapomurudilia Yehova.”

20 Biblia inasema kwamba upendo ‘unatumaini mambo yote.’ (1 Kor. 13:4, 7) Kwa hiyo, ni vizuri kuendelea kutumaini kama siku moja, mutu wa familia unayemupenda atamurudilia Yehova. Kila mwaka, watengwa wengi wanatubu na kurudishwa katika tengenezo la Yehova. Yehova hatilie mashaka kutubu kwao. Lakini, yeye ‘iko tayari kusamehe.’—Zab. 86:5.

FANYA MAAMUZI YA HEKIMA

21, 22. Unapaswa kutumia namna gani uhuru wako wa kuchagua?

21 Yehova, aliwaumba wanadamu wakiwa na uhuru wa kuchagua. (Soma Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.) Lakini uhuru huo unawapa wanadamu daraka nzito. Kila Mukristo anapaswa kujiuliza hivi: ‘Mimi ninafuata njia gani? Je, nimeruhusu kazi, mambo ya kujifurahisha, ao upendo wa familia unitenganishe na Yehova?’

22 Upendo wa Yehova kwa watu wake haubadilike hata kidogo. Tunaweza tu kujitenga na Yehova ikiwa tu tunachagua kufuata njia mbaya. (Rom. 8:38, 39) Lakini, hatutake jambo hilo litupate! Kwa hiyo, tusiruhusu jambo lolote litutenganishe na Yehova. Habari inayofuata itazungumuzia mambo mengine mane yanayoweza kututenganisha na Yehova.

^ Ili kupata maelezo zaidi juu ya kuchagua kazi, soma sura ya 38 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2.

^ Kwa maelezo zaidi, soma Amkeni! ya Mwezi wa 11, 2011 ukurasa 17-19.