Mutumikie Yehova Bila Kusikitika
‘Nayasahau mambo ya nyuma na kujinyoosha kuenda mbele kuelekea mambo yaliyo mbele.’—FLP. 3:13.
1-3. (a) Kusikitika kunamaanisha nini, na tunaweza kujisikia namna gani kuhusu makosa tuliyofanya zamani? (b) Mufano wa mutume Paulo unatufundisha nini?
MUANDIKAJI mumoja anayeitwa Whittier aliandika hivi: “Maneno ‘kama ningejua’ ndio maneno yenye kusikitisha sana kuliko maneno yote ambayo watu wamesema ao kuandika.” Muandikaji huyo alikuwa anazungumuzia mambo ambayo tungependa kubadilisha ao kufanya tofauti na vile tunavyofanya. “Kusikitika” ao kujuta ni kuwa na uchungu moyoni, kuteseka kiakili, kwa sababu ya jambo fulani ambalo tulifanya ao hatukufanya; kunaweza pia kumaanisha “kuendelea kutoa machozi.” Sisi wote tumekwisha kufanya mambo ambayo tungependa kuanzililia tena ili tufanye sasa vizuri zaidi. Je, wewe unasikitika juu ya jambo fulani?
2 Watu fulani wamefanya makosa mazito katika maisha yao, wamefanya hata zambi nzito. Wengine hawajafanya mambo kama hayo, lakini wanajiuliza ikiwa maamuzi ambayo wamefanya katika maisha ni mazuri ao hapana. Kuna pia watu ambao wamesahau mambo ya zamani na wanaendelea na maisha yao kama kawaida. Na wengine wanasumbuliwa sana na “ikiwa ningejua” kuhusu mambo waliyofanya zamani. (Zab. 51:3) Hali yako inafanana na ile ya nani kati ya watu hao? Je, ungependa kumutumikia Mungu bila kusikitika kuanzia sasa na kuendelea? Je, kuna mufano katika Biblia unaoweza kutusaidia kufanya hivyo? Ndiyo, mufano wa mutume Paulo unaweza kutusaidia.
3 Katika maisha yake, Paulo alifanya makosa mazito na alichukua maamuzi ya hekima. Alihuzunishwa sana na makosa aliyofanya zamani, lakini alijifunza pia kwamba kumutumikia Mungu kwa uaminifu ndio siri ya kufanikiwa katika maisha. Acheni tuone namna mufano wa mutume Paulo unavyoweza kutusaidia tumutumikie Mungu bila kusikitika.
MAISHA YA ZAMANI YA MUTUME PAULO
4. Mutume Paulo alikuwa na maisha gani zamani yaliyomuhuzunisha?
4 Alipokuwa kijana Mufarisayo, Paulo alifanya mambo ambayo baadaye alikuja kusikitikia. Kwa mufano, alisimamia kampanye ya kuwatesa sana wanafunzi wa Yesu. Biblia inasema kama, kisha tu Stefano kuuawa, ‘Sauli [aliyeitwa baadaye Paulo] . . . alianza kushugulikia kutaniko kwa njia mbaya kabisa. Alikuwa akivamia nyumba moja baada ya nyingine, akiwakokota inje wanaume na wanawake, na kuwatia gerezani.’ (Mdo. 8:3) Mutu mumoja mwenye elimu ya Biblia anayeitwa Albert Barnes alisema kwamba maneno ya kigiriki yanayotafsiriwa “kushugulikia kwa njia mbaya” ni “maneno yenye nguvu, yanayoonyesha namna [Sauli] alivyokuwa na bidii na hasira nyingi katika kuwatesa wanafunzi wa Yesu.” Kwa hiyo, Barnes anasema kwamba “Sauli aliwashambulia wanafunzi wa Yesu kama munyama mwitu.” Sauli alikuwa Muyahudi mwenye bidii, na aliamini kabisa kwamba Mungu ndiye aliyemupa daraka la kumaliza kabisa kutaniko la Kikristo. Kwa hiyo, aliendelea kuwatesa Wakristo bila huruma, “akiwatisha wanafunzi wa Bwana na akitaka kuwaua . . . wanaume na wanawake pia.”—Mdo. 9:1, 2; 22:4. *
5. Eleza namna Sauli alivyoacha kuwatesa wanafunzi wa Yesu na kuanza kuhubiri juu ya Kristo.
5 Wakati fulani Sauli alitaka kuenda Damasko ili awakamate Wakristo katika nyumba zao kwa kinguvu na kuwapeleka Yerusalemu mbele ya Sanhedrini. Lakini, alishindwa, kwa sababu kwa kufanya hivyo alikuwa anagombana na Yesu, aliye Kichwa cha kutaniko la Kikristo. (Efe. 5:23) Alipokuwa njiani kuenda Damasko, Yesu alimutokea kimuujiza, na mwangaza mukubwa ulimufanya kipofu. Ndipo Yesu akamuambia Sauli aende Damasko ili apewe maagizo zaidi. Tunajua mambo yaliyotokea baadaye.—Mdo. 9:3-22.
6, 7. Ni nini inayoonyesha kwamba Paulo alitambua makosa yake ya zamani?
6 Paulo alipokuwa Mukristo, mawazo yake yalibadilika. Kuliko kuendelea kuwa adui mukali wa wanafunzi wa Yesu, alianza kuhubiri kwa bidii kuhusu Kristo. Na aliandika hivi baadaye juu ya maisha yake ya zamani: ‘Bila shaka, ninyi mulisikia juu ya mwenendo wangu hapo zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba kufikia hatua ya kuzidi muno niliendelea kulitesa kutaniko la Mungu na kuliangamiza.’ (Gal. 1:13) Tena, alizungumuzia maisha yake ya zamani yenye kuhuzunisha alipowaandikia Wakorintho, Wafilipi na Timoteo. (Soma 1 Wakorintho 15:9; Flp. 3:6; 1 Tim. 1:13) Hata kama mutume Paulo hakufurahia kuandika mambo hayo kuhusu maisha yake ya zamani, lakini hakufanya kama kwamba hayakutokea. Alitambua kabisa kwamba alifanya makosa makubwa.—Mdo. 26:9-11.
7 Mutu mumoja mwenye elimu ya Biblia, anayeitwa Frederic Farrar aliandika kwamba, tunapofikiria namna mutume Paulo alivyowatesa sana Wakristo, tunaweza kuelewa uchungu wake na kuelewa namna gani maadui wake walikuwa wakimuzihaki. Inawezekana wakati fulani alipotembelea makutaniko, ndugu waliomuona kwa mara ya kwanza walikuwa wanasema, ‘Si ni wewe Paulo aliyekuwa akitutesa?’—Mdo. 9:21.
8. Mutume Paulo aliona namna gani rehema na upendo ambao Yehova na Yesu walimuonyesha, na mufano wake unatufundisha nini?
8 Hata hivyo, Paulo alitambua kama ikiwa alitimiza huduma yake ni kwa sababu tu ya fazili zisizostahiliwa za Mungu. Mutume Paulo alitaja rehema za Mungu mara 90 katika barua 14 alizoandika na hakuna muandikaji mwengine wa Biblia aliyetaja rehema za Mungu mara nyingi hivyo. (Soma 1 Wakorintho 15:10.) Mutume Paulo aliona rehema ambayo Mungu alimuonyesha kuwa ya bei sana, na alitaka kufanya yake yote ili ionekane kama fazili zisizostahiliwa ambazo alionyeshwa hazikuwa za bure. Kwa hiyo, ‘alifanya kazi kuwapita’ mitume wengine wote. Mufano wake unatufundisha waziwazi kama ikiwa tunatubu zambi zetu na kubadili mwenendo wetu, Yehova, kupitia zabihu ya ukombozi ambayo Yesu alitoa, iko tayari kufuta hata zambi nzito ambazo tumefanya. Mufano wa mutume Paulo, ni fundisho kabisa kwa yeyote anayefikiri kwamba ni vigumu kwake kuamini kwamba anaweza kufaidika kabisa na zabihu ya ukombozi ambayo Yesu alitoa. (Soma 1 Timotheo 1:15, 16.) Hata kama Paulo alimutesa Kristo, yeye aliandika hivi: “Mwana wa Mungu . . . alinipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.” (Gal. 2:20; Mdo. 9:5) Paulo alijifunza namna ya kumutumikia Mungu bila kujiongezea masikitiko zaidi. Je, mufano wake umekufundisha jambo fulani?
Mutume Paulo alijifunza kumutumikia Yehova bila kusikitika
JE, KUNA JAMBO LINALOKUSIKITISHA?
9, 10. (a) Sababu gani Wakristo fulani wanaendelea kuwa na masikitiko? (b) Kwa nini si vizuri kuendelea kusumbua akili yako kwa sababu ya makosa ya zamani?
9 Je, kuna mambo uliyofanya zamani yanayokusikitisha leo? Je, wewe unafikiri kwamba ulipoteza nguvu zako na wakati wako katika mambo yasiyo ya maana? Je, ulifanya jambo fulani ambalo liliwatesa wengine? Ao, labda una mawazo yanayokusumbua kwa sababu unasikitikia jambo fulani? Ikiwa jibu ni ndiyo, unaweza kufanya nini?
10 Watu wengi ni wenye kuishi katika wasiwasi ao katika kusumbua akili zao! Kuishi katika wasiwasi, kunamaanisha kujitesa, kujikasirikia, na kujiazibu. Jambo hilo linafanya mutu aendelee kusumbuliwa sana. Je, kufanya hivyo kunatengeneza mambo? Hapana! Wazia unaketi katika kiti (ao ubao) chenye kuninginia kwenye kamba na kinachoyumba-yumba mbele na nyuma, hata ikiwa unatumia nguvu na wakati mwingi, kiti hicho hakitakupeleka mahali popote! Kuliko kuendelea kujisumbua juu ya makosa ya zamani, fanya mambo yanayoweza kukusaidia kusonga mbele. Unaweza kumuomba musamaha mutu uliyemukosea na kujaribu kurudisha uhusiano muzuri pamoja naye. Unaweza kuepuka jambo lililokuingiza katika kosa fulani, hilo litakusaidia usilirudilie tena. Wakati mwengine hauna jambo lingine la kufanya isipokuwa tu kuvumilia matokeo ya makosa yako. Lakini mutu kujisumbua kwa sababu ya makosa yake ya zamani hakuweze kumuletea faida yoyote, kunaweza hata kumuponda zaidi na kuacha ashindwe kumutumikia Mungu kwa moyo wote.
11. (a) Tunapaswa kufanya nini ili Yehova atuonyeshe rehema na fazili zake zenye upendo? (b) Mungu anatuomba tufanye nini ili akili yetu iwe na amani?
11 Watu fulani wanalemewa na makosa yao ya zamani na hata kufikia kufikiri kama wao ni bure machoni pa Mungu. Wanaweza kufikiri kwamba Mungu haweze kuwasamehe kwa sababu walienda mbali sana ao walirudilia-rudilia makosa yao. Lakini, ukweli ni huu: iwe umefanya makosa ya aina gani wakati wa zamani, unaweza kutubu, kubadilika, na kuomba Mungu musamaha. (Mdo. 3:19) Yehova atakuonyesha rehema na fazili zake zenye upendo, kama vile alivyowaonyesha wengine. Yehova iko tayari kusamehe kabisa mutu aliye munyenyekevu, asiye mudanganyifu na anayetubu kwelikweli. Mungu alimufanyia Ayubu hivyo, naye alisema hivi: “Nami ninatubu [ninasikitika] katika mavumbi ya majivu.” (Ayu. 42:6) Ili akili yetu iwe na amani, sisi wote tunapaswa kufuata shauri hili la Biblia: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” (Met. 28:13; Yak. 5:14-16) Kwa hiyo, tunaweza kuungama makosa yetu kwa Mungu, kumuomba musamaha, na kufanya yote ili kutokurudilia tena mambo hayo. (2 Kor. 7:10, 11) Ikiwa tunafanya hivyo, basi, tutafaidika na rehema ya Yule ‘anayesamehe kwa njia kubwa.’—Isa. 55:7.
12. (a) Namna gani tunaweza kuiga mufano wa Daudi tunaposumbuliwa na zamiri yetu? (b) Ni katika maana gani Yehova alijuta ao alisikitika, na namna gani kujua hilo kunatutia moyo? (Soma kisanduku.)
12 Mungu anaweza kutusaidia kupitia sala; sala ina nguvu. Katika sala ambayo Daudi alitoa kwa imani, yeye alionyesha jinsi alivyokuwa anajisikia kisha kufanya zambi, na sala hiyo imelindwa vizuri katika Zaburi. (Soma Zaburi 32:1-5.) Daudi alijionea kwamba kujaribu kuzuia zamiri yenye kusumbuliwa kulimuchokesha. Inaelekea kwamba alikosa amani ya moyoni, ya akili, akawa na afya mbaya na alipoteza furaha yake kwa sababu alikuwa bado hajatubu. Lakini, ni nini ilimufanya Daudi asamehewe na apate kitulizo? Alitubu kwa Mungu. Yehova alisikia sala za Daudi na akamupa nguvu ya kusonga mbele na maisha yake na kutimiza mambo mazuri. Vilevile, ikiwa unaomba musamaha kweli kutoka moyoni, uwe hakika kwamba Yehova atasikia sala yako. Ikiwa unaendelea kusumbuliwa na makosa yako ya zamani, fanya yote unayoweza ili usiyarudilie tena; na kisha amini kabisa kwamba Yehova amekusamehe.—Zab. 86:5.
SAHAU YA ZAMANI, TAZAMA MBELE
13, 14. (a) Sasa tunapaswa kukaza uangalifu wetu juu ya mambo gani? (b) Ni maulizo gani yanayoweza kutuchochea ili tuchunguze hali yetu leo?
13 Kwa kweli, wakati uliopita na mambo yaliyopita hatuweze kuyabadilisha, lakini yanatufundisha; ni maisha yetu ya wakati ujao tu ndio tunaweza kufanyia kazi. Kwa hiyo, tunapaswa kukaza uangalifu wetu juu ya mambo ya sasa na yale yaliyo mbele. Ujiulize maulizo haya: Ni mambo gani ninayofanya sasa ambayo katika miaka ijayo ningepeda nifanye tofauti, ao ni mambo gani sifanye ambayo ningependa kufanya? Je, ninaendelea kuwa na mwenendo wa uaminifu ambao utanisaidia nisiweze kusikitika siku zinazokuja?
14 Kwa kuwa ziki kubwa inakaribia sana, haitakuwa vizuri siku za usoni tusikitike na kusumbuliwa na mawazo kama haya: ‘Kama tu ningefanya mengi zaidi katika kazi ya Mungu! Kwa nini sikufanya kazi ya upainia na nilikuwa na wakati? Ni nini kilichonizuia kuwa mutumishi wa huduma? Kwa nini sikujikaza kuvaa utu mupya? Mimi ninafanya kabisa yale Yehova anataka ili nistahili kuingia katika dunia mupya?’ Tusitumie maulizo hayo ili kujilaumu, tuyatumie ili kujichunguza na kuhakikisha kama tunamutumikia Yehova kwa nguvu zetu zote. Ikiwa sivyo, tutaendelea kufanya mambo ambayo yatatusikitisha hata zaidi.—2 Tim. 2:15.
USISIKITIKE JUU YA MAMBO ULIYOFANYA KATIKA KAZI YA MUNGU
15, 16. (a) Ndugu na dada wengi wamejinyima namna gani ili kutia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza katika maisha yao? (b) Sababu gani hatupaswe kusikitikia uamuzi wowote wa kujinyima tuliofanya ili kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza?
15 Tuseme nini juu ya ndugu na dada waliojinyima ili kumutumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote? Labda uliacha kazi nzuri ao biashara yenye kuendelea ili urahisishe maisha yako na kuwa na wakati mwingi wa kumutumikia Yehova. Ao labda uliamua kutooa ao kutoolewa ao kutozaa watoto ili kufanya utumishi wa pekee, kama vile kuwa Mwanabeteli, kushiriki katika kazi ya ujenzi, kuwa mwangalizi wa muzunguko, ao misionere. Je, unapaswa kusikitikia uamuzi uliofanya kwa sababu sasa unazeekea katika kazi ya Yehova? Je, unapaswa kuanza kufikiri kwamba umekosea kwa kujinyima hivyo ao ulichukua uamuzi huo mbele ya wakati? Hapana!
16 Ulifanya uamuzi huo kwa sababu umemupenda Yehova na umekuwa na tamaa ya kuwasaidia wengine waweze kumutumikia. Usifikiri kwamba maisha yako yangekuwa mazuri zaidi ikiwa haungefanya uamuzi huo. Kujua kwamba uamuzi uliochukua ni jambo lililo sawa maishani mwako kunaweza kukusaidia usisikitike bali uwe mwenye furaha kabisa. Unapaswa kufurahi kwa sababu umefanya yote unayoweza ili kumutumikia Yehova. Yehova hatasahau namna ulivyojinyima. Katika uzima ulio wa kweli ulio mbele yetu, Yehova atakubariki sana kuliko namna unavyowazia sasa!—Zab. 145:16; 1 Tim. 6:19.
KUMUTUMIKIA MUNGU BILA KUSIKITIKA
17, 18. (a) Ni kanuni gani iliyomusaidia mutume Paulo ili amutumikie Yehova bila kusikitika? (b) Unaazimia nini kuhusu mambo ya zamani, ya sasa na ya wakati ujao katika utumishi wako kwa Yehova?
17 Ni kanuni gani ilimusaidia mutume Paulo amutumikie Mungu bila kusikitikia mambo ya zamani? Aliandika hivi: ‘Nayasahau mambo ya nyuma na kujinyoosha kuenda mbele kuelekea mambo yaliyo mbele.’ (Soma Wafilipi 3:13, 14.) Mutume Paulo hakuendelea kufikiria tena na tena mwenendo wake mubaya katika dini ya Kiyahudi. Badala yake, alitumia nguvu zake zote ili astahili kupata zawadi ya uzima wa milele.
18 Sisi wote tunaweza kupata somo kupitia maneno hayo ya mutume Paulo. Tunajifunza kwamba, kuliko kuendelea kujisumbua-sumbua juu ya mambo ya zamani ambayo hatuweze tena kubadilisha, tukazie fikira yetu juu ya mambo yaliyo mbele. Ni kweli, haiwezekane tusahau kabisakabisa makosa yetu ya zamani, lakini tusiendelee kuyafikiria tena na tena na kujilaumu. Tunapaswa kujikaza kutupa mambo ya zamani nyuma yetu, tumutumikie Mungu wetu kwa uwezo wetu wote, na tuangalie mbele kwenye wakati ujao wenye baraka nyingi.
^ Biblia inataja mara nyingi wanawake kati ya watu ambao Sauli alitesa. Hilo linaonyesha kama wanawake walifanya mengi katika kazi ya kuhubiri, kama wanavyoendelea kufanya leo.—Zab. 68:11.