HABARI YA KUJIFUNZA YA 48
Uendelee Kumutumainia Yehova Wakati wa Magumu
“‘Mukuwe na nguvu, . . . kwa maana niko pamoja na ninyi,’ ni vile Yehova wa majeshi anasema.”—HAG. 2:4.
WIMBO 118 “Unipatie Imani Zaidi”
KIFUPI YA HABARI a
1-2. (a) Namna gani hali yetu inafanana na ya Wayahudi wenye walirudia Yerusalemu? (b) Zungumuzia kwa kifupi magumu yenye Wayahudi walipambana nayo. (Ona kisanduku “ Siku za Hagai, Zekaria, na Ezra.”)
WAKATI fulani unakuwaka na wasiwasi juu ya maisha ya kesho? Pengine umepoteza kazi na uko najiuliza utatimiza namna gani mahitaji ya familia yako. Pengine uko na wasiwasi juu ya usalama wa familia yako kwa sababu ya muvurugo mu mambo ya politike, kwa sababu ya mateso juu ya imani yetu ao kwa sababu kazi yetu ya kuhubiri inapingwa. Uko napambana na matatizo ya vile? Kama ni vile, kuchunguza habari kuhusu namna Yehova alisaidia Waisraeli zamani wakati walipambana na magumu ya vile, kunaweza kukusaidia.
2 Iliomba imani ili Wayahudi wenye walikuwa wameishi Babiloni maisha yao yote waache maisha ya muzuri yenye walikuwa nayo, na kusafiri kuenda mu inchi yenye wengi kati yao hawakujua. Wakati walifika, bila kukawia walianza kupambana na matatizo ya kupata makuta, muvurugo mu mambo ya politike, na upinzani. Kwa hiyo, ilikuwa nguvu kwa wamoja kati yao kukazia akili kazi ya kujenga upya hekalu ya Yehova. Njo maana, mu mwaka wa 520 hivi M.K.Y., Yehova alituma manabii wawili, ni kusema Hagai na Zekaria, ili wachochee tena bidii ya watu. (Hag. 1:1; Zek. 1:1) Sawa vile tutaona, mambo yenye kutia moyo yenye wale manabii walisema, ilisaidia sana. Lakini karibu miaka 50 kisha, wale Wayahudi wenye walitoka Babiloni walikuwa wamevunjika tena moyo. Ile wakati Ezra, mwandishi wa sheria mwenye ufundi, alikuya Yerusalemu kutoka Babiloni ili kutia moyo watu wa Mungu juu watie ibada ya kweli pa nafasi ya kwanza.—Ezr. 7:1, 6.
3. Tutazungumuzia maulizo gani? (Mezali 22:19)
3 Vile tu unabii wa Hagai na unabii wa Zekaria ulisaidia watu wa Mungu zamani waendelee kumutumainia Yehova wakati wa upinzani, unaweza kutusaidia leo pia tuendelee kuwa hakika kama Yehova atatutegemeza wakati tunapambana na magumu ya maisha. (Soma Mezali 22:19.) Wakati tutakuwa nachunguza ujumbe wenye Mungu alipatia nabii Hagai na nabii Zekaria na pia mufano wa Ezra, tutajibia hii maulizo: Magumu yenye Wayahudi wenye walirudia kutoka Babiloni walipambana nayo, ilikuwa na matokeo gani juu yao? Juu ya nini kufanya mapenzi ya Mungu njo tunapaswa kutia pa nafasi ya kwanza wakati tunapambana na magumu? Na namna gani tunaweza kumutumainia Yehova zaidi wakati wa magumu?
MAGUMU ILIKUWA NA MATOKEO GANI JUU YA WAYAHUDI WENYE WALITOKA BABILONI?
4-5. Pengine ni nini njo ilifanya bidii ya Wayahudi ya kujenga hekalu ipunguke?
4 Wakati Wayahudi wenye walitoka Babiloni walifika Yerusalemu, walikuwa na kazi mingi ya kufanya. Bila kukawia walijenga tena mazabahu ya Yehova na kujenga musingi wa hekalu. (Ezr. 3:1-3, 10) Lakini kisha wakati kidogo, bidii yao ilipoa. Juu ya nini? Juu zaidi ya kujenga hekalu, walipaswa pia kujenga nyumba zao, kulima mashamba, na kutimiza mahitaji ya familia zao. (Ezr. 2:68, 70) Zaidi ya ile, walipambana na upinzani wa maadui wao wenye walikuwa nafanya mipango ili kusimamisha kazi ya kujenga upya hekalu.—Ezr. 4:1-5.
5 Wale Wayahudi walipambana pia na matatizo ya kupata feza na hali ya mubaya mu mambo ya politike. Inchi yao ilikuwa sasa sehemu ya Utawala wa Uajemi. Kisha Mufalme Koreshi kufa mu mwaka wa 530 M.K.Y., Cambyses, mwenye alitawala kisha yeye, alianzisha kampanye ya kijeshi ili Misri ikuwe sehemu ya utawala wake. Wakati maaskari wake walikuwa naenda Misri, inawezekana walilazimisha Wayahudi wawapatie chakula, maji, na makao. Na ile iliongezea Wayahudi magumu. Miaka ya kwanza-kwanza ya utawala wa Dario wa Kwanza, mwenye alitawala kisha Cambyses, ilijaa uasi na mivurugo mu mambo ya politike. Bila shaka ile hali ilifanya Wayahudi wenye walirudia kutoka Babiloni wajiulize namna gani watashugulikia mahitaji ya familia zao. Kwa sababu ya magumu yote yenye walipambana nayo, Wayahudi fulani waliona kama haikukuwa wakati wenye kufaa wa kujenga upya hekalu ya Yehova.—Hag. 1:2.
6. Kulingana na Zekaria 4:6, 7, Ni magumu gani ingine yenye Wayahudi walipambana nayo, na Zekaria aliwahakikishia nini?
6 Soma Zekaria 4:6, 7. Zaidi ya matatizo ya kupata makuta na mivurugo mu mambo ya politike, Wayahudi walipaswa pia kupambana na upinzani. Mu 522 M.K.Y., maadui wao waliweza kuchochea serikali ya Waajemi ikataze kazi ya kujenga upya hekalu ya Yehova. Lakini nabii Zekaria alihakikishia Wayahudi kama Yehova atatumia roho yake yenye nguvu ili kuondoa vizuizi vyote. Mu 520 M.K.Y., Mufalme Dario aliruhusu kazi ya kujenga hekalu ianze tena na hata alitolea Wayahudi muchango, na pia aliomba wakubwa wawategemeze.—Ezr. 6:1, 6-10.
7. Wakati Wayahudi wenye walirudia Yerusalemu walitia mapenzi ya Mungu pa nafasi ya kwanza, walipata baraka gani?
7 Kupitia Hagai na Zekaria, Yehova aliahidi watu wake kama atawategemeza ikiwa wanatia kazi ya kujenga tena hekalu pa nafasi ya kwanza. (Hag. 1:8, 13, 14; Zek. 1:3, 16) Kisha kutiwa moya na nabii Hagai na nabii Zekaria, Wayahudi wenye walitoka Babiloni walianza tena kazi ya kujenga hekalu mu mwaka wa 520 M.K.Y., na wakamaliza kuijenga mbele miaka tano ienee. Juu Wayahudi walitanguliza mapenzi ya Yehova hata kama walikuwa na magumu, Yehova aliwategemeza, hapana tu kimwili lakini kiroho pia. Na ile ilifanya waabudu Yehova kwa furaha.—Ezr. 6:14-16, 22.
KAZIA AKILI MAPENZI YA YEHOVA
8. Namna gani maneno yenye kupatikana mu Hagai 2:4 inaweza kutusaidia kukazia akili mapenzi ya Mungu? (Ona pia maelezo ya chini.)
8 Kadiri taabu kubwa inakaribia, tunaona kama ni jambo ya maana kutii amri ya kuhubiri habari njema. (Mk. 13:10) Lakini inaweza kuwa nguvu kwetu kukazia akili kazi yetu ya kuhubiri kama tuko napambana na matatizo ya kupata makuta ao kama kazi yetu ya kuhubiri habari njema iko napingwa. Nini inaweza kutusaidia kutia mapenzi ya Yehova pa nafasi ya kwanza? Kukuwa hakika kama “Yehova wa majeshi” b iko upande wetu. Atatutegemeza kama tunaendelea kutanguliza mapenzi yake kuliko mambo yetu wenyewe. Kwa hiyo, hatuna sababu ya kuogopa.—Soma Hagai 2:4.
9-10. Namna gani bibi na bwana fulani walijionea kama maneno ya Yesu yenye kuwa mu Matayo 6:33 ni ya kweli?
9 Fikiria mufano wa Oleg na Irina, c bibi na bwana wenye kuwa mapainia. Kisha kuhamia mu eneo ingine juu ya kutegemeza kutaniko fulani, walipoteza kazi yao juu mu inchi mulikuwa matatizo ya feza. Hata kama hawakukuwa na kazi ya muzuri kwa karibu mwaka moya, kila mara waliona kama Yehova alikuwa anawategemeza kwa upendo. Na wakati fulani-fulani ndugu na dada zao waliwatolea musaada. Namna gani walipambana na ile magumu? Oleg mwenye ku mwanzo alijisikia sawa vile anashuka moyo, anasema hivi: “Kuendelea kuhubiri kwa bidii kulitusaidia tuendelee kukaza akili juu ya jambo ya maana zaidi mu maisha.” Yeye na bibi yake waliendelea kutafuta kazi, na wakati uleule waliendelea kuhubiri kwa bidii.
10 Siku moya, wakati walirudia ku nyumba kisha mahubiri, walipata habari kama rafiki yao fulani alisafiri karibu kilometre 160 juu awaletee mizigo mbili ya chakula. Oleg anasema hivi: “Ile siku, tulijionea tena namna Yehova anatuhangaikia sana na namna kutaniko pia inatuhangaikia. Tuko hakika kama Yehova hasahau watumishi wake hata hali yao ikuwe nguvu namna gani.”—Mt. 6:33.
11. Tunaweza kutazamia nini ikiwa tunatia mapenzi ya Yehova pa nafasi ya kwanza?
11 Yehova anapenda tukazie akili kazi yenye kuokoa uzima ya kufanya wanafunzi. Sawa vile tuliona mu fungu ya saba, Hagai alitia moyo watu wa Yehova waanze tena kazi yao ya kujenga hekalu, ikuwe sawa vile njo wanaanza sasa kujenga musingi ya hekalu. Kama wangefanya vile, Yehova aliahidi kama ‘atatuma baraka.’ (Hag. 2:18, 19) Siye pia tunaweza kuwa hakika kama Yehova atabariki bidii yetu kama tunajikaza kutia pa nafasi ya kwanza kazi yenye alitupatia tufanye.
NAMNA YA KUMUTUMAINIA ZAIDI YEHOVA
12. Juu ya nini Ezra na Wayahudi wenzake walikuwa na lazima ya imani ya nguvu?
12 Mu 468 M.K.Y., Ezra alisafiri pamoja na kikundi cha pili cha Wayahudi kutoka Babiloni kuenda Yerusalemu. Ili waweze kufanya ile safari, iliomba Ezra na Wayahudi wenzake wakuwe na imani ya nguvu. Wangesafiri mu barabara zenye kuwa hatari wakiwa wamebeba hesabu kubwa ya zahabu na feza yenye ilitolewa kwa ajili ya hekalu. Ile ingefanya wakuwe mu hatari ya kushambuliwa na wanyanganyi. (Ezr. 7:12-16; 8:31) Zaidi ya ile, bila kukawia walitambua kama hata muji wa Yerusalemu haukukuwa salama. Watu hawakukuwa wengi mu muji na kuta na milango mikubwa ya muji ilipaswa kutengenezwa. Mufano wa Ezra unaweza kutufundisha nini kuhusu kumutumainia zaidi Yehova?
13. Ni nini njo ilifanya Ezra amutumainie Yehova zaidi? (Ona pia maelezo ya chini.)
13 Ezra alikuwa amejionea namna Yehova alitegemeza watu wake wakati wa magumu. Miaka fulani mbele ya pale, mu 484 M.K.Y., inawezekana Ezra alikuwa anaishi Babiloni wakati Mufalme Ahasuero alitoa sheria ya kuua Wayahudi mu utawala wote wa Uajemi. (Est. 3:7, 13-15) Maisha ya Ezra ilikuwa mu hatari. Wayahudi walitenda namna gani? “Katika kila jimbo” walifunga na kuomboleza, bila shaka ili kusali kwa Yehova na kumuomba muongozo. (Est. 4:3) Wazia namna Ezra na Wayahudi wenzake walijisikia wakati mambo iligeukia wale wenye walipenda kuharibu Wayahudi! (Est. 9:1, 2) Inawezekana mambo yenye ilimupata Ezra ile wakati ya magumu ilimutayarisha kwa ajili ya magumu ya wakati wenye kuja, na inawezekana kabisa ile ilifanya atumainie zaidi uwezo wa Yehova wa kulinda watu wake. d
14. Dada fulani alijifunza somo gani kisha kuona namna Yehova alimuhangaikia wakati wa magumu?
14 Wakati Yehova anatuhangaikia wakati wa magumu, ile inafanya tumutumainie zaidi. Fikiria mufano wa Anastasia, mwenye anaishi mu Ulaya ya Mashariki. Aliacha kazi yake juu asiunge mukono upande wowote katika mambo ya politike. Anasema hivi: “Ilikuwa mara ya kwanza ninajikuta mu hali yenye ninakosa makuta. Niliacha mambo yote mu mikono ya Yehova na niliona namna alinihangaikia kwa upendo. Kama ninapoteza tena kazi, sitaogopa. Kama Baba yangu wa mbinguni ananihangaikia leo, atanihangaikia pia kesho.”
15. Ni nini ilimusaidia Ezra aendelee kumutumainia Yehova? (Ezra 7:27, 28)
15 Ezra alijionea mukono wa Yehova mu maisha yake. Wakati Ezra alifikiria vile Yehova alimusaidia zamani, bila shaka ile ilimusaidia aendelee kumutumainia Yehova. Ezra aliandika hivi: “Mukono wa Yehova Mungu wangu ulikuwa juu yangu.” (Soma Ezra 7:27, 28.) Ezra alitumia maneno ya kufanana na ile mara sita mu kitabu ya Biblia yenye kuwa na jina yake.—Ezr. 7:6, 9; 8:18, 22, 31.
Ni mu hali gani mbalimbali tunaweza kuona waziwazi mukono wa Yehova mu maisha yetu? (Ona fungu ya 16) e
16. Tunaweza kuona waziwazi mukono wa Yehova mu hali gani mbalimbali? (Ona pia picha.)
16 Yehova anaweza kutusaidia wakati tunakutana na hali ya nguvu. Kwa mufano, tunaweza kuona mukono wa Yehova mu maisha yetu wakati tunaomba mukubwa wetu wa kazi atupatie masiku fulani juu tuweze kuenda ku mukusanyiko, ao wakati tunamuomba abadilishe programu yetu ya kazi juu tuweze kuhuzuria mikutano yote. Tunaweza kushangaa kuona namna mambo itatendeka mu njia yenye hatukuwazia. Na ile itafanya tumutumainie Yehova zaidi na zaidi.
Ezra iko nalia na kusali wakati iko ku hekalu juu anahuzunishwa na zambi za watu. Watu pia wako nalia. Kisha Shekania anamufariji Ezra kwa kumuambia hivi: “Kungali tumaini kwa ajili ya Israel. . . . Sisi tuko pamoja na wewe.”—Ezr. 10:2, 4 (Ona fungu ya 17)
17. Namna gani Ezra alionyesha unyenyekevu wakati wa magumu? (Ona picha ku jalada.)
17 Kwa unyenyekevu Ezra alitafuta musaada wa Yehova. Kila wakati wenye Ezra alikuwa na mahangaiko juu ya mugao wake, alisali kwa Yehova kwa unyenyekevu. (Ezr. 8:21-23; 9:3-5) Juu Ezra alimutegemea Yehova, ile ilichochea wale wenye walimuzunguka wamutegemeze na waige imani yake. (Ezr. 10:1-4) Wakati tuko na mahangaiko juu ya mahitaji yetu ya kimwili ao juu ya usalama wa familia yetu, tunapaswa kutafuta musaada wa Yehova katika sala na kuwa hakika kama atatusaidia.
18. Nini njo inaweza kutusaidia tumutumainie Yehova zaidi?
18 Kama tunatafuta kwa unyenyekevu musaada wa Yehova na tunakubali musaada wa waamini wenzetu, ile itafanya tumutumainie Yehova zaidi. Erika, mama mwenye kuwa na watoto tatu, aliendelea kumutumainia Yehova wakati alikutana na magumu ya nguvu. Mu kipindi kidogo tu ya wakati, mutoto wake mwenye alikuwa hayazaliwa alikufia mu tumbo na bwana yake mupendwa alikufa. Wakati anakumbuka ile mambo anasema hivi: “Hauwezi kujua mbele ya wakati namna Yehova atakusaidia. Musaada unaweza kuya mu njia yenye haukutazamia. Nimetambua kama sala zangu za mingi zilijibiwa kupitia maneno na matendo ya marafiki wangu. Wakati ninafungulia marafiki wangu moyo, inakuwa mwepesi zaidi kwao kunisaidia.”
ENDELEA KUMUTUMAINIA YEHOVA MUPAKA MWISHO
19-20. Mufano wa Wayahudi wenye hawakuweza kurudia Yerusalemu unatufundisha nini?
19 Tunaweza pia kujifunza somo ya maana kutoka kwa Wayahudi wenye hawakuweza kurudia Yerusalemu. Wamoja kati yao hawakuweza kurudia juu walikuwa wamezeeka sana, wengine juu walikuwa na magonjwa ya nguvu, na wengine juu ya hali ya familia yao. Hata vile walikuwa tayari kutegemeza wale wenye walirudia Yerusalemu kwa kuwapatia michango kwa ajili ya hekalu. (Ezr. 1:5, 6) Inaonekana kama miaka 19 kisha kikundi cha kwanza cha Wayahudi kurudia Yerusalemu, wale wenye walibakia Babiloni walikuwa wangali naendelea kutuma Yerusalemu michango yao ya kujipendea.—Zek. 6:10.
20 Hata kama hali yetu haituruhusu kufanya mengi mu kazi ya Yehova vile tungependa, tunaweza kuwa hakika kama Yehova anafurahia mambo yenye tuko najikaza kufanya ili kumufurahisha. Tunajua vile namna gani? Katika siku za Zekaria, Yehova aliomba nabii wake afanye taji kwa kutumia zahabu na feza zenye Wayahudi wenye walibakia Babiloni walituma. (Zek. 6:11) Ile “taji kubwa” ingekuwa “kikumbusho” juu ya michango yao ya kujipendea. (Zek. 6:14, maelezo ya chini) Tunaweza kuwa hakika kama Yehova hatasahau hata kidogo namna tunajikaza kumutumikia kwa moyo wote wakati wa magumu.—Ebr. 6:10.
21. Ni nini itatusaidia tuendelee kumutumainia Yehova hata kutokee nini wakati weye kuya?
21 Bila shaka mu hizi siku za mwisho tutaendelea kupambana na magumu na hata mambo inaweza kuendelea kuharibika zaidi mu wakati wenye kuya. (2 Ti. 3:1, 13) Lakini hatuna lazima ya kuhangaika sana. Kumbuka maneno yenye Yehova aliambia watu wake mu wakati wa Hagai, aliwaambia hivi: “Niko pamoja na ninyi . . . Musiogope.” (Hag. 2:4, 5) Siye pia tunaweza kuwa hakika kama Yehova ataendelea kuwa pamoja na siye kama tunajikaza kuendelea kufanya mapenzi yake. Kama tunatumikisha mambo yenye tunajifunza mu unabii wa Hagai, wa Zekaria, na mufano wa Ezra, tutaendelea kumutumainia Yehova hata tujikute mu magumu ya namna gani mu wakati wenye kuya.
WIMBO 122 Tukuwe na Nguvu na Tusitikisike!
a Hii habari ilitayarishwa ili kutusaidia tumutumainie Yehova zaidi wakati tuko napambana na matatizo ya kupata makuta, wakati wa muvurugo mu mambo ya politike, na wakati kazi yetu ya kuhubiri inapingwa.
b Maneno “Yehova wa majeshi” inapatikana mara 14 mu kitabu ya Hagai. Ile ilikumbusha Wayahudi na inatukumbusha siye pia kama Yehova iko na nguvu zenye hazima mipaka na kama anaongoza jeshi kubwa ya viumbe wa kiroho.—Zb. 103:20, 21.
c Majina fulani imebadilishwa.
d Ezra alikuwa mwandishi mwenye ufundi wa Sheria ya Mungu. Kwa hiyo, alifikia kuwa na imani ya nguvu mu maunabii yenye Yehova alitoa, hata mbele asafiri kuenda Yerusalemu.—2 Ny. 36:22, 23; Ezr. 7:6, 9, 10; Yer. 29:14.
e MAELEZO YA PICHA : Ndugu fulani anaomba mukubwa wake wa kazi amupatie siku fulani juu ahuzurie mukusanyiko, lakini mukubwa wake wa kazi anakatala. Ule ndugu anaomba Yehova amusaidie na amuongoze wakati iko najitayarisha juu aende tena kuzungumuza na mukubwa wake wa kazi. Anaonyesha mukubwa wake wa kazi mwaliko wa mukusanyiko na anamufasiria faida ya mafundisho ya Biblia. Ile inagusa moyo wa mukubwa wake wa kazi na anabadilisha uamuzi wake.