Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA | WAKATI MUTU MWENYE UNAPENDA ANAKUFA

Namna ya Kupiganisha Huzuni Yako

Namna ya Kupiganisha Huzuni Yako

Kuko mashauri mengi sana juu ya namna ya kupiganisha huzuni. Lakini, yote hayawezi kusaidia. Kwa mufano, pengine watu fulani watakushauria usilie ao usionyeshe kwa njia yoyote namna unajisikia. Wengine wanaweza kukuchochea ulie na kuonyesha kabisa namna unajisikia. Biblia inaonyesha mawazo yenye usawaziko ao yenye kuwa katikati; uchunguzi wa leo unaitika mawazo hayo.

Katika desturi fulani, watu wanaona kuwa mwanaume hapaswe kulia. Lakini, kuko sababu kabisa ya kusikia haya ya kulia, hata mbele ya watu? Wanganga wa magonjwa ya akili wanatambua kama kulia ni sehemu ya kawaida ya kuonyesha huzuni. Na kisha wakati fulani, kuonyesha huzuni kunaweza kukusaidia uendelee na maisha hata kama unajisikia mubaya sana. Lakini kuzuia huzuni kunaweza kuwa na matokeo ya mubaya kuliko kuwa na matokeo ya muzuri. Biblia haiunge mukono wazo la kwamba ni mubaya kulia ao kwamba mwanaume hapaswe kulia. Kwa mufano, fikiria Yesu. Hata kama alikuwa na uwezo wa kufufua wafu, alilia mbele ya watu wakati Lazaro, rafiki yake mupendwa alikufa!—Yohana 11:33-35.

Mara nyingi kusikia hasira ni sehemu ya huzuni, zaidi sana kama ni kifo cha kushitukia. Kuko sababu nyingi zenye zinaweza kufanya mutu mwenye alifiwa asikie hasira, kwa mufano wakati mutu mwenye kuheshimika anamuambia bila kufikiri mambo fulani yenye hayana musingi. Mwanaume mumoja wa Afrika Kusini mwenye kuitwa Mike anasema hivi: “Nilikuwa tu na miaka 14 wakati baba yangu alikufa. Kwenye maziko, muhubiri mumoja wa kanisa la Anglikani alisema kama Mungu ana lazima ya watu wazuri na anawachukua mbele ya wakati. * Jambo hilo liliniletea hasira kwa sababu tulikuwa na lazima sana ya baba yetu. Sasa, kisha miaka 63, jambo hilo linaendelea kuniumiza moyoni.”

Na tuseme nini wakati mutu fulani anajisikia kuwa ni kosa lake? Zaidi sana kama ni kifo cha kushitukia, mutu mwenye alifiwa anaweza kuwaza tena na tena, ‘Kifo hakingetokea kama tu nilifanya hiki ao kile.’ Ao pengine mulikosana na marehemu wakati ulikutana naye mara ya mwisho. Tena, hilo linaweza kufanya ujisikie sana kuwa ni kosa lako.

Ikiwa unasumbuliwa na hasira na hali ya kujisikia kuwa ni kosa lako, ni jambo la maana uonyeshe wengine namna unajisikia. Zungumuza na rafiki mwenye atakusikiliza na kukuhakikishia kama ni jambo la kawaida kwa watu wenye walifiwa kujisikia vile. Biblia inatukumbusha hivi: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

Rafiki muzuri zaidi mwenye mutu ambaye alifiwa anaweza kuwa naye ni Muumbaji wetu, Yehova Mungu. Umufungulie moyo wako katika sala kwa sababu ‘yeye anakujali [anakuhangaikia].’ (1 Petro 5:7) Tena, anaahidi kama watu wote wenye wanafanya vile watafarijiwa kupitia “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” (Wafilipi 4:6, 7) Umuache pia Mungu akusaidie kupona kupitia Neno lake lenye kufariji, ni kusema, Biblia. Uandike liste ya maandiko yenye kufariji. (Soma  kisanduku kwenye ukurasa huu.) Unaweza hata kuweka katika akili maandiko fulani kati ya hayo. Kuwaza sana juu ya maandiko hayo kunaweza kukusaidia zaidi sana usiku wakati uko peke yako na haupate usingizi.—Isaya 57:15.

Hivi karibuni, mwanaume wa miaka 40 mwenye tunaweza kuita Jack, alifiwa na bibi yake kwa sababu ya ugonjwa wa kansere. Jack anasema kama wakati fulani anajisikia sana kuwa peke yake. Lakini sala imemusaidia. Anafasiria hivi: “Wakati ninasali kwa Yehova, sijisikie tena kuwa peke yangu. Mara nyingi, ninaamuka usiku na ninashindwa kuenda kulala tena. Kisha kusoma na kuwaza sana juu ya mawazo yenye kufariji ya Maandiko na kufungua moyo wangu katika sala, ninajisikia mwenye kutulia na amani yenye kupita zote inashuka juu yangu, na kufanya akili yangu na moyo wangu vipumuzike na kuniwezesha kulala.”

Kijana mumoja mwanamuke mwenye kuitwa Vanessa alifiwa na mama yake kwa sababu ya ugonjwa. Yeye pia alijionea nguvu ya sala. Anasema hivi: “Katika wakati mugumu zaidi, nilikuwa tu naita jina la Mungu na kuanza kulia. Yehova alisikiliza sala zangu na sikuzote alinipatia nguvu yenye nilikuwa nayo lazima.”

Watu fulani ambao wanashauria watu wenye walifiwa, wanawaambia kama ili kupiganisha huzuni, wajikaze kusaidia wengine ao kutumia wakati wao katika kazi zenye kuletea wengine faida. Kufanya vile kunaleta furaha na kunaweza kupunguza huzuni ya mutu. (Matendo 20:35) Wakristo wengi wenye walifiwa wametambua kama kujikaza kusaidia wengine kumewafariji sana.—2 Wakorintho 1:3, 4.

^ fu. 5 Hilo haliko fundisho la Biblia. Biblia inaonyesha mambo tatu yenye kuleta kifo.—Mhubiri 9:11; Yohana 8:44; Waroma 5:12.