Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tuonyeshe Shukrani kwa Ajili ya Fazili za Mungu Zenye Hatustahili

Tuonyeshe Shukrani kwa Ajili ya Fazili za Mungu Zenye Hatustahili

‘Sisi sote tulipokea . . . fazili zisizostahiliwa juu ya fazili zisizostahiliwa.’YOHANA 1:16.

NYIMBO: 95, 13

1, 2. (a) Eleza mufano wa Yesu wa mutu fulani mwenye alikuwa na shamba la mizabibu. (b) Namna gani mufano huo unaonyesha sifa ya wema na ya fazili zenye hatustahili?

SIKU moja asubui sana, mutu mumoja mwenye alikuwa na shamba la mizabibu alienda kwenye soko kutafuta wanaume wa kutumika katika shamba lake. Aliwaambia kama atawalipa feza fulani, na walikubali kazi hiyo. Lakini, kwa sababu mwenye shamba alikuwa na lazima ya wafanyakazi wengi zaidi, alirudia kwenye soko mara nyingi katika muchana ili kupata wanaume wengi zaidi. Aliwaambia wote kama atawalipa mushahara wenye kufaa. Mangaribi, mwenye shamba alikusanya wafanyakazi ili kuwalipa mushahara wao. Wale wenye walitumika muchana muzima na wale wenye walitumika saa moja tu, aliwalipa wote sawasawa. Lakini, wakati wanaume wenye walitumika muchana wote walianza kunungunika, mwenye shamba aliwaambia hivi: ‘Hamukuitika mushahara wenye tulipatana? Sina haki ya kupatia wafanyakazi wangu wote mushahara wenye ninapenda? Munasikia wivu kwa sababu ninaonyesha wema?’—Mathayo 20:1-15.

2 Mufano wa Yesu unatufundisha jambo la maana sana juu ya ‘fazili zisizostahiliwa’ za Yehova. [1] (Soma maelezo kwenye mwisho wa habari hii.) (Soma 2 Wakorintho 6:1.) Namna gani? Watu fulani wanaweza kufikiri kama wafanyakazi wenye walitumika muchana wote walistahili kupokea feza nyingi kuliko wengine. Lakini mwenye shamba alionyesha wafanyakazi wenye walitumika tu saa fulani fazili zenye hawakustahili. Juu ya neno lenye kutafsiriwa ‘fazili zisizostahiliwa’ katika Biblia, mutu mumoja mwenye elimu alisema hivi: “Wazo la musingi la neno hilo ni zawadi ya bure na yenye mutu hastahili, ao kitu fulani chenye mutu anapewa bila kukitumikia na bila kukistahili.”

ZAWADI KUBWA ZAIDI YA YEHOVA

3, 4. Sababu gani na namna gani Yehova ameonyesha wanadamu wote fazili zenye hawastahili?

3 Biblia inatuambia kama fazili za Mungu zenye hatustahili ni “zawadi ya bure.” (Waefeso 3:7) Kwa sababu hatuwezi kumutii Mungu kabisa-kabisa, hatustahili hata kidogo atuonyeshe wema wake. Kwa kweli, tunastahili kufa. Mufalme Sulemani alisema hivi: ‘Hakuna mwanadamu aliye muadilifu [mukamilifu] duniani ambaye anaendelea kufanya mema na asifanye zambi.’ (Mhubiri 7:20) Kisha, mutume Paulo alisema hivi: ‘Wote wamefanya zambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu,’ na ‘mushahara ambao zambi inalipa ni kifo.’—Waroma 3:23; 6:23a.

4 Kwa sababu Yehova anapenda wanadamu sana, alituma ‘Mwana wake muzaliwa-pekee’ ili akufe kwa ajili yetu. Hilo lilikuwa tendo kubwa zaidi la fazili zenye hatustahili. (Yohana 3:16) Mutume Paulo alisema kama sasa Yesu ‘amevikwa taji la utukufu na heshima kwa kupatwa na kifo, ili kwa fazili zisizostahiliwa za Mungu aonje kifo kwa ajili ya kila mwanadamu.’ (Waebrania 2:9) Ndiyo, ‘zawadi ambayo Mungu anatoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.’—Waroma 6:23b.

5, 6. Tunaweza kupata matokeo gani ikiwa tunatawaliwa (a) na zambi? (b) na fazili zenye hatustahili?

5 Sababu gani tunafanya zambi na tunakufa? Biblia inasema kama ‘kwa kosa la mutu mumoja kifo kilitawala kama mufalme.’ Kwa kuwa tuko watoto wa Adamu, ndiyo sababu hatukamilike na tunakufa. (Waroma 5:12, 14, 17) Lakini, tunaweza kuchagua ikiwa tutaacha zambi itutawale ao hapana. Hilo linawezekana namna gani? Wakati tunaonyesha imani katika zabihu ya ukombozi ya Kristo, tunapata faida za fazili za Yehova zenye hatustahili. Biblia inasema hivi: ‘Mahali ambapo zambi ilizidi, fazili zisizostahiliwa zilizidi hata zaidi. Kwa kusudi gani? Kwamba, kama vile zambi ilivyotawala kama mufalme pamoja na kifo, vivyo hivyo pia fazili zisizostahiliwa zitawale kama mufalme kupitia uadilifu kwa tazamio la uzima wa milele kupitia Yesu Kristo.’—Waroma 5:20, 21.

6 Hata kama tungali watenda-zambi, hatupaswe kuacha zambi itutawale. Kwa hiyo, wakati tunafanya kosa fulani, tunamuomba Yehova atusamehe. Mutume Paulo alituonya hivi: ‘Zambi haipaswe kuwa bwana juu yenu, kwa kuwa ninyi hamuko chini ya sheria bali [lakini] chini ya fazili zisizostahiliwa.’ (Waroma 6:14) Sasa, namna gani fazili za Mungu zenye hatustahili zinaweza kutuletea faida? Mutume Paulo alisema hivi: ‘Fazili zisizostahiliwa za Mungu . . . zinatufundisha kukataa kabisa kutomuogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na tuishi kwa utimamu wa akili [akili nzuri] na uadilifu na ujitoaji-kimungu [kushikamana na Mungu tu] katikati ya mufumo wa mambo wa sasa.’—Tito 2:11, 12.

FAZILI ZENYE HATUSTAHILI ‘ZINAONYESHWA KWA NJIA MBALIMBALI’

7, 8. Kusema kama fazili za Yehova zenye hatustahili ‘zinaonyeshwa kwa njia mbalimbali,’ maana yake nini? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

7 Mutume Petro aliandika hivi: ‘Kwa kadiri ambayo kila mumoja amepokea zawadi, muitumie katika kuhudumiana [kutumikiana] kama wasimamizi-nyumba wazuri wa fazili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.’ (1 Petro 4:10) Kusema kama fazili za Yehova zenye hatustahili ‘zinaonyeshwa kwa njia mbalimbali’ maana yake nini? Ni kusema, hata kama tunapata majaribu ao magumu gani katika maisha, Yehova atatupatia nguvu zenye tuko nazo lazima ili tuvumilie. (1 Petro 1:6) Sikuzote, atatupatia mambo yenye tuko nayo lazima kabisa ili tupate ushindi katika kila jaribu.

Hata kama tunapata majaribu ao magumu gani katika maisha, sikuzote Yehova atatupatia nguvu zenye tuko nazo lazima ili tupate ushindi

8 Mutume Yohana aliandika hivi: ‘Sisi wote tulipokea kutokana na wingi alio nao, hata fazili zisizostahiliwa juu ya fazili zisizostahiliwa.’ (Yohana 1:16) Tunapata baraka nyingi kwa sababu Yehova anatuonyesha fazili zenye hatustahili kwa njia mbalimbali. Ni baraka gani hizo?

9. Fazili za Yehova zenye hatustahili zinatuletea faida gani, na namna gani tunaweza kuonyesha shukrani kwa ajili ya fazili hizo?

9 Yehova anasamehe zambi zetu. Kwa sababu ya fazili zake zenye hatustahili, Yehova anasamehe zambi zetu. Lakini anatusamehe ikiwa tu tunatubu na tunaendelea kupiganisha tamaa zetu za kufanya zambi. (Soma 1 Yohana 1:8, 9.) Mutume Paulo alifasiria Wakristo watiwa-mafuta wa wakati wake namna Yehova anasamehe zambi. Alisema hivi: ‘[Mungu] alitukomboa kutoka katika mamlaka ya giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa upendo wake, ambaye kwa njia yake tunaachiliwa huru kupitia fidia [zabihu ya ukombozi], kusamehewa zambi zetu.’ (Wakolosai 1:13, 14) Tuko wenye shukrani sana kwa ajili ya rehema ya Mungu, ndiyo sababu tunapenda kumusifu. Na kwa sababu Yehova anasamehe zambi zetu, hilo linaweza kutuletea pia baraka zingine nyingi za muzuri sana.

10. Fazili zenye hatustahili za Mungu zinatusaidia kuwa na nini?

10 Tunaweza kuwa na urafiki wenye amani pamoja na Mungu. Kwa sababu hatukamilike, tuko maadui wa Mungu tangu wakati tunazaliwa. Lakini mutume Paulo alisema hivi: “Tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake.” (Waroma 5:10) Kwa sababu ya zabihu ya ukombozi, tunaweza kupatanishwa na Mungu, ni kusema, tunaweza kuwa na amani pamoja naye na kuwa marafiki wake. Mutume Paulo alieleza jambo hilo na namna linapatana na fazili za Yehova zenye hatustahili wakati aliambia ndugu zake watiwa-mafuta hivi: ‘Kwa kuwa sasa tumetangazwa kuwa waadilifu [wenye haki] kutokana na imani, na tufurahie amani pamoja na Mungu kupitia Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kupitia yeye pia tumekaribia kwa njia ya imani kuingia katika fazili hizi zisizostahiliwa ambamo sasa tunasimama.’ (Waroma 5:1, 2) Sisi ni wenye shukrani sana kwa sababu tuko na urafiki wenye amani pamoja na Yehova!

Fazili za Mungu zenye hatustahili zinaonyeshwa kwa njia mbalimbali: Pendeleo la kusikia habari njema (Picha hii inapatana na fungu la 11)

11. Namna gani watiwa-mafuta wanaleta “kondoo wengine” kwenye uadilifu?

11 Tunaweza kuwa wenye haki mbele za Mungu. Nabii Danieli aliandika kama katika siku za mwisho, “wale walio na ufahamu,” ni kusema, watiwa-mafuta, wangeleta “wengi kwenye uadilifu [haki].” (Soma Danieli 12:3.) Namna gani watiwa-mafuta wanafanya hivyo? Wanahubiri habari njema na kufundisha mamilioni ya “kondoo wengine” sheria za Yehova. (Yohana 10:16) Wanawasaidia waonekane kuwa wenye haki mbele za Mungu. Jambo hilo linawezekana tu kupitia fazili za Yehova zenye hatustahili. Mutume Paulo alieleza hivi: ‘Ni zawadi ya bure kwamba wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fazili [za Mungu] zisizostahiliwa kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa.’—Waroma 3:23, 24.

Faida ya sala (Picha hii inapatana na fungu la 12)

12. Sababu gani sala ni mupango wenye kuonyesha fazili za Mungu zenye hatustahili?

12 Tunaweza kumukaribia Mungu kupitia sala. Tunaweza kusali kwa Yehova kwa sababu ya fazili zake zenye hatustahili. Mutume Paulo aliita kiti cha ufalme cha Yehova kuwa ‘kiti cha ufalme cha fazili zisizostahiliwa,’ na anatuomba tukikaribie “na uhuru wa kusema.” (Waebrania 4:16a) Tunaweza kusali kwa Yehova wakati wowote kupitia Yesu. Kwa kweli, hilo ni pendeleo kubwa zaidi! Mutume Paulo alisema hivi: “Tuna uhuru huu wa kusema na tuna uwezo wa kukaribia tukiwa na uhakika kupitia imani yetu katika yeye.”—Waefeso 3:12.

Musaada kwa wakati wenye kufaa (Picha hii inapatana na fungu la 13)

13. Namna gani fazili zenye hatustahili zinaweza kuwa ‘musaada kwa wakati unaofaa’?

13 Tunaweza kupata musaada kwa wakati wenye kufaa. Mutume Paulo alitutia moyo tusali kwa Yehova wakati wowote wenye tuko na lazima ya musaada, ‘ili tupokee rehema na kupata fazili zisizostahiliwa kuwa musaada kwa wakati unaofaa.’ (Waebrania 4:16b) Wakati wowote tuko na majaribu ao magumu katika maisha yetu, tunaweza kumuomba Yehova atusaidie. Na anajibia sala zetu hata kama halazimishwe kufanya hivyo. Mara nyingi anatumia ndugu na dada zetu ili kutusaidia. Yehova anajibia sala zetu “hivi kwamba tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni musaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitendea nini?’”—Waebrania 13:6.

14. Mioyo yetu inapata faida gani kupitia fazili zenye hatustahili?

14 Tunaweza kupata faraja ao kitulizo kwa ajili ya mioyo yetu. Ni baraka kubwa sana kwa sababu Yehova anatufariji kila wakati tunavunjika moyo. (Zaburi 51:17) Wakati Wakristo wa Thesalonike walikuwa wanateswa, mutume Paulo aliwaandikia hivi: ‘Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe na Mungu Baba yetu, aliyetupenda na kutupa sisi faraja ya milele na tumaini njema kwa njia ya fazili zisizostahiliwa, na aifariji mioyo yenu na kuwaimarisha ninyi.’ (2 Wathesalonike 2:16, 17.) Kujua kama Yehova anatupenda na anatuhangaikia kwa sababu ya fazili zake zenye hatustahili kunatufariji sana!

15. Kwa sababu ya fazili za Yehova zenye hatustahili, tuko na tumaini gani?

15 Tuko na tumaini la uzima wa milele. Kwa sababu tuko watenda-zambi, hatungekuwa na tumaini bila musaada wa Yehova. (Soma Zaburi 49:7, 8.) Lakini Yehova ametupatia tumaini la muzuri sana. Ni tumaini gani? Yesu alisema hivi: ‘Haya ndiyo mapenzi ya Baba yangu, kwamba kila mutu ambaye anamutazama Mwana na kumuamini akuwe na uzima wa milele.’ (Yohana 6:40) Kwa hiyo, tuko na tumaini la kuishi milele kwa sababu ya fazili za Yehova zenye hatustahili. Mutume Paulo alisema hivi: ‘Fazili zisizostahiliwa za Mungu zinazowaletea watu wa namna zote wokovu zimeonyeshwa.’—Tito 2:11.

USIGEUZE FAZILI ZA MUNGU ZENYE HATUSTAHILI KUWA SABABU YA KUFANYA ZAMBI

16. Namna gani Wakristo fulani wa kwanza walitumia mubaya fazili za Mungu zenye hatustahili?

16 Fazili za Yehova zenye hatustahili zinatuletea baraka nyingi. Hata hivyo, hatupaswe kutumia mubaya fazili zake, ni kusema, zikuwe sababu ya kufanya zambi. Wakristo fulani wa kwanza walijaribu ‘kugeuza fazili zisizostahiliwa za Mungu . . . kuwa kisingizio [sababu] cha mwenendo mupotovu [mubaya sana].’ (Yuda 4) Inaonekana kama Wakristo hao wenye kukosa uaminifu waliwaza kama wanaweza kufanya zambi na Yehova angeendelea kuwasamehe. Walijaribu hata kuchochea pia Wakristo wenzao wafanye zambi. Leo pia, mutu mwenye anafanya hivyo ‘ameitendea kwa zarau ile roho ya fazili zisizostahiliwa.’—Waebrania 10:29.

17. Mutume Petro alitoa onyo gani nzito?

17 Leo, Shetani amedanganya Wakristo fulani wawaze kama wanaweza kufanya zambi na kama Yehova atawasamehe tu. Ni kweli kama Yehova ni tayari kusamehe watenda-zambi wenye kutubu; hata hivyo, anatuomba tupiganishe tamaa zetu za kufanya zambi. Yehova alimuongoza mutume Petro aandike hivi: ‘Ninyi, wapendwa, mukikuwa na ujuzi huu wa kimbele, mujilinde ili musichukuliwe mbali pamoja nao kwa kosa la watu wanaokaidi [wenye kuvunja] sheria, muanguke kutoka kwenye uimara wenu wenyewe. Hapana, bali [lakini] muendelee kukua [kukomaa] katika fazili zisizostahiliwa na ujuzi juu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.’—2 Petro 3:17, 18.

FAZILI ZENYE HATUSTAHILI ZINATULETEA MADARAKA

18. Fazili za Yehova zenye hatustahili zinatuletea madaraka gani?

18 Tuko wenye shukrani sana kwa ajili ya fazili za Yehova zenye hatustahili. Kwa hiyo, tunapaswa kutumia zawadi zetu ili kumuletea Yehova heshima na kusaidia wengine. Kusaidia wengine ni daraka letu. Namna gani tunaweza kutumia zawadi hizo? Mutume Paulo anasema hivi: ‘Basi, kwa kuwa tuna zawadi zinazotofautiana kulingana na fazili zisizostahiliwa tulizopewa . . . ao ni huduma [utumishi], na tukuwe katika huduma hii; ao yeye anayefundisha, na akuwe katika kufundisha kwake; ao yeye anayehimiza [anayetia moyo], na akuwe katika kuhimiza kwake; . . . yeye anayeonyesha rehema, na afanye hivyo kwa uchangamufu [furaha].’ (Waroma 12:6-8) Fazili za Yehova zenye hatustahili zinatutolea daraka la kuhubiri kwa bidii, kufundisha wengine Biblia, kutia moyo ndugu na dada zetu, na kusamehe kila mutu mwenye anaweza kutukosea.

19. Katika habari yenye kufuata tutazungumuzia daraka gani lenye tuko nalo?

19 Tumebarikiwa na fazili za Yehova zenye hatustahili; kwa hiyo, tunapaswa kufanya nguvu zetu zote ili ‘kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fazili zisizostahiliwa za Mungu.’ (Matendo 20:24) Tutazungumuzia daraka hilo katika habari yenye kufuata.

^ [1] (fungu la 2) Soma habari “Faveur immeritée” katika kitabu Étude Perspicace des Écritures (it-1-F uku. 871)