WASOMAJI WETU WANAULIZA . . .
Noeli ni ya Wakristo?
Mamilioni ya watu katika dunia wanaamini kwamba Noeli ni sikukuu ya kukumbuka kuzaliwa kwa Yesu Kristo. Lakini umekwisha kujiuliza kama Wakristo wa kwanza-kwanza, kama vile mitume na wanafunzi wake, walifanya sikukuu ya Noeli? Na unajua mambo Biblia inasema kuhusu sikukuu za kuzaliwa? Kupata majibu ya maulizo hayo kunaweza kutusaidia kujua kama Noeli ni ya Wakristo ao hapana.
Kwanza, Biblia haizungumuzie sikukuu ya kuzaliwa kwa Yesu ao ya muabudu mwengine muaminifu wa Mungu. Maandiko yanazungumuzia tu watu wawili wenye walifanya sikukuu ya kuzaliwa kwao. Hakuna mumoja kati yao mwenye alikuwa muabudu wa Yehova, Mungu wa kweli, na wakati walifanya sikukuu ya kukumbuka kuzaliwa kwao, jambo fulani la mubaya lilifanyika. (Mwanzo 40:20; Marko 6:21) Kulingana na kitabu Encyclopædia Britannica, Wakristo wa kwanza-kwanza, walipinga “desturi ya kipagani ya kufanya sikukuu za kuzaliwa.”
Yesu alizaliwa tarehe gani?
Biblia haiseme waziwazi ni wakati gani Yesu alizaliwa. Kitabu Cyclopedia cha McClintock na Strong kinasema kwamba “siku ya kuzaliwa kwa Kristo haiwezi kuhakikishwa katika Agano Jipya wala mahali pengine popote.” Kwa kweli, kama Yesu alipenda wafuasi wake wafanye sikukuu ya kuzaliwa kwake, angehakikisha kwamba wanajua pia tarehe yake ya kuzaliwa.
Pili, Biblia haionyeshe kwamba Yesu ao yeyote kati ya wanafunzi wake alifanya sikukuu ya Noeli. Kulingana na kitabu New Catholic Encyclopedia, kufanya sikukuu ya Noeli kulitajwa kwa mara ya kwanza “katika Chronograph ya Philocalus, kitabu cha Waroma cha matukio ya mwaka chenye pengine kiliandikwa mwaka wa 336 [kisha kuzaliwa kwa Yesu].” Ni wazi kwamba, hiyo ilikuwa kisha kumaliza kazi ya kuandika Biblia na mamia ya miaka kisha Yesu kuishi katika dunia. Kwa hiyo, McClintock na Strong wanaonyesha kwamba “kufanya Noeli hakukuanzishwa na Mungu, wala hakutokane na Agano Jipya.” *
Yesu aliambia wanafunzi wake wakumbuke tukio gani?
Akiwa Mwalimu mukuu, Yesu Kristo alitoa maagizo yenye kuwa wazi kuhusu mambo yenye alipenda wanafunzi wake wafanye, na maagizo hayo yanapatikana katika Biblia. Lakini, kufanya sikukuu ya Noeli hakupatikani kati ya maagizo hayo. Kama vile tu mwalimu wa masomo hapendi wanafunzi wake wapite maagizo yenye amewapatia, Yesu pia hapendi wafuasi wake ‘wapite mambo yaliyoandikwa’ katika Maandiko Matakatifu.—1 Wakorintho 4:6.
Kwa upande mwingine, kuko tukio moja la maana lenye Wakristo wa kwanza-kwanza walijua muzuri: Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Yesu mwenyewe aliambia wanafunzi wake ni wakati gani wangekumbuka tukio hilo na aliwaonyesha pia namna ya kulifanya. Maagizo hayo, na pia tarehe ya kifo chake vinapatikana katika Biblia.—Luka 22:19; 1 Wakorintho 11:25.
Kama vile tumeona, Noeli ni sikukuu ya kukumbuka siku ya kuzaliwa, na Wakristo wa kwanza-kwanza hawakufuata desturi hiyo ya kipagani. Zaidi ya hayo, Biblia haionyeshe kwamba Yesu ao mutu mwengine yeyote alifanya sikukuu ya Noeli. Kwa sababu ya mambo hayo, mamilioni ya Wakristo katika dunia wametambua kwamba Noeli haiko yao.
^ fu. 6 Ili kupata habari zaidi kuhusu vyanzo vya desturi nyingi za Noeli, ona habari “Wasomaji Wetu Wanauliza . . . Mambo ya Kweli Ni Gani Juu ya Sikukuu ya Noeli ?” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 12, 2014, inapatikana pia kwenye www.jw.org.