Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAWAZO YA BIBLIA

Kuvumilia Wengine

Kuvumilia Wengine

Kukubali wengine, kuwasamehe, na kuwavumilia kunafanya tuishi nao kwa amani. Lakini kuvumilia wengine kunapaswa kuwa na mipaka?

Ni nini inaweza kutusaidia kuvumilia wengine zaidi?

NAMNA HALI IKO LEO

Katika dunia yote, tabia ya kukosa kuvumilia wengine inaenea sana, inaongezeka hata zaidi kwa sababu ya ubaguzi wa rangi, wa inchi, wa kabila, na wa dini.

MAMBO BIBLIA INASEMA

Wakati Yesu alikuwa katika dunia, alizungukwa na watu wenye kukosa kuvumilia wengine. Kwa mufano, Wayahudi na Wasamaria walikuwa wanachukiana sana. (Yohana 4:9) Wanawake walionwa kuwa wa hali ya chini kuliko wanaume. Na viongozi wa dini ya Wayahudi walikuwa wanazarau watu wa kawaida. (Yohana 7:49) Lakini Yesu hakukuwa kabisa kama viongozi hao. Watu waliomupinga walisema hivi: ‘Mutu huyu anakaribisha watenda-zambi na anakula pamoja nao.’ (Luka 15:2) Yesu alihangaikia wengine, alivumilia wengine na kuwakubali kwa sababu alikuja kuponya watu kiroho lakini haiko kuwahukumu. Upendo ndilo jambo kubwa lenye lilisukuma Yesu kutenda hivyo.—Yohana 3:17; 13:34.

Yesu alionyesha mufano muzuri katika kuvumilia wengine, alikuja kuponyesha watu kiroho lakini haiko kuwahukumu

Upendo ndio unaweza kutusaidia kuvumilia wengine zaidi, unafanya tuwakubali hata kama wako na uzaifu ao tabia fulani yenye hatufurahie. Andiko la Wakolosai 3:13 linasema hivi: ‘Muendelee kuvumiliana na kusameheana kwa hiari [kupenda] ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwengine.’

‘Zaidi ya mambo yote, mukuwe na upendo mukubwa ninyi kwa ninyi, kwa sababu upendo unafunika zambi nyingi.’1 Petro 4:8.

Sababu gani kuvumilia wengine kunapaswa kuwa na mipaka?

NAMNA HALI IKO

Inchi nyingi zinajaribu kuheshimu sheria na kulinda utaratibu. Kwa hiyo, mara nyingi zinatia mipaka yenye kufaa juu ya tabia.

MAMBO BIBLIA INASEMA

‘[Upendo] haujiendeshe bila adabu.’ (1 Wakorintho 13:5) Hata kama Yesu alionyesha mufano muzuri katika kuvumilia wengine, hakuachilia tabia ya kukosa adabu, unafiki, ao tabia zingine mbaya. Lakini, kwa uhodari alionyesha kuwa mambo hayo yalikuwa mabaya. (Mathayo 23:13) Alisema hivi: ‘Yule ambaye anazoea kufanya mambo maovu anachukia nuru [ya kweli].’ —Yohana 3:20.

Mutume Mukristo Paulo aliandika hivi: ‘Muchukie maovu, mushikamane na mema.’ (Waroma 12:9) Katika maisha yake, alifuata maneno hayo. Kwa mufano, wakati Wakristo fulani Wayahudi walijitenga na Wakristo wenye hawakukuwa Wayahudi, kwa upole Paulo alipinga kabisa jambo hilo hata kama yeye mwenyewe alikuwa Muyahudi. (Wagalatia 2:11-14) Alijua kama Mungu mwenye “hana ubaguzi,” hangevumilia ubaguzi kama huo kati ya watu wake.—Matendo 10:34.

Wakristo, Mashahidi wa Yehova, wanatafuta muongozo juu ya mwenendo muzuri katika Biblia. (Isaya 33:22) Kwa hiyo, hawavumilie matendo mabaya kati yao. Kutaniko safi la Kikristo halipaswe kuchafuliwa na watu wenye hawafuate kanuni za Mungu. Ndiyo sababu Mashahidi wa Yehova wanafuata muongozo huu wa Biblia wenye kuwa wazi: ‘Muondoe yule mutu muovu kati yenu.’—1 Wakorintho 5:11-13.

Enyi munaomupenda Yehova, muchukie yaliyo mabaya.’Zaburi 97:10.

Mungu atavumilia mambo mabaya milele?

MAMBO WATU WENGI WANAAMINI

Kwa sababu ya hali ya watu, mambo mabaya yataendelea sikuzote.

MAMBO BIBLIA INASEMA

Nabii Habakuki alisali hivi kwa Yehova Mungu: ‘Kwa nini . . . unaendelea kutazama taabu tupu? Na kwa nini kuna uporaji na jeuri mbele yangu, kwa nini kugombana kunatokea, kwa nini muzozo unaendelezwa?’ (Habakuki 1:3) Mungu hakumuacha nabii wake mwenye kuvurugika aendelee kuwa na mashaka. Alimuhakikishia kama atahukumu watu wabaya. Juu ya ahadi hiyo Mungu alisema hivi: ‘Bila shaka itatimia. Haitachelewa.’—Habakuki 2:3.

Mbele wakati huo ufike, watu wenye kufanya mambo mabaya wako na nafasi ya kubadilika. ‘Je, ninapendezwa hata kidogo na kifo cha mutu muovu, asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, bali kwamba ageuke na kuziacha njia zake, naye kwa kweli aendelee kuishi?’ (Ezekieli 18:23) Wale wenye kumutafuta Yehova kwa kuacha matendo yao mabaya, wanaweza kungojea wakati unaokuja kwa uhakika. Andiko la Methali 1:33 linasema hivi: ‘Mutu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu [woga] ya musiba.’

bado muda kidogo tu, na mutu muovu hatakuwako tena . . . Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.’ Zaburi 37:10, 11.