Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICWA | UZIMA ULIANZA NAMNA GANI?

Maulizo Mawili Tunayopaswa Kuuliza

Maulizo Mawili Tunayopaswa Kuuliza

1 Uzima Ulianza Namna Gani?

Mambo Watu Fulani Wanasema. Uzima ulijitokeza wenyewe kutokana na vitu visivyokuwa na uzima.

SABABU INAYOFANYA WATU FULANI WASITOSHEKE NA JIBU HILO. Wanasayansi wanajua mambo mengi juu ya kemia na muundo wa molekuli ya uzima kuliko zamani, lakini hawawezi kueleza kwa uhakika uzima ni nini. Kuna tofauti kubwa sana kati ya vitu visivyokuwa na uzima na chembe ndogo sana yenye uzima.

Wanasayansi wanaweza tu kuwazia-wazia juu ya namna hali zilikuwa duniani mamiliare ya miaka iliyopita. Wana mawazo yenye kupingana juu ya mahali uzima ulianzia, kwa mufano hawajue ikiwa ulianza ndani ya volkeno ao chini ya bahari. Watu wengine wanaamini kuwa visehemu mbalimbali vya uzima vilifanyizwa kwanza mahali fulani katika ulimwengu na kisha vikafika hapa vikiwa ndani ya vimondo (nyota zinazopita haraka angani). Lakini mawazo hayo hayatoe jibu kuhusu ulizo juu ya namna uzima ulianza, yanaonyesha tu kuwa uzima ulianzia mahali fulani.

Wanasayansi wanawazia-wazia tu kama kuna molekuli zilizotangulia chembe za uriti tunazojua leo. Molekuli hizo zinawaziwa kuwa labda zilijitokeza zenyewe kutokana na vitu visivyokuwa na uzima na kuwa zilikuwa na uwezo wa kuzaana. Lakini sayansi haijapata mambo ya kuhakikisha kuwa molekuli kama hizo zilikuwako, wala wanasayansi hawana uwezo wa kufanya molekuli kama hizo katika chumba cha uchunguzi.

Vitu vyenye uzima ni vya pekee katika namna vinaweka na kushugulikia habari. Chembe zinapokea, zinasoma, na kutenda kulingana na maagizo yaliyo katika chembe za uriti. Wanasayansi fulani wanafananisha chembe za uriti na programu zilizo ndani ya ordinatere na wanafananisha muundo wa kemikali wa chembe na sehemu za inje za ordinatere. Lakini mageuzi hayawezi kufasiria ikiwa habari zilizo katika chembe za uriti zinatoka wapi.

Chembe ina lazima ya molekuli za protini ili kufanya kazi. Protini ya kawaida ina mamia ya asidi-amino zilizofungwa pamoja katika mupangilio wa pekee. Tena, molekuli ya protini inapaswa kujikunja na kufanyiza umbo la pekee lenye nyuso tatu ili ikuwe na mafaa. Wanasayansi fulani wanafikia uamuzi wa kuwa haiwezekane hata molekuli moja ya protini kujifanya yenyewe. Mwanafizikia Paul Davies anasema hivi: “Kwa kuwa chembe ina lazima ya maelfu ya protini tofauti-tofauti ili kufanya kazi, haiwezekane kufikiri kuwa protini hizo zilijifanya zenyewe.”

UAMUZI. Kisha kufanya uchunguzi kwa makumi ya miaka katika karibu kila sehemu ya sayansi, inaonekana wazi kuwa uzima unatokana tu na uzima uliotangulia.

2 Vitu Vyenye Uzima Vilitokea Namna Gani?

MAMBO WATU FULANI WANASEMA. Kiumbe cha kwanza chenye uzima kilitokeza hatua kwa hatua viumbe mbalimbali vyenye uzima, na hata wanadamu, kupitia hatua ya mabadiliko yasiyokuwa na mupango na uteuzi wa asili (fundisho la kwamba viumbe vyenye uzima vinaishi ikiwa ni vyenye nguvu ao vinakufa ikiwa ni zaifu kulingana na namna vinajipatanisha na mazingira).

SABABU INAYOFANYA WATU FULANI WASITOSHEKE NA JIBU HILO. Chembe fulani ni ngumu zaidi kueleweka kupita zingine. Kulingana na kitabu kimoja, namna chembe nyepesi zaidi zingeweza kutokeza chembe ngumu zaidi kueleweka “inaonwa mara nyingi kuwa fumbo kubwa la pili la mageuzi, kisha fumbo la namna uzima ulianza.”

Wanasayansi walivumbua ndani ya kila chembe mashini za molekuli ngumu kueleweka zenye kufanyizwa na molekuli za protini zinazosaidiana ili kutimiza kazi mbalimbali ngumu. Kazi hizo zinatia ndani kusafirisha lishe ao chakula na kuigeuza kuwa nguvu, kutengeneza sehemu zilizoharibika za chembe, na kupeleka habari katika chembe yote. Je, mabadiliko yasiyo na mupango na uteuzi wa asili vingeweza kufanyiza na kuwezesha kutumika kwa sehemu hizo za hali ya juu? Watu wengi wanashindwa kukubali wazo hilo.

Wanyama na wanadamu wanatokana na yai lililowekwa mbegu za kiume. Katika kiini-tete (embryon), chembe zinazaana na kisha zinagawanyika, zinachukua maumbo na kazi tofauti-tofauti ili kufanyiza sehemu mbalimbali za mwili. Mageuzi hayawezi kueleza namna kila chembe “inajua” kile itakuwa na mahali inapaswa kuenda katika mwili.

Sasa wanasayansi wanatambua kuwa ili aina fulani ya wanyama itokeze aina ingine ya wanyama, inaomba mabadiliko yafanyike ndani ya chembe, katika molekuli. Kwa kuwa wanasayansi hawawezi kuonyesha namna mageuzi yanaweza kutokeza hata chembe “nyepesi sana,” je, ni jambo lenye kupatana na akili kusema kama mabadiliko yasiyokuwa na mupango na uteuzi wa asili vingeweza kutokeza aina tofauti-tofauti za wanyama duniani? Juu ya namna wanyama wamefanyizwa, Michael Behe, profesa wa sayansi ya biolojia, anasema kuwa hata ikiwa utafiti “umevumbua mambo ya ajabu yasiyoeleweka, yenye hayakutazamiwa, hakuna maendeleo yoyote yamefanywa ili kuelewa namna mambo yasiyoeleweka yangetokana na hatua zisizotegemea akili.”

Watu wako na zamiri na wanajitambua, wako na uwezo wa kuwaza na kufikiri sana, na wako na sifa za muzuri kama vile kutolea wengine, kujitoa, na uwezo wa kutambua mazuri na mabaya. Mabadiliko yasiyokuwa na mupango na uteuzi wa asili haviwezi kueleza sababu gani mutu iko na sifa hizo za pekee katika akili.

UAMUZI. Hata ikiwa watu wengi wanakazia kuwa fundisho la kwamba uzima ulitokana na mageuzi haliwezi kupingwa, watu wengine hawatosheke na majibu yenye fundisho hilo linatoa juu ya namna uzima ulianza na namna uliendelea.