SEHEMU YA KUULIZA MAULIZO | STEPHEN TAYLOR
Profesa wa Hesabu za Feza Anaeleza Imani Yake
Profesa Stephen Taylor anafundisha na kuongoza uchunguzi kwenye Masomo ya Juu ya Ufundi katika muji wa Sydney, Australia. Anajifunza juu ya masoko ya feza na njia mbalimbali za kuyachunguza muzuri. Gazeti Amuka! lilimuuliza namna uchunguzi wake umekuwa na matokeo juu ya imani yake ya dini.
Tuambie juu ya familia yako.
Nililelewa na wazazi waliokuwa wanaenda kwenye kanisa, walikuwa watu wazuri na wafanyakazi wenye bidii. Walinitia moyo nipate elimu ya muzuri, kwa hiyo nikajifunza mambo ya biashara kwenye Masomo ya Juu ya Nouvelle-Galles du Sud. Nilitambua kuwa nilipenda kufanya uchunguzi na nikaamua kufanya kazi ya uchunguzi na ualimu kwenye masomo ya juu.
Ulifanya uchunguzi juu ya mambo gani?
Nilitaka zaidi sana kuelewa namna masoko ya hisa (biashara ya sehemu ya feza mutu anachanga katika kampuni) yanatumika. * Masoko ya hisa yanawezesha watu kununua na kuuzisha sehemu wanazochangia katika kampuni na kisha kampuni hizo zinatumia feza hizo ili kuendesha biashara zao. Kati ya mambo mengine, ninafanya uchunguzi juu ya mambo yanayochochea bei za hisa katika kampuni.
Unaweza kutupatia mufano?
Kampuni zinaombwa kuripoti faida zao kwa ukawaida. Watu wanaotoa feza zao ili kuendesha kampuni wanachunguza ripoti hizo wakati wanajaribu kujua hali ya feza ya kampuni. Lakini njia fulani zinazotumiwa kuripoti faida hazikubalike. Wachambuzi wanaweza kuona hilo kuwa kosa katika kampuni linaloruhusu kampuni ifiche hali yake ya kweli na faida zake. Namna gani watu wanaotoa feza zao ili kuendesha kampuni wanaweza kupata habari za kweli na zenye kuenea? Watu wanaochunguza namna kampuni inatumika wana lazima ya habari gani ili kuhakikisha kuwa soko za feza zinatumika muzuri? Mimi na wafanyakazi wenzangu tuko tunajaribu kupata majibu ya maulizo hayo.
Ulikomalia katika dini gani?
Nilizoea kuenda kwenye Kanisa la Presbiteri pamoja na wazazi wangu lakini niliacha mambo ya dini wakati nilikuwa na miaka kati ya 13 na 19. Niliamini kuna Muumbaji na nilikuwa ninaheshimia Biblia lakini niliona kuwa dini haisaidie hata kidogo katika magumu ya maisha. Kwangu, vikundi vya dini vilikuwa tu kama vikundi vya jamii. Katika Ulaya, nilitembelea kanisa nyingi kubwa-kubwa na nilijiuliza sababu gani walikuwa na utajiri mwingi wakati dunia inajaa umaskini. Hilo lilikuwa jambo ngumu sana kwangu kuelewa na likanifanya nikuwe na mashaka fulani juu ya dini.
Ni nini ilikufanya ubadilishe mawazo yako?
Bibi yangu, Jennifer, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na kuhuzuria mikutano yao, kwa hiyo niliwaza kuwa ilikuwa vizuri niende naye ili niwachunguze. Bila kukawia, nilivumbua kuwa sikukuwa ninajua karibu kitu chochote juu ya Biblia. Hilo lilinivunja moyo sana! Kwa hiyo, nikaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.
Njia Mashahidi wa Yehova wanatumia ili kufundisha Biblia ilinipendeza. Walitokeza ulizo, walikusanya mambo na kuyachunguza, na kisha walifikia maamuzi ya mwisho yenye kufaa. Njia hiyo ndiyo nilikuwa ninatumia katika uchunguzi kwenye masomo ya juu! Katika mwaka wa 1999, miaka michache kisha Jennifer kubatizwa, mimi pia nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.
Kujua mambo ya feza kulikusaidia utumainie Biblia zaidi?
Bila shaka. Kwa mufano, Sheria iliyoandikwa yenye Mungu alipatia taifa la zamani la Israeli ilizungumuzia matatizo ya feza ambayo watu wenye elimu ya feza leo hawajaweza kumaliza. Sheria iliwaomba Waisraeli waache mavuno kwa ajili ya maskini (aina fulani ya kodi na asiranse), wakopeshe walio na uhitaji bila faida (uwezekano wa kupata deni), warudishe mashamba ya uriti kwa wenye nayo kisha kila miaka 50 (kulinda haki za kuriti mali). (Mambo ya Walawi 19:9, 10; 25:10, 35-37; Kumbukumbu la Torati 24:19-21) Mipango hiyo ya feza na mipango mingine ilisaidia watu katika njia tatu za maana: (1) Iliwasaidia walipokuwa na magumu ya kupata feza, (2) iliwasaidia kutoka katika umaskini wa muda murefu, na (3) ilipunguza hali ya kukosa usawa katika mambo ya feza. Mambo hayo yote yalifanyika kumepita miaka zaidi ya 3000 mbele ya kuanzishwa kwa sayansi ya mambo ya feza!
Tena Biblia inakazia mawazo na tabia zinazosaidia kupata usalama wa feza. Kwa mufano, inafundisha watu kuwa waaminifu, wenye kutumainika, wenye huruma, na wenye kutolea wengine. (Kumbukumbu la Torati 15:7-11; 25:15; Zaburi ya 15) Inafurahisha kujua kuwa, kwa sababu ya matatizo ya feza yaliyotokea duniani pote hivi karibuni, masomo na mashirika fulani ya biashara yalianza kuwaomba watu wenye ujuzi katika mambo ya biashara na ya feza watie watu moyo kushika kanuni fulani za muzuri za mwenendo. Kwa mawazo yangu, kanuni za Biblia za mwenendo zinapita sana kanuni hizo za biashara.
Imani yako imekusaidia katika njia fulani?
Ndiyo, Jennifer ananiambia kuwa nimekuwa mutu mwenye kuelewa wengine. Mbele nilikuwa ninatafuta ukamilifu na nilikuwa ninawaza kuwa mambo yanapaswa kufanyika vile ninataka. Labda ndiyo maana nilielewa muzuri kanuni za hesabu ya feza! Kuishi kulingana na kanuni za Biblia kumenisaidia kabisa kuwa mwenye usawaziko zaidi. Sasa niko mwenye furaha zaidi, na familia yangu pia ni yenye furaha. Tunafurahia pia kusaidia wengine wapate hekima ya Biblia. Kujifunza Biblia lilikuwa jambo linaloleta faida sana lenye nimefanya katika maisha.
^ fu. 7 Yanaitwa pia masoko ya sehemu ao fungu (actions).
Kujifunza Biblia lilikuwa jambo linaloleta faida sana lenye nimefanya katika maisha