Nilipata Tumaini Wakati Niliihitaji Kabisa
Bila kutazamia, siku moja nilijikuta nimeangukia katika maji. Nilijaribu kuinua kichwa ili nipumue, lakini mishipa ya shingo yangu haikutumika. Niliogopa, nikajaribu kugeuka, lakini mikono na miguu haikutikisika. Nilianza kumeza maji. Kuanzia siku hiyo wakati wa joto kali katika mwaka wa 1991, maisha yangu yalibadilika.
NILIZALIWA katika muji wa Szerencs na nikakomalia katika kijiji cha Tiszaladány kusini-mashariki mwa Hungaria. Katika Mwezi wa 6, 1991, mimi na rafiki zangu tulienda mahali ambapo hatukuzoea kwenda, kwenye muto Tisza. Nilijitupa katika maji, mahali ambapo niliwaza maji yalikuwa marefu. Nilikosea sana kufanya hivyo! Nilivunjika mifupa tatu ya shingo, na pia uti wangu wa mugongo. Rafiki zangu waliona kama ninabaki bila kutikisika na kwa uangalifu wakaniinua na kunitosha katika maji mbele nizame.
Sikupoteza akili, lakini nilijua kama nilikuwa nimepatwa na shida fulani. Mutu fulani aliita wale wanaohusika na matunzo ya haraka, na elikopta ilikuja kunichukua na kunipeleka kwenye hospitali, ambako waganga walinipa dawa ya kutuliza uti wa mugongo. Kisha, nilipelekwa kwenye hospitali katika muji mukubwa, Budapest, ili kunyoosha uti wa mugongo. Nililalia mugongo wangu kwa miezi mitatu. Hata kama nilikuwa na uwezo wa kutikisa kichwa changu, nilipooza kuanzia mabega mupaka miguu. Nilipokuwa na miaka 20, wengine ndio walinisaidia kufanya mambo yote. Nilivunjika moyo sana, na kutamani kufa.
Mwishowe wakati nilirudia kwetu, wazazi wangu walipata mazoezi kuhusu namna ya kunitunza. Lakini kunitunza kuliwachosha kimwili na kiakili, na kisha karibu mwaka mumoja, nilikuwa katika hali ya kuvunjika moyo sana. Wakati huo, nilipata mashauri ya waganga wenye ufundi wa pekee, ambayo yalinisaidia kuelewa hali yangu.
Nilianza pia kufikiri sana juu ya maisha. Nilijiuliza: Maisha yana kusudi? Sababu gani mambo haya yamenifikia? Nilisoma magazeti na vitabu ili kutafuta majibu. Nilijaribu pia kusoma Biblia, lakini niliona kwamba ilikuwa nguvu kuielewa. Kwa hiyo niliacha kuisoma. Nilizungumuza hata na padiri, lakini sikutosheka na mafasirio yake.
Kisha, katika majira ya kuchipua ya 1994, Mashahidi wa Yehova wawili walimutembelea baba yangu, na aliwaomba wazungumuze na mimi. Nilisikiliza maelezo yao juu ya kusudi la Mungu la kufanya dunia kuwa paradiso na kumaliza magonjwa na mateso. Mambo waliyonielezea yalikuwa mazuri sana, lakini nilikuwa na mashaka. Hata hivyo, nilikubali vitabu viwili vya kusaidia kujifunza Biblia. Kisha kusoma vitabu hivyo, Mashahidi hao waliniuliza ikiwa wanaweza kujifunza na mimi Biblia, na niliitika. Walinionyesha kama ni jambo la lazima sana kusali.
Nilisadiki kwamba Mungu ananihangaikia kabisa
Kwa kuendelea kuzungumuza nao, nilipata majibu ya Biblia kwa maulizo yangu mengi. Nilisadiki kwamba Mungu ananihangaikia kabisa. Mwishowe, tarehe 13 Mwezi wa 9, 1997, kisha kujifunza Biblia kwa miaka miwili, nilibatizwa kwenye nyumba yetu katika beseni kubwa ya kunawia. Hiyo ilikuwa siku ya furaha sana katika maisha yangu.
Katika mwaka wa 2007, nilihamia Budapest kwenye nyumba ya walemavu na kubaki huko. Kuhamia huko kulinipa nafasi nyingi za kuelezea wengine kuhusu mambo mazuri ambayo nimejifunza. Hewa inapokuwa nzuri, ninaweza hata kutoka inje ili kuhubiria watu, ninasaidiwa na kiti cha kutembezwa na motere ambacho ninaongoza kupitia kidevu changu.
Familia moja katika kutaniko langu ilinipatia feza, kwa hiyo nilinunua ordinatere ndogo ambayo inatumika kwa kufuata namna kichwa changu kinatikisika. Ordinatere hiyo inanisaidia kutumia Internete ili kuzungumuza na kuandikia watu ambao washiriki wa kutaniko hawakupata kwenye nyumba zao. Kusaidia wengine katika njia hii kumenisaidia nisahau matatizo yangu na pia kumefanya uwezo wangu wa kuongea na watu uwe muzuri.
Ninawaelezea wengine ujumbe wa Biblia kupitia Internete kwa kutumia chombo ambacho kinafuata namna kichwa changu kinatikisika
Ninaweza hata kuhuzuria mikutano ya Kikristo. Wakati ninafika kwenye Jumba la Ufalme, ndugu zangu wa kiroho wananibeba kwa uangalifu nikiwa katika kiti changu cha kutembea na kunipandisha mahali pa kukusanyika kwenye gorofa la kwanza. Wakati wa mikutano, watu wanapoombwa kutoa maelezo, ndugu anayekaa pembeni yangu anaonyesha mukono wake kwa ajili yangu. Kisha anakamatisha Biblia yangu ao kitabu wakati ninatoa maelezo.
Ninasikia maumivu kila wakati na nina lazima ya wengine ili kunifanyia karibu kila jambo. Kwa hiyo, wakati fulani ninakuwa mwenye kuvunjika moyo. Lakini urafiki wangu na Yehova Mungu unanifariji, kwa sababu ninajua kwamba ananisikiliza wakati ninamuelezea waziwazi mahangaiko yangu. Tena, ninapata nguvu kwa kusoma Biblia kila siku na kupitia ndugu na dada zangu wa kiroho. Urafiki wao, kunitia moyo, na kusali kwa ajili yangu kunanisaidia niendelee kutulia katika akili na moyo.
Yehova ananifariji wakati ninahitaji kufarijiwa kabisa. Tena, ananipa tumaini la kuwa na afya nzuri katika dunia mupya. Kwa hiyo, ninangojea kwa hamu wakati ‘nitatembea na kuruka-ruka na kumusifu’ Yehova kwa sababu ya upendo na wema wake mukubwa.—Matendo 3:6-9.