Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 KICHWA

Namna Gani Watu Wanaweza Kufanya Amani?

Namna Gani Watu Wanaweza Kufanya Amani?

Frank na Jerry walikuwa majirani wazuri, lakini uhusiano wao uliharibika wakati Jerry alifanya karamu ambayo iliendelea mupaka usiku sana. * Wakati Frank alinungunika kwa sababu ya makelele, Jerry alikasirika juu ya namna Frank aliongea naye. Walibishana. Kisha hapo, hawakusemezana tena.

FRANK na Jerry walipatwa na tatizo ambalo linawapata watu wote. Wakati watu wawili hawasikilizane, mara nyingi wanakasirikiana na pengine kila mumoja anamulaumu mwenzake. Ikiwa hawamalize matatizo yao, urafiki wao unaweza kwisha.

Pengine umekwisha kupatwa na hali kama hiyo. Ikiwa ni hivyo, bila shaka haukupendezwa nayo. Kwa kweli, watu wengi wanataka kuishi kwa amani na umoja pamoja na marafiki na majirani wao. Namna gani basi tunaweza kuishi kwa amani na umoja hata ikiwa hali za kutoelewana zinaweza kutokea? Inawezekana kuepuka kuwa na maoni mabaya juu ya wengine na hivyo kuwasamehe wakati wanatuumiza moyoni? Inawezekana kumaliza kutoelewana kwetu kwa amani?

Fikiria hali ya Frank na Jerry. Urafiki wao ulianza kuharibika zaidi sana wakati walichukua hatua hizi mbaya: (1) Jerry hakufikiria mwenzake, (2) Frank alinungunika kwa njia ambayo ilimuchukiza Jerry, (3) wote wawili walikasirikiana, na (4) kati yao hakuna aliyekubali kosa lake.

Lakini, baada ya muda fulani, kila mumoja wao alitambua kosa lake. Wanaume hao wawili waliachana na jambo hilo na kufanya amani. Ni nini iliwasaidia? Walitumia kanuni fulani nzuri ambazo zimewasaidia marafiki wengi wapambane na vipindi vya matatizo, na kuendelea kuwa na urafiki wenye nguvu.

Kanuni hizo zinapatikana katika kitabu kimoja ambacho kimegawanywa sana katika dunia yote, ni kusema, Biblia. Kitabu hicho kinawatia watu moyo wawe na sifa zinazoweza kuwasaidia waendeleze amani na zinazomaliza huzuni katika moyo. Sifa hizo ni utambuzi, hekima, wema, upendo, na uvumilivu.—Methali 14:29; 1Wakorintho 13:4,5.

Frank na Jerry ni mifano miwili tu inayoonyesha namna Biblia ina nguvu ya kufanya maisha ya watu yawe  mazuri. Kuna mifano mingine mingi, kama vile mifano ya watu waliofikia kuachana na tabia mbaya ambazo zilikuwa zimetia mizizi kabisa katika mioyo yao. Kwa mufano, Robert, anayeishi Australia, alifikia kuachana na tabia ya kukasirika sana. Nelson, katika inchi ya Timor Mashariki, alishinda uadui wa muda murefu na alifanya urafiki wa karibu sana na mutu aliyekuwa adui wake hapo zamani. Namna gani Biblia ilimusaidia Robert na Nelson? Ili kujua mengi, gazeti Amuka! liliwauliza maulizo fulani.

SEHEMU YA KUULIZA MAULIZO 1

ROBERT, tuelezee kidogo juu ya maisha yako

Nilikomalia katika familia isiyokuwa na furaha. Kwa mufano, baba yangu alikuwa mutu mwenye kukasirika haraka na alinipiga mara nyingi. Nyakati fulani, alinipiga mupaka damu ilinitoka na kuniacha mwenye kuzimia. Jambo hilo lilinifanya kuwa mutu mwenye kukasirika sana na mukali. Nilipokuwa ningali kijana, nilifanya miaka miwili katika masomo ya kuadibisha vijana. Baadaye, nilifanya tendo moja kali la kijeuri na kwa hiyo nilipelekwa katika kifungo chenye ulinzi mukali sana. Mwishowe nilipokombolewa, nilihamia Australia, nikifikiria kuanza maisha mapya huko.

Kuhama kulikusaidia ubadilike?

Kuhama kulinisaidia kwa njia fulani, lakini Biblia, ambayo nilijifunza na Mashahidi wa Yehova ndio ilinisaidia sana. Hata hivyo, ningali ninaendelea kujikaza ili kuzuia hasira yangu na mara nyingi ninasumbuka na kujisikia wa bure. Siku moja nilifikiri juu ya andiko la Methali 19:11, linalosema: ‘Ufahamu wa mutu hakika unapunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita juu ya kosa.’ Kwa kuwa nilitaka kuwa na sifa hiyo ya ufahamu, nilianza kufikiri juu ya sababu zinazotufanya tujisikie, tuseme ao tutende kwa njia fulani. Kwa hiyo, pole kwa pole nilianza kuwa mwenye kuwaelewa wengine, mwenye uvumilivu na mwenye kusamehe.

Unaweza kutupatia mufano mumoja?

Wakati mumoja nilimukosea rafiki yangu bila kukusudia, na alinikaripia kwa ukali mbele ya wengine. Ninaweza kusema tu kwamba nilijiona wa bure kabisa! Lakini, nilikumbuka shauri la Biblia linalosema ‘usimulipe yeyote uovu kwa uovu,’ na mara moja nilimuomba anisamehe. (Waroma 12:17) Wakati rafiki yangu alitulizana, nilimuendea kipekee na nilitambua kwamba alikuwa anapambana na matatizo katika familia yake. Tulifanya amani na baadaye alinipatia zawadi ya koti nzuri. Ninafikiri mambo yangekuwa mabaya ikiwa ningetenda kwa ukali wakati alinikaripia kwa ukali mbele ya wengine.

Namna gani unapambana na matatizo ya familia?

Mimi na bibi yangu tuna kijana mwenye miaka 20, na kama familia nyingine, kuna wakati tunakosa kuelewana. Lakini, nimejifunza mambo mengi katika Biblia, kwa mufano, ulazima wa kusema, “Unisamehe, nimekosea.” Ni jambo lenye kushangaza kuona namna maneno hayo, yanaposemwa bila unafiki yanaweza kuzuia ao kutuliza mabishano.

 SEHEMU YA KUULIZA MAULIZO 2

NELSON, una sura ya kicheko na uko mwenye urafiki. Lakini wakati fulani, ulikuwa mwenye chuki sana, ni kweli?

Ni kweli! Nilipokuwa kijana ­nilijiunga na kikundi cha kisiasa ambacho kilipinga serikali. Nilichukia vilevile chama kimoja cha kisiasa ambacho kilitaka kutawala eneo letu. Ili niwe mupiganaji wa nguvu, nilijifunza kupigana, na kwa hiyo, nilipiga kila mutu ambaye alinikasirisha.

Ni nini ilikuchochea ubadilike?

Nilianza kujifunza Biblia na kutumia mafundisho yake, na kuna mafundisho mawili yaliyonigusa moyo sana. Fundisho la kwanza linasema hivi: ‘Mambo yote munayotaka watu wawatendee ninyi, lazima muwatendee wao pia vivyo hivyo.’ (Mathayo 7:12) Fundisho la pili linasema: ‘Mupende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ (Mathayo 22:39) Nilitambua kwamba Mashahidi, walionifundisha Biblia, walionyesha upendo huo, bila kujali kabila la mutu. Nilipenda kuwa kama wao. Kwa kweli, niliweza kubadilika hivi kwamba wale walionijua zamani walishangaa sana na leo hawaniogope tena.

Kuna siku umeangukia tena katika matendo yako ya zamani?

Ndiyo, lakini hapana katikati ya watu. Wakati fulani ninashindwa kuzuia hasira yangu nikiwa nyumbani. Kwa kweli, siku moja nilikasirika na kumupiga bibi yangu, jambo ambalo ninasikitikia sana. Alinisamehe, lakini hilo lilinifanya niazimie hata zaidi kuzuia hasira yangu.

Ulisema kwamba watu wameacha kukuogopa. Unaweza kutupatia mufano?

Ndiyo. Siku moja nilikutana na mutu mumoja mwenye kujulikana sana wa chama cha kisiasa ambacho nilizungumuzia hapo mbele, jina lake ni Augusto. Mwanzoni, aliniogopa sana. Lakini nilimusalimia kwa furaha, nilimuambia asahau mambo yaliyofanya tusielewane zamani, na nilimualika kwangu. Alikubali mwaliko wangu na alishangaa sana kwa sababu ya mabadiliko ambayo nilikuwa nimefanya hivi kwamba yeye pia alianza kujifunza Biblia. Leo Augusto na mimi tumekuwa marafiki wa sana na pia ndugu wa kiroho.

 ‘Muwe Wenye Kufanya Amani na Watu Wote’

Kuna mambo mengi yanayofanya watu wakose kuelewana, na si kila mutu atakayekubali kufanya amani. Ndiyo sababu Biblia inatoa shauri hili lenye usawaziko: ‘Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, muwe wenye kufanya amani na watu wote.’—Waroma 12:18.

Watu waliotajwa katika habari hii wanatusaidia tuone kwamba hekima ya Biblia inafanya kazi kabisa, ni kusema, ina uwezo wa kupindua “ngome zenye nguvu,” maana yake tabia zisizofaa ikiwa tunairuhusu kufanya hivyo. (2Wakorintho 10:4) Kuhusu hekima hiyo, andiko la Methali 3:17,18 linasema hivi: ‘Njia zake ni njia za uzuri, na barabara zake zote ni za amani. Ni muti wa uzima kwa wale wanaoishika, na wale wanaoishika sana wataitwa wenye furaha.’

Unapenda uwe mwenye furaha na mwenye kufanya amani zaidi? Unatamani kuwa na urafiki ambao hautavunjika wakati matatizo yanatokea? Ikiwa ndiyo, hautakata tamaa ao kuvunjika moyo ikiwa unaruhusu Biblia ikuongoze.

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.