Cha Kwanza cha Samweli 6:1-21

  • Wafilisti wanarudishia Israeli Sanduku (1-21)

6  Sanduku+ la Yehova lilikuwa katika eneo la Wafilisti kwa miezi saba (7). 2  Wafilisti wakaita makuhani na waaguzi+ na kuuliza: “Tufanyie nini Sanduku la Yehova? Mutuambie namna tunapaswa kulirudisha mahali pake.” 3  Wakajibu: “Kama munarudisha sanduku la agano la Yehova, Mungu wa Israeli, musilirudishe bila toleo. Musikose kulirudisha kwake pamoja na toleo la hatia.+ Ni kwa kufanya vile tu ndio mutaponyeshwa, na mutajulishwa sababu gani mukono wake haujatoka juu yenu.” 4  Kwa hiyo wakauliza: “Tunapaswa kumutumia toleo gani la hatia?” Wakasema: “Kulingana na hesabu ya mabwana wa Wafilisti,+ mutume emoroide* tano (5) za zahabu na panya tano wa zahabu, kwa maana kila mumoja wenu pamoja na mabwana wenu wamepatwa na pigo lilelile. 5  Munapaswa kutengeneza sanamu za emoroide* zenu na sanamu za panya wenu+ wenye wanaharibu inchi, na munapaswa kumuheshimia Mungu wa Israeli. Pengine atapunguza uzito wa mukono wake wenye uko juu yenu na juu ya mungu wenu na juu ya inchi yenu.+ 6  Sababu gani mufanye moyo wenu kuwa mugumu kama vile Misri na Farao walifanya mioyo yao kuwa migumu?+ Wakati Yeye aliwatendea kwa ukali,+ walilazimika kuruhusu Israeli waende, nao wakaondoka.+ 7  Sasa mutayarishe gari la mupya la kukokotwa na ngombe wawili wenye wako na vitoto-dume na wenye hawajakuwa hata siku moja chini ya nira. Kisha mufungie ngombe hao kwenye gari hilo, lakini murudishe vitoto-dume hivyo nyumbani, mbali na ngombe hao. 8  Muchukue Sanduku la Yehova na kulitia juu ya gari hilo, na mutie ndani ya sanduku lingine pembeni yake vitu vya zahabu vyenye munamutumia kuwa toleo la hatia.+ Kisha mulitume 9  na muangalie: Kama linapanda kwenye barabara yenye inaelekea Bet-shemeshi,+ kwenye eneo lake, basi yeye ndiye ametutendea uovu huu mukubwa. Lakini kama halipande kule, tutajua kwamba haiko mukono wake ndio ulitupiga; ni jambo lenye lilitokea tu.” 10  Watu hao wakafanya vile. Wakachukua ngombe wawili wenye kuwa na vitoto-dume na wakawafungia kwenye gari hilo, na vitoto-dume vya ngombe hao wakavifungia nyumbani ndani ya zizi.* 11  Kisha wakatia Sanduku la Yehova juu ya gari hilo, pamoja na sanduku lenye panya wa zahabu na sanamu za emoroide* zao. 12  Na ngombe hao wakaenda moja kwa moja kwenye barabara yenye inaelekea Bet-shemeshi.+ Walibakia kwenye barabara hiyo kubwa, na walikuwa wanalia wakati walikuwa wanaenda; hawakugeukia kuume wala kushoto. Wakati huo wote mabwana wa Wafilisti walikuwa wanatembea nyuma yao kufikia kwenye mupaka wa Bet-shemeshi. 13  Watu wa Bet-shemeshi walikuwa wanavuna mavuno ya ngano katika bonde tambarare.* Wakati waliinua macho yao na kuona lile Sanduku, wakashangilia sana kuliona. 14  Gari hilo likafika kwenye shamba la Yoshua Mubet-shemeshi na likasimama pale karibu na jiwe kubwa. Kwa hiyo wakapasua mbao za gari hilo, na wakatoa ngombe hao+ kuwa toleo la kuteketezwa kwa Yehova. 15  Walawi+ wakashusha Sanduku la Yehova na sanduku lenye lilikuwa pamoja nalo, lenye ndani yake mulikuwa vile vitu vya zahabu, na wakavitia juu ya lile jiwe kubwa. Watu wa Bet-shemeshi+ wakamutolea Yehova matoleo ya kuteketezwa na kumufanyia zabihu siku hiyo. 16  Wakati mabwana tano (5) wa Wafilisti waliona hayo, wakarudia Ekroni siku hiyo. 17  Basi hizi ndizo emoroide* za zahabu zenye Wafilisti walimutumia Yehova kuwa toleo la hatia:+ moja kwa ajili ya Ashdodi,+ moja kwa ajili ya Gaza, moja kwa ajili ya Ashkeloni, moja kwa ajili ya Gati,+ moja kwa ajili ya Ekroni.+ 18  Na hesabu ya panya wa zahabu ililingana na hesabu ya miji yote ya Wafilisti yenye ilikuwa ya mabwana tano (5)⁠—​miji yenye ngome na vijiji vya eneo la mashamba. Na jiwe kubwa lenye waliweka Sanduku la Yehova juu yake ni ushahidi mupaka leo katika shamba la Yoshua Mubet-shemeshi. 19  Lakini Mungu akapiga na kuua watu wa Bet-shemeshi, kwa sababu walikuwa wameangalia Sanduku la Yehova. Alipiga na kuua elfu makumi tano na makumi saba (50 070)* kati ya watu, na watu wakaanza kuomboleza kwa sababu Yehova alikuwa amewapiga na kuwaua kwa mauaji makubwa.+ 20  Kwa hiyo watu wa Bet-shemeshi wakauliza: “Ni nani ataweza kusimama mbele ya Yehova, huyu Mungu mutakatifu,+ na ataenda kwa nani wakati atatoka kwetu?”+ 21  Kwa hiyo wakatuma wajumbe kwa wakaaji wa Kiriat-yearimu,+ na kusema: “Wafilisti wamerudisha Sanduku la Yehova. Mushuke na kupanda nalo.”+

Maelezo ya Chini

Ao “bawasiri.”
Ao “bawasiri.”
Zizi ni lupango ya kuchungia wanyama.
Ao “bawasiri.”
Ao “eneo tambarare la chini.”
Ao “bawasiri.”
Tnn., “watu 70, watu 50 000.”