Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maana ya Maneno ya Biblia

A B C D E F G H I J K L M N O P R S T U V W Y Z

A

  • Abi.

    Jina la mwezi wa 5 katika kalendari takatifu ya Wayahudi kisha kutoka katika uhamisho wa Babiloni na jina la mwezi wa 11 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 7 mupaka katikati ya Mwezi wa 8 wa kalendari yetu. Jina la mwezi huo halitajwe katika Biblia; unatajwa tu kuwa “mwezi wa tano (5).” (Hes 33:38; Ezr 7:9)​—Angalia Nyongeza B15.

  • Abibu.

    Jina la kwanza-kwanza la mwezi wa 1 katika kalendari takatifu ya Wayahudi na mwezi wa 7 katika kalendari ya watu wote. Jina hilo maana yake ni “Masuke ya Mubichi (ya Nafaka)” na mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 3 mupaka katikati ya Mwezi wa 4 wa kalendari yetu. Kisha Wayahudi kurudia kutoka katika uhamisho, mwezi huo uliitwa Nisani. (Kum 16:1)​—Angalia Nyongeza B15.

  • Abiso.

    Neno hili linatokana na neno la Kigiriki aʹbys·sos, lenye maana yake ni “-refu sana kuenda chini” ao “bila mwisho, bila mipaka.” Linatumiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ili kumaanisha mahali ao hali ya kuwa katika kifungo. Linamaanisha pia kaburi lakini liko na maana pana zaidi.​—Lu 8:31; Ro 10:7; Ufu 20:3.

  • Adari.

    Jina la mwezi wa 12 katika kalendari takatifu ya Wayahudi kisha kutoka katika uhamisho wa Babiloni na jina la mwezi wa 6 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 2 mupaka katikati ya Mwezi wa 3 wa kalendari yetu. (Est 3:7)​—Angalia Nyongeza B15.

  • Agano.

    Mapatano mazito, ao makubaliano, kati ya Mungu na wanadamu ao kati ya wanadamu wawili ili kufanya ao kutokufanya jambo fulani. Nyakati fulani ni upande mumoja tu ndio ulikuwa na daraka la kutimiza masharti ya agano hilo (agano la upande mumoja, lenye kwa kawaida lilikuwa ahadi). Nyakati zingine pande zote mbili zilipaswa kutimiza masharti ya agano hilo (agano la pande mbili). Zaidi ya maagano yenye Mungu alifanya pamoja na wanadamu, Biblia inataja pia maagano kati ya wanadamu, makabila, mataifa, ao vikundi vya watu. Kati ya maagano yenye yamekuwa na matokeo makubwa sana kuko agano lenye Mungu alifanya pamoja na Abrahamu, Daudi, taifa la Israeli (agano la Sheria), na Israeli wa Mungu (agano jipya).​—Mwa 9:11; 15:18; 21:27; Kut 24:7; 2Ny 21:7.

  • Akaya.

    Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, Akaya ni jimbo la Roma lenye lilikuwa kusini mwa Ugiriki, na muji wake mukubwa ulikuwa Korinto. Jimbo la Akaya lilitia ndani eneo lote la Peloponesi na eneo la kati la kontinenti katika inchi ya Ugiriki. (Mdo 18:12)​—Angalia Nyongeza B13.

  • Alabasta..

    Jina la chupa za kidogo za marashi zenye zamani zilitengenezwa kwa jiwe lenye lilipatikana karibu na Alabastroni, Misri. Kwa kawaida chupa hizo zilitengenezwa zikiwa na shingo nyembamba yenye ingeweza kufungwa ili kuzuia marashi hayo yenye samani yasivuye. Jiwe hilo pia lilifikia kujulikana kwa jina hilo.​—Mk 14:3.

  • Alama.

    Kitu, tendo, hali, ao tukio lenye haliko la kawaida lenye liko na maana na lenye linaonyesha jambo lingine la sasa ao lenye litatokea.​—Mwa 9:12, 13; 2Fa 20:9; Mt 24:3; Ufu 1:1.

  • Alamoti.

    Neno la kimuziki lenye kumaanisha “Vijana wanamuke,” pengine linarejelea sauti za juu (soprano) za vijana wanamuke. Inawezekana lilitumiwa ili kuonyesha kwamba muziki ulipaswa kuimbwa kwa sauti ya juu ao chombo cha muziki kilipaswa kuchezwa kwa sauti ya juu.​—1Ny 15:20; Zb 46:Uta.

  • Alfa na Omega.

    Ni majina ya herufi ya kwanza na herufi ya mwisho katika alfabeti ya Kigiriki; yanatumiwa pamoja mara tatu katika kitabu cha Ufunuo ili kuzungumuzia cheo cha Mungu. Katika Maandiko hayo, maneno hayo yako na maana moja na “wa kwanza na wa mwisho” na “mwanzo na mwisho.”​—Ufu 1:8; 21:6; 22:13.

  • Amina.

    “Ikuwe vile,” ao “bila shaka.” Neno hili linatokana na muzizi wa Kiebrania ʼa·manʹ, wenye kumaanisha “kuwa muaminifu, kuwa mwenye kutumainika.” Neno “Amina” lilisemwa ili kukubali kiapo, sala, ao maneno fulani. Katika Ufunuo, linatumiwa likiwa cheo cha Yesu.​—Kum 27:26; 1Ny 16:36; Ufu 3:14.

  • Andiko (Maandiko).

    Maandishi matakatifu ya Neno la Mungu. Neno hilo linapatikana tu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.​—Lu 24:27; 2Ti 3:16.

  • Aramu; Waaramu.

    Wazao wa Aramu mwana wa Shemu wenye waliishi zaidi sana katika maeneo kuanzia Milima ya Lebanoni mupaka Mesopotamia na kuanzia Milima ya Taurusi upande wa kaskazini na kushuka mupaka Damasko na mbali zaidi upande wa kusini. Eneo hilo, lenye linaitwa Aramu katika Kiebrania, kisha wakati fulani liliitwa Siria, na wakaaji wake waliitwa Wasiria.​—Mwa 25:20; Kum 26:5; Ho 12:12.

  • Areopago.

    Kilima kirefu chenye kuwa katika muji wa Atene, upande wa kaskazini-mangaribi wa Akropoli. Lilikuwa pia jina la baraza ao tribinali yenye ilifanyia mikutano kule. Wanafilozofia Wastoa na Waepikurea walimuleta Paulo Areopago ili afasirie mambo yenye aliamini.​—Mdo 17:19.

  • Armagedoni..

    Neno hili linatokana na neno la Kiebrania Har Meghid·dohnʹ, lenye kumaanisha “Mulima wa Megido.” Neno hilo linatumiwa kuhusiana na “vita ya ile siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote” wakati “wafalme wa dunia yote yenye kuikaliwa na watu” watakusanyika ili kupigana vita na Yehova. (Ufu 16:14, 16; 19:11-​21)​—Angalia TAABU KUBWA.

  • Aselgeia.​

    Angalia MWENENDO MUPOTOVU WA BILA HAYA.

  • Ashtoreti.

    Mungu mwanamuke wa Wakanaani, wa vita na uzazi, bibi ya Baali.​—1Sa 7:3.

  • Asia.

    Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, Asia ni jina la jimbo la Roma lenye lilitia ndani eneo lenye sasa ni sehemu ya mangaribi ya inchi ya Uturuki (Turquie), na pia visiwa fulani vya pembeni ya bahari, kama vile Samosi na Patmo. Muji mukubwa ulikuwa Efeso. (Mdo 20:16; Ufu 1:4)​—Angalia Nyongeza B13.

  • Azazeli.

    Jina la Kiebrania lenye pengine linamaanisha “Mbuzi Mwenye Anapotea.” Katika Siku ya Kufunika Zambi, mbuzi mwenye alichaguliwa kwa ajili ya Azazeli alipelekwa na kuachiliwa katika jangwa, na hivyo kwa njia ya mufano alibeba zambi za taifa za mwaka wenye ulipita.​—Law 16:8, 10.

B

  • Baali.

    Mungu wa Wakanaani mwenye alionwa kuwa mwenye anga na mwenye kupatia watu mvua na uzazi. Neno “Baali” lilitumiwa pia ili kutaja miungu mingine midogo. Katika Kiebrania neno hilo linamaanisha “Mumiliki; Bwana.”​—1Fa 18:21; Ro 11:4.

  • Bati.

    Kipimo cha vitu vya majimaji chenye kinakadiriwa kuwa sawa na litre 22 hivi (galoni 5.81), kulingana na uvumbuzi wa vipande vya zamani vya mutungi vyenye vilikuwa na jina hilo. Katika Biblia, vipimo vingine vingi vya vitu vyenye kukauka na vya vitu vya majimaji vinahesabiwa kulingana na ukubwa wa kipimo cha bati. (1Fa 7:38; Eze 45:14)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Beelzebubu.

    Jina hilo linatumiwa ili kumutaja Shetani, ambaye ni mukubwa, ao mutawala, wa pepo wachafu. Pengine ni jina lenye limebadilishwa kidogo la Baal-zebubu, Baali mwenye aliabudiwa na Wafilisti kule Ekroni.​—2Fa 1:3; Mt 12:24.

  • Bei ya ukombozi.

    Bei yenye inalipwa ili kuachilia mutu huru kutokana na utekwa, azabu, mateso, zambi, ao hata jambo fulani lenye aliombwa kufanya. Bei hiyo haikulipwa sikuzote kwa feza tu. (Isa 43:3) Bei ya ukombozi ilihitaji kulipwa kwa ajili ya hali mbalimbali. Kwa mufano, wazaliwa wote wa kwanza wanaume ao wanyama-dume katika Israeli walikuwa wa Yehova, na bei ya ukombozi, ilihitaji kulipwa ili wasilazimike kufanya tu utumishi wa Yehova. (Hes 3:45, 46; 18:15, 16) Kama ngombe-dume hatari mwenye kuachiliwa aliua mutu, mwenye ngombe-dume huyo aliombwa kulipa bei ya ukombozi ili kumuweka huru kutokana na azabu ya kifo yenye alistahili. (Kut 21:29, 30) Hata hivyo, hakuna bei ya ukombozi yenye ilikubaliwa kwa ajili ya muuaji wa kukusudia. (Hes 35:31) Jambo la maana zaidi, Biblia inakazia bei ya ukombozi yenye Kristo alilipa kupitia kifo chake cha kujitoa ili kuweka huru wanadamu watiifu kutoka katika zambi na kifo.​—Zb 49:7, 8; Mt 20:28; Efe 1:7.

  • Bonde la muto.

    Bonde ao sehemu ya chini ya muto mudogo yenye kwa kawaida inakauka isipokuwa katika kipindi cha mvua; neno hilo linaweza pia kumaanisha muto mudogo wenyewe. Mito fulani midogo haikukauka kwa sababu maji yake yalitoka katika chemchemi. Katika habari fulani maneno “bonde la muto” yanaitwa tu “bonde.”​—Mwa 26:19; Hes 34:5; Kum 8:7; 1Fa 18:5; Yob 6:15.

  • Buli.

    Jina la mwezi wa 8 katika kalendari takatifu ya Wayahudi na jina la mwezi wa pili katika kalendari ya watu wote. Jina hilo linatokana na muzizi wenye kumaanisha “tokeza mazao; zaa” na mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 10 mupaka katikati ya Mwezi wa 11 wa kalendari yetu. (1Fa 6:38)​—Angalia Nyongeza B15.

C

  • Chachu.

    Kitu chenye kiliongezwa kwenye donge (unga wenye kuchanganywa na maji) ao kwenye vitu vya majimaji ili kuvifanya vichache; zaidi sana donge lenye lilichachishwa lenye lilikuwa limewekwa. Mara nyingi chachu inatumiwa katika Biblia ili kufananisha zambi na upotovu, inatumiwa pia ili kuonyesha ukuzi wenye unaenea bila kuonekana.​—Kut 12:20; Mt 13:33; Gal 5:9.

  • Chakula cha Mangaribi cha Bwana.

    Chakula cha mikate yenye haina chachu na pia divai, vitu vyenye vinafananisha mwili wa Kristo na damu yake; na vyenye kuwa ukumbusho wa kifo cha Yesu. Kwa kuwa huu ni mwazimisho wenye Maandiko yanasema Wakristo wanapaswa kufanya, kwa kufaa unaitwa pia “Ukumbusho.”​—1Ko 11:20, 23-​26.

  • Chombo cha kusukia nguo.

    Kitu chenye kilitumiwa ili kusuka nyuzi kuwa nguo.​—Kut 39:27.

  • Chupa ya ngozi ya kuwekea divai.

    Chupa ya ngozi yenye ilitengenezwa kwa ngozi ya munyama, kama vile mbuzi ao kondoo, na ilitumiwa ili kuwekea divai. Divai iliwekwa katika chupa za mupya za divai, kwa sababu wakati divai inachacha, inatokeza gaze ya diokside ya karbone yenye kutokeza mukazo mukubwa ndani ya chupa hizo za ngozi. Ngozi za mupya zinapanuka; ngozi ngumu zenye kuzeeka zinapasuka wakati mukazo huo unaongezeka.​—Yos 9:4; Mt 9:17.

D

  • Dagoni.

    Mungu wa Wafilisti. Asili ya neno hilo haijulikane muzuri, lakini watu fulani wenye elimu wanalihusianisha na neno la Kiebrania dagh (samaki).​—Amu 16:23; 1Sa 5:4.

  • Dariki.

    Feza ya kichele ya zahabu ya Waajemi yenye uzito wa grame 8.4 (aunsi troi 0.27). (1Ny 29:7)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Dekapoli.

    Kikundi cha miji ya Kigiriki, yenye zamani ilikuwa miji kumi. Neno hilo linatokana na neno la Kigiriki deʹka, lenye kumaanisha “kumi,” na poʹlis, lenye kumaanisha “muji.” Pia lilikuwa jina la eneo la upande wa mashariki wa Bahari ya Galilaya na Muto Yordani, kwenye miji mingi kati ya hiyo ilikuwa. Miji hiyo ilikuwa mahali pa desturi ya Wagiriki na biashara. Yesu alipitia katika eneo hilo, lakini hakuna maandishi yoyote yenye kuonyesha kama alitembelea moja ya miji hiyo. (Mt 4:25; Mk 5:20)​—Angalia Nyongeza A7 na B10.

  • Dinari.

    Feza ya kichele ya Kiroma yenye ilikuwa na uzito wa grame 3.85 hivi (aunsi troi 0.124) na ilikuwa na picha ya Kaisari upande mumoja. Dinari ilikuwa mushahara wa siku moja wa mufanyakazi na feza ya kichele ya ‘kodi yenye kila mutu alipaswa kulipa’ yenye Waroma walilipisha Wayahudi. (Mt 22:17; Lu 20:24)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Drakma.

    Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno hili linamaanisha feza ya kichele ya Kigiriki, yenye wakati huo ilikuwa na uzito wa grame 3.4 (aunsi troi 0.109). Maandiko ya Kiebrania yanataja feza ya kichele ya drakma ya zahabu ya wakati wa Waajemi yenye inalinganishwa na dariki. (Ne 7:70; Mt 17:24)​—Angalia Nyongeza B14.

E

  • Edomu.

    Jina lingine lenye Esau, mwana wa Isaka, alipewa. Wazao wa Esau (Edomu) walikamata eneo la Seiri, eneo lenye milima kati ya Bahari ya Chumvi na Guba ya ‘Aqaba. Kisha wakati fulani liliitwa Edomu. (Mwa 25:30; 36:8)​—Angalia Nyongeza B3 na B4.

  • Efa.

    Kipimo cha vitu vyenye kukauka na pia chombo chenye kilitumiwa ili kupimia nafaka. Kilikuwa sawa na kipimo cha bati cha vitu vya majimaji, kwa hiyo kilikuwa sawa na litre 22 (vibaba 20). (Kut 16:36; Eze 45:10)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Efodi.

    Nguo yenye kufanana na aproni (tablier) yenye makuhani walivaa. Kuhani mukubwa alivaa efodi ya pekee, na kwenye upande wa mbele wa efodi hiyo kulikuwa kifuko cha kifua chenye kilikuwa na majiwe 12 yenye samani. (Kut 28:4, 6)​—Angalia Nyongeza B5.

  • Efraimu.

    Jina la mwana wa pili wa Yosefu; kisha wakati fulani kabila moja kati ya makabila ya Israeli liliitwa kwa jina hilo. Kisha Israeli kugawanyika, Efraimu, lenye lilikuwa kabila lenye kujulikana zaidi, lilifananisha ufalme wote wa makabila kumi.​—Mwa 41:52; Yer 7:15.

  • Efrati.

    Muto murefu zaidi na wa maana zaidi kusini-mangaribi mwa Asia, na ni moja kati ya mito mbili mikubwa katika Mesopotamia. Unatajwa kwa mara ya kwanza katika Mwanzo 2:14 ukiwa moja kati ya mito ine ya Edeni. Kwa kawaida unaitwa “ule Muto.” (Mwa 31:21) Ulikuwa mupaka wa kaskazini wa eneo lenye Waisraeli walipewa. (Mwa 15:18; Ufu 16:12)​—Angalia Nyongeza B2.

  • Eluli.

    Jina la mwezi wa 6 katika kalendari takatifu ya Wayahudi kisha kutoka katika uhamisho wa Babiloni na jina la mwezi wa 12 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 8 mupaka katikati ya Mwezi wa 9 wa kalendari yetu. (Ne 6:15)​—Angalia Nyongeza B15.

  • Enye haiko safi.

    Usemi huo unaweza kumaanisha kuwa muchafu kimwili ao kuvunja sheria za mwenendo muzuri. Hata hivyo, katika Biblia mara nyingi neno hilo linamaanisha kitu chenye hakikubaliwe, ao chenye hakiko safi, kulingana na Sheria ya Musa. (Law 5:2; 13:45; Mt 10:1; Mdo 10:14; Efe 5:5)​—Angalia SAFI.

  • Enye haina chachu.

    Maneno haya yanatumiwa kuhusu mikate yenye kutengenezwa bila chachu.​—Kum 16:3; Mk 14:12; 1Ko 5:8.

  • Etanimu.

    Jina la mwezi wa 7 katika kalendari takatifu ya Wayahudi na jina la mwezi wa 1 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 9 mupaka katikati ya Mwezi wa 10 wa kalendari yetu. Kisha Wayahudi kurudia kutoka Babiloni, uliitwa Tishri. (1Fa 8:2)​—Angalia Nyongeza B15.

  • Etiopia.

    Taifa la zamani upande wa kusini wa Misri. Lilitia ndani sehemu ya mbali zaidi kusini mwa inchi ya sasa ya Misri na nusu ya upande wa kaskazini wa inchi yenye inaitwa sasa Sudani. Jina hilo linatumiwa nyakati fulani pa nafasi ya jina “Kushi” la Kiebrania.​—Est 1:1.

F

  • Fanya kosa; Kosa.

    Kukosa kufuata sheria yenye iliwekwa; tendo la kukosa kufuata sheria. Katika Biblia, neno “kosa” liko na maana ileile na “zambi.”​—Zb 51:3; Ro 5:14.

  • Farao.

    Jina la cheo lenye wafalme wa Misri walipewa. Mafarao watano wanatajwa kwa majina katika Biblia (Shishaki, So, Tirhaka, Neko, na Hofra), lakini wengine majina yao hayatajwe, kutia ndani wale wenye walikuwa na shuguli nyingi na Abrahamu, Musa, na Yosefu.​—Kut 15:4; Ro 9:17.

  • Fazili zenye hazistahiliwe.

    Maneno haya yametafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki lenye wazo lake kubwa ni kile chenye kukubalika na chenye kupendeza. Mara nyingi maneno hayo yanatumiwa ili kutaja zawadi yenye kutolewa kwa fazili ao kutoa kwa fazili. Wakati yanataja fazili za Mungu zenye hazistahiliwe, maneno hayo yanamaanisha zawadi ya bure yenye Mungu anatoa kwa ukarimu, bila kungojea kulipwa kitu fulani. Kwa hiyo, ni maneno yenye kuonyesha namna Mungu anatoa kwa wingi sana na pia upendo wake mwingi na fazili zake nyingi sana kuelekea wanadamu. Neno la Kigiriki linatafsiriwa pia kwa maneno kama vile “kukubaliwa,” “wema,” “rehema” na “zawadi ya fazili.” Ni zawadi yenye mutu anapewa bila kuifanyia kazi na yenye hastahili; mutoaji anaitoa akichochewa tu na ukarimu wake.​—2Ko 6:1; Efe 1:7.

  • Fimbo ya ufalme.

    Fimbo yenye ilibebwa na mutawala kama alama ya mamlaka ya kifalme.​—Mwa 49:10; Ebr 1:8.

G

  • Gari.

    Gari lenye magurudumu mbili lenye lilikokotwa na farasi na lilitumiwa zaidi sana katika vita.​—Kut 14:23; Amu 4:13; Mdo 8:28.

  • Gavana wa jimbo.

    Gavana mukubwa wa jimbo lenye lilikuwa chini ya usimamizi wa Baraza la Roma. Alikuwa na mamlaka ya kuhukumu na ya kijeshi, na hata kama Baraza la Roma lilikuwa na haki ya kuchunguza matendo yake, alikuwa na mamlaka makubwa katika jimbo.​—Mdo 13:7; 18:12.

  • Gehena.

    Neno la Kigiriki lenye kumaanisha Bonde la Hinomu, lenye lilikuwa upande wa kusini-mangaribi wa muji wa zamani wa Yerusalemu. (Yer 7:31) Neno hilo lilitumiwa kwa njia ya unabii ili kuzungumuzia mahali maiti zingesambazwa. (Yer 7:32; 19:6) Hakuna uhakikisho kwamba wanyama ao wanadamu walitupwa katika Gehena ili wateswe ao kuunguzwa wakiwa wazima. Kwa hiyo mahali pale hapangeweza kufananisha mahali kwenye hakuonekane kwenye nafsi za wanadamu zinateswa milele katika moto wa kwelikweli. Lakini, Yesu na wanafunzi wake walitumia neno “Gehena” ili kufananisha azabu ya milele ya “kifo cha pili,” ni kusema, uharibifu wa milele, kuangamia milele.​—Ufu 20:14; Mt 5:22; 10:28.

  • Gera.

    Uzito wenye ulikuwa sawa na grame 0.57 (aunsi troi 0.01835). Gera moja ilikuwa sehemu moja ya makumi mbili (1/20) ya shekeli. (Law 27:25)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Gileadi.

    Neno hilo linamaanisha zaidi sana eneo lenye mbolea la upande wa mashariki wa Muto Yordani, na lilifika upande wa kaskazini na upande wa kusini wa Bonde la Yaboki. Nyakati fulani neno hilo lilitumiwa ili kuzungumuzia eneo lote la Waisraeli la upande wa mashariki wa Yordani, kwenye kabila la Rubeni, kabila la Gadi, na nusu ya kabila la Manase waliishi. (Hes 32:1; Yos 12:2; 2Fa 10:33)​—Angalia Nyongeza B4.

  • Gititi.

    Neno la kimuziki lenye maana yake haijulikane muzuri, hata kama inaonekana kwamba linatokana na neno la Kiebrania gath. Watu fulani wanaamini kama pengine ni sauti ya muziki yenye inahusiana na nyimbo zenye ziliimbwa wakati wa kutengeneza divai, kwa sababu neno gath linamaanisha kikamulio cha divai.​—Zb 81:Uta.

H

  • Habari njema.

    Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, maneno hayo yanamaanisha habari njema ya Ufalme wa Mungu na ya wokovu wenye unategemea imani katika Yesu Kristo.​—Lu 4:18, 43; Mdo 5:42; Ufu 14:6.

  • Hadesi.

    Neno la Kigiriki lenye maana moja na neno la Kiebrania “Sheoli.” Linatafsiriwa “Kaburi” (kwa herufi kubwa), ili kuonyesha kwamba ni kaburi la wanadamu wote.​—Angalia KABURI.

  • Haki.

    Katika Maandiko, ni mambo yenye kuwa sawa kulingana na viwango vya Mungu vya mema na mabaya.​—Mwa 15:6; Kum 6:25; Mez 11:4; Sef 2:3; Mt 6:33.

  • Hekalu.

    Jengo la kudumu katika Yerusalemu lenye lilikuwa mahali pa maana pa ibada ya Waisraeli lenye lilichukua nafasi ya tabenakulo yenye ilikuwa inabebwa. Hekalu la kwanza lilijengwa na Sulemani na liliharibiwa na Wababiloni. Hekalu la pili lilijengwa na Zerubabeli kisha Wayahudi kutoka katika uhamisho Babiloni na kisha lilijengwa upya na Herode Mukubwa. Katika Maandiko, kwa kawaida hekalu linaitwa “nyumba ya Yehova.” (Ezr 1:3; 6:14, 15; 1Ny 29:1; 2Ny 2:4; Mt 24:1)​—Angalia Nyongeza B8 na B11.

  • Hema ya mukutano.

    Maneno hayo yanatumiwa ili kutaja hema ya Musa na pia hema takatifu ya ibada yenye pale mwanzo ilijengwa katika jangwa.​—Kut 33:7; 39:32.

  • Herme.

    Mungu wa Ugiriki, mwana wa Zeu. Kule Listra, watu walimuita Paulo kimakosa Herme kwa sababu waliwaza kama mungu huyo alikuwa mujumbe wa miungu na mungu wa ufundi wa kuongea.​—Mdo 14:12.

  • Herode.

    Jina la watawala wa familia moja wenye walitawala Wayahudi, wenye waliwekwa na Roma. Herode Mukubwa alijulikana kwa kujenga upya hekalu la Yerusalemu na kuagiza watoto wachinjwe ili kutafuta kumuua Yesu. (Mt 2:16; Lu 1:5) Herode Arkelao na Herode Antipa, wana wa Herode Mukubwa, waliwekwa ili kusimamia sehemu fulani za eneo la utawala wa baba yao. (Mt 2:22) Antipa alikuwa kiongozi wa wilaya, na alijulikana kuwa “mufalme,” mwenye alitawala wakati wa utumishi wa Kristo wa miaka tatu na nusu kufikia kipindi chenye kuzungumuziwa katika Matendo sura 12. (Mk 6:14-​17; Lu 3:1, 19, 20; 13:31, 32; 23:6-15; Mdo 4:27; 13:1) Kisha, malaika wa Mungu alimuua Herode Agripa wa Kwanza, mujukuu wa Herode Mukubwa, kisha kutawala kwa wakati kidogo. (Mdo 12:1-6, 18-23) Mwana wake, Herode Agripa wa Pili, akakuwa mutawala na alitawala mupaka wakati Wayahudi waliasi Roma.​—Mdo 23:35; 25:13, 22-​27; 26:1, 2, 19-​32.

  • Herode, wafuasi wa chama cha.

    Wanajulikana pia kuwa Waherode. Walikuwa wanachama wenye kupenda sana taifa lao, waliunga mukono mipango ya kisiasa ya watawala wa familia ya Herode wenye walitawala chini ya uongozi wa Waroma. Inawezekana wamoja kati ya Wasadukayo walikuwa wafuasi wa chama hicho. Waherode walijiunga na Wafarisayo ili kumupinga Yesu.​—Mk 3:6.

  • Higayoni.

    Neno la kitaalamu la kuongozea muziki. Katika Zaburi 9:16, neno hilo linaweza kumaanisha muziki muzito na wa sauti ya chini wa kinubi ao pumuziko nzito lenye kufanya mutu afikiri sana.

  • Hini.

    Ni kipimo cha vitu vya majimaji na pia chombo cha kupimia hini. Ilikuwa sawa na litre 3.67 (painti 7.75) kulingana na maelezo ya mwanahistoria Yosefo mwenye alisema kama hini ilikuwa sawa na koe mbili za Waatene. (Kut 29:40)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Hisopo.

    Mumea wenye matawi na majani ya muzuri, wenye ulitumiwa ili kunyunyiza damu ao maji kwenye sherehe za kutakasa. Pengine ulikuwa mumea wa marjoramu (Origanum maru; Origanum syriacum). Katika Yohana 19:29, inawezekana ulikuwa mumea wa marjoramu wenye kufungiwa kwenye tawi ao mumea wa dura, aina fulani ya mutama wa kawaida (Sorghum vulgare), kwa sababu pengine mumea huo ulikuwa na kijiti kirefu vya kutosha ili kubeba sponji ya divai kali na kuifikisha kwenye kinywa cha Yesu.​—Kut 12:22; Zb 51:7.

  • Homeri.

    Kipimo cha vitu vyenye kukauka chenye kuwa sawa na kori. Kilikuwa sawa na litre 220 (vibaba 200), kulingana na ukubwa wenye ulikadiriwa wa kipimo cha bati. (Law 27:16)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Horebu; Mulima Horebu.

    Eneo lenye milima kuzunguka Mulima Sinai. Jina lingine la Mulima Sinai. (Kut 3:1; Kum 5:2)​—Angalia Nyongeza B3.

I

  • Ibilisi.

    Jina lenye kutoa maelezo juu ya Shetani katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, lenye linamaanisha “Muchongezi.” Shetani alipewa jina Ibilisi kwa sababu yeye ndiye muchongezi mukubwa na wa kwanza kabisa na mushitaki wa uongo wa Yehova, neno Lake la muzuri, na jina Lake takatifu.​—Mt 4:1; Yoh 8:44; Ufu 12:9.

  • Ilirikamu.

    Jimbo la Roma la upande wa kaskazini-mangaribi wa Ugiriki. Paulo alisafiri mupaka kule wakati wa utumishi wake, lakini Biblia haiseme ikiwa alihubiri Ilirikamu ao alifika tu karibu na jimbo hilo. (Ro 15:19)​—Angalia Nyongeza B13.

  • Israeli.

    Jina lenye Mungu alimupatia Yakobo. Kisha wakati fulani lilitumiwa ili kutaja wazao wake wote kwa ujumla, katika kipindi chochote. Mara nyingi, wazao wa wana 12 wa Yakobo waliitwa wana wa Israeli, nyumba ya Israeli, watu (wanaume) wa Israeli, ao Waisraeli. Pia, jina Israeli lilitumiwa ili kumaanisha ufalme wa kaskazini wa makabila 10 wenye ulitengana na ufalme wa kusini, na kisha wakati fulani lilitumiwa ili kumaanisha Wakristo watiwa-mafuta, “Israeli wa Mungu.”​—Gal 6:16; Mwa 32:28; 2Sa 7:23; Ro 9:6.

J

  • Jiwe la kusagia.

    Jiwe la muviringo lenye liliwekwa juu ya jiwe lingine lenye lilifanana nalo na lilitumiwa ili kusaga nafaka ao mbegu ikuwe unga. Kipande cha muti chenye kilitiwa katikati ya jiwe la chini kilisaidia kuzungusha jiwe la juu. Katika nyakati za Biblia, majiwe ya mukono ya kusagia yalitumiwa na wanamuke katika nyumba nyingi. Kwa kuwa familia ilitegemea jiwe la mukono la kusagia ili kupata mukate wa kila siku, Sheria ya Musa ilikataza kunyanganya mutu jiwe la chini la kusagia ao jiwe la juu ili likuwe kitu chenye kinawekeshwa kwa ajili ya mukopo. Majiwe makubwa zaidi ya kusagia yenye muundo uleule yalizungushwa na wanyama.​—Kum 24:6; Mk 9:42.

  • Jiwe la pembe.

    Jiwe lenye linawekwa kwenye pembe, ao kona, ya jengo mahali kuta mbili zinakutana, lilikuwa la maana sana ili kuunganisha na kufunga kuta pamoja. Jiwe la musingi la pembe ndilo lilikuwa jiwe kubwa la pembe; kwa kawaida jiwe ngumu lilichaguliwa kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya watu wote na kuta za muji. Neno hilo linatumiwa kwa njia ya mufano ili kuzungumuzia kuwekwa kwa musingi wa dunia, na Yesu anatajwa kuwa “jiwe la musingi la pembe” la kutaniko la Kikristo, lenye linafananishwa na nyumba ya kiroho.​—Efe 2:20; Yob 38:6.

K

  • Kabi.

    Kipimo cha vitu vyenye kukauka cha litre 1.22 (vibaba 1.11), kulingana na ukubwa wenye ulikadiriwa wa kipimo cha bati. (2Fa 6:25)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Kaburi.

    Wakati neno hili linaanza na herufi ya kidogo, linamaanisha kaburi lenye mutu anazikwa ndani; wakati linaanza na herufi ya mukubwa, linamaanisha kaburi la wanadamu wote, lenye katika Kiebrania ni “Sheoli” na katika Kigiriki “Hadesi.” Katika Biblia, linaelezwa kuwa mahali pa mufano ao hali yenye ndani yake mutu hawezi kutenda jambo lolote na yenye ndani yake fahamu zake zote zinaisha.​—Mwa 47:30; Muh 9:10; Mdo 2:31.

  • Kaburi la ukumbusho.

    Mahali pa kuzikia kwenye ndani yake mutu mwenye alikufa aliwekwa. Neno hili linatafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki mne·meiʹon, lenye linatokana na tendo “kukumbusha,” na linaonyesha kwamba mutu mwenye amekufa anakumbukwa.​—Yoh 5:28, 29.

  • Kahaba.

    Mutu mwenye kufanya ngono inje ya kifungo cha ndoa, zaidi sana ili apate feza. (Neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “kahaba,” porʹne, linatokana na muzizi wenye kumaanisha “kuuzisha.”) Mara nyingi neno hilo linatumiwa juu ya mwanamuke, hata kama wanaume makahaba wanatajwa pia katika Biblia. Sheria ya Musa ilikataza ukahaba, na malipo ya kahaba hayakukubaliwa kutolewa kuwa muchango wa mahali patakatifu pa Yehova, tofauti kabisa na tabia ya wapagani ya kutumia makahaba wa hekalu kuwa njia ya kupata feza. (Kum 23:17, 18; 1Fa 14:24) Biblia inatumia pia neno hilo kwa njia ya mufano, ili kuzungumuzia watu, mataifa, ao matengenezo yenye kuhusika katika aina fulani ya ibada ya sanamu na wakati uleule yanasema kuwa yanaabudu Mungu. Kwa mufano, muungano wa kidini wenye kuitwa “Babiloni Mukubwa” unaonyeshwa katika kitabu cha Ufunuo kuwa kahaba kwa sababu umekuwa na uhusiano na watawala wa ulimwengu huu ili kupata mamlaka na utajiri.​—Ufu 17:1-5; 18:3; 1Ny 5:25.

  • Kaisari.

    Jina la familia ya Kiroma lenye lilikuja kuwa jina la cheo la watawala wa Waroma. Biblia inataja Augusto, Tiberio, na Klaudio kwa jina, na hata kama haimutaje Nero kwa jina, yeye pia alikuwa Kaisari. Jina “Kaisari” linatumiwa pia katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ili kufananisha mamlaka za kiraia, ao Serikali.​—Mk 12:17; Mdo 25:12.

  • Kanaani.

    Mujukuu wa Noa, na mwana wa ine wa Hamu. Makabila 11 yenye yalitokana na Kanaani mwishowe yaliishi katika eneo la mashariki pembeni-pembeni ya Mediterania kati ya Misri na Siria. Eneo hilo liliitwa “inchi ya Kanaani.” (Law 18:3; Mwa 9:18; Mdo 13:19)​—Angalia Nyongeza B4.

  • Kemoshi.

    Mungu mukubwa wa Wamoabu.​—1Fa 11:33.

  • Kiapo.

    Maneno ya kuapa ili kuhakikisha kwamba jambo fulani ni la kweli, ao ahadi nzito ya kwamba mutu atafanya ao hatafanya jambo fulani. Mara nyingi ni naziri yenye kutolewa kwa mutu mwenye mamlaka, zaidi sana kwa Mungu. Yehova alifanya agano lake pamoja na Abrahamu likuwe imara kupitia kiapo.​—Mwa 14:22; Ebr 6:16, 17.

  • Kiaramu.

    Luga ya Kisemiti yenye inakaribiana sana na Kiebrania, yenye inatumia alfabeti ya Kiebrania. Kwanza ilizungumuzwa na Waaramu lakini kisha wakati fulani ikakuwa luga ya kimataifa ya biashara na ya kupashana habari katika utawala wa Ashuru na utawala wa Babiloni. Pia ilikuwa luga ya serikali katika Utawala wa Uajemi. (Ezr 4:7) Sehemu fulani za kitabu cha Ezra, Yeremia, na Danieli ziliandikwa katika Kiaramu.​—Ezr 4:8–​6:18; 7:12-​26; Yer 10:11; Da 2:4b–​7:28.

  • Kida.

    Kitu chenye kinatokana na ganda la muti wa kida (Cinnamomum cassia), wenye uko katika familia moja na muti wa mudalasini. Kida ilitumiwa kama marashi na ilikuwa moja ya viungo vya mafuta matakatifu ya kutia mafuta.​—Kut 30:24; Zb 45:8; Eze 27:19.

  • Kifuko cha kifua.

    Kifuko chenye kilipambwa kwa majiwe yenye samani chenye kilivaliwa na kuhani mukubwa wa Israeli kwenye moyo wake wakati wowote aliingia katika Patakatifu. Kiliitwa “kifuko cha kifua cha hukumu” kwa sababu kilikuwa na Urimu na Tumimu, vitu vyenye vilitumiwa ili kufunua hukumu za Yehova. (Kut 28:15-30)​—Angalia Nyongeza B5.

  • Kifuniko cha kufunika zambi.

    Kifuniko cha sanduku la agano, mbele yake kuhani mukubwa alinyunyiza damu ya matoleo ya zambi Siku ya Kufunika Zambi. Neno la Kiebrania linatokana na kitenzi (verbe) chenye kumaanisha “kufunika (zambi)” ao pengine “kufuta (zambi).” Kifuniko hicho kilitengenezwa kwa zahabu, kilikuwa na makerubi wawili, kila mumoja akiwa kwenye mwisho mumoja. Wakati fulani kinaitwa tu “kifuniko.” (Kut 25:17-​22; 1Ny 28:11; Ebr 9:5)​—Angalia Nyongeza B5.

  • Kifuniko cha nguzo.

    Kilikuwa kifuniko chenye kupamba chenye kilikuwa juu ya nguzo. Vifuniko vikubwa vya nguzo vilikuwa juu ya nguzo mbili zenye ziliitwa Yakini na Boazi zenye zilisimama upande wa mbele wa hekalu la Sulemani. (1Fa 7:16)​—Angalia Nyongeza B8.

  • Kigiriki, Mugiriki.

    Kigiriki ni luga yenye inazungumuzwa na watu wa Ugiriki. Mugiriki ni mwenyeji wa Ugiriki ao mutu mwenye asili ya familia yake ni Ugiriki. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno “Mugiriki” liko na maana pana, linamaanisha watu wote wenye hawako Wayahudi ao watu wenye walianza kutumia luga na desturi za Ugiriki.​—Yoe 3:6; Yoh 12:20.

  • Kikamulio cha divai.

    Kwa kawaida kikamulio hicho kilitengenezwa kwa kuchimba mashimo mbili katika jiwe la chokaa, shimo moja lilikuwa juu kuliko lingine, na mashimo hayo yaliunganishwa kwa mufereji mudogo. Wakati zabibu zilipondwa katika shimo la juu, umajimaji wa zabibu ulitiririka katika shimo la chini. Maneno hayo yanatumiwa kwa njia ya mufano ili kutaja hukumu ya Mungu.​—Isa 5:2; Ufu 19:15.

  • Kilemba.

    Kitambaa chenye kilivaliwa kwa kuzungushwa kwenye kichwa. Kuhani mukubwa alivaa kilemba cha kitani kizuri, chenye kilikuwa na bamba la zahabu lenye lilifungwa upande wa mbele kwa uzi ya bluu. Mufalme alivaa kilemba ndani ya taji lake. Yobu alitumia neno hilo kwa njia ya mufano wakati alifananisha haki yake na kilemba.​—Kut 28:36, 37; Yob 29:14; Eze 21:26.

  • Kilima.

    Sehemu ya kijiografia ao sehemu yenye ilijengwa katika Muji wa Daudi. Pengine kilima hicho kilikuwa kuta za kutegemeza zenye matuta ao kitu cha kutegemeza cha aina ingine.​—2Sa 5:9; 1Fa 11:27.

  • Kiongozi.

    Wakati linatumiwa katika Zaburi, inaonekana neno hilo katika Kiebrania linamaanisha mutu mwenye kwa njia fulani alitunga nyimbo na kuongoza uimbaji wa nyimbo hizo, alifundisha na kuzoeza waimbaji Walawi, na hata aliongoza waimbaji kwenye matukio ya pekee. Tafsiri zingine zinatafsiri neno hilo kuwa “mwimbaji mukubwa” ao “kiongozi wa muziki.”​—Zb 4:Uta; 5:Uta.

  • Kiongozi Mukubwa.

    Jina la cheo “Kiongozi Mukubwa” linaonyesha daraka la maana la Yesu Kristo la kuweka huru wanadamu waaminifu kutoka katika matokeo ya mubaya ya zambi na kuwaongoza kwenye uzima wa milele.​—Mdo 3:15; 5:31; Ebr 2:10; 12:2.

  • Kislevu.

    Jina la mwezi wa 9 katika kalendari takatifu ya Wayahudi kisha kutoka katika uhamisho wa Babiloni na jina la mwezi wa 3 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 11 mupaka katikati ya Mwezi wa 12 wa kalendari yetu. (Ne 1:1; Zek 7:1)​—Angalia Nyongeza B15.

  • Kitabu cha kukunjwa.

    Ukurasa murefu wa ngozi ao mafunjo (papyrus), wenye ulikuwa na maandishi upande mumoja, wenye kwa ukawaida ulikunjwa kwenye kipande cha muti. Maandiko yaliandikwa na kufanyiwa kopi kwenye vitabu vya kukunjwa, ni hivyo vilikuwa vitabu vyenye vilitumiwa wakati Biblia ilikuwa inaandikwa.​—Yer 36:4, 18, 23; Lu 4:17-​20; 2Ti 4:13.

  • Kitabu cha ngozi.

    Ngozi ya kondoo, ya mbuzi, ao ya kitoto cha ngombe yenye ilitayarishwa ili itumiwe kama kitu cha kuandikia. Ilikuwa ya kudumu kuliko mafunjo na ilitumiwa ili kutengeneza vitabu vya kukunjwa vya Biblia. Pengine vitabu vya ngozi vyenye Paulo aliomba Timoteo amuletee vilikuwa sehemu fulani za Maandiko ya Kiebrania. Vitabu fulani vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi vilikuwa vya ngozi.​—2Ti 4:13.

  • Kiti cha hukumu.

    Kwa kawaida lilikuwa jukwaa lenye kuinuliwa lenye lilikuwa inje; lenye mutu angefikia kwa kupanda ngazi, na maofisa wenye walikaa kwenye jukwaa hilo walizungumuza na vikundi vya watu na kutangaza maamuzi yao. Maneno “kiti cha hukumu cha Mungu” na “kiti cha hukumu cha Kristo” ni maneno ya mufano yenye kumaanisha mupango wa Yehova wa kuhukumu wanadamu.​—Ro 14:10; 2Ko 5:10; Yoh 19:13.

  • Kitu chenye kinawekeshwa kwa ajili ya mukopo.

    Kitu chenye mutu mwenye kuwa na deni alimupatia ule mwenye alimukopesha ili kikuwe uhakikisho wa kwamba atalipa deni. Kiliitwa pia rehani. Sheria ya Musa ilikuwa na maagizo kuhusu vitu vyenye vinawekeshwa kwa ajili ya mukopo ili kulinda faida za maskini na watu wazaifu wa taifa.​—Kut 22:26; Eze 18:7.

  • Kiwanja.

    Eneo lenye lilikuwa wazi kuzunguka tabenakulo na lenye lilikuwa na lupango; kisha wakati fulani kiwanja hicho kilimaanisha moja la maeneo yenye kuta yenye yalikuwa wazi kuzunguka jengo kubwa la hekalu. Mazabahu ya toleo la kuteketezwa ilikuwa katika kiwanja cha tabenakulo na katika kiwanja cha ndani cha hekalu. (Angalia Nyongeza B5, B8, B11.) Biblia inataja pia viwanja wakati inazungumuzia nyumba za watu na nyumba za wafalme.​—Kut 8:13; 27:9; 1Fa 7:12; Est 4:11; Mt 26:3.

  • Komamanga.

    Tunda lenye kufanana na tofaa, lenye kuwa na ua ao taji kwenye mwisho mumoja. Ndani ya ganda lake ngumu muko punje nyingi za kidogo zenye kujaa umajimaji, na kila punje iko na mbegu ya kidogo ya rangi ya waridi ao nyekundu. Mapambo yenye umbo ya komamanga yalipamba sehemu ya chini ya koti yenye haina mikono ya bluu ya kuhani mukubwa na pia vifuniko vya nguzo zenye ziliitwa Yakini na Boazi zenye zilikuwa mbele ya hekalu.​—Kut 28:34; Hes 13:23; 1Fa 7:18.

  • Kombeo.

    Kamba ya ngozi ao kamba yenye kusukwa kwa mishipa ya wanyama, matete, ao manyoya. Kwa kawaida kitu chenye kilipaswa kutupwa, zaidi sana jiwe, kiliwekwa katika sehemu pana ya katikati. Mwisho mumoja wa kombeo ulifungwa kwenye mukono ao kwenye kiganja cha mukono, na mwisho mwingine ulishikwa katika mukono na kuachiliwa wakati kombeo ilizungushwa. Mataifa ya zamani yalitumia wapiga-kombeo katika majeshi yao.​—Amu 20:16; 1Sa 17:50.

  • Kori.

    Kipimo cha vitu vyenye kukauka na vya majimaji. Kilikuwa sawa na litre 220 (galoni 58.1 ao vibaba 200), kulingana na ukubwa wenye ulikadiriwa wa kipimo cha bati. (1Fa 5:11)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Kristo.

    Jina la cheo la Yesu lenye linatokana na neno la Kigiriki Khri·stosʹ, lenye liko sawa na neno la Kiebrania lenye linatafsiriwa “Masiya,” ao “Mutiwa-Mafuta.”​—Mt 1:16; Yoh 1:41.

  • Kufunga.

    Kujizuia kula vyakula vya aina yote kwa kipindi fulani. Waisraeli walifunga katika Siku ya Kufunika Zambi, nyakati za taabu, na wakati walihitaji muongozo wa Mungu. Wayahudi walikuwa na pindi ine za kufunga kila mwaka ili kukumbuka matukio ya mubaya katika historia yao. Wakristo hawaombwe kufunga.​—Ezr 8:21; Isa 58:6; Lu 18:12.

  • Kufunika zambi.

    Katika Maandiko ya Kiebrania, tendo hilo lilihusiana na zabihu zenye zilitolewa ili kuwezesha watu wamukaribie Mungu na kumuabudu. Chini ya Sheria ya Musa, zabihu zilitolewa, zaidi sana katika Siku ya kila mwaka ya Kufunika Zambi, ili watu waweze kupatanishwa na Mungu ijapokuwa zambi za mutu mumoja-mumoja na za taifa lote. Zabihu hizo zilifananisha zabihu ya Yesu, yenye ilifunika kabisa zambi za wanadamu mara moja kwa wakati wote, na hivyo kupatia wanadamu nafasi ya kupatanishwa na Yehova.​—Law 5:10; 23:28; Kol 1:20; Ebr 9:12.

  • Kuhani.

    Mwanaume mwenye alipewa mamlaka ya kuwakilisha Mungu kwa watu wenye alitumikia, na aliwafundisha juu ya Mungu na sheria zake. Pia, makuhani waliwakilisha watu mbele ya Mungu, wakitoa zabihu na pia kutetea na kuombea watu musamaha. Mbele Sheria ya Musa iwekwe, kichwa cha familia alitumika akiwa kuhani wa familia yake. Chini ya Sheria ya Musa, wanaume wa familia ya Haruni katika kabila la Lawi walikuwa makuhani. Wanaume wengine Walawi walikuwa wasaidizi wao. Wakati agano jipya lilianzishwa, taifa la kiroho la Israeli likakuwa taifa la makuhani, Yesu Kristo akiwa Kuhani Mukubwa.​—Kut 28:41; Ebr 9:24; Ufu 5:10.

  • Kuhani mukubwa.

    Chini ya Sheria ya Musa, alikuwa kuhani mwenye cheo cha juu mwenye aliwakilisha watu mbele ya Mungu na kusimamia makuhani wengine. Anaitwa pia “mukubwa wa makuhani.” (2Ny 26:20; Ezr 7:5) Yeye tu ndiye aliruhusiwa kuingia Patakatifu Zaidi, chumba cha ndani zaidi cha tabenakulo na kisha wakati fulani alikuwa anaingia katika chumba cha ndani zaidi cha hekalu. Alifanya vile wakati tu wa Siku ya kila mwaka ya Kufunika Zambi. Maneno “kuhani mukubwa” yanatumiwa pia kumuhusu Yesu Kristo.​—Law 16:2, 17; 21:10; Mt 26:3; Ebr 4:14.

  • Kuokota masalio.

    Ni tendo la kukusanya mazao yoyote yenye wavunaji waliacha nyuma kimakusudi ao bila kukusudia. Sheria ya Musa iliagiza watu wasivune mavuno yote ya mipaka ya mashamba yao na wasikamate zeituni zote ao zabibu zote. Mungu alipatia maskini, mutu mwenye kuteseka, mukaaji mugeni, mutoto mwenye hakukuwa na baba, na mujane haki ya kuokota masalio yoyote kisha mavuno.​—Rut 2:7.

  • Kupashana habari na pepo wachafu.

    Imani ya kwamba roho za wanadamu wenye wamekufa zinaendelea kuishi kisha mwili kufa na kwamba zinaweza kupashana habari na watu wenye kuishi, zaidi sana kupitia mutu (mutu mwenye kupashana habari na pepo wachafu) mwenye anaweza kutumiwa na pepo hizo. Neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “kupashana habari na pepo wachafu” ni phar·ma·kiʹa, lenye kumaanisha “kutumia dawa za kulewesha.” Neno hilo limefikia kuhusianishwa na tendo la kupashana habari na pepo wachafu kwa sababu zamani, dawa za kulewesha zilitumiwa wakati wa kuomba nguvu za pepo wachafu ili kufanya ulozi.​—Gal 5:20; Ufu 21:8.

  • Kupiga-piga nafaka; Kiwanja cha kupigia-pigia nafaka.

    Kazi ya kuondoa nafaka kwenye shina lake na katika maganda yake; kazi hiyo ilifanywa kwenye kiwanja cha kupigia-pigia nafaka. Kupiga-piga nafaka kulifanywa kwa mukono kwa kutumia fimbo, ao ikiwa ni kiasi kikubwa zaidi, iliomba kutumia vyombo vya pekee, kama vile vifaa vya kupiga-piga nafaka ao magurudumu ya kupiga-piga nafaka yenye yalikokotwa na wanyama. Vifaa hivyo vilipitishwa juu ya nafaka yenye ilianikwa kwenye kiwanja cha kupigia-pigia nafaka, eneo tambarare la muviringo lenye kwa kawaida lilikuwa sehemu yenye kuinuka yenye ilipigwa na upepo.​—Law 26:5; Isa 41:15; Mt 3:12.

  • Kura.

    Majiwe ya kidogo ya muviringo ao vipande vya kidogo vya mbao vyenye vilitumiwa ili kufanya maamuzi. Vitu hivyo vilitiwa katika mikunjo ya nguo ao katika chombo na kutikiswa. Kura yenye ilianguka inje ao kutoka mule ndiyo ilichaguliwa. Mara nyingi sala zilitolewa wakati wa kupiga kura. Neno “kura” linatumiwa katika maana yake ya kwanza na katika maana ya mufano ili kumaanisha “sehemu” ao “fungu.”​—Yos 14:2; Zb 16:5; Met 16:33; Mt 27:35.

  • Kutahiriwa.

    Tendo la kuondoa govi ao ngozi yenye kufunika sehemu ya mbele ya kiungo cha uzazi cha mwanaume. Abrahamu na wazao wake waliombwa watahiriwe, lakini Wakristo hawaombwe watahiriwe. Neno hilo linatumiwa kwa njia ya mufano katika maandiko mbalimbali.​—Mwa 17:10; 1Ko 7:19; Flp 3:3.

  • Kutaniko.

    Kikundi cha watu wenye kukusanyika pamoja kwa ajili ya kusudi ao kazi fulani ya pekee. Katika Maandiko ya Kiebrania, kwa ujumla neno hilo linamaanisha taifa la Israeli. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, linamaanisha kutaniko mojamoja la Wakristo lakini mara nyingi linamaanisha kutaniko la Kikristo kwa ujumla.​—1Fa 8:22; Mdo 9:31; Ro 16:5.

  • Kuvu.

    Ni moja kati ya magonjwa mengi ya mimea yenye kutokana na viyoga. Imesemwa kwamba ugonjwa wa kuvu wenye unatajwa katika Biblia ni kutu nyeusi (Puccinia graminis).​—1Fa 8:37.

  • Kuwapo.

    Katika habari fulani za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno hili linaonyesha kuwapo kwa Yesu Kristo akiwa mufalme kuanzia wakati aliwekwa kuwa Mufalme wa Kimasiya bila kuonekana na kuendelea mupaka katika siku za mwisho za mupangilio huu wa mambo. Kuwapo kwa Kristo haiko tukio la kuja na kisha kuondoka haraka; lakini, kunadumu kwa kipindi cha wakati chenye kiliwekwa.​—Mt 24:3.

  • Kuweka mikono juu ya.

    Mikono iliwekwa juu ya mutu ili kumuweka katika kazi ya pekee ao kumuchagua apate baraka, uponyaji, ao zawadi ya roho takatifu. Nyakati zingine mikono iliwekwa juu ya wanyama mbele watolewe kuwa zabihu.​—Kut 29:15; Hes 27:18; Mdo 19:6; 1Ti 5:22.

  • Kuwekwa pembeni kwa ajili ya kusudi la pekee, alama takatifu ya.

    Bamba lenye kungaa la zahabu safi lenye juu yake kulichongwa maneno haya katika Kiebrania: “Utakatifu ni wa Yehova.” Liliwekwa upande wa mbele wa kilemba cha kuhani mukubwa. (Kut 39:30)​—Angalia Nyongeza B5.

L

  • Laana.

    Kuogopesha ao kutakia mutu ao kitu uovu. Neno hilo liko tofauti na maneno ya kutukana ao kasirani kali. Kwa kawaida laana ni tangazo la kiapo ao la kutabiria mutu ao kitu uovu, na wakati laana hiyo inasemwa na Mungu ao na mutu mwenye amepewa mamlaka inakuwa na uzito na nguvu kama unabii.​—Mwa 12:3; Hes 22:12; Gal 3:10.

  • Lawi; Mulawi.

    Mwana wa tatu wa Yakobo mwenye alizaliwa na bibi yake Lea; pia ni jina la kabila lenye liliitwa kwa jina lake. Wana watatu wa Lawi walianzisha vikundi vikubwa tatu vya Walawi. Nyakati zingine, neno “Walawi” linamaanisha kabila lote, lakini kwa kawaida halihusu familia ya kikuhani ya Haruni. Kabila la Lawi halikupewa sehemu ya udongo katika Inchi ya Ahadi lakini lilipewa miji 48 katika mipaka ya inchi yenye makabila mengine yaligawiwa.​—Kum 10:8; 1Ny 6:1; Ebr 7:11.

  • Leptoni.

    Katika kipindi cha Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, leptoni ilikuwa feza ya kichele ya kidogo zaidi ya Kiyahudi ya shaba ao shaba nyekundu. Tafsiri fulani za Biblia zinaiita “senti kidogo.” (Mk 12:42; Lu 21:2; maelezo ya chini.)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Leviatani.

    Ni munyama fulani mwenye kwa kawaida inasemekana kama anakaa katika maji. Katika Yobu 3:8 na 41:1, inaonekana ni mamba ao munyama mwingine mwenye kukaa ndani ya maji mwenye kuwa mukubwa sana na mwenye nguvu nyingi. Katika Zaburi 104:26, pengine ni aina fulani ya nyangumi. Katika Maandiko mengine neno hilo linatumiwa kwa njia ya mufano na halihusiane na munyama fulani yeyote.​—Zb 74:14; Isa 27:1.

  • Liwali.

    Mwakilishi wa mufalme, ao gavana wa jimbo, katika utawala wa Babiloni na wa Uajemi. Liwali aliwekwa na mufalme kuwa mutawala mukubwa.​—Ezr 8:36; Da 6:1.

  • Logi.

    Kipimo kidogo zaidi cha vitu vya majimaji chenye kutajwa katika Biblia. Talmudi ya Wayahudi inasema kama logi ni 1/12 ya hini, basi kwa musingi huo, logi ingekuwa sawa na litre 0.31 (painti 0.66). (Law 14:10)​—Angalia Nyongeza B14.

M

  • Mafunjo.

    Mumea wenye kuota katika maji wenye kufanana na matete na ulitumiwa ili kutengeneza vitu kama vile vitunga, vyombo, na mashua. Ulitumiwa pia ili kutengeneza vitu vya kuandikia vyenye kufanana na karatasi na ulitumiwa katika vitabu vingi vya kukunjwa.​—Kut 2:3.

  • Maganda ya mbegu.

    Maganda yenye yanatenganishwa na sehemu yenye inakuliwa ya mbegu wakati wa kupiga-piga na kupepua nafaka. Maganda ya mbegu yanatumiwa katika maneno ya mufano ili kufananisha kitu chenye hakina mafaa yoyote ao chenye hakitamanike.​—Zb 1:4; Mt 3:12.

  • Mahalati.

    Ni wazi kwamba neno hili ni la kimuziki, na linapatikana katika utangulizi wa Zaburi ya 53 na ya 88. Pengine linahusiana na kitenzi (verbe) cha Kiebrania chenye kumaanisha “kuwa muzaifu; kuwa mugonjwa,” na kwa hiyo kitenzi hicho kinaonyesha sauti ya huzuni, yenye inapatana na mambo ya kuhuzunisha yenye kutajwa katika nyimbo hizo mbili.

  • Mahali pa juu.

    Kwa kawaida ni mahali pa ibada kwenye kulikuwa juu ya kilima, mulima, ao jukwaa lenye lilitengenezwa na watu. Hata kama nyakati fulani watu walitumia mahali pa juu kumuabudia Mungu, mara nyingi kunahusianishwa na ibada ya kipagani ya miungu ya uongo.​—Hes 33:52; 1Fa 3:2; Yer 19:5.

  • Maili.

    Kipimo cha umbali chenye kutajwa mara moja tu katika maandishi ya kwanza ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kwenye Matayo 5:41, pengine kipimo hicho kinamaanisha maili ya Kiroma yenye ilikuwa sawa na metre 1479.5 (futi 4854). Maandiko mengine tatu (3) yenye kutaja “maili,” ni kusema, Luka 24:13, Yohana 6:19, na Yohana 11:18 yanazungumuzia kipimo chenye kilikubalika cha maili chenye kilipatikana kwa kubadilisha kipimo cha zamani cha stadia chenye kutajwa katika maandishi ya kwanza.​—Angalia Nyongeza B14.

  • Makedonia.

    Eneo lenye kuwa upande wa kaskazini wa Ugiriki lenye lilikuja kujulikana sana wakati wa Aleksanda Mukubwa na liliendelea kuwa huru mupaka wakati Waroma walilishinda. Makedonia ilikuwa jimbo la Roma wakati mutume Paulo alitembelea Ulaya kwa mara ya kwanza. Paulo alitembelea eneo hilo mara tatu. (Mdo 16:9)​—Angalia Nyongeza B13.

  • Makerubi.

    Malaika wa cheo cha juu wenye migao ya pekee. Wako tofauti na maserafi.​—Mwa 3:24; Kut 25:20; Isa 37:16; Ebr 9:5.

  • Malaika.

    Linatokana na neno la Kiebrania mal·ʼakhʹ na neno la Kigiriki agʹge·los. Maana ya kwanza ya maneno hayo mbili ni “mujumbe” lakini yanatafsiriwa kuwa “malaika” wakati yanazungumuzia wajumbe wenye miili ya roho. (Mwa 16:7; 32:3; Yak 2:25; Ufu 22:8) Malaika ni viumbe vya roho vyenye nguvu, vyenye Mungu aliumba mbele ya kuumba wanadamu. Katika Biblia wanaitwa pia “makumi ya maelfu ya watakatifu,” “wana wa Mungu,” na “nyota za asubui.” (Kum 33:2; Yob 1:6; 38:7) Hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kuzaa malaika wengine lakini waliumbwa mumoja mumoja. Hesabu yao inapita milioni mia moja. (Da 7:10) Biblia inaonyesha kama kila malaika iko na jina lake na utu wake, lakini wanakataa kwa unyenyekevu kuabudiwa, na wengi hata wanakataa kufunua majina yao. (Mwa 32:29; Lu 1:26; Ufu 22:8, 9) Wako na vyeo tofauti-tofauti na wamepewa madaraka mbalimbali, kama vile kutumikia mbele ya kiti cha Ufalme cha Yehova, kupeleka ujumbe wake mbalimbali, kusaidia watumishi wa Yehova wenye kuwa katika dunia, kutimiza hukumu za Mungu, na kuunga mukono kazi ya kuhubiri habari njema. (2Fa 19:35; Zb 34:7; Lu 1:30, 31; Ufu 5:11; 14:6) Wakati wenye kuja watamusaidia Yesu kupigana vita ya Armagedoni.​—Ufu 19:14, 15.

  • Malaika mukubwa.

    Maana yake “mukubwa wa malaika.” Maana hiyo, pamoja na ukweli wa kwamba Biblia inatumia tu hali ya umoja ili kutaja “malaika mukubwa,” inaonyesha kwamba kuko malaika mukubwa mumoja tu. Biblia inataja jina la huyo malaika mukubwa, inamutambulisha kuwa Mikaeli.​—Da 12:1; Yud 9; Ufu 12:7.

  • Malkamu.

    Pengine ni sawa na neno Moleki, mungu mukubwa wa Waamoni. (Sef 1:5)​—Angalia MOLEKI.

  • Malkia wa Mbinguni.

    Jina la cheo la mungu mwanamuke mwenye aliabudiwa na Waisraeli waasi-imani katika siku za Yeremia. Watu fulani wanasema kama ni jina la mungu mwanamuke wa Babiloni mwenye kuitwa Ishtari (Astarte). Jina la mungu mwanamuke wa Wasumeri wa zamani, Inanna, linamaanisha “Malkia wa Mbinguni.” Zaidi ya kuhusianishwa na mbingu, alikuwa pia mungu mwanamuke wa uzazi. Astarte anaitwa pia “Malkia wa Mbinguni” katika maandishi yenye yalichongwa na Wamisri.​—Yer 44:19.

  • Mana.

    Chakula cha maana chenye Waisraeli walikula kwa miaka 40 katika jangwa. Yehova ndiye aliwatolea chakula hicho. Kilitokea kwa muujiza kwenye udongo chini juu ya umande kila asubui isipokuwa siku ya Sabato. Wakati Waisraeli walikiona kwa mara ya kwanza, walisema, “Hii ni nini?” ao, katika Kiebrania, “man huʼ?” (Kut 16:13-​15, 35) Katika Maandiko mengine, kinaitwa “nafaka ya mbinguni” (Zb 78:24), “mukate kutoka mbinguni” (Zb 105:40), na “mukate wa wenye nguvu” (Zb 78:25). Yesu pia alizungumuzia mana kwa njia ya mufano.​—Yoh 6:49, 50.

  • Manemane.

    Umajimaji wenye kunata wenye harufu ya muzuri ambao unatokana na miti mbalimbali midogo-midogo ya miiba ao miti midogo-midogo ya jamii ya Commiphora. Manemane ni moja kati ya vitu vyenye vilitumiwa ili kutengeneza mafuta matakatifu ya kutia mafuta. Ilitumiwa ili kutia harufu ya muzuri kwenye nguo ao vitanda, na iliongezwa kwenye mafuta yenye yalitumiwa ili kufinyanga mwili na kwenye mafuta ya kujipakaa. Manemane pia ilitumiwa ili kutayarisha miili mbele ya kuizika.​—Kut 30:23; Mez 7:17; Yoh 19:39.

  • Maombolezo.

    Huzuni yenye inaonyeshwa waziwazi kwa sababu ya kifo ao musiba mwingine. Katika nyakati za Biblia, ilikuwa desturi kuomboleza kwa wakati fulani. Zaidi ya kulia kwa sauti kubwa, waombolezaji walivaa nguo za pekee, walitia majivu juu ya vichwa vyao, walipasua nguo zao, na kujipiga-piga kifua. Nyakati zingine waombolezaji wa kulipwa walialikwa kwenye kilio.​—Mwa 23:2; Est 4:3; Ufu 21:4.

  • Marijani.

    Kitu kigumu chenye kufanana na jiwe chenye kinafanyizwa na mifupa ya wanyama wadogo wa bahari. Kinapatikana katika bahari kikiwa na rangi mbalimbali, kama vile nyekundu, nyeupe, na nyeusi. Marijani yalikuwa mengi sana zaidi sana katika Bahari Nyekundu. Katika nyakati za Biblia, marijani yenye rangi nyekundu yalikuwa na bei kubwa sana na yalitumiwa ili kutengeneza shanga na mapambo mengine.​—Mez 8:11.

  • Maserafi.

    Viumbe vya roho vyenye kusimama kuzunguka kiti cha ufalme cha Yehova mbinguni. Neno la Kiebrania sera·phimʹ linamaanisha “wenye kuwaka moto.”​—Isa 6:2, 6.

  • Masiya.

    Neno hili linatokana na neno la Kiebrania lenye kumaanisha “mutiwa-mafuta” ao “mwenye alitiwa mafuta.” Katika Kigiriki neno hili linatafsiriwa “Kristo.”​—Da 9:25; Yoh 1:41.

  • Maskili.

    Ni neno la Kiebrania lenye kupatikana katika mautangulizi ya zaburi 13 lenye maana yake haijulikane muzuri. Pengine linamaanisha “shairi la kufikiri sana.” Watu fulani wanafikiri kama neno lenye kuwa sawa na hilo, lenye kutafsiriwa ‘kutumikia kwa busara,’ linaweza kuwa na maana sawa na neno hilo.​—2Ny 30:22; Zb 32:Uta.

  • Matayarisho.

    Jina la siku yenye ilitangulia Sabato, yenye ilitumiwa na Wayahudi kufanya matayarisho yenye yalihitajiwa. Siku hiyo ilifikia mwisho wakati jua lilishuka siku yenye inaitwa leo Siku ya Tano, ni wakati huo ndio Sabato ilianza. Siku ya Wayahudi ilianza mangaribi na ilimalizika mangaribi yenye ilifuata.​—Mk 15:42; Lu 23:54.

  • Matunda ya kwanza.

    Mazao ya kwanza kabisa katika kipindi cha mavuno; kitu chenye kinapatikana kwanza ao malimbuko ya kitu chochote. Yehova aliomba taifa la Israeli limutolee matunda ya kwanza ao muzaliwa wa kwanza wa mwanadamu, munyama, ao mazao ya kwanza ya inchi. Wakiwa taifa, Waisraeli walimutolea Mungu matunda ya kwanza wakati wa Sikukuu ya Mikate Yenye Haina Chachu na wakati wa Pentekoste. Usemi “matunda ya kwanza” ulitumiwa pia kwa njia ya mufano ili kuzungumuzia Kristo na wafuasi wake watiwa-mafuta.​—1Ko 15:23; Hes 15:21; Mez 3:9; Ufu 14:4.

  • Mazabahu.

    Sehemu yenye kuinuliwa ao jukwaa yenye ilitengenezwa kwa udongo, majiwe, majiwe yenye kuchongwa, ao mbao zenye kufunikwa kwa metali; zabihu ao uvumba vilitolewa juu yake wakati wa ibada. Katika chumba cha kwanza cha tabenakulo na cha hekalu, kulikuwa ‘mazabahu ya kidogo ya zahabu’ ya kutolea uvumba. Ilitengenezwa kwa mbao zenye zilifunikwa kwa zahabu. ‘Mazabahu kubwa zaidi ya shaba’ yenye ilitumiwa kutolea zabihu za kuteketezwa ilikuwa inje katika kiwanja. (Kut 27:1; 39:38, 39; Mwa 8:20; 1Fa 6:20; 2Ny 4:1; Lu 1:11)​—Angalia Nyongeza B5 na B8.

  • Merodaki.

    Mungu mukubwa wa muji wa Babiloni. Kisha mufalme wa Babiloni na mutunga-sheria Hamurabi kufanya Babiloni kuwa muji mukubwa wa Babilonia, Merodaki (ao, Marduki) alifikia kuwa wa maana sana, na mwishowe akakamata nafasi ya miungu mingi ya zamani na akakuwa mungu mukubwa wa miungu ya Wababiloni. Kisha wakati fulani, jina la cheo “Belu” (“Mumiliki”) lilianza kutumiwa pa nafasi ya Merodaki (ao, Marduki), na kwa kawaida watu walimuita Merodaki kwa jina Beli.​—Yer 50:2.

  • Mezali.

    Usemi wa hekima ao hadisi fupi yenye kufundisha somo ao yenye kueleza ukweli wa maana kwa kutumia maneno ya kidogo sana. Mezali ya Biblia inaweza kuwa fumbo ao kitendawili. Mezali inatoa ukweli kwa kutumia luga yenye kuvutia, mara nyingi kupitia mifano. Masemi fulani yalianza kutumiwa sana kama maneno ya kuchekelea ao kuzarau watu fulani.​—Muh 12:9; 2Pe 2:22.

  • Miji ya makimbilio.

    Miji ya Walawi kwenye mutu mwenye aliua mutu bila kukusudia angeweza kukimbilia ili asiuawe na mulipiza-kisasi cha damu. Miji sita ya makimbilio, yenye ilienea katika Inchi ya Ahadi, ilichaguliwa na Musa na kisha wakati fulani na Yoshua, chini ya muongozo wa Yehova. Wakati tu alifika katika muji wa makimbilio, mutu mwenye alikimbilia kule aliambia wazee wenye walikuwa katika mulango mukubwa wa muji huo jambo lake, kisha walimukaribisha muzuri. Ili kuzuia watu wenye waliwaua wengine kimakusudi wasitumie mubaya mupango huo, mutu mwenye alitafuta kimbilio alipaswa kusambishwa katika muji kwenye mauaji yalifanyika ili aonyeshe kama hakuua kimakusudi. Kama ilionekana kwamba hakuua kimakusudi, alirudishwa katika muji wa makimbilio, na alipaswa kuishi ndani ya mipaka ya muji huo maisha yake yote ao mupaka kifo cha kuhani mukubwa.​—Hes 35:6, 11-​15, 22-29; Yos 20:2-8.

  • Mikatale.

    Kifaa chenye kutumiwa kufunga mutu ili kumupatia azabu. Mikatale fulani ilifunga miguu tu, na mingine ilipinda mwili kwa njia yenye kuchokesha, pengine kwa kufunga miguu, mikono, na shingo.​—Yer 20:2; Mdo 16:24.

  • Mikate ya toleo.​

    Angalia MIKATE YA WONYESHO.

  • Mikate ya wonyesho.

    Mikate kumi na mbili yenye ilipangwa katika mistari mbili ya mikate sita kila mustari na iliwekwa kwenye meza katika chumba cha Patakatifu cha tabenakulo na cha hekalu. Inaitwa pia “mikate yenye kupangwa moja juu ya ingine” na “mikate ya toleo.” Kwenye kila Sabato, mikate hiyo yenye ilitolewa kwa Mungu ilibadilishwa na mikate ya mupya. Kwa kawaida mikate yenye iliondolewa ilikuliwa na makuhani tu. (2Ny 2:4; Mt 12:4; Kut 25:30; Law 24:5-9; Ebr 9:2)​—Angalia Nyongeza B5.

  • Miktamu.

    Neno la Kiebrania lenye kutumiwa katika mautangulizi sita ya zaburi (Zb 16, 56-​60). Ni neno la kitaalamu lenye maana yake haijulikane muzuri, hata kama pengine linahusiana na neno “maandishi.”

  • Milkomu.

    Mungu mwenye aliabudiwa na Waamoni, pengine ndiye mungu mwenye anaitwa Moleki. (1Fa 11:5, 7) Wakati Sulemani alikaribia mwisho wa utawala wake, alijengea mungu huyu wa uongo mahali pa juu.​—Angalia MOLEKI.

  • Mina.

    Inaitwa pia mane katika kitabu cha Ezekieli. Ni kipimo cha uzito chenye kilitumika pia kama feza. Kwa kutegemea vitu vya zamani vyenye vilivumbuliwa katika udongo, mina ilikuwa sawa na shekeli 50, na shekeli ilikuwa na uzito wa grame 11.4, katika Maandiko ya Kiebrania mina ilikuwa na uzito wa grame 570 (aunsi troi 18.35). Inawezekana pia kulikuwa mina ya kifalme, kama vile kulikuwa kipimo cha kifalme cha mukono. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, mina ilikuwa sawa na drakma 100. Ilikuwa na uzito wa grame 340 (aunsi troi 10.9). Mina 60 zilikuwa sawa na talanta moja. (Ezr 2:69; Lu 19:13)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Mistari ya Nguzo za Sulemani.

    Katika hekalu katika siku za Yesu, mistari hiyo ilikuwa njia yenye kufunikwa yenye ilikuwa upande wa mashariki wa kiwanja cha inje, na wengi waliamini kama hiyo ilikuwa sehemu zenye zilibakia za hekalu la Sulemani. Yesu alitembea kwenye mistari hiyo katika “kipindi cha baridi,” na Wakristo wa kwanza walikutana pale kwa ajili ya ibada. (Yoh 10:22, 23; Mdo 5:12)​—Angalia Nyongeza B11.

  • Miujiza; Matendo yenye nguvu.

    Matendo ao matukio yenye yanapita nguvu zote zenye kujulikana na wanadamu na yanaonwa kuwa yanatokezwa na nguvu zenye kupita za mwanadamu. Maneno kama vile “alama” na “jambo la ajabu,” yanatumiwa nyakati zingine katika Biblia ili kumaanisha jambo lilelile.​—Kut 4:21; Mdo 4:22; Ebr 2:4.

  • Moleki.

    Mungu wa Waamoni; pengine ndiye mungu mwenye anaitwa Malkamu, Milkomu, na Moloki. Pengine ni jina la cheo lakini haiko jina la mungu fulani. Sheria ya Musa ilisema kama mutu yeyote mwenye alitoa watoto wake kuwa zabihu kwa Moleki alipaswa kuuawa.​—Law 20:2; Yer 32:35; Mdo 7:43.

  • Moloki.​

    Angalia MOLEKI.

  • Muchokoo.

    Fimbo ya murefu yenye chongo kali ya chuma, yenye ilitumiwa na walimaji ili kumuongoza munyama kwa kumutoboa-toboa nayo. Maneno ya mutu mwenye hekima yenye yanachochea musikilizaji kutii shauri lenye hekima yanafananishwa na muchokoo. Maneno “kupiga-piga miguu kwenye michokoo” yanatokana na tendo la ngombe-dume mwenye kuwa kichwa-nguvu mwenye anakataa kufuata muongozo wa muchokoo kwa kupiga-piga miguu kwenye muchokoo, na hivyo anajiumiza mwenyewe.​—Mdo 26:14; Amu 3:31.

  • Mufinyanzi.

    Mutu mwenye kutengeneza kwa udongo vyungu, mabakuli, na vyombo vingine. Neno la Kiebrania lenye kutafsiriwa mufinyanzi linamaanisha “mwenye kufanya umbo.” Mara nyingi mamlaka yenye mufinyanzi iko nayo juu ya udongo yanatumiwa ili kuonyesha mamlaka makubwa zaidi ya Yehova juu ya watu na mataifa.​—Isa 64:8; Ro 9:21.

  • Mufumo wa mambo (mifumo ya mambo).

    Angalia MUPANGILIO WA MAMBO (MIPANGILIO YA MAMBO).

  • Mugeuzwa-imani.

    Katika Maandiko, neno hili linamaanisha mutu mwenye alijiunga na dini ya Kiyahudi, mwenye kama ni mwanaume alitahiriwa.​—Mt 23:15; Mdo 13:43.

  • Muhuri.

    Kifaa chenye kilitumiwa ili kutia alama (kwa kawaida kwenye udongo wa mufinyanzi ao nta) ili kuonyesha mwenye kitu fulani, ili kuonyesha kama ni cha kweli, ao makubaliano. Mihuri ya zamani ilitengenezwa kwa kitu kigumu (jiwe, pembe ya tembo, ao muti) chenye kilikuwa na herufi zenye kuchongwa ao michoro yenye kuandikwa kwa kurudia nyuma. Muhuri unatumiwa kwa njia ya mufano ili kutaja kitu chenye kuhakikishwa kuwa cha kweli, ao ili kuonyesha kwamba mutu fulani ndiye mwenye kitu, ao kuonyesha kitu chenye kufichwa ao siri.​—Kut 28:11; Ne 9:38; Ufu 5:1; 9:4.

  • Muji wa Daudi.

    Jina hilo lilipewa muji wa Yebusi kisha Daudi kuushinda na kujenga makao yake ya kifalme kule. Unaitwa pia Sayuni. Ni sehemu ya kusini-mashariki ya Yerusalemu na pia ya zamani sana.​—2Sa 5:7; 1Ny 11:4, 5.

  • Mukono.

    Kipimo cha urefu chenye kinaanzia kwenye kiko cha mukono mupaka kwenye mwisho-mwisho wa kidole cha katikati. Kwa kawaida Waisraeli walitumia kipimo cha mukono chenye urefu wa santimetre 44.5 hivi (inchi 17.5), lakini walitumia pia kipimo kirefu zaidi cha mukono chenye kilizidi mukono wa kawaida kwa upana wa kiganja cha mukono, santimetre 51.8 hivi (inchi 20.4). (Mwa 6:15; Lu 12:25)​—Angalia Nyongeza B14.

  • Mukristo.

    Jina lenye Mungu alipatia wafuasi wa Yesu Kristo.​—Mdo 11:26; 26:28.

  • Mukubwa wa makuhani.

    Ni jina lingine la “kuhani mukubwa” katika Maandiko ya Kiebrania. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ni wazi kwamba usemi “wakubwa wa makuhani” ulimaanisha wanaume wenye walisimamia ukuhani, pengine kutia ndani makuhani wowote wakubwa wenye walikuwa wameondolewa na pia vichwa vya ile migawanyo 24 ya makuhani.​—2Ny 26:20; Ezr 7:5; Mt 2:4; Mk 8:31.

  • Mukusanyiko.

    Kundi la watu wenye kukusanyika kwa kukubali mualiko. Katika Maandiko ya Kiebrania, mara nyingi neno hili linatumiwa ili kuzungumuzia watu wa Israeli wenye walikusanyika kwa ajili ya sikukuu za kidini ao matukio ya maana sana ya kitaifa.​—Kum 16:8; 1Fa 8:5.

  • Mulinzi.

    Mutu mwenye analinda watu ao mali kutokana na hatari, kwa kawaida wakati wa usiku, na mwenye anaweza kutoa mulio fulani wakati anaona hatari. Mara nyingi walinzi waliwekwa juu ya kuta za miji na minara ili waone watu wakiwa mbali mbele wakaribie. Mulinzi mwenye kuwa mwanajeshi anaitwa askari-mulinzi. Kwa njia ya mufano, manabii walitumikia wakiwa walinzi wa taifa la Israeli, wakitoa onyo juu ya uharibifu wenye ulikuwa unakuja.​—2Fa 9:20; Eze 3:17.

  • Munazareti.

    Jina lenye Yesu aliitwa, lenye kuonyesha kama alitoka katika muji wa Nazareti. Pengine linahusiana na neno la Kiebrania lenye linatumiwa katika Isaya 11:1 kumaanisha “chipukizi.” Kisha, wafuasi wa Yesu waliitwa pia vile.​—Mt 2:23; Mdo 24:5.

  • Munaziri.

    Linatokana na neno la Kiebrania lenye kumaanisha “Mwenye Alitengwa,” “Mwenye Alitolewa kwa Mungu,” “Mwenye Aliwekwa Pembeni.” Kulikuwa Wanaziri wa aina mbili: wale wenye walijitoa wenyewe na wale wenye waliwekwa na Mungu kuwa Wanaziri. Mwanaume ao mwanamuke angeweza kuweka naziri ya pekee kwa Yehova ili aishi akiwa Munaziri kwa kipindi fulani. Wale wenye walifanya naziri kwa kujitolea walikuwa na vizuizi tatu vikubwa: hawakupaswa kunywa pombe yoyote wala kula mazao yoyote ya muzabibu, hawakupaswa kukata nywele zao, na hawakupaswa kugusa maiti. Wale wenye waliwekwa na Mungu kuwa Wanaziri walibakia Wanaziri maisha yao yote, na Yehova alitaja mambo yenye walipaswa kutimiza.​—Hes 6:2-7; Amu 13:5.

  • Mungu wa kweli.

    Tafsiri ya maneno ya Kiebrania “ule Mungu.” Mara nyingi, matumizi ya kibainishi zahiri (article défini) katika Kiebrania yanasaidia kuonyesha kwamba Yehova peke yake ndiye Mungu wa kweli tofauti na miungu ya uongo. Maneno “Mungu wa kweli” yanaleta maana kamili kabisa ya maneno hayo ya Kiebrania katika habari zenye kuwa na maneno hayo.​—Mwa 5:22, 24; 46:3; Kum 4:39.

  • Muonaji.

    Mutu mwenye Mungu alipatia uwezo wa kutambua mapenzi ya Mungu, mwenye macho yake yalifunguliwa ili yaone ao kuelewa mambo yenye wanadamu kwa ujumla hawakuona. Neno la Kiebrania linatokana na neno lenye kumaanisha “kuona,” kwa njia ya kweli-kweli ao kwa njia ya mufano. Watu walienda kwa muonaji ili kupata shauri la hekima kuhusu matatizo yenye yaliwapata.​—1Sa 9:9.

  • Muovu, ule muovu.

    Usemi wenye kutaja Shetani Ibilisi, mwenye kupinga Mungu na viwango vyake vya haki.​—Mt 6:13; 1Yo 5:19.

  • Mupangilio wa Mambo (Mipangilio ya mambo).

    Tafsiri ya neno la Kigiriki ai·onʹ wakati linataja hali ya sasa ya mambo ao matukio ya pekee katika kipindi fulani cha wakati. Biblia inatumia maneno “mupangilio wa mambo wa sasa,” ili kuonyesha hali ya sasa ya ulimwengu kwa ujumla na njia ya maisha ya ulimwengu. (2Ti 4:10) Kupitia agano la Sheria, Mungu alianzisha mupangilio wa mambo wenye watu fulani wanaweza kuita kipindi cha Waisraeli ao cha Wayahudi. Kupitia bei yake ya ukombozi, Yesu Kristo alitumiwa na Mungu ili kuanzisha mupangilio tofauti wa mambo, wenye musingi wake ni kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta. Huo ulikuwa mwanzo wa kipindi kipya, chenye kuwa na mambo mbalimbali yenye yalionyeshwa mbele ya wakati kupitia agano la Sheria. Wakati maneno hayo yanatumiwa katika uwingi yanaonyesha mipangilio mbalimbali ya mambo, ao hali mbalimbali za mambo, zenye zimekuwa ao zenye zitakuwa.​—Mt 24:3; Mk 4:19; Ro 12:2; 1Ko 10:11.

  • Mupatanishi.

    Mutu mwenye anaingilia kati ili kupatanisha vikundi mbili. Katika Maandiko, Musa na Yesu ni wapatanishi, Musa ni mupatanishi wa agano la Sheria na Yesu ni mupatanishi wa agano jipya.​—Gal 3:19; 1Ti 2:5.

  • Mupinga-Kristo.

    Neno hilo katika Kigiriki liko na maana mbili. Linamaanisha chochote chenye kuwa kinyume cha Kristo, ao chenye kumupinga Kristo. Linaweza pia kumaanisha Kristo wa uongo, mutu mwenye anakamata nafasi ya Kristo. Watu wote, matengenezo yote, ao vikundi vyote vyenye vinasema kwa uongo kama vinamuwakilisha Kristo ao vyenye vinajiita kuwa Masiya ao vyenye vinamupinga Kristo na wanafunzi wake vinaweza kwa kufaa kuitwa wapinga-Kristo.​—1Yo 2:22.

  • Musa, Sheria ya.

    Sheria yenye Yehova alipatia Israeli kupitia Musa katika jangwa la Sinai mwaka wa 1513 M.K.Y. Mara nyingi vitabu tano vya kwanza vya Biblia vinaitwa Sheria.​—Yos 23:6; Lu 24:44.

  • Musaidizi wa liwali.

    Mutu mwenye cheo cha chini kuliko liwali katika serikali ya Babiloni. Katika Biblia, wasaidizi wa maliwali walisimamia watu wenye hekima katika makao ya mufalme wa Babiloni. Wasaidizi wa maliwali wanatajwa pia wakati wa utawala wa Mufalme Dario Mumedi.​—Da 2:48; 6:7.

  • Mushindio.

    Katika kusuka nguo, mushindio ni nyuzi za kitambaa zenye kutoka kushoto kuenda kuume. Nyuzi hizi zilipita juu na chini ya mutanda, ni kusema, nyuzi za kitambaa zenye kutoka juu kuenda chini.​—Law 13:59.

  • Mustari wa Milima ya Lebanoni.

    Moja ya mistari mbili ya milima katika inchi ya Lebanoni. Mustari wa milima ya Lebanoni uko upande wa mangaribi, na mustari wa milima ya Anti-Lebanoni uko upande wa mashariki. Bonde la murefu lenye mbolea linatenganisha mistari hiyo mbili ya milima. Mustari wa milima ya Lebanoni umeinuka juu kama vile ni moja kwa moja kutoka kwenye eneo la pembeni ya bahari ya Mediterania, na vichwa vyake vimeinuka kufikia urefu kati ya metre 1800 na 2100 (futi 6000 na 7000) kwa kukadiria. Nyakati za zamani, inchi ya Lebanoni ilifunikwa na miti mirefu sana ya mierezi, na mataifa jirani yaliona miti hiyo kuwa yenye samani kubwa sana. (Kum 1:7; Zb 29:6; 92:12)​—Angalia Nyongeza B7.

  • Mutanda.

    Katika kusuka nguo, mutanda ni nyuzi za kitambaa zenye kutoka juu kuenda chini. Nyuzi za kitambaa zenye kutoka kushoto kuenda kuume zinaitwa mushindio.​—Amu 16:13.

  • Muti.

    Nguzo yenye kuwa wima yenye mutu alifungwa juu yake. Ulitumiwa katika mataifa fulani ili kuua watu na/ao kuonyesha maiti ili kuonya wengine ao kupatisha mutu haya mbele ya watu. Waashuru, wenye kujulikana kwa sababu ya vita zao zenye jeuri, walitundika watu wenye walikamatwa kwa kuingiza miti yenye kuchongwa katika tumbo zao mupaka kwenye kifua na kuacha miili ya watu hao ininginie juu ya miti hiyo. Hata hivyo, katika Sheria ya Wayahudi, watu wenye walikuwa na hatia ya kufanya makosa mazito kama vile kumutukana Mungu ao kuabudu sanamu waliuawa kwanza kwa kupigwa majiwe ao kwa njia zingine, kisha maiti zao zilitundikwa kwenye miti, ili kuonya wengine. (Kum 21:22, 23; 2Sa 21:6, 9) Wakati fulani Waroma walifunga tu wakosaji kwenye muti, kwa hiyo mukosaji angeishi kwa siku fulani mbele ya kufa kwa sababu ya maumivu, kiu, njaa, na kuunguzwa na jua. Wakati mwingine, kama vile Yesu aliuawa, waliweka mushitakiwa kwenye muti kwa kumupigilia misumari kwenye mikono na miguu yake. (Lu 24:20; Yoh 19:14-​16; 20:25; Mdo 2:23, 36)​—Angalia MUTI WA MATESO.

  • Muti mutakatifu.

    Neno la Kiebrania (ʼashe·rahʹ) linazungumuzia (1) muti mutakatifu wenye kufananisha Ashera, mungu mwanamuke wa uzazi wa Wakanaani, ao (2) sanamu ya mungu huyo mwanamuke Ashera. Inaonekana kama miti hiyo ilisimama wima na sehemu fulani ilitengenezwa kwa mbao. Pengine zilikuwa nguzo zenye hazikukuwa zimechongwa, ao hata miti.​—Kum 16:21; Amu 6:26; 1Fa 15:13.

  • Muti wa mateso.

    Tafsiri ya neno la Kigiriki stau·rosʹ, lenye kumaanisha muti wenye kuwa wima ao nguzo, kama ule wenye Yesu aliuawa juu yake. Hakuna jambo lenye kuhakikisha kama neno hilo la Kigiriki lilimaanisha musalaba, kama ule wenye ulitumiwa na wapagani kuwa alama ya dini kwa miaka mingi mbele ya Kristo kuja. Maneno “muti wa mateso” yanatoa maana kamili ya neno la luga ya kwanza, kwa kuwa neno stau·rosʹ linatumiwa pia ili kuonyesha mateso, na haya yenye wafuasi wa Yesu wangepambana nayo. (Mt 16:24; Ebr 12:2)​—Angalia MUTI.

  • Muti wa ujuzi wa mema na mabaya.

    Muti fulani wenye ulikuwa katika bustani ya Edeni wenye ulitumiwa na Mungu ili kuwakilisha haki yake ya kuwekea wanadamu viwango vya “mema” na “mabaya.”​—Mwa 2:9, 17.

  • Muti wa uzima.

    Muti fulani wenye ulikuwa katika bustani ya Edeni. Biblia haiseme kama matunda yake yalikuwa na uwezo fulani wa kuendeleza uzima; lakini, muti huo uliwakilisha uhakikisho wa kwamba Mungu atapatia uzima wa milele wale wenye angeruhusu kula matunda yake.​—Mwa 2:9; 3:22.

  • Mut-labeni.

    Usemi wenye kupatikana katika utangulizi wa Zaburi ya 9. Kulingana na desturi, maana yake ni “kuhusu kifo cha mwana.” Watu fulani wanasema kama lilikuwa jina ao pengine maneno ya kwanza ya wimbo wenye ulijulikana yenye yangetumiwa ili kuimba zaburi hiyo.

  • Mutu huru; Mutu mwenye aliwekwa huru.

    Wakati wa utawala wa Roma, “mutu huru” alikuwa mutu mwenye alizaliwa akiwa huru, akiwa na haki zote za uraia. Lakini, “mutu mwenye aliwekwa huru” alikuwa mutumwa mwenye alifunguliwa kutoka katika utumwa. Mutumwa mwenye aliwekwa huru kulingana na sheria alipata uraia wa Roma, lakini hakustahili kupata cheo fulani cha kisiasa. Mutumwa mwenye hakuwekwa huru kulingana na sheria alipata uhuru lakini hakupata haki zote za uraia.​—1Ko 7:22.

  • Mutu mwenye elimu ya nyota.

    Mutu mwenye anachunguza mizunguko ya jua, mwezi, na nyota ili atabiri matukio ya wakati wenye kuja.​—Da 2:27; Mt 2:1.

  • Mutu mwenye kupashana habari na pepo wachafu.

    Mutu mwenye anasema kwamba anazungumuza na watu wenye wamekufa.​—Law 20:27; Kum 18:10-​12; 2Fa 21:6.

  • Mutu mwenye kutabiri matukio.

    Mutu mwenye anasema kuwa iko na uwezo wa kutabiri matukio ya wakati wenye kuja. Makuhani wenye kufanya uchawi, watu wenye kuwa na uhusiano na pepo wachafu, watu wenye elimu ya nyota, na wengine wanatajwa katika Biblia kuwa watu wenye kutabiri matukio.​—Law 19:31; Kum 18:11; Mdo 16:16.

  • Mutume.

    Maana ya kwanza ya neno hili ni “mwenye alitumwa,” na linatumiwa ili kuzungumuzia Yesu na watu fulani wenye walitumwa ili kutumikia wengine. Mara nyingi, linatumiwa ili kuzungumuzia wanafunzi wenye Yesu mwenyewe alichagua wakiwa kikundi cha wawakilishi 12 wenye waliwekwa.​—Mk 3:14; Mdo 14:14.

  • Mutumishi wa huduma.

    Ni tafsiri ya neno la Kigiriki di·aʹko·nos, lenye mara nyingi linatafsiriwa “muhudumu” ao “mutumishi.” “Mutumishi wa huduma” ni ule mwenye anatumikia akiwa musaidizi wa baraza la wazee katika kutaniko. Anapaswa kutimiza sifa zenye kuombwa na Biblia ili astahili kupata pendeleo hilo la utumishi.​—1Ti 3:8-​10, 12.

  • Muyahudi.

    Neno lenye linatumiwa ili kumaanisha mutu wa kabila la Yuda kisha kuanguka kwa ufalme wa Israeli wa makabila 10. (2Fa 16:6) Kisha Waisraeli kutoka katika uhamisho wa Babiloni, neno hilo lilitumiwa ili kumaanisha Waisraeli wa makabila mbalimbali wenye walirudia Israeli. (Ezr 4:12) Kisha, lilitumiwa katika dunia yote ili kutofautisha Waisraeli na watu wenye hawako Waisraeli. (Est 3:6) Mutume Paulo anatumia pia neno hilo kwa njia ya mufano wakati anaonyesha kwamba kuwa mutu wa taifa fulani haiko jambo la maana katika kutaniko la Kikristo.​—Ro 2:28, 29; Gal 3:28.

  • Muzaliwa wa kwanza.

    Neno hilo linamaanisha zaidi sana mutoto mukubwa mwanaume wa baba (lakini haiko mutoto wa kwanza mwenye anazaliwa na mama). Katika nyakati za Biblia, mwana muzaliwa wa kwanza aliheshimiwa katika familia na alipewa daraka la kuwa kichwa cha familia wakati baba yake alikufa. Usemi huo unamaanisha pia munyama wa kiume mwenye anazaliwa wa kwanza.​—Kut 11:5; 13:12; Mwa 25:33; Kol 1:15.

  • Muzee; Mwanaume muzee.

    Mwanaume mwenye kukomaa, lakini katika Maandiko, maneno hayo yanamaanisha zaidi sana mutu mwenye kuwa na mamlaka na madaraka katika jamii ao taifa. Maneno hayo yanatumiwa pia kuhusu viumbe vya mbinguni katika kitabu cha Ufunuo. Neno la Kigiriki pre·sbyʹte·ros linatafsiriwa “muzee” wakati linamaanisha wale wenye kuwa na daraka la kuongoza katika kutaniko.​—Kut 4:29; Mez 31:23; 1Ti 5:17; Ufu 4:4.

  • Mwana wa binadamu.

    Maneno hayo yanapatikana mara 80 hivi katika Vitabu vya Injili. Yanamuhusu Yesu Kristo na yanaonyesha kama kwa kuzaliwa katika mwili wa nyama, alikuja kuwa mwanadamu na hakukuwa tu kiumbe cha roho chenye kilivaa mwili wa kibinadamu. Maneno hayo yanaonyesha pia kama Yesu angetimiza unabii wa Danieli 7:13, 14. Katika Maandiko ya Kiebrania, maneno hayo yalitumiwa kuhusu Ezekieli na Danieli, yakikazia tofauti yenye kuwa kati ya wasemaji hao wenye wanaweza kufa na Mungu mwenye kuwa Chanzo cha ujumbe wao.​—Eze 3:17; Da 8:17; Mt 19:28; 20:28.

  • Mwana wa Daudi.

    Kwa kawaida maneno hayo yanatumiwa ili kumutaja Yesu, yakikazia kwamba yeye ndiye Muriti wa agano la Ufalme lenye lingetimizwa na mutu fulani katika ukoo wa Daudi.​—Mt 12:23; 21:9.

  • Mwandishi.

    Mwandikaji wa Maandiko ya Kiebrania. Kufikia wakati Yesu alikuja duniani, neno hilo lilimaanisha watu wenye walikuwa na ujuzi wa Sheria. Walimupinga Yesu.​—Ezr 7:6, maelezo ya chini; Mk 12:38, 39; 14:1.

  • Mwangalizi.

    Mwanaume mwenye daraka lake la kwanza ni kulinda na kuchunga kutaniko. Wazo la musingi la neno la Kigiriki e·piʹsko·pos ni kuangalia ili kulinda. Maneno “mwangalizi” na “muzee” (pre·sbyʹte·ros) yanaonyesha cheo kilekile katika kutaniko la Kikristo; neno “muzee” linaonyesha kama mutu mwenye amewekwa katika cheo hicho iko na sifa za ukomavu, na neno “mwangalizi” linakazia mambo yenye madaraka hayo yanamuomba kutimiza.​—Mdo 20:28; 1Ti 3:2-7; 1Pe 5:2.

  • Mwebrania, Kiebrania.

    Neno “Mwebrania” lilitumiwa kwanza ili kumutaja Abramu (Abrahamu), na hivyo kumutofautisha na majirani wake Waamori. Kisha lilitumiwa ili kutaja wazao wa Abrahamu kupitia Yakobo mujukuu wake. Neno “Kiebrania” lilitumiwa ili kutaja luga yao. Kufikia siku za Yesu, luga ya Kiebrania ilikuwa na maneno mengi ya Kiaramu na ndiyo luga yenye Kristo na wanafunzi wake walizungumuza.​—Mwa 14:13; Kut 5:3; Mdo 26:14.

  • Mwenendo mupotovu wa bila haya.

    Usemi huo unatokana na neno la Kigiriki a·selʹgei·a na unamaanisha matendo mazito ya kuvunja sheria za Mungu na yenye kuonyesha mutazamo wa kiburi ao kuzarau, ni kusema, roho yenye kuonyesha kukosa heshima ao hata kuzarau mamlaka, sheria, na kanuni. Usemi huo haumaanishe mwenendo mubaya wenye unahusiana na makosa ya kidogo.​—Gal 5:19; 2Pe 2:7.

  • Mwezi mupya.

    Siku ya kwanza ya kila mwezi katika kalendari ya Wayahudi, yenye ilikumbukwa kuwa siku ya kukusanyika pamoja, kufanya karamu, na kutoa zabihu za pekee. Kisha, siku hiyo ilifikia kuwa siku ya maana ya kitaifa ya sikukuu, na watu hawakufanya kazi siku hiyo.​—Hes 10:10; 2Ny 8:13; Kol 2:16.

N

  • Nabii.

    Mutu mwenye anatumiwa ili kutangaza makusudi ya Mungu. Manabii walikuwa wasemaji wa Mungu, hawakutoa tu unabii lakini pia mafundisho ya Yehova, amri zake, na hukumu zake.—Am 3:7; 2Pe 1:​21.

  • Nafsi.

    Tafsiri yenye watu walizoea ya neno la Kiebrania neʹphesh na neno la Kigiriki psy·kheʹ. Kwa kuchunguza namna maneno hayo yanatumiwa katika Biblia, inaonekana wazi kwamba yanamaanisha (1) watu, (2) wanyama, ao (3) uzima wa mutu ao wa munyama. (Mwa 1:​20; 2:7; Hes 31:​28; 1Pe 3:​20; pia maelezo ya chini.) Tofauti na namna neno “nafsi” linatumiwa katika mafundisho mengi ya dini, Biblia inaonyesha kama maneno yote mbili neʹphesh na psy·kheʹ, wakati yanatumiwa kuhusiana na viumbe vya dunia, yanamaanisha kiumbe cha kweli-kweli, chenye kinaweza kuguswa, chenye kuonekana, na chenye kinaweza kufa. Katika tafsiri hii, mara nyingi maneno hayo ya luga za zamani yametafsiriwa kulingana na maana yake katika kila habari, kwa kutumia maneno kama vile “uzima,” “kiumbe,” “mutu,” ao kama kiwakilishi nafsi (kwa mufano, “mimi” ili kuwakilisha “nafsi yangu”). Mara nyingi, maelezo ya chini yanataja neno “nafsi” lenye linaweza pia kutumika. Wakati neno “nafsi” linatumiwa, katika mistari ao katika maelezo ya chini, linapaswa kueleweka kulingana na mafasirio hayo. Wakati yanazungumuzia kufanya jambo fulani kwa nafsi yote, yanamaanisha kulifanya kwa mwili wote, moyo wote, ao kwa uzima wote wa mutu. (Kum 6:5; Mt 22:​37) Katika habari fulani, maneno hayo ya luga za kwanza yanaweza kutumiwa ili kumaanisha tamaa ao hamu ya kiumbe chenye uzima. Yanaweza pia kumaanisha mutu mwenye amekufa ao maiti.—Hes 6:6; Met 23:2; Isa 56:​11; Hag 2:​13.

  • Nardo.

    Mafuta ya harufu ya muzuri ya bei kali yenye yalikuwa na rangi nyekundu yenye kungaa, yenye yalitengenezwa kutokana na mumea wa nardo (Nardostachys jatamansi). Kwa sababu yalikuwa ya bei kali, mara nyingi mafuta ya nardo yalichanganywa na mafuta mengine ya hali ya chini, na wakati fulani watu walitengeneza nardo ya uongo. Inapendeza kujua kama Marko na Yohana wanasema kuwa “nardo ya kweli” ilipakwa kwenye mwili wa Yesu.—Mk 14:3; Yoh 12:3.

  • Naziri.

    Ahadi nzito yenye mutu anatoa kwa Mungu kwamba atafanya jambo fulani, atatoa zabihu ao zawadi fulani, ataanza utumishi fulani, ao atajiepusha na vitu fulani vyenye kimusingi havikatazwe. Naziri ilikuwa na uzito kama kiapo.—Hes 6:2; Muh 5:4; Mt 5:​33.

  • Ndoa ya mutu na shemeki yake.

    Ni desturi yenye iliongezwa baadaye katika Sheria ya Musa, yenye iliruhusu mwanaume kuoa mujane wa ndugu yake mwenye alikufa bila mwana ili mwanaume huyo azae watoto na kuendeleza kizazi cha ndugu yake. Inaitwa pia ndoa ya ndugu-mukwe.—Mwa 38:8; Kum 25:5.

  • Nehiloti.

    Neno lenye kupatikana katika utangulizi wa Zaburi ya 5 lenye maana yake haijulikane muzuri. Watu fulani wanaamini kama linazungumuzia chombo cha muziki cha kupulizwa, na wanalilinganisha na neno la Kiebrania cha·lilʹ (filimbi). Hata hivyo, linaweza kumaanisha muziki.

  • Ngano ya kusemeti.

    Aina fulani ya ngano ya hali ya chini (Triticum spelta), yenye mbegu yake haiwezi kutenganishwa kwa vyepesi na maganda yake.—Kut 9:​32.

  • Nguo za magunia.

    Nguo zenye zilitengenezwa kwa kitambaa kigumu chenye kutumiwa kutengeneza magunia, ao mifuko, kama ile ya kubebea nafaka. Kwa kawaida nguo hizo zilisukwa kwa kutumia manyoya ya mbuzi yenye rangi ya giza-giza, na zilikuwa nguo za kidesturi za maombolezo.—Mwa 37:​34; Lu 10:13.

  • Nguzo.

    Kitu chenye kuwa wima chenye kufanana na munara. Nguzo fulani zilijengwa ili kukumbusha watu matendo ao matukio fulani ya kihistoria. Nguzo za kutegemeza jengo zilitumiwa katika hekalu na katika majengo mbalimbali ya kifalme yenye yalijengwa na Sulemani. Wapagani walijenga nguzo takatifu kwa ajili ya dini yao ya uongo, na wakati fulani Waisraeli walianza kufanya vile. (Amu 16:​29; 1Fa 7:​21; 14:23)—Angalia KIFUNIKO CHA NGUZO.

  • Nguzo takatifu.

    Nguzo yenye kuwa wima, kwa kawaida ilikuwa ya majiwe, na ni wazi kwamba ilikuwa sanamu ya kiungo cha kiume cha Baali ao cha miungu mingine ya uongo.—Kut 23:24.

  • Nira.

    Kipande cha muti chenye kiliwekwa juu ya mabega ya mutu na mizigo iliwekwa kila upande, ao kipande cha muti chenye kiliwekwa juu ya shingo za wanyama wawili wenye kukokota mizigo (kwa kawaida ngombe); wanyama hao walifungiwa nira wakati walikokota kifaa cha kulimia ao gari la kukokotwa. Kwa kuwa mara nyingi watumwa walitumia nira ili kubeba mizigo mizito, nira ilitumiwa kwa njia ya mufano ili kufananisha utumwa ao kutiishwa chini ya mutu mwingine, na pia mateso. Kuondoa ao kuvunja nira kulimaanisha kuweka mutu huru kutoka katika kifungo, kutoka katika mateso, na kuacha kumutumikisha.—Law 26:​13; Mt 11:​29, 30.

  • Nisani.

    Kisha Wayahudi kutoka katika uhamisho Babiloni, nisani lilikuwa jina mupya la Abibu, mwezi wa 1 katika kalendari takatifu ya Wayahudi na jina la mwezi wa 7 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 3 mupaka katikati ya Mwezi wa 4 wa kalendari yetu. (Ne 2:1)—Angalia Nyongeza B15.

  • Njia, ile Njia.

    Usemi huu unatumiwa kwa njia ya mufano katika Maandiko ili kumaanisha matendo ao mwenendo wenye kukubaliwa ao wenye haukubaliwe na Yehova. Wale wenye walifikia kuwa wafuasi wa Yesu Kristo waliitwa watu wa “Ile Njia,” ni kusema, waliishi kwa njia yenye kutegemea imani katika Yesu Kristo, wakifuata mufano wake.—Mdo 19:9.

  • Nyota ya asubui.

    Angalia NYOTA YA MUCHANA.

  • Nyota ya muchana.

    Iko na maana moja na “nyota ya asubui.” Ndiyo nyota ya mwisho kutokea kwenye upande wa mashariki mbele ya jua kutokea, na hivyo inatangaza kupambazuka kwa siku mupya.—Ufu 22:​16; 2Pe 1:​19.

  • Nzige.

    Aina mbalimbali za panzi wenye kuhama-hama katika makundi makubwa. Katika Sheria ya Musa, walionwa kuwa safi na wangeweza kukuliwa. Makundi makubwa ya nzige yenye kutafuna kila kitu kwenye yanapita na kutokeza uharibifu mukubwa, yalionwa kuwa pigo.—Kut 10:14; Mt 3:4.

O

  • Omeri.

    Kipimo cha vitu vyenye kukauka chenye kilikuwa sawa na litre 2.2 (vibaba 2), ao sehemu moja ya kumi ya efa (1/10). (Kut 16:​16, 18)—Angalia Nyongeza B14.

P

  • Pakanga.

    Mimea mbalimbali yenye kuwa na shina ngumu yenye uchungu sana na yenye harufu kali yenye kuvutia. Pakanga inatumiwa kwa njia ya mufano katika Biblia ili kueleza matokeo machungu ya uasherati, utumwa, ukosefu wa haki, na uasi-imani. Katika Ufunuo 8:​11, “pakanga” inamaanisha kitu kichungu na chenye sumu.—Kum 29:​18; Met 5:4; Yer 9:​15; Amo 5:7.

  • Paradiso.

    Bustani yenye kupendeza, ao shamba lenye kufanana na bustani. Mahali pa kwanza pa namna hiyo palikuwa Edeni, Yehova ndiye alipafanya kwa ajili ya wanadamu wawili wa kwanza. Wakati Yesu alikuwa anazungumuza na mumoja wa watenda mabaya wenye walitundikwa pembeni yake kwenye muti wa mateso, alionyesha kama dunia itakuwa paradiso. Katika 2 Wakorinto 12:4, neno hilo linazungumuzia waziwazi paradiso ya wakati wenye kuja, na katika Ufunuo 2:7, linazungumuzia paradiso ya kimbingu.—Wim 4:​13; Lu 23:43.

  • Pasaka.

    Sikukuu ya kila mwaka yenye ilifanywa siku ya 14 ya mwezi wa Abibu (kisha uliitwa Nisani) ili kukumbuka kukombolewa kwa Waisraeli kutoka Misri. Ilikumbukwa kwa kuchinja na kuchoma mwana-kondoo (ao mbuzi), na kisha kumukula pamoja na mboga chungu za majani na mikate yenye haina chachu.—Kut 12:​27; Yoh 6:4; 1Ko 5:7.

  • Patakatifu 1.

    Chumba cha kwanza na kikubwa zaidi katika tabenakulo ao katika hekalu, na kiko tofauti na chumba cha ndani zaidi, ni kusema, Patakatifu Zaidi. Katika tabenakulo, Patakatifu palikuwa na kinara cha taa cha zahabu, mazabahu ya uvumba ya zahabu, meza ya mikate ya wonyesho, na vyombo vya zahabu; katika hekalu, mahali pale kulikuwa mazabahu ya zahabu, vinara kumi vya taa vya zahabu, na meza kumi za mikate ya wonyesho. (Kut 26:​33; Ebr 9:2)—Angalia Nyongeza B5 na B8.

  • Patakatifu 2.

    Kwa ujumla, ni mahali kwenye kulitengwa kwa ajili ya ibada, mahali patakatifu. Hata hivyo, mara nyingi neno hilo linamaanisha tabenakulo ao hekalu katika Yerusalemu. Neno hilo linatumiwa pia ili kutaja makao ya Mungu mbinguni.—Kut 25:​8, 9; 2Fa 10:​25; 1Ny 28:​10; Ufu 11:19.

  • Patakatifu Zaidi.

    Chumba cha ndani zaidi katika tabenakulo na katika hekalu, kwenye sanduku la agano liliwekwa; kinaitwa pia Patakatifu pa Patakatifu. Kulingana na Sheria ya Musa, ni kuhani mukubwa peke yake ndiye aliruhusiwa kuingia Patakatifu Zaidi, na angeweza kuingia mule siku moja tu ya kila mwaka ya Kufunika Zambi.—Kut 26:​33; Law 16:​2, 17; 1Fa 6:​16; Ebr 9:3.

  • Pazia.

    Nguo yenye kusukwa muzuri na kupambwa kwa michoro ya makerubi yenye ilitenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi katika tabenakulo na pia katika hekalu. (Kut 26:​31; 2Ny 3:​14; Mt 27:​51; Ebr 9:3)—Angalia Nyongeza B5.

  • Pembe.

    Neno hili linamaanisha pembe za wanyama, zenye zilitumiwa kama vyombo vya kunywea, vyombo vya mafuta, vyombo vya wino na vyombo vya vitu vya kujipodoa, na vyombo vya muziki, ao vyombo vya kutoa ujumbe fulani. (1Sa 16:​1, 13; 1Fa 1:​39; Eze 9:2) Neno “pembe” linatumiwa mara nyingi kwa njia ya mufano ili kumaanisha nguvu na ushindi.—Kum 33:​17; Mik 4:​13; Zek 1:​19.

  • Pembe za mazabahu.

    Sehemu zenye kusimama kama pembe kwenye kona ine za mazabahu fulani. (Law 8:​15; 1Fa 2:​28)—Angalia Nyongeza B5 na B8.

  • Pentekoste.

    Sikukuu ya pili kati ya sikukuu tatu kubwa zenye wanaume wote Wayahudi walipaswa kufanya katika Yerusalemu. Neno Pentekoste, lenye kumaanisha “(Siku) ya Makumi Tano,” ndilo neno lenye linatumiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kwa ajili ya ile yenye kuitwa Sikukuu ya Mavuno ao Sikukuu ya Majuma katika Maandiko ya Kiebrania. Ilifanywa siku ya 50 kuanzia Nisani 16.—Kut 23:​16; 34:​22; Mdo 2:1.

  • Pepo wachafu.

    Viumbe vyenye uovu vya roho vyenye havionekane vyenye nguvu zavyo zinapita za wanadamu. Kwa sababu wanaitwa “wana wa Mungu wa kweli” katika Mwanzo 6:2 na “malaika” katika Yuda 6, hilo linaonyesha kwamba hawakuumbwa wakiwa waovu; lakini, walikuwa malaika wenye walijifanya wenyewe kuwa maadui wa Mungu kwa kukosa kumutii katika siku za Noa na kwa kujiunga na Shetani katika kumuasi Yehova.—Kum 32:​17; Lu 8:​30; Mdo 16:16; Yak 2:​19.

  • Pete ya muhuri.

    Aina fulani ya muhuri yenye ilivaliwa kwenye kidole ao kutiwa kwenye kamba, pengine kuzunguka shingo. Pete hiyo ilikuwa alama ya mamlaka ya mutawala ao mutu mwenye cheo. (Mwa 41:42)​—Angalia MUHURI.

  • Pigo.

    Katika Maandiko ya Kiebrania, kwa kawaida neno hili linamaanisha ugonjwa wa kuambukiza, ugonjwa, ao azabu ya mateso yenye kutoka kwa Yehova. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo linamaanisha kupiga kwa kiboko ao mujeledi wenye kuwa na vifundo ao sehemu za mwisho zenye kuumiza sana.—Hes 16:​49; Yoh 19:1.

  • Pima.

    Kipimo cha urefu chenye kinatumiwa ili kupima urefu wa maji kuenda chini, kiko sawa na metre 1.8 (futi 6). (Mdo 27:28)—Angalia Nyongeza B14.

  • Pimu.

    Kipimo cha uzito na pia bei yenye Wafilisti waliomba ilipwe ili kunoa vifaa mbalimbali vya metali. Majiwe mengi ya kupimia uzito yenye yalipatikana katika vitu vyenye vilichimbuliwa katika Israeli yako na konsonanti za zamani za Kiebrania za neno “pimu”; kwa kukadiria majiwe hayo yako na uzito wa grame 7.8 (aunsi 0.2508), karibu sehemu mbili za tatu (2/3) za shekeli.—1Sa 13:20, 21.

  • Porneia.​

    Angalia UASHERATI.

  • Purimu.

    Sikukuu ya kila mwaka yenye ilifanywa siku ya 14 na ya 15 ya mwezi wa Adari. Ilikumbusha namna Wayahudi walikombolewa ili wasiharibiwe katika siku za Malkia Esta. Neno pu·rimʹ lenye haliko la Kiebrania linamaanisha “kura.” Sikukuu ya Purimu, ao Sikukuu ya Kura, iliitwa vile kwa sababu ya tendo la Hamani la kupiga Puri (Kura) ili kuamua siku yenye angetimiza mupango wake wa kuharibu Wayahudi.—Est 3:7; 9:​26.

R

  • Rahabu.

    Jina lenye linatumiwa kwa njia ya mufano katika kitabu cha Yobu, cha Zaburi, na cha Isaya (haiko mwanamuke Rahabu mwenye kutajwa katika kitabu cha Yoshua). Katika kitabu cha Yobu, habari inasaidia kufunua Rahabu kuwa munyama mukubwa sana wa bahari; katika habari zingine munyama huyu mukubwa sana wa bahari anafananisha Misri.—Yob 9:​13; Zb 87:4; Isa 30:7; 51:​9, 10.

  • Roho.

    Neno la Kiebrania ruʹach na neno la Kigiriki pneuʹma, yenye kwa kawaida yanatafsiriwa kuwa “roho,” yako na maana nyingi. Yote mbili yanamaanisha kitu chenye macho ya mwanadamu hayawezi kuona na yanaonyesha kuwapo kwa nguvu yenye kutenda. Maneno hayo ya Kiebrania na Kigiriki yanatumiwa ili kumaanisha (1) upepo, (2) nguvu ya uzima yenye kutenda ndani ya viumbe vya dunia, (3) nguvu za musukumo zenye kutoka katika moyo wa mufano wa mutu na kumufanya aseme na kutenda mambo kwa njia fulani, (4) maneno yenye kuongozwa na roho yenye kutoka katika chanzo chenye hakionekane, (5) watu wa roho, na (6) nguvu ya utendaji ya Mungu, ao roho takatifu.—Kut 35:​21; Zb 104:​29; Mt 12:​43; Lu 11:13.

  • Roho takatifu.

    Nguvu ya utendaji yenye haionekane yenye Mungu anatumia ili kutimiza mapenzi yake. Ni takatifu kwa sababu inatoka kwa Yehova, mwenye haki kwa kiwango cha juu zaidi, na kwa sababu ndiyo njia yenye Mungu anatumia ili kutimiza mambo matakatifu.—Lu 1:​35; Mdo 1:8.

S

  • Sabato.

    Neno la Kiebrania lenye kumaanisha “kupumuzika; kuacha.” Ni siku ya saba katika juma la Kiyahudi (ilianza Siku ya Tano kisha jua kushuka mupaka Siku ya Posho kisha jua kushuka). Siku zingine za sikukuu katika mwaka, na pia mwaka wa 7 na mwaka wa 50, ziliitwa pia sabato. Katika siku ya Sabato, hakuna kazi yenye ilipaswa kufanywa isipokuwa kazi ya makuhani katika mahali patakatifu. Katika miaka ya Sabato, inchi haikupaswa kulimwa, na Waebrania hawakulazimisha Waebrania wenzao kulipa madeni. Sheria ya Musa ilikuwa na usawaziko kuhusu mambo yenye kukatazwa siku ya Sabato, lakini viongozi wa dini waliongeza mambo hayo hatua kwa hatua hivi kwamba kufikia siku za Yesu ilikuwa vigumu kwa watu kushika mambo hayo.—Kut 20:8; Law 25:4; Lu 13:​14-​16; Kol 2:​16.

  • Safi.

    Katika Biblia, neno hili halimaanishe tu usafi wa kimwili lakini pia linamaanisha kuendeleza ao kurudisha katika hali yenye haina alama ya uchafu, doa, na kutokuwa na kitu chochote chenye kinachafua, chenye kinatia unajisi, ao chenye kinaharibu mwenendo ao hali ya kiroho. Chini ya Sheria ya Musa, neno hilo linamaanisha kuwa safi kulingana na desturi.—Law 10:​10; Zb 51:7; Mt 8:2; 1Ko 6:​11.

  • Samaria.

    Muji mukubwa wa ufalme wa kaskazini wa Israeli wa makabila kumi kwa miaka 200 hivi, na pia lilikuwa jina la eneo lake lote. Muji huo ulijengwa juu ya mulima wenye ulikuwa na jina hilo. Katika siku za Yesu, Samaria lilikuwa jina la wilaya ya Roma yenye ilikuwa kati ya Galilaya upande wa kaskazini na Yudea upande wa kusini. Kwa kawaida Yesu aliepuka kuhubiri katika eneo hilo katika safari zake, lakini wakati mwingine alipitia pale na kuzungumuza na wakaaji wa eneo hilo. Petro alitumia funguo ya pili ya mufano ya Ufalme wakati Wasamaria walipokea roho takatifu. (1Fa 16:​24; Yoh 4:7; Mdo 8:​14)—Angalia Nyongeza B10.

  • Sanamu; Ibada ya sanamu.

    Sanamu ni mufano wa kitu chochote, kitu cha kweli ao cha kuwaziwa, chenye watu wanaweza kutumia katika ibada. Kuabudu sanamu ni kuiheshimia, kuipenda, kuiabudu, ao kuipenda sana.—Zb 115:4; Mdo 17:​16; 1Ko 10:14.

  • Sanduku la agano.

    Sanduku lenye lilitengenezwa kwa mbao za mugunga na kufunikwa kwa zahabu, lenye liliwekwa katika Patakatifu Zaidi katika tabenakulo na kisha wakati fulani katika Patakatifu Zaidi ndani ya hekalu lenye lilijengwa na Sulemani. Lilikuwa na kifuniko kigumu cha zahabu na makerubi wawili wenye waliangaliana. Vitu vya maana sana vyenye vilikuwa ndani yake ni yale mabamba mbili ya zile Amri Kumi. (Kum 31:​26; 1Fa 6:​19; Ebr 9:4)—Angalia Nyongeza B5 na B8.

  • Sanhedrini.

    Tribinali kubwa ya Wayahudi yenye ilikuwa katika Yerusalemu. Katika siku za Yesu, ilikuwa na washiriki 71, kutia ndani kuhani mukubwa na watu wengine wenye zamani walikuwa makuhani wakubwa, washiriki wa familia za makuhani wakubwa, wazee, vichwa vya makabila na familia, na waandishi.—Mk 15:1; Mdo 5:​34; 23:​1, 6.

  • Sayuni; Mulima Sayuni.

    Ni jina la muji wa Wayebusi wenye ngome, wenye kuitwa Yebusi, wenye ulikuwa kwenye kilima upande wa kusini-mashariki wa Yerusalemu. Kisha Daudi kukamata muji huo, alijenga kule makao yake ya kifalme, na muji huo ukaanza kuitwa “Muji wa Daudi.” (2Sa 5:​7, 9) Mulima Sayuni ukakuwa mulima mutakatifu sana kwa Yehova wakati Daudi alihamishia kule sanduku la agano. Kisha, jina hilo lilitia ndani eneo la hekalu kwenye Mulima Moria, na nyakati zingine muji wote wa Yerusalemu. Mara nyingi jina “Sayuni” linatumiwa kwa njia ya mufano katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.—Zb 2:6; 1Pe 2:6; Ufu 14:1.

  • Sea.

    Kipimo cha vitu vyenye kukauka. Kulingana na kipimo cha bati cha ujazo wa vitu vya majimaji, sea ilikuwa sawa na litre 7.33 (vibaba 6.66). (2Fa 7:1)—Angalia Nyongeza B14.

  • Sehemu moja ya kumi (zaka).

    Sehemu moja ya kumi, ao asilimia kumi (10%), ilitolewa ao kulipwa kuwa ushuru, zaidi sana kwa ajili ya makusudi ya dini. Inaitwa pia “zaka,” na kuitoa kunaitwa “kutoa sehemu moja ya kumi.” (Mal 3:​10; Kum 26:​12; Mt 23:​23) Chini ya Sheria ya Musa, kila mwaka Walawi walipewa sehemu moja ya kumi ya mazao ya inchi na sehemu moja ya kumi ya ongezeko la mifugo na makundi ili kuwategemeza. Walawi walipatia makuhani wa ukoo wa Haruni sehemu moja ya kumi ya sehemu hiyo moja ya kumi ili kuwategemeza. Kulikuwa pia sehemu moja zingine za kumi. Wakristo hawaombwe leo kutoa sehemu moja ya kumi.

  • Sela.

    Neno la kitaalamu lenye kuhusiana na muziki ao kurudilia maneno lenye kupatikana katika kitabu cha Zaburi na Habakuki. Linaweza kumaanisha kutua katika uimbaji ao katika muziki, ao katika yote mbili, ili kufikiri sana kimya-kimya ao kufanya hisia yenye imetoka kuonyeshwa ikuwe wazi. Katika Septante ya Kigiriki neno hilo linatafsiriwa kuwa di·aʹpsal·ma, linamaanisha “pumuziko la muziki.”—Zb 3:4; Hab 3:3.

  • Shebati.

    Kisha Wayahudi kutoka katika uhamisho Babiloni, Shebati lilikuwa jina la mwezi wa 11 katika kalendari takatifu ya Wayahudi na jina la mwezi wa 5 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 1 mupaka katikati ya Mwezi wa 2 wa kalendari yetu. (Zek 1:7)—Angalia Nyongeza B15.

  • Shekeli.

    Kipimo cha musingi cha uzito chenye kilitumiwa na Waebrania na pia kilitumika kama feza. Kipimo hicho kilikuwa na uzito wa grame 11.4 (aunsi 0.403; aunsi troi 0.367). Pengine maneno “shekeli ya mahali patakatifu” yalitumiwa ili kukazia kwamba kipimo hicho kilipaswa kuwa sawasawa kabisa ao kilipaswa kulingana kabisa na kipimo cha kawaida cha uzito chenye kiliwekwa kwenye tabenakulo. Pengine kulikuwa shekeli ya kifalme (yenye ilikuwa tofauti na shekeli ya kawaida) ao kipimo cha kawaida cha uzito chenye kiliwekwa katika makao ya mufalme.—Kut 30:13.

  • Sheminiti.

    Neno la kimuziki lenye kumaanisha “ya munane” lenye pengine linamaanisha sauti ya chini zaidi ao mutindo wa chini. Wakati lilitumiwa kuhusu vyombo vya muziki, pengine neno hilo lilimaanisha vyombo vyenye kutoa sauti nzito katika muziki. Wakati lilitumiwa katika nyimbo, inawezekana lilionyesha aina fulani ya muziki wenye ulipigwa kwa sauti nzito za chini zenye kufuatana pamoja na nyimbo zenye ziliimbwa kwa sauti hizo.—1Ny 15:​21; Zb 6:Uta; 12:Uta.

  • Sheoli.

    Neno la Kiebrania lenye kuwa na maana moja na neno la Kigiriki “Hadesi.” Linatafsiriwa kuwa “Kaburi” (kwa herufi kubwa), ili kuonyesha kwamba ni kaburi la wanadamu wote lakini hapana kaburi la mutu mumoja.—Mwa 37:​35; Zb 16:​10; Mdo 2:​31 (maelezo ya chini).

  • Sheria.

    Wakati neno hili linaandikwa kwa herufi ya mukubwa, linamaanisha Sheria ya Musa ao vitabu tano vya kwanza vya Biblia. Wakati linaandikwa kwa herufi ya kidogo, linaweza kumaanisha sheria moja moja katika Sheria ya Musa ao kanuni fulani ya sheria.—Hes 15:​16; Kum 4:8; Mt 7:​12; Gal 3:​24.

  • Shetani.

    Neno la Kiebrania lenye kumaanisha “Mupinzani.” Wakati linatumiwa na kibainishi zahiri (article défini) katika luga za kwanza, linaonyesha Shetani Ibilisi, Adui mukubwa wa Mungu.—Yob 1:6; Mt 4:​10; Ufu 12:9.

  • Shohamu.

    Jiwe lenye samani ya kadiri, aina ngumu ya jiwe la akiki, ao jiwe la kalkedoni lenye sehemu mbalimbali. Jiwe la shohamu liko na sehemu nyeupe katikati ya sehemu nyeusi, za kahawia, nyekundu, za kijivu, ao za kijani. Jiwe hilo lilitumiwa kwenye nguo za pekee za kuhani mukubwa.—Kut 28:​9, 12; 1Ny 29:2; Yob 28:16.

  • Shubiri.

    Kipimo cha urefu chenye kwa kukadiria kinaanzia kwenye sehemu ya juu ya kidole kikubwa mupaka kwenye sehemu ya juu ya kidole kidogo, kiganja cha mukono kikiwa kimepanuliwa. Kwa musingi wa kipimo cha mukono cha santimetre 44.5 (inchi 17.5), shubiri iko na urefu wa santimetre 22.2 (inchi 8.75). (Kut 28:​16; 1Sa 17:4)—Angalia Nyongeza B14.

  • Siku ya Hukumu.

    Siku, ao kipindi fulani, wakati Mungu ataomba vikundi fulani, mataifa, ao wanadamu kwa ujumla watoe hesabu. Pengine wakati huo wale wenye watahukumiwa kuwa wanastahili kifo watauawa, ao pengine hukumu hiyo itapatia watu fulani nafasi ya kuokolewa na kupata uzima wa milele. Yesu Kristo na mitume wake walitaja “Siku ya Hukumu” yenye kuja ambayo itahusu wazima na pia wale wenye walikufa zamani.—Mt 12:36.

  • Siku ya Kufunika Zambi.

    Siku takatifu ya maana zaidi kwa Waisraeli, inaitwa pia Yom Kippur (maneno hayo yanatokana na neno la Kiebrania yohm hak·kip·pu·rimʹ, “siku ya kufunika”), yenye ilifanywa tarehe 10 ya mwezi wa Etanimu. Ndiyo siku pekee ya mwaka yenye kuhani mukubwa aliingia katika Patakatifu Zaidi katika tabenakulo. Mule alitoa damu ya zabihu kwa ajili ya zambi zake, zambi za Walawi wengine, na zambi za watu. Ulikuwa wakati wa mukusanyiko mutakatifu na kufunga, na pia ilikuwa siku ya sabato, wakati huo watu hawakupaswa kufanya kazi za kawaida.—Law 23:​27, 28.

  • Siku za mwisho.

    Maneno haya yanatumiwa katika unabii wa Biblia ili kumaanisha wakati wenye matukio ya kihistoria yatafikia mwisho wake. (Eze 38:​16; Da 10:​14; Mdo 2:​17) Ikitegemea unabii wenye kuzungumuziwa, maneno hayo yanaweza kumaanisha kipindi cha miaka kidogo tu ao mingi. Biblia inatumia zaidi sana maneno hayo ili kumaanisha “siku za mwisho” za mupangilio huu wa mambo, wakati wa kuwapo kwa Yesu kwenye hakuonekane.—2Ti 3:1; Yak 5:3; 2Pe 3:3.

  • Sikukuu ya Kumutolea Mungu Hekalu.

    Ilikuwa sikukuu ya kila mwaka ya kukumbuka kutakaswa kwa hekalu kisha kuchafuliwa na Antioko Epifane. Sikukuu hiyo ilianza tarehe 25 ya mwezi wa Kislevu na ilifanya siku 8.—Yoh 10:22.

  • Sikukuu ya Mavuno; Sikukuu ya Majuma.​

    Angalia PENTEKOSTE.

  • Sikukuu ya Mikate Yenye Haina Chachu.

    Sikukuu ya kwanza kati ya sikukuu tatu kubwa za kila mwaka za Waisraeli. Ilianza tarehe 15 ya mwezi wa Nisani, siku yenye ilifuata siku ya Pasaka, na ilifanya siku saba. Ni mikate yenye haina chachu tu ndiyo ilipaswa kukuliwa, ili kukumbuka safari yao ya kutoka Misri.—Kut 23:​15; Mk 14:1.

  • Sikukuu ya Vibanda.

    Iliitwa pia Sikukuu ya Tabenakulo, ao Sikukuu ya Kukusanya. Ilifanywa tarehe 15-​21 ya mwezi wa Etanimu. Waisraeli walisherehekea kipindi cha mavuno mwishoni mwa mwaka wa kilimo katika Israeli na ulikuwa wakati wa kushangilia na kushukuru kwa sababu Yehova alibariki mazao yao. Wakati wa sikukuu hiyo, watu walikaa katika vibanda, ao makao yenye kuwa kama sehemu ya juu ya nyumba, ili kukumbuka safari yao ya kutoka Misri. Ilikuwa kati ya sikukuu tatu zenye wanaume walipaswa kuenda kufanyia Yerusalemu.—Law 23:​34; Ezr 3:4.

  • Silaha.

    Vifaa vya kujilinda vyenye vilivaliwa na maaskari, ni kusema, kofia ya chuma, koti ya chuma, mukaba, vyuma vya kuvaa kwenye sehemu ya muguu kati ya goti na kikanyangio, na ngao.—1Sa 31:9; Efe 6:​13-​17.

  • Sinagogi.

    Neno lenye kumaanisha “kukusanya pamoja; mukusanyiko,” lakini katika maandiko mengi, ni jengo ao mahali kwenye Wayahudi walikusanyika kwa ajili ya usomaji wa Maandiko, mafundisho, mahubiri, na sala. Katika siku za Yesu, kila muji mukubwa wa Israeli ulikuwa na sinagogi, na miji mikubwa zaidi ilikuwa na sinagogi zaidi ya moja.—Lu 4:​16; Mdo 13:​14, 15.

  • Siri takatifu.

    Sehemu ya kusudi la Mungu yenye mwanzilishi wake ni Mungu, inabakia ikiwa siri mupaka wakati wake ufike, na inafunuliwa tu kwa wale wenye anachagua kuwajulisha.—Mk 4:11; Kol 1:​26.

  • Siria; Wasiria.​

    Angalia ARAMU; WAARAMU.

  • Sirti.

    Guba mbili kubwa zenye hazina urefu sana kuenda chini zenye kuwa kwenye sehemu ya pembeni ya bahari katika Libya, Kaskazini mwa Afrika, zenye watumishi wa mashua wa zamani waliogopa kwa sababu zilikuwa na muchanga hatari wenye ulikuwa unahamishwa-hamishwa na mawimbi. (Mdo 27:17)—Angalia Nyongeza B13.

  • Sivani.

    Kisha Wayahudi kutoka katika uhamisho Babiloni, Sivani ulikuwa mwezi wa 3 katika kalendari takatifu ya Wayahudi na jina la mwezi wa 9 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 5 mupaka katikati ya Mwezi wa 6 wa kalendari yetu. (Est 8:9)—Angalia Nyongeza B15.

  • Suria.

    Bibi wa cheo cha pili mwenye kwa kawaida alikuwa mutumwa mwanamuke.—Kut 21:8; 2Sa 5:​13; 1Fa 11:3.

T

  • Taabu kubwa.

    Neno la Kigiriki lenye linatafsiriwa “taabu” linatoa wazo la magumu ao mateso yenye kutokana na mikazo yenye kuletwa na hali fulani. Yesu alizungumuzia “taabu kubwa” yenye haijapata kutokea yenye ingepata muji wa Yerusalemu na zaidi sana ile yenye kisha wakati fulani ingepata wanadamu ‘wakati atakuja akiwa na utukufu,’ katika siku zenye kuja. (Mt 24:​21, 29-31) Paulo alieleza kwamba taabu hiyo ni tendo la haki la Mungu juu ya “wale wenye hawamujue Mungu na wale wenye hawatii habari njema” juu ya Yesu Kristo. Kitabu cha Ufunuo sura ya 19 kinaonyesha kama Yesu ndiye anaongoza majeshi ya mbinguni ili kupigana na “ule munyama wa pori na wafalme wa dunia na majeshi yao.” (2Te 1:​6-8; Ufu 19:​11-​21) “Kundi kubwa la watu” linaonekana likiokoka taabu hiyo. (Ufu 7:9, 14)—Angalia ARMAGEDONI.

  • Tabenakulo.

    Hema ya ibada yenye ingeweza kubebwa yenye ilitumiwa na Waisraeli kisha Kutoka Misri. Ndani yake mulikuwa sanduku la agano la Yehova, lenye liliwakilisha kuwapo kwa Mungu, na ilitumiwa kuwa mahali pa zabihu na ibada. Wakati fulani pia inaitwa “hema ya mukutano.” Lilikuwa jengo la mbao lenye kufunikwa kitani na lilipambwa kwa michoro ya makerubi. Iligawanywa katika vyumba mbili; chumba cha kwanza kiliitwa Patakatifu, na cha pili, Patakatifu Zaidi. (Yos 18:1; Kut 25:9)—Angalia Nyongeza B5.

  • Takatifu; Utakatifu.

    Sifa yenye Yehova iko nayo kiasili; hali ya kuwa na usafi kamili katika mwenendo na utakato. (Kut 28:​36; 1Sa 2:2; Mez 9:​10; Isa 6:3) Wakati linatumiwa kuhusu wanadamu (Kut 19:6; 2Fa 4:9), wanyama (Hes 18:17), vitu (Kut 28:​38; 30:​25; Law 27:14), mahali (Kut 3:5; Isa 27:13), vipindi vya wakati (Kut 16:​23; Law 25:12), na kazi (Kut 36:4), neno la kwanza la Kiebrania linatoa wazo la hali ya kutengwa, upekee, ao kutakaswa kwa ajili ya Mungu mutakatifu; hali ya kuwekwa pembeni kwa ajili ya utumishi wa Yehova. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, maneno “takatifu” na “utakatifu” yanaonyesha pia hali ya kuwekwa pembeni kwa ajili ya Mungu. Maneno hayo yanatumiwa pia ili kuzungumuzia usafi katika mwenendo wa mutu.—Mk 6:​20; 2Ko 7:1; 1Pe 1:​15, 16.

  • Talanta.

    Kipimo kikubwa zaidi cha uzito na cha feza chenye kilitumiwa na Waebrania. Kilikuwa na uzito wa kilograme 34.2 (ratili 75.5; ratili troi 91.75; aunsi troi 1.101). Talanta ya Wagiriki ilikuwa ya kidogo zaidi, ilikuwa na uzito wa karibu kilograme 20.4 (ratili 44.8; ratili troi 54.5; aunsi troi 654). (1Ny 22:​14; Mt 18:24)—Angalia Nyongeza B14.

  • Tamuzi.

    (1) Jina la mungu mwenye wanamuke waasi-imani Waebrania katika Yerusalemu walikuwa wanalilia. Inasemekana kama pale mwanzo Tamuzi alikuwa mufalme mwenye alifanywa kuwa mungu kisha kifo chake. Katika maandishi ya Wasumeri, Tamuzi anaitwa Dumuzi na anatajwa kuwa bwana ao mupenzi wa mungu mwanamuke wa uzazi Inanna (Ishtari wa Wababiloni). (Eze 8:​14) (2) Kisha Wayahudi kutoka katika uhamisho Babiloni, Tamuzi lilikuwa jina la mwezi wa 4 katika kalendari takatifu ya Wayahudi na jina la mwezi wa 10 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 6 mupaka katikati ya Mwezi wa 7 wa kalendari yetu.—Angalia Nyongeza B15.

  • Tanuru.

    Jiko la kuyeyushia majiwe yenye madini ao la kuyeyushia metali; lilitumiwa pia ili kuchomea ndani vyombo vya udongo na vyombo vingine vya kauri ao seramike. Katika nyakati za Biblia, matanuru yalitengenezwa kwa matofali ao majiwe. Tanuru ya kuchomea vyombo vya udongo na vya kauri ao seramike na chokaa inaitwa kalibu.—Mwa 15:​17; Da 3:​17; Ufu 9:2.

  • Tarshishi, mashua za.

    Pale mwanzo neno Tarshishi lilitumiwa ili kutaja mashua zenye zilisafiri kuenda katika eneo la zamani la Tarshishi (lenye kuitwa leo Hispania). Inaonekana kwamba kisha, neno hilo lilitumiwa ili kutaja mashua kubwa zenye zilikuwa na uwezo wa kusafiri mbali. Sulemani na Yehoshafati walitumia mashua hizo ili kufanya biashara.—1Fa 9:​26; 10:​22; 22:48.

  • Tartaro.

    Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, Tartaro ni hali ya kushushwa cheo kama vile hali ya mufungwa katika gereza; malaika wenye waliasi katika siku za Noa walitupwa katika hali hiyo. Katika 2 Petro 2:4, kutumia kitenzi (verbe) tar·ta·roʹo (“kutupa ndani ya Tartaro”) hakumaanishe kama “malaika wenye walifanya zambi” walitupwa ndani ya Tartaro yenye kutajwa katika hadisi za kuwazia-wazia za wapagani (ni kusema, gereza lenye kuwa chini ya udongo na mahali penye giza pa miungu midogo). Tofauti na hilo, kitenzi (verbe) hicho kinaonyesha kama Mungu aliwashusha kutoka mahali pao mbinguni na kutoka katika mapendeleo yao na kuwaweka katika hali ya giza nzito sana la kiakili kuhusiana na makusudi yenye kungaa ya Mungu. Giza linaonyesha pia kile chenye kitawapata, chenye Maandiko yanaonyesha kwamba ni uharibifu wa milele, wenye utawapata wao pamoja na mutawala wao, Shetani Ibilisi. Kwa hiyo, Tartaro inafananisha hali ya kushushwa cheo kabisa ya malaika hao waasi. Tartaro ni tofauti na “abiso” yenye kutajwa katika Ufunuo 20:​1-3.

  • Tarumbeta.

    Chombo cha muziki cha kupulizwa chenye kilitengenezwa kwa metali, na kilitumiwa ili kutoa alama na pia katika muziki. Kulingana na Hesabu 10:2, Yehova alitoa maagizo ya kutengeneza tarumbeta mbili za feza zenye zingepigwa ili kutoa mulio fulani wenye kujulikana wa kuita mukusanyiko, kuvunja kambi, ao kutangaza vita. Inawezekana tarumbeta hizo zilikuwa zenye kunyooka, tofauti na “baragumu” zenye zilijikunja zenye zilitengenezwa na pembe za wanyama. Tarumbeta zenye hazitajwe waziwazi namna zilitengenezwa zilikuwa pia kati ya vyombo vya muziki vya hekalu. Kwa kawaida sauti za tarumbeta zilipatana kwa njia ya mufano na matangazo ya hukumu za Yehova ao matukio mengine ya maana yenye kutoka kwa Mungu.—2Ny 29:​26; Ezr 3:​10; 1Ko 15:​52; Ufu 8:7–​11:15.

  • Tebeti.

    Kisha Wayahudi kutoka katika uhamisho Babiloni, Tebeti lilikuwa jina la mwezi wa 10 katika kalendari takatifu ya Wayahudi na jina la mwezi wa 4 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 12 mupaka katikati ya Mwezi wa 1 wa kalendari yetu. Kwa kawaida mwezi huo unaitwa “mwezi wa kumi (10).” (Est 2:​16)—Angalia Nyongeza B15.

  • Terafimu.

    Miungu ya familia ao sanamu, wakati fulani ilitumiwa ili kutafuta alama za mambo yenye yatatokea. (Eze 21:​21) Sanamu fulani za terafimu zilikuwa na ukubwa na umbo ya mwanadamu, na zingine zilikuwa za kidogo sana. (Mwa 31:​34; 1Sa 19:​13, 16) Vitu vya zamani vyenye vilivumbuliwa ndani ya udongo kule Mesopotamia vinaonyesha kama ule mwenye alikuwa na sanamu za terafimu angepokea uriti wa familia. (Hilo linasaidia kuelewa sababu gani Raheli alikamata terafimu za baba yake.) Inaonekana kama Waisraeli hawakukuwa na desturi hiyo, hata kama ibada ya sanamu ya kutumia terafimu ilikuwa katika siku za waamuzi na siku za wafalme, na zilikuwa kati ya vitu vyenye viliharibiwa na Mufalme muaminifu Yosia.—Amu 17:5; 2Fa 23:​24; Ho 3:4.

  • Tia mafuta.

    Neno la Kiebrania lenye kimusingi linamaanisha “kupakaa umajimaji juu ya kitu fulani.” Mutu ao kitu kilipakwa mafuta ili kuonyesha kama kimewekwa pembeni kwa ajili ya utumishi wa pekee. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno hilo linatumiwa pia kuhusiana na kumwangwa kwa roho takatifu juu ya wale wenye walichaguliwa ili kuenda mbinguni.—Kut 28:​41; 1Sa 16:​13; 2Ko 1:​21.

  • Tishri.​

    Angalia ETANIMU na Nyongeza B15.

  • Toba; Kutubu.

    Katika Biblia, neno hili linatumiwa ili kumaanisha kubadilisha akili na kusikitika katika moyo kwa sababu ya njia ya zamani ya maisha, matendo ya mubaya, ao mambo yenye mutu alikosa kufanya. Toba ya kweli inazaa matunda, inamufanya mutu abadilishe mwenendo wake.—Mt 3:8; Mdo 3:​19; 2Pe 3:9.

  • Toleo la hatia.

    Zabihu kwa ajili ya zambi zenye mutu mwenyewe alifanya. Lilitofautiana kidogo na matoleo mengine ya zambi kwa sababu lilipatia ao kurudishia mutenda-zambi mwenye alitubu haki fulani za agano zenye alipoteza kwa sababu ya zambi na kumufanya asipewe azabu yenye alipaswa kupewa kwa sababu ya zambi yake.—Law 7:​37; 19:​22; Isa 53:10.

  • Toleo la kinywaji.

    Toleo la divai lenye lilimwangwa kwenye mazabahu na kutolewa pamoja na matoleo mengine mengi. Paulo alitumia maneno hayo kwa njia ya mufano ili kuonyesha kwamba alikuwa tayari kujitoa kabisa kwa ajili ya Wakristo wenzake.—Hes 15:​5, 7; Flp 2:​17.

  • Toleo la kuteketezwa.

    Zabihu ya munyama mwenye aliteketezwa kwa moto juu ya mazabahu na kutolewa kwa Mungu akiwa toleo nzima; muabudu hakubakia na sehemu yoyote ya munyama huyo (ngombe-dume, kondoo-dume, mbuzi-dume, njiwa-tetere, ao njiwa mudogo).—Kut 29:18; Law 6:9.

  • Toleo la kutikiswa.

    Toleo lenye wakati lilifanywa inaonekana kama kuhani aliweka mikono yake chini ya mikono ya muabudu mwenye alikuwa ameshika zabihu yenye ilipaswa kutolewa, na kuhani alitikisa mikono ya muabudu huyo kuenda mbele na nyuma; ao kuhani mwenyewe alitikisa toleo hilo. Kwa kufanya hivyo ni kama vile walikuwa wakimutolea Yehova matoleo ya zabihu.—Law 7:​30.

  • Toleo la naziri.

    Toleo la kujipendea lenye lilitolewa pamoja na naziri fulani.—Law 23:​38; 1Sa 1:​21.

  • Toleo la shukrani.

    Toleo la ushirika lenye lilitolewa ili kumusifu Mungu kwa sababu ya mambo yenye anapatia watu na upendo wake mushikamanifu. Nyama ya munyama wa toleo ilikuliwa pamoja na mikate yenye chachu na mikate yenye haina chachu. Nyama hiyo ilipaswa kukuliwa siku ileile.—2Ny 29:31.

  • Toleo la ushirika.

    Zabihu yenye ilitolewa kwa Yehova ili kuomba uhusiano wa amani pamoja na Yehova. Muabudu na watu wa nyumba yake, kuhani mwenye alifanya utumishi huo, na makuhani wenye walikuwa wanafanya kazi siku hiyo walikula wote pamoja toleo hilo. Ni kama vile Yehova alipokea moshi wenye kupendeza wa mafuta yenye yalikuwa yanateketea kwa moto. Alipewa pia damu yenye inafananisha uzima. Ni kama vile makuhani na waabudu walikaa na kula pamoja na Yehova, na hilo lilionyesha kama walikuwa na uhusiano wenye amani.—Law 7:29, 32; Kum 27:7.

  • Toleo la zambi.

    Zabihu yenye ilitolewa kwa ajili ya zambi yenye ilifanywa bila kukusudia kwa sababu ya uzaifu wa mwili wenye haukamilike. Zabihu mbalimbali za wanyama, kuanzia ngombe-dume mupaka njiwa, zilitolewa, kulingana na cheo na hali za ule mwenye zambi zake zingefunikwa.—Law 4:​27, 29; Ebr 10:8.

  • Towashi.

    Maana ya kwanza ya neno hilo ni mwanaume mwenye kuvunjwa mapumbu. Kwa kawaida wanaume hao waliwekwa katika makao ya wafalme ili wakuwe watumishi ao watunzaji wa malkia na masuria. Neno hilo linamaanisha pia mwanaume mwenye hakukuwa amevunjwa mapumbu, lakini mwenye alikuwa ofisa ambaye alipewa migao mbalimbali katika makao ya mufalme. Linatumiwa kwa njia ya mufano ili kuzungumuzia ‘towashi kwa ajili ya Ufalme,’ ni kusema, mutu mwenye anajizuia ili ajitoe kwa ukamili zaidi katika utumishi wa Mungu.—Mt 19:​12; Est 2:​15; Mdo 8:​27.

U

  • Uadilifu.​

    Angalia HAKI.

  • Uajemi; Waajemi.

    Inchi na watu wenye kutajwa mara nyingi pamoja na Wamedi; ni wazi kwamba wako na uhusiano nao. Katika historia yao ya kwanza-kwanza, Waajemi walikuwa tu na eneo lenye kuwa upande wa kusini-mangaribi wa bonde la juu la Irani. Chini ya Koreshi Mukubwa (mwenye kulingana na wanahistoria fulani wa zamani alizaliwa na baba Mwajemi na mama Mumedi), Waajemi walikuwa na mamlaka juu ya Wamedi, hata kama utawala huo uliendelea kuwa wa sehemu mbili. Koreshi alishinda Utawala wa Babiloni katika mwaka wa 539 M.K.Y. na aliruhusu Wayahudi wenye walikuwa wamekamatwa mateka warudie katika inchi yao. Utawala wa Uajemi ulianzia kwenye Muto Indus upande wa mashariki mupaka kwenye Bahari ya Aegea upande wa mangaribi. Wayahudi walikuwa chini ya utawala wa Waajemi mupaka wakati Aleksanda Mukubwa alishinda Waajemi katika mwaka wa 331 M.K.Y. Katika maono, Danieli aliona mbele ya wakati Utawala wa Uajemi, na unatajwa pia katika vitabu vya Biblia kama vile Ezra, Nehemia, na Esta. (Ezr 1:1; Da 5:​28)—Angalia Nyongeza B9.

  • Uasherati.

    Neno hili linatokana na neno la Kigiriki por·neiʹa, lenye kwa ujumla linamaanisha ngono yoyote yenye hairuhusiwe. Linatia ndani uzinifu, ukahaba, ngono kati ya watu wenye hawajaoana, ngono kati ya wanaume na wanaume na wanamuke na wanamuke, na kufanya ngono na wanyama. Linatumiwa kwa njia ya mufano katika kitabu cha Ufunuo ili kueleza namna kahaba wa kidini mwenye kuitwa “Babiloni Mukubwa” iko na uhusiano na watawala wa ulimwengu huu ili kupata mamlaka na utajiri. (Ufu 14:8; 17:2; 18:3; Mt 5:​32; Mdo 15:​29; Gal 5:​19)—Angalia KAHABA.

  • Uasi-imani.

    Katika Kigiriki neno hili (a·po·sta·siʹa) linatokana na tendo lenye maana yake ya kwanza ni “kusimama mbali na.” Nomino hiyo inamaanisha “kuondoka, kuacha, ao kuasi.” Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno “uasi-imani” linatumiwa zaidi sana ili kuzungumuzia wale wenye wanaasi ibada ya kweli.—Mez 11:9; Mdo 21:​21; 2Te 2:3.

  • Ubatizo; Batiza.

    Tendo “batiza” linamaanisha “kuzamisha,” ao kutumbukiza ndani ya maji. Yesu alionyesha kwamba wafuasi wake wote wanapaswa kubatizwa. Maandiko yanataja pia ubatizo wa Yohana, kubatizwa kwa roho takatifu, na kubatizwa kwa moto, na maubatizo mengine.—Mt 3:​11, 16; 28:​19; Yoh 3:​23; 1Pe 3:​21.

  • Ubani.

    Umajimaji wenye kukaushwa wenye unatoka katika miti na mimea fulani ya aina ya Boswellia. Wakati ulichomwa, ulitoa harufu ya muzuri sana. Ulikuwa moja kati ya viungo vya uvumba mutakatifu wenye ulitumiwa katika tabenakulo na katika hekalu. Ulitolewa pia pamoja na matoleo ya nafaka na uliwekwa juu ya kila mustari wa mikate ya wonyesho ndani ya Patakatifu.—Kut 30:​34-​36; Law 2:1; 24:7; Mt 2:​11.

  • Ufalme wa Mungu.

    Maneno hayo yanatumiwa zaidi sana ili kumaanisha mamlaka makubwa zaidi ya Mungu yenye kuwakilishwa na serikali ya kifalme ya Mwana wake, Kristo Yesu.—Mt 12:​28; Lu 4:​43; 1Ko 15:50.

  • Ufilisti; Wafilisti.

    Inchi yenye kuwa pembeni ya bahari upande wa kusini wa Israeli yenye kisha ilifikia kuitwa Ufilisti. Wahamiaji kutoka Krete wenye waliishi katika inchi hiyo waliitwa Wafilisti. Daudi aliwatiisha, lakini waliendelea kuwa huru na kuwa maadui wa Israeli. (Kut 13:​17; 1Sa 17:4; Amo 9:7)—Angalia Nyongeza B4.

  • Ufufuo.

    Kuinuka kutoka katika kifo. Maana ya kwanza ya neno la Kigiriki a·naʹsta·sis ni “kuinuka; kusimama.” Biblia inataja ufufuo kenda, kutia ndani ufufuo wa Yesu kupitia Yehova Mungu. Hata kama ufufuo mwingine ulifanywa na Eliya, Elisha, Yesu, Petro, na Paulo, ni wazi kwamba miujiza hiyo ilifanywa kupitia nguvu za Mungu. Ufufuo wa kidunia wa “wenye haki na wenye hawako wenye haki” ni wa lazima katika kusudi la Mungu. (Mdo 24:​15) Biblia inataja pia ufufuo wa kimbingu, wenye kuitwa ufufuo “wa kwanza,” wenye ni ufufuo wa ndugu za Yesu wenye walitiwa mafuta kwa roho.—Flp 3:​11; Ufu 20:​5, 6; Yoh 5:​28, 29; 11:25.

  • Ugonjwa wa kuambukiza.

    Ugonjwa wowote wenye kuenea haraka na wenye kuambukiza wenye unaweza kuenea sana na kutokeza vifo. Mara nyingi unatajwa ili kuzungumuzia kutimizwa kwa hukumu ya Mungu.—Hes 14:​12; Eze 38:22, 23; Amo 4:​10.

  • Uhamisho.

    Tendo la kuondoa mutu katika inchi yake ya kizalikio ao katika makao yake, kwa kawaida washindi ndio walitoa amri ya kufanya vile. Neno la Kiebrania linamaanisha “kuondoka.” Waisraeli wengi sana walipelekwa katika uhamisho mara mbili. Waashuru walipeleka ufalme wa kaskazini wa makabila kumi katika uhamisho, na kisha wakati fulani Wababiloni wakapeleka ufalme wa kusini wa makabila mbili katika uhamisho. Mara hiyo mbili wahamishwa wenye walibakia walirudishwa katika inchi yao wakati wa utawala wa Koreshi, mutawala wa Uajemi.—2Fa 17:6; 24:​16; Ezr 6:​21.

  • Ukaldayo; Wakaldayo.

    Kwanza maneno hayo yalitumiwa ili kutaja inchi na watu wenye waliishi katika eneo kwenye mito ya Tigre na Efrati imejigawanya katika mito midogo; kisha wakati fulani maneno hayo yalitumiwa ili kutaja eneo lote la Babilonia na watu wake. Neno “Wakaldayo” lilitumiwa pia ili kutaja kikundi cha watu wenye elimu wenye walijifunza sayansi, historia, luga, na elimu ya nyota lakini wenye pia walizoea kufanya uchawi na kutabiri matukio kwa kuangalia mizunguko ya jua, mwezi, na nyota.—Ezr 5:​12; Da 4:7; Mdo 7:4.

  • Ukoma; Mwenye ukoma.

    Ugonjwa mubaya sana wa ngozi. Ukoma wenye unatajwa katika Maandiko haulingane sana na ugonjwa wenye kuitwa ukoma leo, kwa sababu zamani ugonjwa huo ulipata wanadamu na pia nguo na nyumba. Mutu mwenye ugonjwa huo anaitwa mutu mwenye ukoma.—Law 14:​54; Lu 5:​12.

  • Ulozi.

    Matumizi ya nguvu zenye kujulikana kama zinatoka kwa roho waovu.—2Ny 33:6.

  • Umalizio wa mupangilio wa mambo.

    Kipindi cha wakati chenye kinaongoza mupaka kwenye mwisho wa mupangilio wa mambo, ao hali ya mambo, chenye kinaongozwa na Shetani. Kinaenda pamoja na wakati wa kuwapo kwa Kristo. Wakiongozwa na Yesu, malaika ‘watatenganisha waovu kutoka kati ya wenye haki’ na kuwaharibu. (Mt 13:​40-​42, 49) Wanafunzi wa Yesu walitaka kujua ni wakati gani “umalizio” huo ungekuja. (Mt 24:3) Mbele ya kurudia mbinguni, Yesu aliahidi wafuasi wake kwamba angekuwa pamoja nao mupaka wakati huo.—Mt 28:20.

  • Unabii.

    Ujumbe wenye uliongozwa na roho takatifu, ikuwe ni ufunuo wa mapenzi ya Mungu ao tangazo la mapenzi yake. Unabii unaweza kuwa fundisho kuhusu mwenendo muzuri lenye kuongozwa na roho takatifu, amri ya Mungu ao hukumu, ao tangazo la jambo lenye litatokea.—Eze 37:​9, 10; Da 9:​24; Mt 13:​14; 2Pe 1:​20, 21.

  • Upatanisho.​

    Angalia KUFUNIKA ZAMBI.

  • Upendo mushikamanifu.

    Kwa kawaida usemi huo unatafsiriwa kutokana na neno la Kiebrania cheʹsedh, lenye kumaanisha upendo wenye kuchochewa na kujitoa, uaminifu-mushikamanifu, ushikamanifu, na kuambatana sana. Mara nyingi usemi huo unatumiwa ili kuzungumuzia upendo wa Mungu kwa wanadamu, lakini pia upendo wenye wanadamu wanaweza kuonyeshana.—Kut 34:6; Rut 3:​10.

  • Urimu na Tumimu.

    Vitu vyenye vilitumiwa na kuhani mukubwa kama vile kura zilitumiwa ili kujua mapenzi ya Mungu wakati maulizo ya maana ya kitaifa yalihitaji majibu kutoka kwa Yehova. Urimu na Tumimu viliwekwa ndani ya kifuko cha kifua cha kuhani mukubwa wakati aliingia katika tabenakulo. Inaonekana kwamba vitu hivyo viliacha kutumiwa wakati Wababiloni waliharibu Yerusalemu.—Kut 28:​30; Ne 7:​65.

  • Ushikamanifu kwa Mungu.

    Heshima, ibada, na utumishi wenye unatolewa kwa Yehova Mungu, na kushikamana na mamlaka yake makubwa zaidi katika ulimwengu wote.—1Ti 4:8; 2Ti 3:​12.

  • Ushuhuda.

    Kwa kawaida “Ushuhuda” ni zile Amri Kumi zenye ziliandikwa kwenye mabamba mbili ya majiwe yenye Musa alipewa.—Kut 31:18.

  • Ushuru.

    Malipo yenye Taifa ao mutawala alipatia mwingine kuwa alama ya ujitiisho, ili kuendeleza amani ao kupata ulinzi. (2Fa 3:4; 18:​14-​16; 2Ny 17:​11) Neno hilo linatumiwa pia ili kumaanisha kodi yenye mutu mumoja-mumoja aliombwa kulipa.—Ne 5:4; Ro 13:7.

  • Utangulizi (katika kitabu cha Zaburi).

    Maneno yenye kupatikana kwenye mwanzo wa zaburi yenye kutambulisha mwandikaji, yanaeleza habari za zaidi juu ya zaburi hiyo, yanatoa maagizo ya muziki, ao yanaonyesha matumizi ao kusudi la zaburi hiyo.—Angalia utangulizi wa Zaburi ya 3, 4, 5, 6, 7, 30, 38, 60, 92, 102.

  • Utete.

    Neno lenye linatumiwa ili kuzungumuzia mimea mingi yenye kwa kawaida inakomaa katika sehemu zenye umajimaji. Mumea wenye kuitwa utete katika Maandiko mengi ni Arundo donax. (Yob 8:​11; Isa 42:3; Mt 27:​29; Ufu 11:1)—Angalia UTETE WA KUPIMIA.

  • Utete wa kupimia.

    Utete wa kupimia ulikuwa na urefu wa mikono sita. Kulingana na kipimo cha kawaida cha mukono, utete huo ulikuwa na urefu wa metre 2.67 (futi 8.75); kulingana na kipimo cha mukono murefu, ulikuwa na urefu wa metre 3.11 (futi 10.2). (Eze 40:​3, 5; Ufu 11:1)—Angalia Nyongeza B14.

  • Utumishi mutakatifu.

    Utumishi, ao kazi, yenye kuwa takatifu, yenye kuhusiana moja kwa moja na ibada yenye mutu anamutolea Mungu.—Ro 12:1; Ufu 7:​15.

  • Uvumba.

    Muchanganyiko wa umajimaji wenye kunata na zeri mbalimbali wenye unaungua polepole na kutoa harufu ya muzuri sana. Uvumba wa pekee wenye viungo ine ulitengenezwa ili utumiwe kwenye tabenakulo na kwenye hekalu. Ulichomwa asubui na usiku kwenye mazabahu ya uvumba ndani ya Patakatifu, na Siku ya Kufunika Zambi, ulichomwa ndani ya Patakatifu Zaidi. Ulifananisha sala zenye kukubalika za watumishi waaminifu wa Mungu. Wakristo hawaombwe kutumia uvumba.—Kut 30:​34, 35; Law 16:​13; Ufu 5:8.

  • Uzinifu.

    Ni ngono yenye inafanywa kwa kujipendea kati ya mwanaume mwenye kuoa na mwanamuke mwenye haiko bibi yake ao kati ya mwanamuke mwenye kuolewa na mwanaume mwenye haiko bwana yake.—Kut 20:​14; Mt 5:​27; 19:9.

V

  • Vifaa vya kushikia tambi.

    Vifaa vyenye vilitengenezwa kwa zahabu, vyenye pengine vilifanana na koleo, vilitumiwa katika tabenakulo na katika hekalu ili kuzimisha taa.—Kut 37:23.

  • Vitu vyenye vinachukuliwa katika vita.

    Vitu vya kipekee ao vya nyumba, mifugo, ao vitu vingine vyenye samani vyenye vinanyanganywa kwa adui mwenye kushindwa.—Yos 7:​21; 22:8; Ebr 7:4.

  • Vizimisha-moto.

    Vifaa vyenye vilitumiwa katika tabenakulo na katika hekalu, vyenye vilitengenezwa kwa zahabu ao shaba. Pengine vifaa hivyo vilifanana na mikasi na vilitumiwa ili kukata tambi za taa.—2Fa 25:14.

  • Vyetezo.

    Vyombo vyenye vilitengenezwa kwa zahabu, feza, ao shaba, vyenye vilitumiwa kwenye tabenakulo na kwenye hekalu ili kuchoma uvumba na kuondoa makaa kwenye mazabahu ya zabihu na kuondoa tambi zenye ziliungua za taa kwenye kinara cha taa cha zahabu.—Kut 37:​23; 2Ny 26:​19; Ebr 9:4.

W

  • Waamuzi.

    Wanaume wenye Yehova aliinua ili kuokoa watu wake mbele ya kipindi cha wanadamu wenye walitawala wakiwa wafalme wa Israeli.—Amu 2:​16.

  • Waamuzi wa raia.

    Katika serikali ya Babiloni, waamuzi-polisi walikuwa watu wenye cheo kati ya raia katika wilaya za utawala wenye walijua sheria na walikuwa na mamlaka fulani ya kuhukumu. Katika makoloni ya Roma, waamuzi wa raia walikuwa wasimamizi wa serikali. Kazi zao zilitia ndani kuendeleza utaratibu, kuangalia namna feza zinatumiwa, kuhukumu watu wenye walivunja sheria, na kuagiza azabu itolewe.—Da 3:2; Mdo 16:20.

  • Wafarisayo.

    Zehebu la dini lenye kujulikana sana la Kiyahudi wakati wa mitume. Hawakukuwa wa uzao wa kikuhani, lakini walifuata sana Sheria, hata katika mambo ya kidogo zaidi, na waliinua mapokeo yenye yalipitishwa kwa mudomo na kuyaona kuwa sawa na Sheria. (Mt 23:​23) Walipinga desturi zote za Kigiriki, na wakiwa wasomi wa Sheria na mapokeo, walikuwa na mamlaka makubwa juu ya watu. (Mt 23:​2-6) Wamoja kati yao walikuwa pia washiriki wa Sanhedrini. Mara nyingi walimupinga Yesu kuhusu kushika Sabato, mapokeo, na kuhusu kushirikiana na watenda-zambi na wakusanya-kodi. Wamoja waligeuka na kuwa Wakristo, kutia ndani Sauli wa Tarso.—Mt 9:​11; 12:​14; Mk 7:5; Lu 6:2; Mdo 26:5.

  • Wafuasi wa chama cha Herode.​

    Angalia HERODE; WAFUASI WA CHAMA CHA.

  • Walinzi wa Mufalme.

    Kikundi cha maaskari Waroma chenye kiliwekwa ili kulinda mutawala Muroma. Kikundi hicho kilifikia kuwa na uvutano mukubwa sana wa kisiasa katika kuunga mutawala mukono ao kumuondoa.—Flp 1:​13.

  • Wamedi; Umedi.

    Wazao wa Madai, mwana wa Yafeti; waliishi katika eneo lenye milima la eneo tambarare la juu la Irani lenye lilikuja kuwa inchi ya Umedi. Wamedi walijiunga na Wababiloni ili kushinda Waashuru. Wakati huo, inchi ya Uajemi ilikuwa jimbo la Umedi, lakini Koreshi aliasi na inchi ya Umedi ikaungana na Uajemi ili kufanyiza Utawala wa Umedi na Uajemi wenye ulishinda Utawala mupya wa Babiloni katika mwaka wa 539 M.K.Y. Wamedi walikuwa Yerusalemu katika siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 K.K.Y. (Da 5:​28, 31; Mdo 2:9)—Angalia Nyongeza B9.

  • Wana wa Haruni.

    Wazao wa Haruni, mujukuu wa Lawi; Haruni alichaguliwa kuwa kuhani mukubwa wa kwanza chini ya Sheria ya Musa. Wana wa Haruni walitimiza madaraka ya kikuhani katika tabenakulo na katika hekalu.—1Ny 23:28.

  • Wanafilozofia Waepikurea.

    Wafuasi wa mwanafilozofia Mugiriki Epikurasi (341-​270 M.K.Y.). Filozofia yao ilitegemea wazo la kwamba raha ndilo jambo la maana sana lenye mutu anapaswa kutafuta katika maisha.—Mdo 17:18.

  • Wanafilozofia Wastoa.

    Masomo ya Kigiriki ya wanafilozofia wenye kuamini kwamba ili kuwa na furaha inaomba kuishi kulingana na akili na mambo ya asili. Kulingana na maoni yao, mutu mwenye hekima ya kweli, hakuhangaika kuhusu maumivu ao furaha.—Mdo 17:18.

  • Wanefili.

    Wana wenye jeuri wenye walizaliwa na malaika wenye walivaa miili ya wanadamu na kufanya ngono na mabinti wa wanadamu mbele ya Garika.—Mwa 6:4.

  • Wanetini.

    Watumishi wa hekalu wenye hawakukuwa Waisraeli. Neno hilo la Kiebrania linamaanisha “Wenye walitolewa,” na linaonyesha kama walikuwa wametolewa kwa ajili ya utumishi wa hekalu. Inawezekana Wanetini wengi walikuwa wazao wa Wagibeoni, wenye Yoshua alikuwa amefanya kuwa “watu wa kukusanya kuni na kushota maji kwa ajili ya mukusanyiko na kwa ajili ya mazabahu ya Yehova.”—Yos 9:23, 27; 1Ny 9:2; Ezr 8:​17.

  • Wasadukayo.

    Zehebu lenye kujulikana la dini ya Kiyahudi lenye washiriki wake walikuwa watu wenye kujulikana wenye walikuwa matajiri na makuhani wenye walikuwa na mamlaka makubwa kuhusiana na kazi katika hekalu. Walikataa mapokeo mengi yenye yalipitishwa kwa mudomo yenye yalifuatwa na Wafarisayo na pia mafundisho mengine ya Kifarisayo. Hawakuamini ufufuo na hawakuamini kwamba kuko malaika. Walimupinga Yesu.—Mt 16:1; Mdo 23:8.

  • Wasamaria.

    Pale mwanzo neno hili lilimaanisha Waisraeli wa ufalme wa kaskazini wa makabila kumi, lakini kisha Waashuru kushinda Samaria katika mwaka wa 740 M.K.Y., neno hilo lilitia ndani wageni wenye waliletwa na Waashuru. Katika siku za Yesu, neno hilo halikuhusianishwa na jamii fulani ao siasa, kwa kawaida lilimaanisha wafuasi wa zehebu la dini lenye lilikuwa karibu na miji ya zamani ya Shekemu na Samaria. Wafuasi wa zehebu hilo walifuata mafundisho fulani yenye yalikuwa tofauti sana na ya dini ya Kiyahudi.—Yoh 8:​48.

  • Wimbo wa huzuni.

    Wimbo wa maneno ao wa chombo cha muziki, wenye kuonyesha huzuni kubwa, kama vile huzuni yenye inaonyeshwa na mutu mwenye alifiwa na rafiki yake ao na mupendwa wake; wimbo wa maombolezo.​—2Sa 1:​17; Zb 7:Uta.

  • Wimbo wa Safari za Kupanda.

    Utangulizi wa Zaburi ya 120-​134. Hata kama watu wako na mawazo mbalimbali juu ya maana ya maneno hayo, wengi wanaamini kama zaburi hizo 15 ziliimbwa na waabudu Waisraeli wenye furaha wakati walikuwa ‘wanapanda’ kuenda Yerusalemu, muji wenye ulikuwa juu katika milima ya Yuda, ili kuhuzuria kule sikukuu tatu kubwa za kila mwaka.

Y

  • Yakobo.

    Mwana wa Isaka na Rebeka. Kisha wakati fulani Mungu alimupatia jina Israeli, na akakuwa muzee wa ukoo wa watu wa Israeli (wenye waliitwa pia Waisraeli na kisha, Wayahudi). Alikuwa baba ya wana 12 wenye, pamoja na wazao wao, walifanyiza makabila kumi 12 ya taifa la Israeli. Jina Yakobo liliendelea kutumiwa ili kumaanisha taifa la Israeli ao watu wa Israeli.—Mwa 32:​28; Mt 22:32.

  • Yedutuni.

    Maana ya neno hili lenye kupatikana katika mautangulizi ya Zaburi ya 39, ya 62, na ya 77 haijulikane muzuri. Inaonekana utangulizi huo ni maagizo ya kuimba zaburi hizo, pengine yanaonyesha mutindo ao chombo cha muziki. Kulikuwa mwanamuziki Mulawi mwenye aliitwa Yedutuni, kwa hiyo inawezekana mutindo huo ao chombo hicho vimeitwa kwa jina lake ao la wana wake.

  • Yehova.

    Kwa kawaida jina hili ni tafsiri ya Kiswahili ya Tetragramatoni (zile herufi ine za Kiebrania za jina la pekee la Mungu), na linapatikana zaidi ya mara 7 000 katika tafsiri hii.—Angalia Nyongeza A4 na A5.

  • Yubile.

    Kila mwaka wa 50, kuanzia wakati Waisraeli waliingia katika Inchi ya Ahadi. Inchi haikupaswa kulimwa katika mwaka wa Yubile, na watumwa Waebrania walipaswa kuwekwa huru. Maeneo ya uriti yenye yalikuwa yameuzishwa yalirudishwa. Kwa njia fulani, mwaka wote huo wa Yubile ulikuwa mwaka wa sikukuu, mwaka wa uhuru wenye ulirudisha taifa katika hali yenye lilikuwa ndani wakati Mungu alilianzisha.​—Law 25:10.

  • Yuda.

    Mwana wa ine wa Yakobo mwenye alizaliwa na Lea bibi yake. Katika unabii wenye alitoa wakati alikuwa karibu kufa, Yakobo alitabiri kwamba mutawala mukubwa na wa kudumu angetoka katika kizazi cha Yuda. Akiwa mwanadamu, Yesu alitokana na kizazi cha Yuda. Pia, jina Yuda linamaanisha kabila hilo na kisha wakati fulani lilimaanisha ufalme wenye uliitwa kwa jina hilo. Ufalme wa Yuda unatajwa pia kuwa ufalme wa kusini, na ulifanyizwa na makabila haya ya Israeli: Kabila la Yuda na la Benyamini, na pia makuhani na Walawi. Kabila la Yuda liliishi upande wa kusini wa inchi yenye ilitia ndani Yerusalemu na hekalu.​—Mwa 29:​35; 49:​10; 1Fa 4:​20; Ebr 7:​14.

Z

  • Zabihu.

    Toleo lenye mutu anamutolea Mungu ili kumushukuru, kukubali kosa, na kurudisha tena uhusiano muzuri pamoja naye. Kuanzia Abeli, wanadamu walitoa zabihu mbalimbali kwa kujipendea, kutia ndani wanyama, mupaka wakati agano la Sheria ya Musa liliomba kufanya jambo hilo. Zabihu za wanyama hazikuhitajika tena kisha Yesu kutoa uzima wake mwenyewe kuwa zabihu kamilifu, hata kama Wakristo wanaendelea kumutolea Mungu zabihu za kiroho.​—Mwa 4:4; Ebr 13:​15, 16; 1Yo 4:​10.

  • Zaburi.

    Wimbo wa kumusifu Mungu. Zaburi zilitungwa kama muziki na kuimbwa na waabudu, kutia ndani wakati watu walimuabudu Yehova Mungu kwenye hekalu lake katika Yerusalemu.—Lu 20:​42; Mdo 13:​33; Yak 5:​13.

  • Zawadi za rehema.

    Zawadi zenye zilitolewa ili kusaidia mutu mwenye kuhitaji musaada. Zawadi hizo hazitajwe moja kwa moja katika Maandiko ya Kiebrania, lakini Sheria ilipatia Waisraeli maagizo yenye kuwa wazi kuhusu daraka lao la kusaidia maskini.—Mt 6:2.

  • Zehebu.

    Kikundi cha watu wenye kufuata imani fulani ao kiongozi fulani na wenye kuwa na mafundisho yao wenyewe. Neno hili linatumiwa ili kutaja vikundi mbili vikubwa vya dini ya Kiyahudi, Wafarisayo na Wasadukayo. Watu wenye hawako Wakristo waliita pia Ukristo “zehebu” ao “zehebu la Wanazareti,” inawezekana waliwaona kuwa kikundi chenye kilijitenga na dini ya Kiyahudi. Kisha mazehebu yaliendelea katika kutaniko la Kikristo; “zehebu la Nikolao” linatajwa waziwazi katika kitabu cha Ufunuo.—Mdo 5:​17; 15:5; 24:5; 28:​22; Ufu 2:6; 2Pe 2:1.

  • Zeu.

    Mungu mukubwa wa Wagiriki wenye walikuwa wanaabudu miungu mingi. Katika Listra, Barnaba aliitwa kimakosa Zeu. Maandishi ya zamani yenye kuchongwa yenye yalipatikana karibu na Listra yanataja “makuhani wa Zeu” na “Zeu mungu-jua.” Kwenye upande wa mbele wa mashua yenye Paulo alisafiri ndani kutoka katika kisiwa cha Malta kulikuwa sanamu ya “Wana wa Zeu,” ni kusema, ndugu mapacha Castor na Pollux.—Mdo 14:​12; 28:11.

  • Zivu.

    Jina la zamani la mwezi wa 2 katika kalendari takatifu ya Wayahudi na jina la mwezi wa 8 katika kalendari ya watu wote. Mwezi huo ulianzia katikati ya Mwezi wa 4 mupaka katikati ya Mwezi wa 5 wa kalendari yetu. Unaitwa Iyari katika Talmudi ya Kiyahudi na pia katika maandishi mengine kisha Wayahudi kutoka katika uhamisho Babiloni. (1Fa 6:​37)—Angalia Nyongeza B15.

  • Ziwa la moto.

    Mahali pa mufano ‘kwenye kunawaka moto na kiberiti,’ kunaitwa pia “kifo cha pili.” Watenda-zambi wenye hawatubu, Ibilisi, na hata kifo na Kaburi (ao, Hadesi) vinatupwa ndani. Kwa kuwa kiumbe wa roho na pia kifo na Hadesi, vitu vyenye haviwezi kuunguzwa na moto, vinatajwa kuwa vinatupwa ndani, hilo linaonyesha kama ziwa hili ni la mufano, halifananishe mateso ya milele, lakini linafananisha uharibifu wa milele.—Ufu 19:​20; 20:​14, 15; 21:8.