Hamia kwenye habari

Majumba ya Ufalme Elfu Moja​—Na Kazi Haijakwisha

Majumba ya Ufalme Elfu Moja​—Na Kazi Haijakwisha

Mnamo Agosti 2013, Mashahidi wa Yehova nchini Filipino walifikia hatua muhimu katika historia kwa kujenga Jumba la Ufalme la elfu moja kupitia mpango wa pekee wa ujenzi. Kama hali ilivyo katika maeneo mengine, Mashahidi wa Yehova nchini Filipino hawana pesa za kutosha au uzoefu wa kujijengea Majumba yao wenyewe ya Ufalme. Kwa miaka mingi, baadhi ya Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakikutanika katika nyumba za watu binafsi, huku wengine wakikutanika kwenye vibanda vidogo vilivyojengwa kwa mianzi.

Kuongezeka kwa idadi ya Mashahidi wa Yehova nchini Filipino na katika nchi nyinginezo kumeongeza uhitaji wa kuwa na Majumba ya Ufalme. Kwa sababu hiyo, katika mwaka wa 1999 Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lilianzisha mpango wa ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika nchi zenye uwezo mdogo wa kifedha. Katika mpango huo, Mashahidi katika nchi hizo huchangia kile wanachoweza, na pesa zinazochangwa katika nchi nyingine zinaongezwa kwenye kiasi hicho. Wajenzi waliozoezwa huwekwa katika vikundi ili kuyasaidia makutaniko yajenge Majumba yao ya Ufalme. Mpango huu wa ulimwenguni pote ulianzishwa nchini Filipino mnamo Novemba 2001.

Iluminado ni mshiriki wa kutaniko la Marilao, Bulacan, mahali ambapo Jumba la Ufalme la elfu moja lilijengwa. Alisema hivi: “Nilijionea undugu wa Kikristo. Watu wengi walijitolea​—wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee. Tulifanya kazi pamoja chini ya jua kali. Hata ingawa tulichoka baada ya kufanya kazi siku nzima, tulifurahi sana kuona kile tulichotimiza.”

Watu ambao si Mashahidi wa Yehova walivutiwa pia na jitihada za wajitoleaji hao. Mmiliki wa lori moja lililoleta mchanga na changarawe kwenye eneo la ujenzi alisema: “Ninyi watu ni kama mchwa​—mko wengi sana! Kila mtu anasaidia. Sijawahi kamwe kuona jambo kama hili.”

Jumba la Ufalme lililokamilika

Wajitoleaji hao walikamilisha ujenzi wa Jumba hilo katika muda usiozidi majuma sita. Kwa kujenga Jumba la Ufalme haraka, washiriki wa kutaniko hilo waliweza kuendelea na kazi muhimu ya kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu.​—Mathayo 24:14.

Ellen, mshiriki mwingine wa kutaniko katika eneo hilo, anasema: “Hatungeweza kutoshea katika Jumba letu la Ufalme la zamani, na wengi wetu tulilazimika kuketi nje ya Jumba. Jumba letu jipya la Ufalme ni maridadi sana na linastarehesha zaidi, hivyo sote tunaweza kufaidika zaidi tunapoendelea kufundishwa na kutiwa moyo katika mikutano yetu.”