Hamia kwenye habari

Mzima-Moto Aliye Likizoni Aokoa Uhai

Mzima-Moto Aliye Likizoni Aokoa Uhai

Jumapili, Januari 5, 2014, Serge Gerardin alikuwa akisafiri kwa basi kuelekea kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova karibu na jiji la Paris nchini Ufaransa, aliposhuhudia aksidenti mbaya sana. Alisema hivi: “Gari ndogo liligonga ukuta wa saruji kando ya daraja na kupaa hewani. Kisha likagonga daraja, likawaka moto, na kupinduka.”

Serge amefanya kazi ya zimamoto kwa miaka zaidi ya 40. Akiwa kapteni katika shirika la kuzima moto, alichukua hatua upesi. Anasema: “Ingawa tulikuwa upande wa pili wa barabara, nilimwambia dereva asimamishe basi, kisha nikarudi mbio kwenye gari lililopata aksidenti.” Serge alisikia sauti ikisema: “Nisaidie! Nisaidie!” Anasema: “Nilikuwa nimevaa suti na tai, na sikuwa na vifaa vyovyote vya usalama. Lakini niliposikia mayowe, nilijua kwamba ninaweza kuokoa uhai wa watu!”

Alipozunguka upande wa pili wa gari, Serge alimwona abiria aliyekuwa amechanganyikiwa na kumpeleka mahali salama. Serge anasema: “Aliniambia kwamba kuna abiria wengine wawili ndani ya gari. Kufikia wakati huo, magari kadhaa yalikuwa yamesimama katika eneo hilo. Lakini kwa sababu ya moto mkali uliokuwa ukiwaka, watu hawakuweza kukaribia eneo hilo.”

Madereva kadhaa wa malori walikuja na vifaa vya kuzimia moto. Serge aliwaelekeza madereva hao jinsi ya kuvitumia kuzima moto uliowaka ndani ya gari, na kwa muda mfupi moto ulizima. Hata hivyo, dereva alikuwa amekwama chini ya gari. Kwa hiyo Serge na wenzake wakainua gari lililopinduka, wakamburuta dereva huyo na kumpeleka mahali salama.

Serge anasema: “Kisha moto ukalipuka tena kwa kishindo!” Lakini bado kulikuwa na abiria mmoja aliyening’inia kwenye mkanda wa kiti cha gari. Kisha mwanamume mwingine anayefanya kazi ya zimamoto aliyekuwa likizoni aliwasili pia, akiwa amevalia nguo za kuendeshea pikipiki zilizotengenezwa kwa ngozi. Serge anaendelea kusema: “Nilimweleza kwamba huenda gari hilo lilikuwa karibu kulipuka, kwa hiyo tukaamua kuvuta mikono ya mtu aliyekuwa ndani ya gari na tukafaulu kumtoa nje.” Sekunde chache baadaye, gari lililipuka na kuteketea kabisa.

Gari la wazima-moto na madaktari lilipowasili, waliwashughulikia walioumia na kuuzima moto kabisa. Serge alipewa huduma ya kwanza kwa ajili ya majeraha mikononi. Alipokuwa akirudi kwenye basi ili aelekee kusanyikoni, wanaume wengi walimkimbilia Serge na kumshukuru.

Serge anafurahi kwamba alikuwa karibu na aliweza kusaidia. Alisema: “Nilihisi kuwajibika mbele za Yehova, Mungu wangu, kuokoa uhai wa watu hao. Kinachoniridhisha ni kwamba nilisaidia kuwaokoa watu hao.”