Hamia kwenye habari

JW.ORG​—Inabadili Maisha ya Watu

JW.ORG​—Inabadili Maisha ya Watu

Watu kutoka kila sehemu wananufaika na Tovuti ya jw.org. Zifuatazo ni kati ya barua nyingi za shukrani ambazo zimetumwa kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova kufikia Mei 2014.

Kuwasaidia Watoto

“Mtoto wangu anayesoma katika shule ya chekechea alizoea kurudi nyumbani na penseli, vifaa vya kuchezea, na hata miwani ya jua ya rafiki zake. Tulimsaidia mara nyingi aelewe kwamba kufanya hivyo ni sawa na kuiba na kwamba kuiba ni vibaya. Hatukufaulu mpaka tulipopakua video katika tovuti ya jw.org yenye kichwa Ni Vibaya Kuiba. Video hiyo ilikuwa kifaa muhimu sana na ilimsaidia sana mwana wetu. Baada ya kuitazama, alisema kwamba angependa kurudisha vitu vyote alivyokuwa amechukua, kwa kuwa alisadiki kwamba kuiba ni vibaya machoni pa Mungu. Tovuti hiyo ilitusaidia kwelikweli!”​—D. N., Afrika.

“Video ya jw.org Ni Vibaya Kuiba . . . ilikuwa kifaa muhimu sana na ilimsaidia sana mwana wetu”

“Watoto wangu wanaipenda tovuti hiyo. Wanapakua video fupi za vibonzo ambazo huwasaidia kutumia vizuri kanuni za Biblia kuhusu kusema uwongo na kuiba. Pia, wanajifunza sifa nyingine muhimu wanazoweza kutumia maishani, na hivyo kuwafanya wawe wenye thamani katika jamii.”​—O. W., West Indies.

Kuwasaidia Watoto Walio Shuleni

“Niliiona shule kuwa mzigo, na nilifikiria kuacha. Lakini siku moja, nilisoma makala yenye kichwa ‘Nataka Kuacha Shule’ kwenye tovuti ya jw.org. Ilinisaidia kuwa na mtazamo mzuri kuhusu shule. Katika makala hiyo nilijifunza kuwa kwenda shule kunanitayarisha kwa ajili ya wakati ujao na kunisaidia kuwa mtu anayewajibika.”​—N. F., Afrika.

“Mashauri yanayotolewa kwa ajili ya vijana katika tovuti hiyo yamenifundisha jinsi ya kudumisha maadili mazuri shuleni”

“Mashauri yanayotolewa katika tovuti hiyo kwa ajili ya vijana yamenifundisha jinsi ya kudumisha maadili mazuri shuleni. Nimejifunza jinsi ya kuzingatia masomo yangu na kuepuka mambo yanayoweza kunikengeusha.”​—G., Afrika.

“Mfanyakazi mwenzangu alilalamika kwamba msichana fulani alimnyanyasa binti yake shuleni. Hilo lilimwathiri sana mtoto wake kiasi cha kwamba hakwenda shuleni kwa siku kadhaa kwa sababu aliogopa. Nilizungumzia na mfanyakazi mwenzangu mambo fulani kutoka katika video ya vibonzo kwenye ubao Mshinde Mnyanyasaji Bila Kutumia Ngumi, inayopatikana kwenye jw.org. Alipenda hasa pendekezo la kutumia ucheshi kutuliza hali. Alizungumza na binti yake kuhusu jinsi anavyoweza kushinda unyanyasaji. Matokeo ni kwamba, msichana huyo alienda shuleni akiwa mjasiri zaidi. Baada ya muda, hali ilianza kuwa nzuri, na msichana aliyekuwa akimnyanyasa akaanza kuwa mwenye urafiki.”​—V. K., Ulaya Mashariki.

Kuwasaidia Vijana

“Asanteni kwa makala iliyo kwenye Tovuti yenye kichwa ‘Kwa Nini Mimi Hujikata Kimakusudi?’ Nimepambana na tatizo hilo kwa muda mrefu. Nilifikiri niko peke yangu na kwamba ikiwa ningewaambia wengine, hawangeelewa. Mifano iliyo kwenye makala hiyo ilinisaidia sana. Kumbe kuna mtu anayeelewa!”​—Msichana kutoka Australia.

“Mifano iliyo kwenye makala hiyo ilinisaidia sana. Kumbe kuna mtu anayeelewa!”

“Tovuti ya jw.org imefanya iwe rahisi zaidi kwangu kupata habari zinazoweza kuwasaidia vijana kukabiliana na mambo mbalimbali. Makala moja ilinisaidia kutambua aina mbalimbali za kusumbuliwa kingono, kujua kuwa nimewahi kupitia hali hizo, na kujifunza njia zinazofaa za kukabiliana na jambo hilo.”​—T. W., West Indies.

Kuwasaidia Wazazi

“Kijana wangu ni machachari sana. Mara nyingi ninahisi kulemewa na tabia yake inayobadilika-badilika. Hilo limefanya iwe vigumu kwetu kuwasiliana. Siku moja, nilitembelea tovuti ya jw.org na nikachagua sehemu inayohusu wenzi wa ndoa na wazazi. Nilipata makala nyingi sana zilizohusu hali niliyokuwa napitia na zilinisaidia jinsi ya kuwasiliana na mwana wangu. Yeye pia amenufaika kutokana na tovuti hii. Sasa anazungumza waziwazi nami na ananieleza mambo yanayomfurahisha na yanayomhuzunisha.”​—C. B., Afrika.

“Mara nyingi makala fulani hutokea kwenye jw.org wakati unaofaa kabisa kutusaidia kushughulika na tatizo fulani ambalo watoto wetu wanakabili”

“Kwa upande wetu sisi wazazi, tunatumia jw.org kuwafundisha watoto wetu kwa njia inayowachangamsha. Kwa mfano, video ya vibonzo kwenye ubao inayoonyesha jinsi ya kupata rafiki wa kweli imewasaidia watoto wetu kuwa na maoni yanayofaa kuhusu urafiki na kuchagua marafiki watakaowasaidia kuwa watu bora zaidi. Mara nyingi makala fulani hutokea kwenye jw.org wakati unaofaa kabisa kutusaidia kushughulika na tatizo fulani ambalo watoto wetu wanakabili. Ni kituo kinachotoa ushauri mzuri sana.”​—E. L., Ulaya.

Kuwasaidia Wenzi wa Ndoa

“Mimi na mke wangu tumefunga ndoa kwa miaka sita. Kama ilivyo kwa watu wote waliofunga ndoa, tumekabili changamoto ya kupatanisha njia zetu za kuwasiliana, malezi yetu, na maoni yetu kuelekea mambo. Makala kwenye jw.org yenye kichwa ‘Jinsi ya Kumsikiliza Mwenzi Wako’ ilinivutia mara moja. Ilitoa mashauri mazuri kuhusu jinsi ya kuwa msikilizaji mzuri. Niliisoma na kisha nikazungumzia mambo hayo na mke wangu. Tumejitahidi kutumia mapendekezo hayo mazuri.”​—B. B., West Indies.

“Nimekuwa nikishirikiana na Mashahidi wa Yehova kwa mwaka mmoja sasa, na ninataka kuwashukuru sana kwa ajili ya tovuti ya jw.org. Nimejifunza mambo mengi kutoka kwenye kituo hicho, kutia ndani jinsi ya kudhibiti hasira yangu na jinsi ya kuwa baba na mume mzuri. Kwa kweli ninaweza kusema kwamba ndoa yangu imeokoka kwa sababu ya tovuti hii.”​—L. G., West Indies.

Kuwasaidia Viziwi

“Tovuti ya jw.org imenisaidia kuwa hai tena. Kupitia video za Lugha ya Ishara ya Marekani, nimeweza kuboresha uwezo wangu wa kutumia lugha ya ishara. Nimekuwa nikihisi kuwa siwezi kujiwekea malengo yoyote muhimu maishani, lakini baada ya kutazama video Kuliona Neno la Mungu Katika Lugha Yangu, ilichangamsha moyo wangu na kuchochea azimio langu la kukazia fikira mambo mazuri katika maisha.”​—J. N., Afrika.

“Tovuti ya jw.org imenisaidia kuwa hai tena”

“Kwa kweli tovuti hiyo ni yenye thamani sana. Mimi ni mfanyakazi anayejitolea kusaidia viziwi, hasa vijana. Habari mbalimbali zinazotolewa katika lugha ya ishara zimenisaidia kuboresha uwezo wangu wa kutumia lugha ya ishara. Tovuti hii imeniwezesha kuwasaidia wale wanaotaka kuboresha maisha yao ya familia na kuimarisha urafiki wao na wengine.”​—K. J., West Indies.

Kuwasaidia Vipofu

“Mimi ni kipofu ambaye amenufaika sana na jw.org. Imenisaidia kupata habari ambazo zingechukua miezi mingi kunifikia. Tovuti hiyo imeboresha maisha ya familia yangu na kunisaidia kuwa mtu mzuri katika jamii yangu. Pia, imenisaidia kupata habari sambamba na rafiki zangu wanaoona.”​—C. A., Amerika Kusini.

“Tovuti hiyo imeboresha maisha ya familia yangu na kunisaidia kuwa mtu mzuri katika jamii yangu”

“Kwa wale wasioweza kusoma maandishi ya vipofu au ambao hawana pesa za kutosha kununua vitabu vya maandishi ya vipofu, jw.org imewasaidia sana. Kupitia rekodi za sauti zenye kuelimisha, vipofu wanaweza kupata habari zinazohusu mambo mbalimbali kwa wakati mmoja. Tovuti hiyo imeandaliwa kwa ajili ya wote bila ubaguzi. Inatusaidia sisi ambao ni viziwi kuhisi tunaheshimiwa na kuhusishwa katika jamii.”​—R. D., Afrika.

Kuwasaidia Wenye Njaa Kiroho

“Tofauti kati ya tovuti yenu na za dini nyingine ni kwamba haina maneno na misemo mingi ya kidini inayoweza tu kueleweka na kasisi. Na pia haimchoshi mtu kwa habari nyingi kupita kiasi. Tovuti yenu imepangwa kwa njia rahisi na ya moja kwa moja. Haina maneno mengi wala falsafa. Haimfanyi mtu aone kuwa na imani ni jambo gumu sana. Badala yake, inaonyesha kuwa mtu wa kawaida anaweza kuwa na imani.”​—A. G., Asia.

“Tovuti yenu imepangwa kwa njia rahisi na ya moja kwa moja . . . Haimfanyi mtu aone kuwa na imani ni jambo gumu sana”

“Maisha yangu yangekuwa magumu sana bila jw.org! Katika ulimwengu wenye giza la kiroho, tovuti hii ni kama taa ninayoweza kuwasha katikati ya giza hilo. Mara moja, ninaweza kutazama na kusikiliza makala zinazoeleza maoni ya Mungu kuhusu mambo mbalimbali na kupata majibu ya maswali mengi maishani.”​—J. C., West Indies.

“Ninathamini msaada wa kiroho ninaopata nikiwa katikati ya msitu huku Amerika Kusini. Bila tovuti hii, ningekosa mwongozo.”​—M. F., Amerika Kusini.

“Ndoa yangu imeokoka kwa sababu ya tovuti hii”