Hamia kwenye habari

Kuwafundisha Watu Kuhusu Tumaini Letu Linalotegemea Biblia Jijini Paris

Kuwafundisha Watu Kuhusu Tumaini Letu Linalotegemea Biblia Jijini Paris

Katika Mkutano wa Umoja wa Mataifa Kuhusu Mabadiliko ya Hali ya Hewa (COP21), uliofanyika kuanzia Novemba 30 hadi Desemba 12, 2015, wajumbe kutoka mataifa 195 walikutana jijini Paris, Ufaransa, kujadili kuhusu jinsi ya kupunguza madhara ya shughuli za wanadamu kwa hali ya hewa ya duniani pote. Watu 38,000 hivi​—kutia ndani maofisa wa serikali, wanasayansi, wanamazingira, na wafanyabiashara wakubwa​—walihudhuria mkutano huo. Watu wengine wengi walitembelea eneo la matangazo ya umma ili wajifunze mengi kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa.

Ingawa Mashahidi wa Yehova hawakushiriki katika mkutano huo, wanapendezwa na mazingira. Mamia ya Mashahidi walishiriki katika kampeni ya pekee jijini Paris ya kuwaeleza wengine kuhusu tumaini lao linalotegemea Biblia la kuishi katika dunia isiyo na uchafuzi.

Alipokuwa akisafiri kwa kutumia usafiri wa umma, Shahidi mmoja alizungumza na mwanamume fulani kutoka Peru, aliyekuwa amevaa mavazi ya kitamaduni ya Peru. Mwanamume huyo alisema kwamba ingawa alikuwa na afya nzuri na alifurahia kuishi kwenye mlima maridadi, bado anahangaishwa sana na hali ya wakati ujao ya dunia yetu. Aliguswa moyo sana kusikia tumaini hilo lenye kuvutia. Huku akitabasamu akachukua kadi yetu ya mawasiliano ambayo inamwelekeza kwenye tovuti yetu, www.jw.org.

Walipokuwa wakisafiri kwa garimoshi, Mashahidi wawili walizungumza na mwanasayansi wa mazingira kutoka Marekani. Alishangaa kusikia kwamba Mashahidi wa Yehova wamepokea mara mbili tuzo ya Four Green Globes kutoka kwa Shirika la Majengo Yasiyoharibu Mazingira (GBI) kwa sababu ya utayari wao wa kutumia mbinu za ujenzi ambazo haziharibu mazingira katika majengo yao mawili mapya yaliyoko Wallkill, New York kwenye ofisi ya tawi ya Marekani. Mtu huyo pia alifurahi kuchukua kadi ya mawasiliano.

Watu wengi waliahidi kutembelea tovuti yetu kwa sababu walivutiwa sana kujua kwamba Mashahidi wanapendezwa kikweli na mazingira. Mjumbe mmoja kutoka Kanada aliposikia kwamba Mashahidi walifanya jitihada za kulinda eneo ambalo ndege aina ya bluebird hutagia kule Warwick, New York, katika eneo la makao makuu mapya ya Mashahidi, alisema hivi: “Kabla sijaanza kutetea mazingira, nilikuwa mtaalamu wa ndege. Sikufahamu kuwa Mashahidi wa Yehova waliheshimu wanyama sana. Nitasoma machapisho yenu na nitatembelea tovuti yenu ili nijifunze mengi zaidi kuwahusu!”