SOMO LA 9
Ni Njia Gani Bora ya Kujitayarisha kwa Ajili ya Mikutano?
Kambodia
Ukrainia
Ikiwa unajifunza Biblia na Shahidi wa Yehova, huenda wewe husoma mapema habari ambazo mtajifunza. Ili ufaidike na mikutano pia, ni vizuri ufanye vivyo hivyo kabla ya kuhudhuria. Ukiwa na ratiba nzuri, utafanikiwa.
Amua wakati na mahali pa kujifunzia. Ni wakati gani unapoweza kukaza fikira? Je, ni asubuhi na mapema kabla ya kuanza kazi za kila siku au ni usiku baada ya watoto kulala? Hata ikiwa huwezi kujifunza kwa muda mrefu, amua wakati unaoweza kutenga kwa ajili ya kujifunza, nawe usiruhusu chochote kivuruge ratiba yako. Tafuta mahali patulivu, na uepuke vitu vinavyokengeusha fikira kwa kuzima redio, televisheni, na hata simu ya mkononi. Kusali kabla ya kujifunza kutakusaidia upunguze mahangaiko ili uweze kukazia fikira Neno la Mungu.—Wafilipi 4:6, 7.
Tia alama mambo makuu, na ujitayarishe kushiriki katika mikutano. Kwanza, jaribu kuelewa wazo kuu la habari unayojifunza. Fikiria kichwa kikuu cha makala au sura hiyo, chunguza jinsi kila kichwa kidogo kinavyohusiana na kichwa kikuu, na uchunguze picha na maswali yanayokazia mambo makuu. Kisha, usome kila fungu, na utafute majibu ya maswali yaliyochapishwa. Fungua na usome maandiko ambayo yametajwa, na ufikirie jinsi yanavyounga mkono kichwa kikuu. (Matendo 17:11) Unapopata majibu ya maswali, tia alama au upige mstari chini ya maneno makuu machache yatakayokusaidia kukumbuka majibu. Kwenye mikutano, unaweza kuinua mkono na kutoa maelezo mafupi ukitumia maneno yako mwenyewe.
Ukichanganua habari tofauti-tofauti ambazo zinazungumziwa kila juma katika mikutano, utaongeza “hazina” yako ya ujuzi wa Biblia.—Mathayo 13:51, 52.
-
Ni maamuzi gani unayohitaji kufanya ili kuwa na ratiba nzuri ya kujitayarisha kwa ajili ya mikutano?
-
Unaweza kujitayarishaje ili uweze kutoa maelezo katika mikutano?