Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 3

Jinsi ya Kutatua Matatizo

Jinsi ya Kutatua Matatizo

“Iweni na upendo mkubwa ninyi kwa ninyi, kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.” ​—1 Petro 4:8

Wewe na mwenzi wako mnapoanza kuishi pamoja, matatizo yatatokea. Yanaweza kuletwa na tofauti za kufikiri, hisia, na malezi yenu. Au huenda yakasababishwa na mambo mengine na hali zisizotarajiwa.

Ni rahisi kujidanganya kwamba mambo ni shwari lakini Biblia inatushauri tuyakabili matatizo yetu. (Mathayo 5:23, 24) Ukitumia kanuni za Biblia utapata suluhisho bora kabisa la matatizo yako.

1 ZUNGUMZIENI TATIZO PAMOJA

BIBLIA INASEMA HIVI: “Kuna . . . wakati wa kusema.” (Mhubiri 3:1, 7) Tumieni wakati wa kutosha kuzungumzia tatizo lolote. Mweleze mwenzi wako kwa unyoofu hisia na maoni yako kuhusu jambo hilo. Sikuzote ‘sema kweli’ na mwenzi wako. (Waefeso 4:25) Hata kama linahusisha hisia kali, epuka kugombana. Jibu la upole linaweza kusaidia ili mazungumzo ya kawaida yasigeuke na kuwa ugomvi.​—Methali 15:4; 26:20.

Hata msipokubaliana, endelea kuwa mwenye fadhili, na usisahau kumwonyesha mwenzi wako upendo na heshima. (Wakolosai 4:6) Jaribu kutatua tatizo haraka iwezekanavyo, na msiache kuwasiliana.​—Waefeso 4:26.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Panga wakati unaofaa wa kuzungumzia tatizo hilo

  • Inapofika wakati wako wa kusikiliza usimkatize mwenzi wako anapozungumza. Utapata nafasi ya kuongea

2 MSIKILIZE NA UMWELEWE MWENZI WAKO

BIBLIA INASEMA HIVI: “Iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Waroma 12:10) Ni muhimu sana kusikiliza kwa makini. Jitahidi kuelewa maoni ya mwenzi wako na uwe na ‘hisia-mwenzi na unyenyekevu.’ (1 Petro 3:8; Yakobo 1:19) Usijifanye unasikiliza. Ikiwezekana, acha unachofanya na umsikilize mwenzi wako, au umuulize ikiwa mnaweza kuzungumzia jambo hilo baadaye. Ikiwa utamwona mwenzi wako kama mshirika wako badala ya kumwona kama mpinzani, hutakuwa na “haraka kuudhika.”​—Mhubiri 7:9.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Endelea kusikiliza ukiwa na mtazamo unaofaa, hata ikiwa hufurahii anachosema

  • Jitahidi kuelewa anachomaanisha. Zingatia pia sauti na ishara za mwenzi wako

3 TIMIZENI MAMBO MNAYOKUBALIANA

BIBLIA INASEMA HIVI: “Kwa kila kazi ngumu hutokea faida, lakini neno la midomo tu huelekea kuleta uhitaji.” (Methali 14:23) Haitoshi tu kukubaliana. Mnahitaji kutimiza mambo mliyokubaliana. Huenda hilo likahitaji jitihada nyingi, lakini si kazi bure. (Methali 10:4) Mkishirikiana, mtapata “thawabu nzuri” kwa ajili ya kazi yenu ngumu.​—Mhubiri 4:9.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Amueni mambo hususa ambayo kila mmoja wenu atafanya ili kusuluhisha tatizo lenu

  • Mara kwa mara, changanueni maendeleo mnayofanya