Kiswahili
Misukosuko ya Kisiasa Yatimiza Unabii wa Biblia
https://cms-imgp.jw-cdn.org/img/p/501100118/univ/art/501100118_univ_sqr_xl.jpg
mrt makala 125

Misukosuko ya Kisiasa Yatimiza Unabii wa Biblia

Misukosuko ya Kisiasa Yatimiza Unabii wa Biblia

 Leo, masuala ya kisiasa yamewafanya watu wagawanyike sana. Hawakubaliani hata kuhusu sheria zinazohusu maisha yao ya kila siku na kila mtu anatetea vikali msimamo wake wa kisiasa. Serikalini, watunga sheria na maofisa wengine huwa na maoni tofauti ya kisiasa na mara nyingi hakuna anayetaka kujishusha na kukubali maoni ya wenzake. Tofauti hizo hutokeza misukosuko ya kisiasa ambayo inafanya serikali ishindwe kutimiza wajibu wake.

 Misukosuko ya kisiasa iliyo Marekani na Uingereza ni jambo muhimu la kufikiria. Kwa nini? Kwa sababu Biblia ilitabiri kwamba mataifa hayo mawili yangekuwa na misukosuko katika kipindi ambacho serikali ya Mungu ingeingilia kati na kubadili mambo hapa duniani.

Misukosuko ya kisiasa “katika kipindi cha mwisho cha zile siku”

 Biblia ina unabii wenye kusisimua ulioandikwa kwenye kitabu cha Danieli. Katika unabii huo Mungu alifunua “mambo yatakayotukia katika kipindi cha mwisho cha zile siku.” Kipindi hicho kilirejelea wakati fulani ujao ambapo kungekuwa na mabadiliko makubwa ambayo yangewaathiri wanadamu.​—Danieli 2:28.

 Mungu alimpatia mfalme wa Babiloni unabii huo kupitia ndoto. Katika ndoto hiyo, mfalme aliona sanamu kubwa iliyotengenezwa kwa madini mbalimbali. Baadaye, nabii Danieli alifafanua kwamba sehemu mbalimbali za sanamu hiyo, kuanzia kichwa hadi miguu, zinawakilisha serikali kuu za ulimwengu ambazo zingetawala na kisha kuanguka. a Hatimaye, sanamu hiyo ingepigwa kwa jiwe na kuharibiwa kabisa. Jiwe hilo liliwakilisha Ufalme, au serikali ya Mungu.​—Danieli 2:36-45.

 Kulingana na unabii huo, Ufalme wa Mungu utaziondoa serikali zote za wanadamu na kutawala badala ya serikali hizo. Huu ndio Ufalme ambao Yesu aliwaambia wafuasi wake wasali kuuhusu aliposema: “Ufalme wako na uje.”​—Mathayo 6:10.

 Lakini ni sehemu gani ya unabii huo ambayo inazungumzia misukosuko ya kisiasa? Ona kwamba nyayo za sanamu hiyo “zilikuwa za chuma na kwa sehemu zilikuwa za udongo wa mfinyanzi.” (Danieli 2:33) Nyayo zilikuwa na mchanganyiko wa madini mbalimbali, tofauti na sehemu nyingine za sanamu hiyo na hilo lilionyesha serikali hiyo kuu ingekuwa tofauti na zile serikali zingine. Jinsi gani? Unabii wa Danieli unafafanua jambo hilo:

 “Na kama tu ulivyoona kwamba nyayo na vidole vya miguu kwa sehemu vilikuwa vya udongo wa mfinyanzi na kwa sehemu vilikuwa vya chuma, ufalme huo utagawanyika, lakini ugumu fulani wa chuma utakuwa ndani yake, kama tu ulivyoona chuma kikiwa kimechanganyika na udongo laini wa mfinyanzi. Na kama vile vidole vyake vya miguu vilikuwa kwa sehemu vya chuma na kwa sehemu vya udongo wa mfinyanzi, ndivyo ufalme huo utakavyokuwa na nguvu kwa sehemu na kuwa dhaifu kwa sehemu. Kama tu ulivyoona chuma kikiwa kimechanganyika na udongo laini wa mfinyanzi, sehemu hizo zitachanganyika na wanadamu; lakini hazitashikamana na wanadamu, kama tu chuma kisivyochanganyika na udongo wa mfinyanzi.”​—Danieli 2:41-43.

 Unabii huo unasema kwamba serikali kuu ya ulimwengu inayowakilishwa na nyayo za sanamu hiyo ingekabili misukosuko ya kisiasa. Raia wa serikali hiyo wangefanya mambo ambayo yangeidhoofisha.

Jinsi unabii wa Danieli unavyotimizwa leo

 Nyayo za sanamu hiyo zinawakilisha serikali kuu ya ulimwengu leo, muungano wa Marekani na Uingereza. Matukio ya hivi karibuni yanathibitishaje jambo hilo?

 Nyayo za sanamu hiyo zilikuwa ‘kwa sehemu za chuma na kwa sehemu za udongo wa mfinyanzi’ na hivyo zingekuwa dhaifu. (Danieli 2:42) Leo, nguvu za Marekani na Uingereza zinadhoofishwa na migawanyiko kati ya raia wao. Kwa mfano, katika nchi zote mbili kumekuwa na migogoro miongoni mwa raia. Watu wamekuwa wakifanya maandamano yenye fujo ili kutetea haki zao. Mara nyingi viongozi waliochaguliwa hushindwa kukubaliana kuhusu masuala mbalimbali. Kwa kuwa watu wamegawanyika sana, serikali hizo hushindwa kutimiza sera zao.

Danieli sura ya 2 inaeleza serikali zingekuwa katika hali gani

 Tuchunguze kwa kina zaidi maana ya unabii huo wa Danieli na jinsi unavyotimizwa leo:

 Unabii: “Ufalme huo utagawanyika, lakini ugumu fulani wa chuma utakuwa ndani yake.”​—Danieli 2:41.

 Maana: Ingawa Marekani na Uingereza zinakabili migawanyiko ya kisiasa ndani ya nchi zao, bado wana majeshi yenye nguvu. Kwa sababu hiyo wanaweza kutenda kwa mamlaka, kama kwa nguvu za chuma.

 Utimizo

 Orodha ya mwaka wa 2023 ya nchi zinazotumia pesa nyingi kugharimia shughuli za kijeshi ilionyesha kwamba kwa pamoja Marekani na Uingereza zilitumia pesa nyingi zaidi kugharimia shughuli za kijeshi kuliko nchi 12 zinazofuata katika orodha hiyo zikijumuishwa pamoja.​—Taasisi ya Stockholm International Peace Research.

 “Uhusiano uliopo kati ya Uingereza na Marekani wa kulinda nchi zao . . . umekuwa muungano wenye nguvu zaidi baina ya nchi mbili na unatumia teknolojia na mikakati ya kisasa zaidi. . . . Tunafanya kazi pamoja, tunasimama pamoja, tunapigana pamoja.”​—Shirika la Strategic Command, Wizara ya Ulinzi ya Uingereza, Aprili 2024.

 Unabii: “Kama vile vidole vyake vya miguu vilikuwa kwa sehemu vya chuma na kwa sehemu vya udongo wa mfinyanzi, ndivyo ufalme huo utakavyokuwa na nguvu kwa sehemu na kuwa dhaifu kwa sehemu.”​—Danieli 2:42.

 Maana: Ingawa Marekani na Uingereza zina majeshi yenye nguvu, zinashindwa kutimiza mambo yote ambayo zingependa kufanya kwa sababu ya jinsi serikali zao za kidemokrasia zinavyofanya kazi. Ikiwa watu wana maoni yanayopingana kuhusu sera za serikali, inaweza kuwa vigumu kwa serikali kutekeleza mipango yake.

 Utimizo

 “Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanasema kwamba migawanyiko katika serikali ya Marekani inafanya iwe vigumu kwa serikali hiyo kutimiza mambo ambayo inasema inaweza kutimiza ulimwenguni, kutia ndani mambo yanayohusu usalama au biashara.”​—Gazeti la “The Wall Street Journal.”

 “Kuliko wakati mwingine wowote, Uingereza imekumbwa na misukosuko ya kisiasa ambayo imewakengeusha wanasiasa na kufanya iwe vigumu kwa wafanyakazi wa serikali kutekeleza mabadiliko yanayohitajika.”​—Taasisi ya Mambo ya Serikali.

 Unabii: ‘Ufalme huo utachanganyika na watu wa kawaida; lakini hautashikamana nao.’​—Danieli 2:43, maelezo ya chini.

 Maana: Katika serikali za kidemokrasia, watu wa kawaida nyakati nyingine hutoa maoni ya jinsi ya kufanya mambo katika serikali, lakini mara nyingi matokeo hayawaridhishi wapiga kura wala maofisa wa serikali.

 Utimizo

 “Leo, Wamarekani wengi hawafurahishwi hata kidogo na siasa na wanasiasa.”​—Kituo cha Utafiti cha Pew.

 “Waingereza leo hawaitumaini kabisa serikali na wanasiasa. Wamepoteza imani kabisa na mifumo ya serikali kuliko wakati mwingine wowote katika miaka hamsini iliyopita.”​—“Kituo cha Kitaifa cha Utafiti wa Kijamii.”

Jinsi unabii wa Danieli utakavyotimia wakati ujao

 Kulingana na unabii wa Danieli, muungano wa Marekani na Uingereza ndio utakaokuwa ukitawala kama serikali kuu ya ulimwengu, Ufalme wa Mungu utakapokuja kuziondoa serikali zote za wanadamu.​—Danieli 2:44.

 Katika kitabu cha Ufunuo, kuna unabii mwingine unaozungumzia kipindi hicho. Unabii huo unaonyesha kwamba “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” watakusanyika dhidi ya Yehova b Mungu katika vita vya Har-Magedoni, “vita vya siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” (Ufunuo 16:14, 16; 19:19-21) Katika vita hivyo, Yehova ataharibu serikali zote za wanadamu na hakuna sehemu yoyote ya serikali kuu za ulimwengu, zinazowakilishwa na sanamu iliyo katika unabii wa Danieli, itakayobaki.

 Ili kujifunza mengi zaidi, soma makala yenye kichwa “Vita vya Har-Magedoni Ni Nini?

Utanufaikaje kutokana na unabii wa Danieli unaozungumzia misukosuko ya kisiasa?

 Biblia ilitabiri kwa usahihi kwamba kungekuwa na misukosuko ya kisiasa Marekani na Uingereza. Kujifunza jambo hilo kutakusaidia kuona mambo yanayotokea ulimwenguni leo kwa njia tofauti.

  •   Utaelewa kwa nini Yesu hakutaka wafuasi wake waunge mkono upande wowote katika siasa za ulimwengu huu. (Yohana 17:16) Pia utajifunza kwa nini Yesu, mtawala ambaye Mungu amemchagua aongoze Ufalme wake, alisema hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.”​—Yohana 18:36.

  •   Utafarijika kujua kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utachukua hatua na kwamba utawaletea wanadamu baraka nyingi kama tu Mungu alivyoahidi.​—Ufunuo 21:3, 4.

  •   Utakuwa na uhakika kuhusu wakati ujao na hutakuwa tena na wasiwasi kwamba mataifa yanayozozana yataharibu dunia.​—Zaburi 37:11, 29.

 Unabii wa Danieli unaonyesha kwamba muungano wa Marekani na Uingereza, unaowakilishwa na nyayo za ile sanamu, ndio serikali ya mwisho itakayowatawala wanadamu. Baada ya serikali hiyo kufikia mwisho wake, Ufalme wa Mungu, serikali kamilifu inayotawala kutoka mbinguni, itaitawala dunia!

 Ili upate habari zaidi kuhusu mambo ambayo Ufalme wa Mungu utafanya kwa ajili ya wanadamu, tazama video Ufalme wa Mungu Ni Nini?

b Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?