Ni Nini Kitakachoipata Dini?—Kile Ambacho Biblia Inafundisha
Je, umekatishwa tamaa au hata kuchukizwa na dini? Dini imefanya mambo fulani mazuri ambayo yamenufaisha jamii na mtu mmoja-mmoja. Hata hivyo, imesababisha madhara makubwa pia. Kitabu Encyclopedia of Religion and War kinasema hivi: “Baadhi ya vita vibaya zaidi katika historia ya wanadamu vimetokana na tofauti za kidini.” Mara nyingi, viongozi wa kidini wametumia dini si kwa ajili ya ibada tu bali kuendeleza masuala ya kisiasa. Isitoshe, viongozi wengine wa kidini wameficha maovu ambayo viongozi wa dini yao wamefanya, kama vile kuwatendea watu vibaya kingono au kuhusika katika uhalifu wa kifedha.
Ikiwa umetamaushwa na dini, huenda ukajiuliza, Mungu ana maoni gani kuhusu dini? Biblia inaonyesha kwamba Mungu hapendezwi na dini nyingi kwa sababu ya mambo ambayo zimefanya. Isitoshe, Biblia ina unabii mbalimbali unaoonyesha jinsi Mungu atakavyoshughulika na dini. Inatumia lugha ya mfano kufafanua kwamba hivi karibuni, Mungu atachukua hatua kali dhidi ya dini ulimwenguni pote.
Biblia inasema ni nini kitakachoipata dini wakati ujao?
Unabii: Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinazungumzia kuhusu kahaba anayeitwa Babiloni Mkubwa. Kahaba huyo ameketi juu ya mnyama wa mwituni mwenye rangi nyekundu. Hata hivyo, baadaye, mnyama huyo wa mwituni anamgeukia na kumuua kahaba huyo.—Ufunuo 17:3, 5, 16.
Maana: Kahaba huyo, Babiloni Mkubwa, anawakilisha dini zote za uwongo, yaani, dini ambazo Mungu amezikataa. a Mnyama wa mwituni mwenye rangi nyekundu anawakilisha Umoja wa Mataifa (UN). b Kahaba anaonekana akiwa ameketi juu ya mnyama wa mwituni mwenye rangi nyekundu, na hilo linaonyesha jinsi dini za uwongo zimekuwa zikijaribu kudhibiti au kuwa na uvutano juu ya shirika hilo la kisiasa. Mnyama huyo anamuua kahaba, na hilo linaonyesha kwamba shirika la Umoja wa Mataifa na nchi zinazounga mkono shirika hilo zitashambulia dini zote za uwongo ulimwenguni na kuziharibu. Dini za uwongo zitatokomea kabisa!
Dini za uwongo zitaangamizwa jinsi gani?
Unabii: “Zile pembe kumi ulizoona, na yule mnyama wa mwituni, hao watamchukia yule kahaba na kumfanya kuwa ukiwa na . . . kumteketeza kabisa kwa moto. Kwa maana Mungu alitia hilo ndani ya mioyo yao [mioyo ya viongozi wa ulimwengu] ili kutekeleza wazo lake, ndiyo, kutekeleza lile wazo lao moja kwa kumpa yule mnyama wa mwituni ufalme wao . . . Mapigo yake yatakuja katika siku moja, kifo na kuomboleza na njaa kali, naye atateketezwa kabisa kwa moto, kwa sababu Yehova c Mungu, aliyemhukumu, ni mwenye nguvu.”—Ufunuo 17:16, 17; 18:8.
Maana: Mungu atalitia “wazo lake” katika mataifa ya ulimwengu huu. Atayachochea kulipa shirika la Umoja wa Mataifa “ufalme wao” au nguvu zao za kisiasa. Baada ya kupokea nguvu kutoka kwa mataifa, Umoja wa Mataifa utaangamiza dini za uwongo ulimwenguni pote. Ni kana kwamba tukio hilo lenye kushangaza linatokea “katika siku moja.” Linatokea haraka na bila kutarajiwa na watu wengi watashangaa sana kwa kuwa hawakulitazamia.—Ufunuo 18:21.
Kwa nini dini za uwongo zinastahili kuangamizwa?
Unabii: “Dhambi zake zimekusanyika pamoja mpaka mbinguni, naye Mungu amekumbuka matendo yake yasiyo ya haki.”—Ufunuo 18:5.
Maana: Kwa karne nyingi, dini za uwongo zimekuwa zikifanya mambo mengi maovu. Ona baadhi ya “dhambi” zinazofanywa na dini za uwongo ambazo zitafanya Mungu aziangamize.
Kujihusisha na siasa. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwamba hawapaswi kujihusisha na siasa. Badala yake, wanapaswa kuweka tumaini lao katika Ufalme wa Mungu, serikali inayotawala kutoka mbinguni ambayo itaondoa serikali za wanadamu. d (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10; Yohana 6:15; 18:36) Dini za uwongo zimewatia watu moyo kutumaini serikali za wanadamu. Kwa kuwa Babiloni Mkubwa amejihusisha katika siasa badala ya kuwa mshikamanifu kwa Mungu, unabii ulio katika kitabu cha Ufunuo unasema kwamba anafanya “uasherati” na kwa sababu hiyo anaitwa “kahaba mkubwa.”—Ufunuo 17:1, 2; Yakobo 4:4.
Ukatili. Dini za uwongo zimehusika katika vifo vya “wale wote ambao wameuawa duniani.” (Ufunuo 18:24) Dini nyingi hazijawafundisha waumini wao kufuatilia amani. Isitoshe, baadhi ya dini zimeunga mkono vita na hata ugaidi.
Pupa. Dini za uwongo zinaishi katika “anasa isiyo na aibu.” (Ufunuo 17:4; 18:7) Dini nyingi zimetumia uvutano wake na pia uhusiano wake na watu mbalimbali ili kujikusanyia utajiri. Pupa haimpendezi Mungu.—Tito 1:7.
Uwongo. Dini za uwongo huendeleza mafundisho na mazoea ambayo yanapingana na kweli ya Biblia. e Kwa kuwa dini za uwongo ndiyo chanzo cha mafundisho na mazoea mengi yanayowapotosha watu na kumvunjia Mungu heshima, katika unabii zinaitwa “mama . . . wa machukizo ya dunia.”—Ufunuo 17:5; 18:23.
Je, ni dini zote zitakazoangamizwa?
Hapana. Kitabu cha Ufunuo kinazungumza kuhusu kikundi cha watu kutoka mataifa yote kinachoitwa “umati mkubwa.” (Ufunuo 7:9) Watu walio katika umati huu mkubwa wanaonekana “wakiwa wamevaa kanzu nyeupe.” Hilo linamaanisha kwamba wao ni washikamanifu kwa Mungu na wanamwabudu kwa njia anayokubali. Umati mkubwa unaokoka “dhiki kuu.” Hiki ni kipindi ambacho dini za uwongo na pia maadui wengine wa Mungu wanaangamizwa. (Ufunuo 7:13, 14; 19:11, 19-21) Watu walio katika umati mkubwa ambao wamevaa kanzu nyeupe, ni washiriki wa dini ya kweli—dini ambayo itakuwepo milele. f
Umati mkubwa wa waabudu wa kweli wa Mungu utaokoka uharibifu wa dini za uwongo
Kuharibiwa kwa dini za uwongo kunamaanisha nini kwako?
Kujua kwamba Mungu haungi mkono mambo maovu ambayo dini zimefanya, kunaweza kukupa amani moyoni. Unaweza kutazamia wakati ujao kwa hamu ukijua kwamba hivi karibuni hakutakuwa tena na dini zinazomvunjia Mungu heshima na kuwafanya watu wateseke.
Na uwe na uhakika kwamba inawezekana kumwabudu Mungu katika njia anayokubali. Biblia inasema kwamba “waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.” (Yohana 4:23) Mungu anawaambia: “Tokeni kwake [Babiloni Mkubwa], watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya mapigo yake.” (Ufunuo 18:4, 5) Naam, Mungu anawaalika watu wamwabudu katika kweli. (1 Timotheo 2:3, 4) Anaahidi kwamba wale wanaokubali mwaliko wake, wataishi milele.—1 Yohana 2:17.
a Ili kujifunza kuhusu mambo manne yanayoweza kukusaidia kumtambua Babiloni Mkubwa, soma makala yenye kichwa, “Babiloni Mkubwa Ni Nani?”
b Ili ujifunze kuhusu mambo sita yanayomtambulisha mnyama huyu wa mwituni, soma makala yenye kichwa, “Mnyama-Mwitu Mwenye Rangi Nyekundu wa Ufunuo Sura ya 17 Ni Nani?”
c Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Tazama makala yenye kichwa “Yehova ni Nani?”
d Ili ujifunze mengi, tazama video yenye kichwa, Ufalme wa Mungu Ni Nini?
e Ili uone mifano, tazama sanduku “ Je, Dini za ‘Kikristo’ ni Sehemu ya Babiloni Mkubwa?”
f Ili ujifunze jinsi Biblia inavyoweza kukusaidia kuitambua dini ya kweli, soma makala yenye kichwa, “Ninaweza Kuipataje Dini ya Kweli?”

