Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | YESU ANATUOKOA—KUTOKANA NA NINI?

Kwa Nini Tunahitaji Kuokolewa?

Kwa Nini Tunahitaji Kuokolewa?

“Mwanadamu, aliyezaliwa na mwanamke, ana maisha mafupi na yenye kujaa msukosuko. Amechanuka kama ua na kukatiliwa mbali, naye hukimbia kama kivuli wala haendelei kuwako.”—Ayubu 14:1, 2.

Tangu zamani wanadamu wametamani sana kuishi milele wakiwa na afya bora na nguvu za ujana. Hata hivyo, inasikitisha kwamba tunakufa. Maneno hayo ya Ayubu yaliyotamkwa zaidi ya miaka 3000 iliyopita bado ni ya kweli.

Watu ulimwenguni pote wanatamani sana kuishi milele. Biblia inatuambia kwamba Mungu ameweka ndani ya mioyo yetu tamaa ya kuishi milele. (Mhubiri 3:11) Kwa sababu hali iko hivyo, je, unafikiri kwamba Mungu mwenye upendo angeweka ndani yetu tamaa ya jambo tusiloweza kufikia? Ikiwa umejibu hapana, uko sahihi. Neno la Mungu linasema kwamba kifo ni adui, na linaahidi kwamba ‘ataangamizwa.’—1 Wakorintho 15:26.

Ni wazi kwamba kifo ni adui. Hakuna mtu anayependa kifo. Hatari inapotokea sisi huiepuka kwa kujificha, au kuikimbia. Tunapokuwa wagonjwa, tunajitahidi kutafuta matibabu bora. Tunafanya yote tuwezayo ili kuepuka mambo yanayoweza kutusababishia kifo.

Je, kuna sababu yoyote ya kuamini kwamba adui huyo wa zamani ataondolewa? Bila shaka! Yehova Mungu, Muumba wetu, hakuwaumba wanadamu ili waishi miaka michache tu kisha wafe. Mungu hakukusudia wanadamu wafe. Alikusudia wanadamu waishi milele duniani, na siku zote makusudi yake hutimia.—Isaya 55:11.

Hata hivyo, kifo kitaangamizwa jinsi gani? Katika historia yote, wanadamu wamejitahidi kumaliza kifo bila mafanikio. Hata leo bado wanaendelea na jitihada hizo. Wanasayansi wamegundua chanjo na madawa yanayodhibiti baadhi ya magonjwa. Pia, wamechunguza muundo wa chembe za urithi za viumbe hai. Katika nchi nyingi, kwa wastani, watu wanaishi muda mrefu zaidi kuliko ilivyokuwa karne iliyopita. Hata hivyo, wanadamu hawajafaulu kuondoa kifo. Kama Biblia inavyosema, “wote wanarudi mavumbini.”—Mhubiri 3:20.

Hata hivyo, habari njema ni kwamba hatuhitaji kutegemea jitihada za wanadamu za kumaliza kifo. Yehova Mungu amefanya mpango wa kutukomboa kutokana na kifo, na atamtumia Yesu kufanya hivyo.