Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Kujifunza Biblia Kulikata Kiu Yangu ya Kupata Majibu

Kujifunza Biblia Kulikata Kiu Yangu ya Kupata Majibu
  • ALIZALIWA: 1987

  • CHI: AZERBAIJAN

  • HISTORIA: BABA MWISLAMU NA MAMA MYAHUDI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa jijini Baku, nchini Azerbaijan nikiwa wa pili kati ya watoto wawili. Baba yangu alikuwa Mwislamu na mama yangu alikuwa muumini wa dini ya Kiyahudi. Wazazi wangu walipendana na kila mmoja aliheshimu imani ya mwenzake. Mama alimuunga mkono Baba alipofunga mwezi wa Ramadhani, naye Baba akamuunga mkono Mama aliposherehekea Pasaka. Nyumbani tulikuwa na Kurani, Torati, na Biblia.

Niliamua kuwa Mwislamu. Ingawa niliamini kwamba Mungu yupo, bado nilikuwa na maswali yaliyonitatiza. Nilijiuliza hivi: ‘Kwa nini Mungu aliwaumba wanadamu, na kuna faida gani mtu ateseke maisha yake yote na kisha baadaye ateswe milele motoni?’ Kwa kuwa watu husema kwamba mambo yote yanayotendeka ni mapenzi ya Mungu, nilijiuliza, ‘Je, Mungu ndiye anayewasababishia wanadamu mateso na kufurahia kuwaona wakiteseka?’

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilianza kusali zile sala tano wanazosali Waislamu kila siku. Wakati huo, Baba alitupeleka mimi na dada yangu kwenye shule ya Kiyahudi. Baadhi ya masomo tuliyojifunza ni desturi za Kiyahudi na lugha ya Kiebrania. Kabla ya kuanza masomo yetu darasani, kila siku, tulihitaji kusali sala za Kiyahudi. Hivyo basi, asubuhi nilisali sala za Kiislamu, kisha baadaye nilipoenda shuleni nilisali sala za Kiyahudi.

Nilitamani sana kupata majibu yenye kuridhisha ya maswali yangu. Mara nyingi niliwauliza marabi waliofundisha shuleni: “Kwa nini Mungu aliwaumba wanadamu? Mungu anamwonaje baba yangu ambaye ni Mwislamu? Yeye ni mtu mzuri, kwa nini basi anaonwa kuwa najisi? Kwa nini Mungu alimuumba?” Majibu machache niliyopata hayakuniridhisha wala kunisadikisha hata kidogo.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Imani yangu katika Mungu iliyumba ghafla mwaka wa 2002. Tulikuwa tu tumehamia nchini Ujerumani, kisha juma moja baadaye baba yangu akapatwa na kiharusi na akapoteza fahamu. Kwa miaka mingi, nilikuwa nimesali familia yetu iwe na afya njema na maisha bora. Nilisali kila siku baba yangu apone kwani niliamini kwamba ni Mweza-Yote tu aliye na uwezo juu ya uhai na kifo. Niliwaza hivi: ‘Mungu hawezi kushindwa kutimiza ombi langu.’ Niliamini kwamba angejibu sala zangu. Kwa kusikitisha baba yangu alikufa.

Nilivunjika moyo sana kwa sababu nilihisi Mungu hanijali. Nikawaza hivi: ‘Huenda sijui kusali au pengine hakuna Mungu.’ Nililemewa na hisia hizo na nikaacha kusali zile sala tano. Dini nyingine hazikuniridhisha, hivyo basi nikaamua kwamba hakuna Mungu.

Miezi sita baadaye, Mashahidi wa Yehova walitutembelea nyumbani. Kwa kuwa tuliwadharau Wakristo, mimi na dada yangu tulitaka kuwaonyesha kwa upole kwamba walikuwa wamepotea. Tuliwauliza hivi: “Kwa nini Wakristo wanamwabudu Yesu, Maria, msalaba, na hata sanamu nyingine ilhali ni kuvunja zile Amri Kumi?” Wakitumia Maandiko, Mashahidi hao walituthibitishia kwamba Wakristo wa kweli hawaabudu sanamu na pia tunapaswa kusali kwa Mungu peke yake. Jambo hilo lilinishangaza sana.

Kisha tukauliza: “Vipi kuhusu Utatu? Ikiwa Yesu ni Mungu, angewezaje kuishi duniani na kuuawa na wanadamu?” Kwa mara nyingine tena walitumia Biblia kueleza kwamba Yesu si Mungu na wala halingani Naye. Mashahidi walisema kwamba hawaamini fundisho la Utatu kwa sababu hiyo. Nilishangaa na kuwaza, ‘Hawa kwa kweli ni Wakristo wa ajabu sana.’

Hata hivyo, bado nilitaka kujua kwa nini watu hufa na kwa nini Mungu anawaruhusu wateseke? Mashahidi walinionyesha kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, * kilichokuwa na majibu ya maswali yangu. Kisha wakaanza kunifundisha Biblia.

Kila tulipojifunza, nilipata majibu yenye kuridhisha kutoka kwenye Biblia. Nikajua jina la Mungu ni Yehova. (Zaburi 83:18) Na sifa yake kuu ni upendo. (1 Yohana 4:8) Pia, aliwaumba wanadamu kwa sababu alitaka wafurahie uhai. Nikaelewa kwamba ingawa Mungu huruhusu ukosefu wa haki uwepo, anauchukia na atauondoa milele. Pia nikajifunza kwamba uasi wa Adamu na Hawa umewaletea wanadamu madhara mengi. (Waroma 5:12) Baadhi ya madhara hayo ni kufiwa na wapendwa wetu, kama nilivyofiwa na baba yangu. Hata hivyo, Mungu ataondoa misiba kama hiyo katika dunia mpya inayokuja ambapo wafu watafufuliwa.—Matendo 24:15.

Kujifunza Biblia kulikata kiu yangu ya kupata majibu. Nikaanza tena kumwamini Mungu. Nilipoendelea kuwafahamu Mashahidi wa Yehova, nilitambua kwamba wao ni undugu wa ulimwenguni pote. Umoja na upendo wao ulinivutia sana. (Yohana 13:34, 35) Yale niliyojifunza kumhusu Yehova yalinichochea nitake kumtumikia, hivyo nikaamua kuwa Shahidi wa Yehova. Nilibatizwa Januari 8 mwaka wa 2005.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Majibu yenye kuridhisha niliyopata kwenye Biblia yalifanya niwe na mtazamo mzuri maishani. Nimepata amani ya moyoni. Ninapata shangwe kubwa na faraja kutokana na tumaini la kumwona baba yangu tena atakapofufuliwa, kama Neno la Mungu linavyoahidi.—Yohana 5:28, 29.

Mimi na mume wangu Jonathan tunamtumikia Mungu, na tumekuwa na ndoa yenye furaha kwa miaka sita. Tumejifunza kwamba ukweli kumhusu Mungu ni rahisi na unaeleweka, na ukweli huo ni hazina yenye thamani sana. Ndio maana tunapenda kuwaeleza wengine kuhusu imani yetu na tumaini letu zuri. Sasa ninaelewa kwamba Mashahidi wa Yehova si Wakristo wa ajabu bali ni Wakristo wa kweli.

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.