Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tunapaswa Kusali kwa Yesu?

Je, Tunapaswa Kusali kwa Yesu?

MTAFITI mmoja aliwauliza vijana 800 kutoka dini mbalimbali ikiwa wanaamini kwamba Yesu anajibu sala. Zaidi ya asilimia 60 ya vijana hao walisema kwamba Yesu anajibu sala. Hata hivyo, msichana mmoja alisema kwamba Mungu ndiye anayejibu sala.

Wewe una maoni gani? Je, tunapaswa kusali kwa Yesu au kwa Mungu? * Ili tupate jibu, kwanza acheni tuchunguze jinsi Yesu alivyowafundisha wanafunzi wake kusali.

YESU ALITUFUNDISHA TUSALI KWA NANI?

Yesu alitufundisha jinsi ya kusali, na alituambia yule tunayepaswa kusali kwake.

Aliposali kwa Baba yake wa mbinguni, Yesu aliweka mfano tunaopaswa kuufuata

MAFUNDISHO YAKE: Mmoja wa wanafunzi wake alipomwambia Yesu, “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali,” Yesu alimjibu hivi: “Wakati wowote mnaposali, semeni, ‘Baba.’” (Luka 11:1, 2) Pia, katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu aliwahimiza wasikilizaji wake wasali. Alisema hivi: “Sali kwa Baba yako.” Kisha akawahakikishia hivi: “Baba yenu anajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla hamjamwomba.” (Mathayo 6:6, 8) Katika usiku wake wa mwisho akiwa binadamu, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mkimwomba Baba jambo lolote atawapa katika jina langu.” (Yohana 16:23) Kwa hiyo, Yesu alifundisha kwamba tunapaswa kusali kwa Baba yake ambaye pia ni Baba yetu, Yehova Mungu.—Yohana 20:17.

MFANO WAKE: Kama alivyowafundisha wengine, Yesu mwenyewe alisali hivi kwa Mungu: “Ninakusifu hadharani wewe, Baba, Bwana wa mbingu na dunia.” (Luka 10:21) Wakati mmoja, “Yesu akainua macho yake kuelekea mbinguni na kusema: ‘Baba, ninakushukuru kwamba umenisikia.’”(Yohana 11:41) Pia muda mfupi kabla hajafa, Yesu alisali hivi: “Baba, ninaikabidhi roho yangu mikononi mwako.” (Luka 23:46) Yesu alituwekea mfano mzuri wa kufuata tunaposali kwa Baba yake—“Bwana wa mbingu na dunia.” (Mathayo 11:25; 26:41, 42; 1 Yohana 2:6) Je, wanafunzi wake wa mapema walifuata maagizo ya Yesu?

WAKRISTO WA MAPEMA WALISALI KWA NANI?

Muda mfupi baada ya Yesu kurudi mbinguni, wanafunzi wake walianza kuteswa na kunyanyaswa na wapinzani. (Matendo 4:18) Kwa kweli walisali ili wapate msaada—lakini walisali kwa nani? “Wakampaazia Mungu sauti zao kwa umoja,” ili awasaidie “kupitia jina la mtumishi [wake] mtakatifu Yesu.” (Matendo 4:24, 30) Kwa hiyo, wanafunzi walifuata maelekezo ya Yesu kuhusu jinsi ya kusali. Walisali kwa Mungu, siyo kwa Yesu.

Miaka kadhaa baadaye, mtume Paulo alieleza jinsi yeye na wenzake walivyosali. Aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Sikuzote sisi humshukuru Mungu Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo tunaposali kwa ajili yenu.” (Wakolosai 1:3) Pia Paulo aliwaandikia waamini wenzake hivi: “Katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo mkimtolea shukrani sikuzote Mungu na Baba yetu.” (Waefeso 5:20) Kwa msingi wa maneno hayo, tunaona kwamba Paulo aliwatia moyo waamini wenzake wasali kwa “Mungu na Baba yetu kwa ajili ya mambo yote”—na bila shaka kupitia jina la Yesu.—Wakolosai 3:17.

Kama walivyofanya Wakristo wa mapema, tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Yesu kwa kufuata maelekezo yake kuhusu jinsi ya kusali. (Yohana 14:15) Tunaposali kwa Baba yetu wa mbinguni—yeye peke yake—maneno ya andiko la Zaburi 116:1, 2 yatakuwa na maana kwetu: “Ninajawa na upendo, kwa sababu Yehova husikia sauti yangu . . . nami nitaita siku zangu zote.” *

^ fu. 3 Kulingana na Maandiko, Yesu na Mungu hawalingani. Kwa habari zaidi, soma sura ya 4 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 11 Ili sala zetu zisikiwe na Mungu, ni lazima tujitahidi kufuata sheria zake. Kwa habari zaidi, soma sura ya 17 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.