Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Peshitta ya Kisiria—Inafunua Historia ya Utafsiri wa Biblia

Peshitta ya Kisiria—Inafunua Historia ya Utafsiri wa Biblia

Kwa siku tisa mwaka wa 1892, dada wawili mapacha Agnes Smith Lewis na Margaret Dunlop Gibson walisafiri kwa ngamia jangwani na kufika kwenye Makao ya Watawa ya St. Catherine yaliyo chini ya Mlima Sinai. Kwa nini wanawake hao waliokuwa na umri wa karibu miaka 50 walisafiri katika eneo hilo ambalo wakati huo lilikuwa hatari sana? Jibu la swali hilo linaweza kukusadikishia zaidi kwamba Biblia ni sahihi.

Agnes Smith Lewis na Makao ya Watawa ya St. Catherine

KABLA hajarudi mbinguni, Yesu aliwaagiza wanafunzi wake watoe ushahidi kumhusu “katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Wanafunzi walifanya hivyo kwa bidii na ujasiri. Lakini huduma yao huko Yerusalemu ilipingwa vikali na hata Stefano akauawa. Wanafunzi wengi wa Yesu walikimbilia Antiokia ya Siria, mojawapo ya majiji makubwa zaidi katika Milki ya Roma, ambalo lilikuwa kilomita 550 kaskazini ya Yerusalemu.—Matendo 11:19.

Walipofika Antiokia, wanafunzi waliendelea kuhubiri, “habari njema” kuhusu Yesu, na watu wengi wasio Wayahudi wakawa waamini. (Matendo 11:20, 21) Ingawa lugha ya Kigiriki ndiyo iliyozungumzwa katika jiji la Antiokia, watu walizungumza Kisiria katika eneo lililozunguka jiji hilo.

HABARI NJEMA YATAFSIRIWA KATIKA KISIRIA

Idadi ya Wakristo waliozungumza Kisiria ilipozidi kuongezeka katika karne ya pili, kukawa na uhitaji wa kutafsiri habari njema katika lugha yao. Basi, inaonekana kwamba Kisiria, bali si Kilatini, ndiyo lugha ya kwanza  iliyotumika kutafsiri Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

Karibu mwaka wa 170 W.K., mwandishi Msiria Tatian (karibu 120-173 W.K.) aliunganisha vitabu vinne vinavyokubalika vya Injili na akaandika katika Kigiriki au Kisiria maandishi yanayojulikana kama Diatessaron, neno la Kigiriki linalomaanisha “ujumbe wa vitabu vinne vya [Injili].” Baadaye, Ephraem Msiria (karibu 310-373 W.K.) aliandika kitabu cha ufafanuzi kuhusu maandishi ya Diatessaron, na hivyo kuthibitisha kwamba yalitumiwa na Wakristo Wasiria.

Maandishi ya Diatessaron ni muhimu sana kwetu leo. Kwa nini? Katika karne ya 19, wasomi fulani walidai kwamba vitabu vya Injili viliandikwa katika karne ya pili, kati ya 130 W.K. na 170 W.K., na hivyo haviwezi kuwa na masimulizi sahihi ya maisha ya Yesu. Hata hivyo, hati za kale za Diatessaron ambazo zimepatikana zimethibitisha kwamba vitabu vya Injili vya Mathayo, Marko, Luka, na Yohana tayari vilikuwa vimesambazwa sana kufikia karne ya pili. Hivyo, lazima viliandikwa mapema zaidi. Isitoshe, kwa vile Tatian alikusanya vitabu vinne vya Injili vinavyokubalika katika Diatessaron, na hakutia ndani vitabu vya injili vya kiapokrifa, inaonekana injili za kiapokrifa hazikuonwa kuwa halali.

Vitabu vya Pentateuki vya Peshitta ya Kisiria, 464 W.K., ndiyo hati ya pili ya kale zaidi ya maandishi ya Biblia yenye tarehe

Kufikia mwanzoni mwa karne ya tano, tafsiri ya Biblia ya Kisiria ilikuwa ikisomwa na watu wengi kaskazini mwa Mesopotamia. Inaelekea tafsiri hiyo ilitokezwa katika karne ya pili au ya tatu W.K., na ilitia ndani vitabu vyote vya Biblia isipokuwa barua ya 2 ya Petro, barua ya 2 na ya 3 ya Yohana, Yuda, na Ufunuo. Tafsiri hiyo inaitwa Peshitta, jina linalomaanisha “Rahisi” au “Wazi.” Peshitta ni mojawapo ya maandishi ya kale na muhimu zaidi ya historia ya utafsiri wa Biblia.

Inapendeza kwamba hati moja ya Peshitta ina tarehe inayolingana na mwaka wa 459/460 W.K., na hivyo kuifanya iwe hati ya kale zaidi ya Biblia yenye tarehe hususa. Karibu mwaka wa 508 W.K., tafsiri ya Peshitta ilifanyiwa marekebisho na vitabu vitano vilivyokosekana vikaongezwa. Tafsiri hiyo ikaitwa Philoxenia Version.

HATI ZAIDI ZA KISIRIA ZAPATIKANA

Kufikia karne ya 19, karibu nakala zote za Kigiriki za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zilikuwa za kuanzia karne ya tano na kuendelea. Kwa hiyo, wasomi wa Biblia walipendezwa hasa na matoleo ya kale zaidi kama vile Vulgate ya Kilatini na Peshitta ya Kisiria. Wakati huo, watu fulani waliamini kwamba Peshitta ilikuwa marekebisho ya toleo la kale zaidi la Kisiria. Lakini toleo hilo halikuwa limepatikana. Kwa vile Biblia ilitafsiriwa katika Kisiria karne ya pili, toleo hilo lingefunua historia ya utafsiri wa Biblia, na lingekuwa muhimu sana kwa wasomi wa Biblia! Je, kulikuwa na toleo la kale la tafsiri ya Kisiria? Je, lingepatikana?

Hati ya Kisiria ya Sinai. Pambizoni kuna maandishi ya vitabu vya Injili

Ndiyo! Hati mbili zenye thamani zilipatikana. Hati ya kwanza ilikuwa ya karne ya tano. Ni mojawapo ya hati nyingi za Kisiria zilizoletwa katika Jumba la Makumbusho la Uingereza kutoka makao ya watawa ya Jangwa la Nitria huko Misri mwaka wa 1842. Hati hiyo iliitwa Cureton ya Kisiria kwa sababu William Cureton, msaidizi wa mtunza-hati wa Jumba la Makumbusho la Uingereza ndiye aliyeipata na kuichapisha. Hati hiyo muhimu ina vitabu vinne vya Injili kwa mpangilio huu Mathayo, Marko, Yohana, na Luka.

Hati ya pili ambayo ipo mpaka leo ni hati ya Kisiria ya Sinai. Inaaminika kwamba wale dada wawili mapacha waliotajwa mwanzoni mwa makala hii ndio walioipata. Ingawa Agnes hakuwa na shahada ya chuo kikuu, alijifunza lugha nane za kigeni, kutia ndani Kisiria. Mwaka wa 1892, Agnes alipata hati muhimu sana katika makao ya watawa ya St. Catherine huko Misri.

 Alipata hati ya Kisiria katika kabati fulani lenye giza. Simulizi lake linasema, “haikunivutia kwa sababu ilikuwa na uchafu, na kurasa zake zilikuwa zimeshikamana kwa vile hazikuwa zimefunguliwa” kwa karne nyingi. Maandishi ya awali ya hati hiyo yalikuwa yamefutwa na kuandikwa upya katika Kisiria kuhusu watawa wa kike. Hata hivyo, chini ya maandishi hayo Agnes aliona maneno yaliyofutwa na juu ya kurasa maneno “ya Mathayo,” “ya Marko,” au “ya Luka.” Alikuwa amepata karibu kodeksi nzima ya Kisiria ya vitabu vinne vya Injili! Wasomi wanaamini kwamba kodeksi hiyo iliandikwa mwishoni mwa karne ya nne.

Hati ya Kisiria ya Sinai inaonwa kuwa mojawapo ya hati muhimu zaidi za Biblia zilizopatikana, kutia ndani hati nyingine za Kigiriki kama vile Kodeksi ya Sinai na Kodeksi ya Vatikani. Sasa, inaaminiwa kwamba hati ya Cureton na hati ya Sinai ni nakala za Kisiria za vitabu vya Injili zilizoandikwa mwishoni mwa karne ya pili au mwanzoni mwa karne ya tatu.

“NENO LA MUNGU WETU, LITADUMU MPAKA WAKATI USIO NA KIPIMO”

Je, hati hizo zinaweza kuwasaidia wanafunzi wa Biblia leo? Bila shaka! Kwa mfano, fikiria umalizio mrefu wa Injili ya Marko ulio katika Biblia fulani baada ya Marko 16:8. Unapatikana katika Kodeksi ya Alexandria ya karne ya tano, Vulgate ya Kilatini, na kwingineko. Hata hivyo, hati mbili za karne ya nne za Kigiriki ambazo zinaaminiwa—Kodeksi ya Sinai na Kodeksi ya Vatikani—zinaishia kwenye Marko 16:8. Hati ya Kisiria ya Sinai pia haina umalizio huo mrefu, hivyo inazidi kuthibitisha kwamba umalizio huo uliongezwa baadaye na kwamba haukuwepo mwanzoni kwenye Injili ya Marko.

Fikiria mfano mwingine. Katika karne ya 19, karibu tafsiri zote za Biblia zilikuwa na maneno yanayounga mkono Utatu kwenye 1 Yohana 5:7. Hata hivyo, maneno hayo hayako kwenye hati za kale zaidi za Kigiriki. Wala hayako kwenye Peshitta, na hivyo kuthibitisha kwamba maneno hayo yaliyoongezwa kwenye 1 Yohana 5:7 yanapotosha maandishi ya Biblia.

Ni wazi kwamba kama ilivyoahidiwa, Yehova Mungu amelihifadhi Neno lake Takatifu. Linatuhakikishia hivi: “Majani mabichi yamekauka, ua limenyauka; lakini kwa habari ya neno la Mungu wetu, litadumu mpaka wakati usio na kipimo.” (Isaya 40:8; 1 Petro 1:25) Tafsiri inayoitwa Peshitta inatimiza sehemu ndogo lakini muhimu katika kutafsiri kwa usahihi ujumbe wa Biblia kwa wanadamu wote.