Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

2 Tusali Kwa Nani?

2 Tusali Kwa Nani?

Sala

2 Tusali Kwa Nani?

JE, MUNGU anasikiliza sala zote bila kujali zinaelekezwa kwa nani? Leo, watu wengi wanafikiria hivyo. Wazo hilo linaungwa mkono na watu wanaopendelea kuchanganya ibada na wanaotaka dini zote zikubalike, ijapokuwa kuna tofauti kati ya dini hizo. Hata hivyo, je, inawezekana kwamba wazo hilo si la kweli?

Biblia inafundisha kwamba mara nyingi watu hawaelekezi sala zao kwa Mungu wa kweli. Zamani Biblia ilipokuwa ikiandikwa, lilikuwa jambo la kawaida kwa watu kuelekeza sala zao kwa sanamu za kuchongwa. Hata hivyo, Mungu alionya tena na tena kuhusu zoea hilo. Kwa mfano, andiko la Zaburi 115:4-6 linasema hivi kuhusu sanamu: “Zina masikio, lakini haziwezi kusikia.” Wazo hilo liko wazi. Kwa nini usali kwa mungu ambaye hawezi kukusikia?

Simulizi fulani la Biblia linaeleza zaidi kuhusu jambo hilo. Nabii wa kweli Eliya aliwaambia manabii wa Baali wasali kwa mungu wao, kisha yeye asali kwa Mungu wake. Eliya alisema kwamba Mungu wa kweli angejibu sala lakini yule wa uwongo hangejibu. Manabii hao wa Baali walikubali kufanya hivyo, nao wakasali kwa bidii kwa muda mrefu, huku wakilia kwa sauti kubwa—lakini hawakufanikiwa! Simulizi hilo linasema: “Hapakuwa na yeyote aliyejibu, wala aliyewasikiliza.” (1 Wafalme 18:29) Lakini ni nini kilichotokea Eliya aliposali?

Baada ya Eliya kusali, Mungu wake alijibu mara moja kwa kutuma moto kutoka mbinguni ili kuteketeza dhabihu ambayo Eliya alitayarisha. Kwa nini sala hiyo ilijibiwa? Kuna jambo moja muhimu katika sala ya Eliya ambayo inapatikana katika 1 Wafalme 18:36, 37. Sala yake ilikuwa fupi sana. Katika Kiebrania cha awali, sala hiyo ina maneno 30 hivi. Hata hivyo, katika maneno hayo machache, Eliya alitumia mara tatu jina la Mungu la kibinafsi, Yehova.

Baali, ambaye jina lake linamaanisha “mmiliki” au “bwana,” alikuwa mungu wa Wakanaani, na kila eneo lilikuwa na sanamu yake ya Baali. Hata hivyo, Yehova ni jina la kipekee, linalomrejelea Mungu mmoja tu katika ulimwengu wote. Mungu huyu aliwaambia watu wake hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu; nami sitampa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe, wala sitazipa sanamu za kuchongwa sifa yangu.”—Isaya 42:8.

Je, sala ya Eliya na zile za manabii wa Baali zilienda kwa yule Mungu wa kweli? Ibada ya Baali iliwashushia watu heshima kwa kuwataka wafanye ukahaba na hata kutoa watu dhabihu. Kinyume cha hilo, ibada ya Yehova iliwakweza watu wake, Israeli, kwa kuwaepusha na matendo hayo mapotovu. Hebu fikiria hili: Ikiwa unamwandikia barua rafiki unayemheshimu sana, je, unaweza kutarajia barua hiyo ipelekwe kwa mtu mwenye jina tofauti na ambaye ana sifa tofauti na zile za rafiki yako? Bila shaka, hapana!

Ikiwa unasali kwa Yehova, unasali kwa Muumba, ambaye ni Baba ya wanadamu wote. a Nabii Isaya alisali hivi: “Wewe, Ee Yehova, ni Baba yetu.” (Isaya 63:16) Huyo ndiye ambaye Yesu Kristo alimrejelea alipowaambia wafuasi wake: “Mimi ninapanda kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu na kwa Mungu wangu na Mungu wenu.” (Yohana 20:17) Yehova ndiye Baba ya Yesu. Huyo ndiye Mungu ambaye Yesu alisali kwake na kuwafundisha wafuasi wake wafanye vivyo hivyo.—Mathayo 6:9.

Je, Biblia inatuagiza tusali kwa Yesu, kwa Maria, kwa watakatifu, au kwa malaika? Hapana—tunapaswa kusali kwa Yehova tu. Acheni tuchunguze sababu mbili za kufanya hivyo. Kwanza, sala ni ibada, na Biblia inasema kwamba ni Yehova pekee anayepaswa kuabudiwa. (Kutoka 20:5) Pili, Biblia inafunua kwamba Yehova pekee ndiye mwenye jina la cheo “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Hata ingawa Yehova amewapa wengine majukumu mengi, hajampa mtu yeyote jukumu la kusikiliza sala. Ameahidi kusikiliza sala zetu yeye mwenyewe.

Hivyo, ikiwa unataka Mungu asikilize sala zako, kumbuka himizo hili linalopatikana katika Maandiko: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” (Matendo 2:21) Hata hivyo, je, Yehova anasikiliza sala zote bila masharti yoyote? Au kuna jambo lingine tunalohitaji kujua ikiwa tunataka Yehova asikilize sala zetu?

[Maelezo ya Chini]

a Mapokeo fulani ya kidini yanasema kwamba ni kosa kutaja jina la kibinafsi la Mungu, hata katika sala. Hata hivyo, jina hilo linapatikana karibu mara 7,000 katika lugha za awali za Biblia, hasa katika sala na zaburi za watumishi waaminifu wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Jambo ambalo Eliya aliwaambia manabii wa Baali wafanye linathibitisha kwamba sala zote hazielekezwi kwa Mungu wa kweli