Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuungama Dhambi Ni Takwa la Mungu?

Je, Kuungama Dhambi Ni Takwa la Mungu?

Je, Kuungama Dhambi Ni Takwa la Mungu?

Kuungama dhambi zako kwa padri au kwa mhudumu wa dini, bado ni sehemu ya desturi za kidini na ya ibada katika makanisa mengi. Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo ambapo chochote kinakubalika, je, kuungama dhambi ni jambo linalofaa au hata la lazima?

WATU wana maoni tofauti-tofauti kuhusu jambo hilo. Kwa mfano, gazeti National Post la Kanada linaripoti kuhusu mtu mmoja anayekubali kwamba ingawa si rahisi kumwambia kila mtu kosa lako, “unajisikia vizuri sana unapomjulisha mtu mwingine kosa hilo, anaposali pamoja nawe, na kukuambia la kufanya.” Kinyume cha hilo, kitabu Bless Me, Father, for I Have Sinned (Padre Nibariki kwa Kuwa Nimetenda Dhambi), kinamnukuu mtu aliyesema: “Kuungama ni kati ya mambo yenye kuumiza hisia zaidi katika Kanisa. Kunasababisha wasiwasi mwingi sana.” Biblia inasema nini kuhusu kuungama dhambi?

Maoni ya Biblia

Katika Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli kuna maagizo hususa kuhusu hatua zilizopaswa kuchukuliwa mtu akifanya dhambi. Kwa mfano, mtu alipomtendea mwenzake dhambi au kuvunja mojawapo ya sheria za Mungu, alipaswa kuungama mbele ya kuhani aliyewekwa rasmi wa kabila la Lawi. Kuhani angetoa dhabihu ya upatanisho kwa Mungu ili mtenda dhambi huyo asamehewe dhambi yake.—Mambo ya Walawi 5:1-6.

Miaka mingi baadaye, nabii Nathani alipomkemea Mfalme Daudi kwa sababu ya dhambi zake, Daudi aliitikia jinsi gani? Alikubali kosa lake mara moja kwa kusema: “Nimemtendea Yehova dhambi.” (2 Samweli 12:13) Pia, alisali, akimwomba Mungu amwonyeshe rehema. Matokeo yakawa nini? Baadaye Daudi aliandika: “Mwishowe niliungama dhambi yangu kwako, wala sikufunika kosa langu. Nilisema: ‘Nitaungama makosa yangu kwa Yehova.’ Nawe mwenyewe ukanisamehe kosa la dhambi zangu.”—Zaburi 32:5; 51:1-4.

Kuungama dhambi bado lilikuwa takwa la Mungu katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza. Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, ambaye alikuwa mmoja kati ya wanaume waliokuwa kama nguzo katika kutaniko jijini Yerusalemu, aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Ungameni waziwazi dhambi zenu kwa mtu na mwenzake na kusali kwa ajili ya mtu na mwenzake, ili mponywe.” (Yakobo 5:16) Hivyo basi, Wakristo wanapaswa kuungama kuhusu nini na kwa nani?

Tunapaswa Kuungama Nini?

Sisi wanadamu wasio wakamilifu tuna mwelekeo wa kutenda bila kufikiri au kutumia ulimi wetu vibaya na hivyo kukoseana kila siku. (Waroma 3:23) Je, hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kuungama kila kosa kwa mtu fulani mwenye mamlaka?

Ingawa kila dhambi ni kosa mbele za Mungu, yeye huzingatia udhaifu wetu na kutuonyesha rehema kwa sababu sisi ni binadamu wasio wakamilifu. Mtunga-zaburi alisema: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama? Kwa maana kwako wewe kuna msamaha wa kweli, ili upate kuogopwa.” (Zaburi 130:3, 4) Kwa hiyo, tunapaswa kufanya nini tunapowakosea wengine, labda bila kukusudia? Kumbuka kwamba sala ya kielelezo ya Yesu aliyowafundisha wafuasi wake inatia ndani ombi hili: “Utusamehe dhambi zetu, kwa maana sisi wenyewe pia humsamehe kila mtu aliye na deni letu.” (Luka 11:4) Ndiyo, Mungu atatusamehe ikiwa tutamwomba msamaha katika jina la Yesu.—Yohana 14:13, 14.

Ona kwamba Yesu alionyesha ni lazima sisi pia tuwasamehe watu ‘walio na deni letu.’ Mtume Paulo aliwakumbusha waamini wenzake: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.” (Waefeso 4:32) Tunapowasamehe wengine makosa yao, tunakuwa na sababu nzuri ya kutarajia Mungu atusamehe makosa yetu pia.

Lakini, namna gani dhambi nzito kama vile kuiba, kudanganya kimakusudi, uasherati, ulevi, na kadhalika? Yeyote anayefanya dhambi hizo anavunja sheria za Mungu na hivyo anamtendea Mungu dhambi. Je, mtu anapaswa kuungama dhambi hizo?

Tunapaswa Kuungama Dhambi kwa Nani?

Mungu hajawapa wanadamu mamlaka ya kusamehe dhambi anazotendewa. Ni yeye tu anayeweza kufanya hivyo. Biblia inatuambia hivi waziwazi: “Tukiungama dhambi zetu, [Mungu] ni mwaminifu na mwadilifu hata atusamehe dhambi zetu na kutusafisha ukosefu wote wa uadilifu.” (1 Yohana 1:9) Hata hivyo, tunapaswa kuungama dhambi hizo kwa nani?

Kwa kuwa Mungu peke yake ndiye anayeweza kusamehe dhambi, basi tunapaswa kuungama kwake. Daudi alifanya hivyo, kama tulivyoona. Hata hivyo, msamaha unaweza kutolewa kwa msingi gani? Biblia inatuambia: “Tubuni na mgeuke ili dhambi zenu zipate kufutwa, ili majira ya kuburudisha yapate kuja kutoka kwa uso wa Yehova.” (Matendo 3:19) Naam, ili mtu asamehewe, inabidi akubali dhambi yake, aiungame, na pia awe tayari kuacha mwenendo huo mbaya. Mara nyingi, hatua hii huwa ngumu. Lakini kuna msaada.

Kumbuka maneno haya ya mwanafunzi Yakobo ambayo tayari yametajwa: “Ungameni waziwazi dhambi zenu kwa mtu na mwenzake na kusali kwa ajili ya mtu na mwenzake, ili mponywe.” Yakobo aliendelea kusema: “Dua ya mtu mwadilifu, inapofanya kazi, ina nguvu nyingi.” (Yakobo 5:16) “Mtu mwadilifu” anaweza kuwa mmoja wa “wanaume wazee wa kutaniko,” ambao Yakobo anawataja katika mstari wa 14. Katika kutaniko la Kikristo, kuna “wanaume wazee” kiroho, au wazee, waliowekwa rasmi kuwasaidia wale wanaotafuta msamaha wa Mungu. ‘Wanaume hao wazee’ hawawezi kusamehe dhambi, kwa kuwa hakuna mwanadamu ambaye amepewa mamlaka ya kumsamehe mtu ambaye amemtendea Mungu dhambi. * Hata hivyo, wanaume hao wana sifa za kiroho zinazowafanya wastahili kukaripia na kumrekebisha mtu aliyefanya dhambi nzito, wakimsaidia atambue uzito wa dhambi yake na uhitaji wa kutubu.—Wagalatia 6:1.

Kwa Nini Uungame Dhambi Zako?

Iwe dhambi iliyofanywa ni nzito au si nzito, mtu aliyeifanya ameharibu uhusiano wake pamoja na Mungu na mwanadamu mwenzake. Kwa hiyo, anaweza kuteseka moyoni. Hiyo ni kwa sababu ya dhamiri tuliyopewa na Muumba wetu. (Waroma 2:14, 15) Mtu anaweza kufanya nini?

Tukirejelea tena kitabu cha Yakobo, tunapata maneno haya yenye kutia moyo: “Je, kuna yeyote mgonjwa [kiroho] kati yenu? Na awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, nao wasali juu yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamponya huyo asiyejisikia vizuri, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”—Yakobo 5:14, 15.

Kwa mara nyingine tena, wanaume wazee, au wazee, wanahimizwa washughulikie mahitaji ya kondoo. Jinsi gani? Si kwa kumsikiliza tu mtu anapoungama. Badala yake, kwa kuwa ugonjwa wa kiroho unahusika, wazee wanapaswa kuchukua hatua ili ‘kumponya mtu huyo asiyejisikia vizuri.’ Kuna mambo mawili yaliyotajwa na Yakobo ambayo yanaweza kufanywa.

Kwanza, Yakobo anataja ‘kupaka mafuta.’ Hilo linarejelea nguvu za kuponya za Neno la Mungu. Mtume Paulo alisema kwamba “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu . . . nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo,” kwa kuwa linapenya ndani kabisa katika akili na moyo wa mtu. (Waebrania 4:12) Kwa kutumia Biblia kwa ustadi, wanaume wazee wanaweza kumsaidia mtu aliye mgonjwa kiroho aone chanzo cha tatizo lake na kuchukua hatua zinazofaa kurekebisha mambo mbele za Mungu.

Kisha, anataja “sala ya imani.” Ingawa sala za wanaume wazee haziwezi kumfanya Mungu asifuate haki, sala hizo ni muhimu kwa Mungu, ambaye anatamani kusamehe dhambi kwa msingi wa fidia, au dhabihu ya ukombozi ya Kristo. (1 Yohana 2:2) Mungu yuko tayari kumsaidia mtenda dhambi yeyote anayetubu kikweli na anayefanya “matendo yanayostahili toba.”—Matendo 26:20.

Sababu iliyo kuu zaidi ya kuungama dhambi—iwe tumemtendea mwanadamu mwenzetu au tumemtendea Mungu—ni kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Yesu Kristo alionyesha kwamba tunapaswa kwanza kutatua tatizo lolote lile kati yetu na wanadamu wenzetu na kufanya amani pamoja nao ili tuweze kumwabudu Mungu tukiwa na dhamiri safi. (Mathayo 5:23, 24) Andiko la Methali 28:13 linasema: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” Tunapojinyenyekeza mbele za Yehova Mungu na kuomba msamaha, tunakubalika machoni pake na atatuinua katika wakati unaofaa.—1 Petro 5:6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Watu fulani wana maoni kwamba maneno ya Yesu katika Yohana 20:22, 23, yanaunga mkono kuungama dhambi zetu kwa wanadamu. Kwa habari zaidi kuhusu jambo hilo, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1996 (15/4/1996), ukurasa wa 28-29.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Mungu atatusamehe makosa yetu iwapo tutamwomba msamaha katika jina la Yesu

[Picha katika ukurasa wa 24]

Sababu iliyo kuu zaidi ya kuungama dhambi ni kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu