Hadithi ya Nne ya Uwongo: Mungu Ni Utatu
Hadithi ya Nne ya Uwongo: Mungu Ni Utatu
Ni nini chanzo cha hadithi hiyo? “Huenda watu wakafikiri kwamba fundisho la Utatu lilianzishwa mwishoni mwa karne ya 4. Kwa njia fulani, hilo ni kweli . . . Fundisho la ‘Mungu mmoja katika Watatu’ halikuwa limetia mizizi, na bila shaka, halikukubalika kabisa katika maisha na imani ya Wakristo kabla ya mwisho wa karne ya 4.”—New Catholic Encyclopedia (1967), Buku la 14, ukurasa wa 299.
“Baraza la Nisea lilikutana mnamo Mei 20, 325 (20/5/325) [W.K.]. Konstantino mwenyewe alikuwa mwenyekiti, na ndiye aliyeongoza mazungumzo, akapendekeza . . . njia muhimu ya kuonyesha uhusiano kati ya Kristo na Mungu katika fundisho lililotolewa na baraza hilo, kwamba Kristo ‘na Baba ni kitu kimoja.’ . . . Kwa sababu ya kumwogopa maliki au mfalme, maaskofu wote, isipokuwa wawili tu, walitia sahihi hati ya kukubali fundisho hilo, wengi wao walifanya hivyo bila kupenda.”—Encyclopædia Britannica (1970), Buku la 6, ukurasa wa 386.
Biblia inasema nini? “Akiwa amejaa roho takatifu, [Stefano] akakaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu, naye akasema: ‘Tazameni! Ninaziona mbingu zimefunguka na Mwana wa binadamu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.’”—Matendo 7:55, 56.
Maono hayo yalifunua nini? Akiwa amejaa nguvu ya utendaji ya Mungu, Stefano alimwona Yesu “akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.” Basi ni wazi kwamba Yesu hakugeuka na kuwa Mungu baada ya kufufuliwa na kwenda mbinguni badala yake, alikuwa mtu wa roho aliye tofauti na Mungu. Simulizi hilo halitaji kwamba kulikuwa na mtu wa tatu kando ya Mungu. Ingawa wanajaribu kutafuta Maandiko yanayounga mkono fundisho la Utatu, padri fulani kutoka Dominika Marie Émile Boismard, aliandika hivi katika kitabu chake À l’aube du christianisme—La naissance des dogmes (Wakati wa Mapambazuko ya Ukristo—Mwanzo wa Mafundisho ya Dini): “Fundisho la kwamba kuna watu watatu katika Mungu mmoja . . . halipatikani mahali popote katika Agano Jipya.”
Fundisho ambalo lilitetewa na Konstantino lilikusudiwa kukomesha mabishano ndani ya Kanisa la karne ya nne. Hata hivyo, kwa kweli fundisho hilo lilitokeza swala lingine: Je, Maria, mwanamke ambaye alimzaa Yesu, ni “Mama ya Mungu”?
Linganisha mistari hii ya Biblia: Mathayo 26:39; Yohana 14:28; 1 Wakorintho 15:27, 28; Wakolosai 1:15, 16
UKWELI:
Fundisho la Utatu lilianzishwa baadaye katika karne ya nne
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]
Museo Bardini, Florence