Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri

Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri

Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri

“Akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa.”—Wakolosai 3:21, Biblia Habari Njema.

BABA anaweza jinsi gani kuwafanya watoto wake wakate tamaa? Ni muhimu kwake kutambua jukumu lake akiwa baba. “Kuwa baba ni jukumu muhimu na la pekee linaloweza kuwa na matokeo katika ukuzi wa kiakili na kihisia wa watoto,” linasema jarida moja la afya ya akili.

Jukumu la baba ni nini? Katika familia nyingi baba hasa ndiye anayetoa nidhamu. Mara nyingi akina mama huwa wanawaambia watoto wao watundu, ‘Ngoja baba yako arudi utakiona!’ Bila shaka, watoto wanahitaji nidhamu inayotolewa kwa njia yenye usawaziko na uthabiti ili wawe watu wazima wenye sifa nzuri. Hata hivyo, kuwa baba mzuri kunahusisha mengi zaidi.

Inahuzunisha kwamba si baba wote waliokuwa na mfano mzuri wa kuwasaidia. Wanaume fulani walilelewa bila baba. Lakini katika visa vingine, huenda wanaume waliolelewa na baba mkali asiyeonyesha upendo wakawatendea watoto wao kwa njia hiyohiyo. Baba aliyelelewa chini ya hali hizo anaweza jinsi gani kuepuka kufuata kielelezo cha baba yake na kuwa baba mzuri?

Kuna chanzo chenye mashauri yanayofaa na yenye kutegemeka cha jinsi ya kuwa baba mzuri. Biblia ina mashauri bora kuhusu maisha ya familia. Mashauri yake si maneno matupu tu; na mwongozo wake hautudhuru kamwe. Mashauri ya Biblia yanaonyesha hekima ya Mtungaji wake, Yehova Mungu, ambaye ndiye Mwanzilishi wa familia. (Waefeso 3:14, 15) Ikiwa wewe ni baba, ingefaa uchunguze kile ambacho Biblia inasema kuhusu kuwalea watoto. *

Kuwa baba mzuri si muhimu tu kwa ajili ya afya ya kimwili na ya kihisia ya watoto wako bali pia kwa afya yao ya kiroho. Inaweza kuwa rahisi zaidi kwa mtoto aliye na uhusiano wa karibu na wenye upendo pamoja na baba yake kusitawisha uhusiano wa karibu sana na Mungu. Kwa kweli, Biblia inaonyesha kwamba kwa njia fulani, Yehova, Muumba wetu, ni Baba yetu. (Isaya 64:8) Acheni tuchunguze mambo sita ambayo watoto wanahitaji kutoka kwa baba. Katika kila jambo, tutachunguza jinsi kutumia kanuni za Biblia kunavyoweza kumsaidia baba kutimiza mahitaji hayo.

1 Watoto Wanahitaji Upendo wa Baba Yao

Yehova anatuwekea mfano mkamilifu akiwa Baba. Ikifafanua jinsi Mungu anavyohisi kumhusu Yesu, Mwana wake mzaliwa wa kwanza, Biblia inasema hivi: “Baba humpenda Mwana.” (Yohana 3:35; Wakolosai 1:15) Zaidi ya mara moja, Yehova alisema wazi kwamba anampenda Mwana wake na kumkubali. Yesu alipobatizwa, Yehova alizungumza kutoka mbinguni na kusema: “Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali wewe.” (Luka 3:22) Yesu hakuwahi kutia shaka ikiwa Baba yake anampenda. Baba wa kibinadamu anaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Mungu?

Usikose kuwaambia watoto wako unawapenda. Kelvin, baba mwenye watoto watano anasema: “Sikuzote nimejaribu kuwaonyesha watoto wangu upendo si kwa maneno tu, bali pia kwa kupendezwa na kila mmoja wao kibinafsi. Nilisaidia kuwabadili nepi na kuwaosha.” Kwa kuongezea, watoto wako wanahitaji kujua kwamba wana kibali chako. Kwa hiyo, usiwachambue kupita kiasi, na kuwasahihisha kila wakati. Badala yake, wapongeze kwa ukawaida. Donizete, ambaye ana binti wawili wanaobalehe, anapendekeza, “Baba anapaswa kutafuta nafasi za kuwapongeza watoto wake.” Watoto wakijua wana kibali chako watajiheshimu. Hilo litawasaidia kumkaribia Mungu.

2 Watoto Wanahitaji Kuwekewa Mfano Mzuri

Yesu anaweza kufanya “tu lile analomwona Baba akifanya,” inasema Yohana 5:19. Ona kwamba andiko hilo linasema kwamba Yesu aliona na kufanya yale ambayo Baba yake alikuwa “akifanya.” Mara nyingi watoto watafanya vivyo hivyo. Kwa mfano, ikiwa baba anamtendea mke wake kwa heshima na staha, huenda mwana wake akawaheshimu na kuwastahi wanawake anapokuwa mtu mzima. Si wavulana peke yao wanaojifunza kutoka kwa mfano wa baba yao bali pia mfano wa baba unaweza kuamua maoni ya wasichana kuhusu wanaume.

Je, ni vigumu kwa watoto wako kuomba msamaha? Mfano wako katika jambo hilo ni muhimu pia. Kelvin anakumbuka pindi moja wavulana wake wawili walipovunja kamera ya bei ghali. Alikasirika sana na kupiga meza ya mbao mpaka ikavunjika mara mbili. Lakini baadaye, Kelvin alihisi vibaya sana na akawaomba wote msamaha, kutia ndani mke wake, kwa kulipuka kwa hasira. Anahisi kwamba kuomba msamaha kulikuwa na matokeo mazuri kwa watoto wake; kwa kuwa si vigumu kwao kuomba msamaha.

3 Watoto Wanahitaji Mazingira Yenye Furaha

Yehova ni “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Haishangazi kwamba Mwana wake, Yesu, alifurahia sana kuwa pamoja na Baba yake. Methali 8:30 inatusaidia kuelewa uhusiano kati ya Yesu na Baba yake: “Nilipokuwa kando yake [Baba] nikiwa stadi wa kazi, . . . nikawa nikifurahi [“nikishangilia,” BHN] mbele zake wakati wote.” Kulikuwa na uhusiano wa karibu kama nini kati ya Baba na Mwana!

Watoto wako wanahitaji mazingira yenye furaha. Kucheza na watoto wako kunaweza kutokeza mazingira kama hayo. Kucheza pamoja kunawasaidia wazazi na watoto kuwa na uhusiano wa karibu. Felix, ambaye ana kijana anakubaliana na maoni hayo na anasema hivi: “Kutenga wakati kwa ajili ya tafrija pamoja na mwana wangu kumesaidia sana uhusiano wetu. Tunacheza pamoja, tunajumuika na marafiki, na kutembelea maeneo yenye kupendeza. Hilo limeimarisha umoja wa familia yetu.”

4 Watoto Wanahitaji Kufundishwa Mambo ya Kiroho

Yesu alifundishwa na Baba yake. Kwa hiyo, Yesu angeweza kusema hivi: “Mambo yale niliyoyasikia kutoka kwake [Baba] ninayasema ulimwenguni.” (Yohana 8:26) Kwa maoni ya Mungu, baba ana daraka la kuwafundisha watoto wake maadili na mambo ya kiroho. Moja kati ya madaraka yako ukiwa baba ni kukazia kanuni zinazofaa katika mioyo ya watoto wako. Mafundisho hayo yanapaswa kuanza mapema maishani. (2 Timotheo 3:14, 15) Felix alianza kumsomea mwanawe hadithi za Biblia alipokuwa mdogo. Felix alitumia hadithi zinazopendeza na picha zenye kuvutia kama zile zilizo katika Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. * Mwana wake alipokua, Felix alichagua vichapo vingine vinavyotegemea Biblia ambavyo vilifaa umri wa mwana wake.

Donizete anasema: “Ni kazi ngumu kufanya funzo la Biblia la familia lipendeze. Ni muhimu kwa wazazi kuonyesha wanathamini mambo ya kiroho kwa sababu watoto wanatambua haraka wazazi wasipofanya mambo wanayowaambia watoto wao.” Carlos, aliye na wana watatu, anasema: “Kila juma tunakuwa na mkutano wa kuchunguza mahitaji ya familia. Kila mshiriki wa familia ana nafasi ya kuchagua kile kitakachozungumziwa.” Sikuzote Kelvin alijitahidi kuzungumza na watoto wake kuhusu Mungu popote walipokuwa na walipofanya jambo lolote. Hilo linatukumbusha maneno haya ya Musa: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.”—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

5 Watoto Wanahitaji Nidhamu

Watoto wanahitaji nidhamu ili wawe watu wazima wenye mafanikio na wenye kutegemeka. Wazazi fulani wanafikiri kwamba kuwatia nidhamu watoto kunamaanisha kuwaadhibu vikali kwa kuwatisha au kuwatusi. Hata hivyo, Biblia haihusianishi nidhamu ya wazazi na ukali. Tofauti na hilo, wazazi wanapaswa kuwatia nidhamu watoto wao kwa upendo, kama Yehova anavyofanya. (Waebrania 12:4-11) Biblia inasema: “Akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Waefeso 6:4.

Mara kwa mara, huenda adhabu ikahitajika. Hata hivyo, mtoto anapaswa kuelewa kwa nini anaadhibiwa. Nidhamu kutoka kwa wazazi haipaswi kumfanya mtoto ahisi kwamba anachukiwa. Biblia haipendekezi kumchapa mtoto vibaya hadi umjeruhi. (Methali 16:32) Kelvin anasema, “Nilipohitaji kuwasahihisha watoto wangu kuhusu mambo mazito, sikuzote nilijaribu kuwafanya waelewe kwamba ninafanya hivyo kwa sababu ninawapenda.”

6 Watoto Wanahitaji Kulindwa

Watoto wanahitaji kulindwa dhidi ya uvutano usiofaa na mashirika yanayoweza kuwadhuru. Kwa kusikitisha, kuna “watu waovu” katika ulimwengu huu ambao wameazimia kuwatumia watoto vibaya. (2 Timotheo 3:1-5, 13) Unaweza kumlinda mtoto wako jinsi gani? Biblia inatoa shauri hili lenye hekima: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.” (Methali 22:3) Ili kuwakinga watoto wako dhidi ya msiba, unapaswa kuwa macho kutambua hatari. Fikiria hali zinazoweza kutokeza matatizo na uchukue hatua zinazofaa. Kwa mfano, ukiwaruhusu watoto wako watumie Intaneti, hakikisha kwamba wanajua kuitumia kwa njia salama. Huenda ikafaa kuiweka kompyuta mahali palipo wazi ambapo unaweza kuchunguza jinsi watoto wako wanavyoitumia.

Baba anahitaji kuwatayarisha na kuwazoeza watoto wake kwa ajili ya hatari ambazo huenda wakakabili katika ulimwengu huu uliojaa watu wanaotaka kuwatendea watoto vibaya. Je, watoto wako wanajua jinsi ya kushughulika na mtu anayetaka kuwatendea vibaya usipokuwepo? * Watoto wako wanapaswa kujua matumizi yanayofaa na yasiyofaa ya viungo vyao vya uzazi. Kelvin anasema: “Sikuwaachia watu wengine daraka la kuwafundisha watoto wangu jambo hilo, hata walimu. Nilihisi kwamba lilikuwa daraka langu kuwafundisha watoto wangu kuhusu ngono na hatari za watu wanaowatendea watoto vibaya.” Watoto wake wote walifaulu kuwa watu wazima bila madhara na sasa wameoa.

Tafuta Msaada wa Mungu

Zawadi bora zaidi ambayo baba anaweza kuwapa watoto wake ni ile ya kuwasaidia kusitawisha uhusiano wa karibu na ulio imara pamoja na Mungu. Mfano wa baba ni muhimu sana. Donizete anasema: “Akina baba wanahitaji kuonyesha jinsi wanavyothamini uhusiano wao na Mungu. Hilo linapaswa kuwa wazi hasa wanapokabili matatizo ya kibinafsi au magumu. Katika pindi hizo, baba anaonyesha jinsi anavyomtegemea sana Yehova. Sala ya familia, inayokazia mara kwa mara kumthamini Mungu kwa sababu ya wema Wake, itawafundisha watoto umuhimu wa kumfanya Mungu kuwa Rafiki yao.”

Basi, ni nini siri ya kuwa baba mzuri? Tafuta mashauri ya yule anayejua vizuri zaidi jinsi ya kuwalea watoto, yaani, Yehova Mungu. Ukiwazoeza watoto wako kulingana na mwongozo wa Neno la Mungu, huenda ukaona matokeo yanayoelezwa katika Methali 22:6: “Hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ingawa mashauri ya Kimaandiko yanayozungumziwa katika habari hii yanakazia hasa jukumu la baba, kanuni nyingi zinawahusu pia akina mama.

^ fu. 18 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 25 Kwa habari zaidi kuhusu kuwalinda watoto dhidi ya watu wanaowatendea watoto vibaya kingono, ona Amkeni! la Oktoba (Mwezi wa 10) 2007, ukurasa wa 3–11, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Baba anahitaji kuwawekea watoto wake mfano mzuri

[Picha katika ukurasa wa 20]

Baba anapaswa kutimiza mahitaji ya kiroho ya watoto wake

[Picha katika ukurasa wa 21]

Watoto wanahitaji nidhamu inayotolewa kwa upendo