Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Yangu Ilivyonisaidia Kukabiliana na Misiba

Imani Yangu Ilivyonisaidia Kukabiliana na Misiba

Imani Yangu Ilivyonisaidia Kukabiliana na Misiba

Limesimuliwa na Soledad Castillo

Karibu nilemewe na upweke mara kadhaa maishani mwangu, lakini haikuwa hivyo. Nilipokuwa na umri wa miaka 34, mume wangu mpendwa alikufa. Miaka sita baadaye, baba yangu alikufa. Miezi minane baada ya kifo cha baba yangu, niligundua kwamba mwana wangu wa pekee alikuwa na ugonjwa usioweza kupona.

NINAITWA Soledad, jina linalomaanisha “Upweke.” Tofauti na jina langu, sijawahi kujihisi mpweke kabisa. Nilipokabili misiba, niliamini kwamba Yehova Mungu alikuwa hapo, ‘akinishika mkono wangu, na kunisaidia hivi kwamba sikuogopa.’ (Isaya 41:13) Niruhusu nikueleze jinsi nilivyopitia misiba yangu na jinsi ilivyonisaidia kumkaribia Yehova zaidi.

Maisha Yenye Furaha Bila Matatizo Mengi

Nilizaliwa Mei 3, 1961 (3/5/1961), huko Barcelona, nchini Hispania. Wazazi wangu wanaitwa José na Soledad nami ndiye mtoto wao wa pekee. Nilipokuwa na umri wa miaka tisa, mama yangu alijifunza kweli ya Neno la Mungu. Alikuwa ametafuta majibu ya maswali yake ya kidini lakini hakupata majibu yenye kuridhisha katika kanisa lake. Siku moja, Mashahidi wawili wa Yehova walimtembelea nyumbani na kujibu maswali yake yote kupitia Maandiko. Alikubali funzo la Biblia kwa msisimuko.

Baada ya muda mfupi, mama yangu alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, na miaka michache baadaye, baba yangu akabatizwa pia. Eliana, ambaye alijifunza na mama yangu, alitambua kwamba nilipendezwa na Neno la Mungu. Ingawa nilikuwa msichana mdogo, Eliana alipendekeza kwamba nianze kujifunza Biblia. Kwa sababu Eliana alinisaidia sana na mama akanitia moyo, nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 13.

Nilipokuwa kijana, mara nyingi nilisali kwa Yehova, hasa nilipohitaji kufanya maamuzi. Kusema kweli, sikuwa na matatizo mengi nilipokuwa nikibalehe. Nilikuwa na marafiki wengi kutanikoni, na nilikuwa na uhusiano wa karibu na wazazi wangu. Mnamo 1982, niliolewa na Felipe, Shahidi aliyekuwa na miradi ya kiroho kama yangu.

Kumlea Mtoto Wetu Ampende Yehova

Miaka mitano baadaye, nilizaa mvulana anayependeza ambaye tulimwita Saúl. Mimi na Felipe tulifurahi sana kupata mtoto. Tulitumaini kwamba Saúl angekuwa mtoto mwenye afya na usawaziko anayempenda Mungu. Mimi na Felipe tulitumia wakati mwingi na Saúl, tukizungumza naye kuhusu Yehova, tukila pamoja, tukimpeleka bustanini, na kucheza naye. Saúl alipenda kwenda kuhubiri pamoja na Felipe, na Felipe alimhusisha katika mahubiri alipokuwa mdogo sana, akimfundisha kubisha milango na kuwapa watu trakti.

Upendo na mazoezi yetu yalimsaidia Saúl. Alipokuwa na umri wa miaka sita, alihubiri kwa ukawaida pamoja nasi. Alipenda kusikiliza hadithi za Biblia na alitazamia kwa hamu funzo letu la Biblia la familia. Muda mfupi baada ya kuanza kwenda shule, alianza kufanya maamuzi madogo yaliyotegemea ujuzi wake wa Biblia.

Hata hivyo, Saúl alipokuwa na umri wa miaka saba, maisha ya familia yetu yalibadilika sana. Felipe aliambukizwa virusi vilivyoathiri mapafu yake. Kwa miezi 11, alikabiliana na ugonjwa huo na hakuweza kufanya kazi, mara nyingi akilala tu kitandani. Mume wangu alikufa akiwa na umri wa miaka 36.

Bado ninalia ninapokumbuka mwaka huo mgumu. Nilitazama tu mume wangu akilemewa na ugonjwa huo na hakuna chochote nilichoweza kufanya. Wakati huo wote, nilijaribu kumtia moyo Felipe, ingawa moyoni mwangu nilihisi matumaini na mipango yangu ya wakati ujao ikivunjwa-vunjwa. Nilimsomea habari za Kimaandiko, na zilituimarisha wakati ambapo hatungeweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Alipokufa, nilifadhaika sana.

Hata hivyo, Yehova alinitegemeza. Nilimwomba mara nyingi anipe roho yake. Nilimshukuru kwa miaka yenye furaha ambayo mimi na Felipe tulikuwa tumeishi pamoja na kwa tumaini la kumwona Felipe tena katika ufufuo. Nilimwomba Mungu anisaidie nifurahie kumbukumbu za mambo ambayo mimi na mume wangu tulikuwa tumefurahia pamoja na anipe hekima ya kumlea mtoto wetu awe Mkristo wa kweli. Ingawa nilikuwa na uchungu mwingi, nilifarijika.

Wazazi wangu na wengine kutanikoni walinitegemeza sana. Hata hivyo, nilipaswa kujifunza Biblia na Saúl na kumfundisha jinsi ya kumtumikia Yehova. Mwajiri wangu wa awali alinipa kazi nzuri ya ofisini, lakini niliamua kufanya kazi ya kusafisha ili niweze kutumia wakati mwingi na Saúl na niwe pamoja naye alipotoka shuleni kila siku.

Andiko moja lilinifanya nione umuhimu wa kumzoeza Saúl kiroho: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.” (Methali 22:6) Andiko hilo lilinipa tumaini kwamba nikifanya yote niwezayo kumfundisha Saúl viwango vya kiroho, Yehova angebariki jitihada zangu. Ni kweli kwamba nilihitaji kujidhabihu kifedha, lakini nilihitaji kuwa pamoja na mwana wangu, na hilo lilikuwa muhimu kuliko faida za kifedha.

Saúl alipokuwa na umri wa miaka 14, baba yangu alikufa. Saúl alihuzunika sana, kwani kifo cha babu yake kilimfanya ahisi uchungu aliohisi baba yake alipokufa. Pia baba yangu alikuwa ametuwekea mfano mzuri wa kumpenda Yehova. Baada ya kifo hicho, Saúl aliamua kwamba yeye ndiye “mwanamume” aliyebaki katika familia, na sasa alihitaji kumtunza mama na nyanya yake.

Kukabiliana na Lukemia

Miezi minane baada ya baba yangu kufa, daktari wetu aliniambia nimpeleke Saúl hospitalini kwani alikuwa akichoka sana. Baada ya uchunguzi, madaktari waliniambia kwamba Saúl alikuwa na lukemia. *

Kwa miaka miwili na nusu iliyofuata, Saúl alilazwa hospitalini mara nyingi alipokuwa akikabiliana na ugonjwa huo na matibabu ambayo madaktari walitumia wakijaribu kumtibu kwa kemikali. Miezi sita ya kwanza ya matibabu hayo, yalimfanya apate nafuu kwa miezi 18 hivi. Lakini kansa ilirudi tena na Saúl akatibiwa tena kwa kemikali kwa muda mfupi. Matibabu hayo yalimdhoofisha sana. Saúl alipata nafuu kwa muda mfupi tu na hangeweza kustahimili matibabu mengine ya kemikali. Saúl alijiweka wakfu kwa Mungu na alitaka kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, lakini alikufa baada ya kufikia umri wa miaka 17.

Mara nyingi, madaktari walipendekeza atiwe damu mishipani ili kupunguza madhara ya matibabu ya kemikali. Bila shaka, kutiwa damu mishipani hakungetibu ugonjwa. Madaktari walipogundua ana lukemia, mimi na Saúl tulihitaji kuwaambia waziwazi kwamba hatungeweza kukubali matibabu hayo, kwani tulitaka kutii sheria ya Yehova ya ‘kujiepusha na damu.’ (Matendo 15:19, 20) Mara kadhaa, Saúl alihitaji kuwasadikisha madaktari wakati sikuwepo kwamba huo ulikuwa uamuzi wake mwenyewe. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 31.)

Mwishowe, madaktari walikata kauli kwamba Saúl alikuwa mtoto mkomavu ambaye alielewa vizuri ugonjwa wake. Walikubali kuheshimu msimamo wetu na wakapendekeza matibabu yasiyohusisha damu, ingawa tulishinikizwa mara nyingi tubadili uamuzi wetu. Nilifurahi sana kumsikia Saúl akieleza msimamo wake mbele ya madaktari. Kwa wazi, alikuwa amesitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova.

Tulipogundua kwamba Saúl alikuwa na ugonjwa huo, kitabu Mkaribie Yehova kilitolewa katika kusanyiko la wilaya huko Barcelona. Kitabu hicho chenye thamani kilithibitika kuwa kama nanga iliyotuimarisha tulipokabili wakati ujao usio hakika na wenye kuogopesha. Tulipokuwa hospitalini, tulitumia wakati huo kusoma sehemu za kitabu hicho pamoja. Katika pindi nyingi ngumu ambazo tulivumilia baadaye, mara nyingi tulikumbuka habari zake. Wakati huo andiko la Isaya 41:13, lililonukuliwa mwanzoni mwa kitabu hicho, lilikuwa na maana ya pekee kwetu. Linasema: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”

Imani ya Saúl Inagusa Mioyo ya Wengine

Ukomavu na mtazamo mzuri wa Saúl uliwapendeza sana madaktari na wauguzi katika Hospitali ya Vall d’Hebrón. Wote waliomtunza walimpenda sana. Tangu wakati huo, mtaalamu mkuu wa damu anayeshughulika na kansa amewatibu watoto wengine Mashahidi wanaougua lukemia, na amewaheshimu sana. Anakumbuka uamuzi imara wa Saúl wa kushikilia imani yake, ujasiri wake alipokabili kifo, na mtazamo wake wenye furaha maishani. Wauguzi waliomshughulikia walimwambia Saúl kwamba alikuwa mgonjwa bora zaidi waliowahi kupata katika wodi hiyo. Walisema hakuwahi kulalamika na hakuacha ucheshi wake, hata alipokuwa karibu kufa.

Mwanasaikolojia mmoja aliniambia kwamba watoto wengi wanaopata ugonjwa usioweza kupona wakiwa na umri huo wanaasi madaktari na wazazi kwa sababu ya maumivu na kukata tamaa. Aliona kwamba Saúl hakuwa hivyo. Alishangaa kuona kwamba Saúl alikuwa mtulivu na mwenye mtazamo mzuri. Hilo lilitupatia nafasi ya kumhubiria kuhusu imani yetu.

Pia ninakumbuka jinsi Saúl alivyomsaidia Shahidi mmoja katika kutaniko letu katika njia isiyo ya moja kwa moja. Alikuwa ameshuka moyo kwa miaka sita hivi na dawa hazikuwa zimemsaidia. Alikaa hospitalini mara kadhaa usiku mzima akimtunza Saúl. Aliniambia kwamba alipendezwa sana na mtazamo wa Saúl ingawa alikuwa na lukemia. Aliona kwamba hata kama alikuwa amechoka, Saúl alijaribu kumtia moyo kila mtu aliyemtembelea. “Mfano wa Saúl ulinipa ujasiri wa kukabiliana na mshuko wa moyo,” akasema Shahidi huyo.

Miaka mitatu imepita tangu Saúl alipokufa. Bila shaka, bado ninahisi uchungu. Sina nguvu, lakini Mungu amenipa “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Wakorintho 4:7) Nimejifunza kwamba hata hali ngumu na zenye kuumiza sana zinaweza kuwa na matokeo mazuri. Kujifunza kukabiliana na kifo cha mume, baba, na mwana wangu kumenisaidia nisiwe na ubinafsi na niwaelewe watu wengine wanaoteseka. Zaidi ya yote, kumenisaidia nimkaribie Yehova zaidi. Ninaweza kuutazamia wakati ujao bila woga kwa sababu Baba yangu wa kimbingu bado ananisaidia. Bado anaushika mkono wangu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Saúl alikuwa na kansa hatari sana ya damu ambayo inaharibu chembe nyeupe za damu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 31]

JE, UMEJIULIZA?

Huenda umesikia kwamba Mashahidi wa Yehova hawakubali kutiwa damu mishipani. Je, umewahi kujiuliza ni kwa nini?

Mara nyingi msimamo huo wa Kimaandiko unaeleweka vibaya. Wakati mwingine watu wanadhani kwamba Mashahidi wa Yehova wanakataa matibabu ya aina zote au hawathamini uhai. Huo ni uwongo mtupu. Mashahidi wa Yehova wanatafuta matibabu bora zaidi kwa ajili yao na familia zao. Hata hivyo, wao wanatafuta matibabu yasiyohusisha damu. Kwa nini?

Msimamo wao unategemea sheria ya msingi ambayo Mungu aliwapa wanadamu. Baada tu ya Gharika ya siku za Noa, Mungu aliruhusu Noa na familia yake wale nyama. Lakini Mungu aliweka sheria hii moja: Hawakupaswa kula damu. (Mwanzo 9:3, 4) Jamii zote za wanadamu zilitoka kwa Noa, kwa hiyo, sheria hiyo inawahusu wanadamu wote. Haikuwahi kufutwa. Zaidi ya karne nane baadaye, Mungu alirudia sheria hiyo kwa taifa la Israeli, akieleza kwamba damu ni takatifu na inawakilisha nafsi, au uhai. (Mambo ya Walawi 17:14) Zaidi ya miaka 1,500 baadaye, mitume Wakristo waliwaamuru Wakristo wote ‘waendelee kujiepusha na damu.’—Matendo 15:29.

Kwa Mashahidi wa Yehova, ni wazi kwamba haiwezekani kujiepusha na damu huku wakitiwa damu mishipani. Kwa hiyo, wanasisitiza wapewe matibabu yasiyohusisha damu. Mara nyingi msimamo huo wa Kimaandiko unafanya watibiwe kwa njia ya hali ya juu zaidi. Si ajabu kwamba watu wengi ambao si Mashahidi wa Yehova pia wanaomba watibiwe bila damu.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikiwa na mume wangu, Felipe, na mwana wetu, Saúl

[Picha katika ukurasa wa 29]

Wazazi wangu, José na Soledad

[Picha katika ukurasa wa 30]

Mwezi mmoja kabla ya Saúl kufa