Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Mwenye Bidii kwa Ajili ya Ibada ya Kweli

Uwe Mwenye Bidii kwa Ajili ya Ibada ya Kweli

Uwe Mwenye Bidii kwa Ajili ya Ibada ya Kweli

“Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.”—MT. 9:37.

1. Unaweza kueleza jinsi gani maana ya kuwa na hisi ya uharaka?

UNA barua ambayo inapaswa kushughulikiwa na mtu fulani kabla ya siku kwisha. Utafanya nini? Unaandika juu ya barua hiyo “JAMBO LA HARAKA!” Uko njiani kwenda mahali ambapo unangojewa sana, lakini umechelewa. Utafanya nini? Unamwambia dereva, “Tafadhali harakisha; ninataka kutimiza jambo fulani HARAKA!” Ndiyo, unapokuwa na jambo linalopaswa kufanywa haraka na wakati uliobaki ni mfupi, bila shaka unakuwa na wasiwasi na msisimko mwingi. Moyo wako unapigapiga haraka, nawe unafanya kazi kwa bidii na haraka sana kadiri uwezavyo. Hiyo ndiyo maana ya kuwa na hisi ya uharaka!

2. Ni kazi gani iliyo ya haraka zaidi kwa Wakristo wa kweli leo?

2 Kwa Wakristo wa kweli leo, hakuna jambo lililo la haraka zaidi kuliko kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Akitaja maneno ya Yesu, mwanafunzi Marko aliandika kwamba ni lazima kazi hii ifanywe “kwanza,” yaani, kabla ya mwisho kuja. (Marko 13:10) Bila shaka, hilo ni jambo linalofaa. Yesu alisema hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.” Mavuno hayawezi kungoja; ni lazima yakusanywe kabla ya majira ya mavuno kwisha.—Mt. 9:37.

3. Wengi wameitikia jinsi gani uhitaji wa haraka wa kuhubiri?

3 Kwa kuwa kazi ya kuhubiri ni ya maana sana hivyo kwetu, tunastahili kutumia wakati mwingi zaidi, nguvu, na kuipa uangalifu mkubwa kadiri iwezekanavyo. Inapendeza kwamba ndugu na dada wengi wanafanya vivyo hivyo. Wengine wamerahisisha mambo yao ya kibinafsi ili kuanza huduma ya wakati wote wakiwa mapainia au wamishonari au kutumikia katika mojawapo ya makao ya Betheli ulimwenguni. Maisha yao yana shughuli nyingi sana. Huenda wamejidhabihu sana, na wanapambana na matatizo mengi. Hata hivyo, Yehova anawabariki sana. Wanatufurahisha. (Soma Luka 18:28-30.) Ingawa wengine hawawezi kuwa wahubiri wa wakati wote, wanatumia wakati mwingi iwezekanavyo katika kazi hii inayookoa uhai, ambayo pia inatia ndani kuwasaidia watoto wetu ili waokolewe.—Kum. 6:6, 7.

4. Kwa nini huenda wengine wakawa na mwelekeo wa kupoteza hisi ya uharaka?

4 Kama tulivyoona, hisi ya uharaka kwa kawaida inahusiana na wakati uliowekwa wa kutimiza jambo fulani, wakati ulio na kikomo, yaani, mwisho. Tunaishi katika wakati wa mwisho, na kuna uthibitisho mwingi wa Kimaandiko na wa kihistoria unaoonyesha jambo hilo. (Mt. 24:3, 33; 2 Tim. 3:1-5) Hata hivyo, hakuna mtu anayejua wakati kamili ambao mwisho utakuja. Alipokuwa akitaja mambo yanayohusu “ishara” ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alisema hivi waziwazi: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mt. 24:36) Kwa kuwa ndivyo ilivyo, huenda wengine wakaona kwamba ni vigumu kudumisha hisi ya uharaka mwaka baada ya mwaka, na hasa ikiwa wamekuwa wakifanya hivyo kwa muda mrefu. (Met. 13:12) Je, nyakati nyingine unajikuta ukihisi hivyo? Ni nini kinachoweza kutusaidia tusitawishe au kudumisha hisi ya uharaka kwa ajili ya kazi ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wanataka tufanye leo?

Fikiria Kielelezo Chetu, Yesu

5. Ni katika njia gani Yesu alionyesha hisi ya uharaka katika huduma?

5 Bila shaka, Yesu Kristo ndiye kielelezo bora zaidi kati ya wote ambao walionyesha hisi ya uharaka katika utumishi wao kwa Mungu. Sababu moja iliyomfanya Yesu awe na hisi ya uharaka ni kwamba alikuwa na mambo mengi ya kufanya kwa muda wa miaka mitatu na nusu tu. Hata hivyo, Yesu alitimiza mambo mengi kwa ajili ya ibada ya kweli kuliko mtu mwingine yeyote yule. Alitangaza jina na kusudi la Baba yake, alihubiri habari njema ya Ufalme, alifunua unafiki na mafundisho ya uwongo ya viongozi wa kidini, na alitetea enzi kuu ya Yehova hata kufikia kifo. Alijitahidi sana kusafiri kotekote nchini akiwafundisha, akiwasaidia, na kuwaponya watu. (Mt. 9:35) Hakuna mtu ambaye amewahi kutimiza mambo mengi sana kwa muda mfupi hivyo. Yesu alifanya kazi kwa bidii kadiri iwezekanavyo kuliko mtu mwingine yeyote yule.—Yoh. 18:37.

6. Yesu alikazia fikira nini katika maisha yake?

6 Ni nini kilichomchochea Yesu kufanya kazi kwa bidii katika huduma yake yote? Kutokana na unabii wa Danieli, huenda Yesu alijua ni muda gani uliokuwa umebaki ili atimize kazi yake kulingana na ratiba au programu ya Yehova. (Dan. 9:27) Kwa hiyo, kama tulivyoona, huduma yake duniani ilipaswa kumalizika “katika nusu ya juma hilo,” au baada ya miaka mitatu na nusu. Muda mfupi baada ya kuingia Yerusalemu kwa ushindi mwaka wa 33 W.K., Yesu alisema hivi: “Saa imekuja Mwana wa binadamu atukuzwe.” (Yoh. 12:23) Ingawa Yesu alijua kwamba kifo chake kilikuwa kimekaribia, hakukazia fikira jambo hilo maishani, hiyo haikuwa sababu kuu iliyomchochea kufanya kazi kwa bidii. Badala yake, alikazia fikira kutumia kila nafasi kufanya mapenzi ya Baba yake na kuwaonyesha upendo wanadamu wenzake. Upendo huo ulimchochea kuwakusanya na kuwazoeza wanafunzi wake, akiwatuma katika kampeni za kuhubiri. Alifanya hivyo ili waweze kuendeleza kazi ambayo alikuwa ameanzisha na wangetimiza kazi kubwa hata zaidi kuliko zake.—Soma Yohana 14:12.

7, 8. Wanafunzi walikuwa na maoni gani Yesu alipolisafisha hekalu, na kwa nini Yesu alifanya hivyo?

7 Tukio moja katika maisha ya Yesu lilionyesha waziwazi bidii yake. Lilitukia mwanzoni mwa huduma yake, katika majira ya Pasaka ya mwaka wa 30 W.K. Yesu na wanafunzi wake walienda Yerusalemu na wakaona katika hekalu “wale waliokuwa wakiuza ng’ombe na kondoo na njiwa na waliokuwa wakivunja pesa wakiwa wameketi.” Yesu alifanya nini, na hilo lilikuwa na uvutano gani juu ya wanafunzi wake?—Soma Yohana 2:13-17.

8 Jambo ambalo Yesu alifanya na kusema katika pindi hiyo liliwakumbusha vizuri wanafunzi maneno ya kinabii ya zaburi moja iliyoandikwa na Daudi: “Bidii nyingi kwa ajili ya nyumba yako imenila.” (Zab. 69:9) Kwa nini? Kwa sababu jambo ambalo Yesu alifanya lilikuwa hatari sana. Ukweli ni kwamba wasimamizi wa hekalu, yaani, makuhani, waandishi, na wengine, waliunga mkono biashara hiyo ya kupata faida kwa udanganyifu iliyokuwa ikifanywa hekaluni. Kwa kuwafunua na kuvuruga mbinu zao, Yesu alikuwa akijifanya kuwa adui wa viongozi hao wa kidini. Kama wanafunzi walivyochanganua hali hiyo kwa usahihi, ‘bidii kwa ajili ya nyumba ya Mungu,’ au bidii kwa ajili ya ibada ya kweli, ilionekana waziwazi. Hata hivyo, bidii ni nini? Je, kuna tofauti kati ya bidii na hisi ya uharaka?

Tofauti Kati ya Bidii na Hisi ya Uharaka

9. Eleza maana ya neno “bidii.”

9 Kamusi moja inasema kwamba “bidii” ni “hamu kubwa na juhudi ya kufuatilia jambo fulani,” na neno hilo linaweza pia kumaanisha hamu, joto, shauku, na uchangamfu. Bila shaka, huduma ya Yesu inaweza kuelezwa kwa maneno hayo yote. Hivyo, tafsiri moja ya Biblia (Today’s English Version) inatafsiri hivi mstari huo: “Ujitoaji wangu kwa ajili ya nyumba yako, Ee Mungu, unawaka ndani yangu kama moto.” Inapendeza kujua kwamba katika lugha fulani za Mashariki, neno linalotafsiriwa “bidii” linatokana na maneno mawili ambayo kihalisi yanamaanisha “moyo motomoto,” kana kwamba moyo unawaka moto. Haishangazi kwamba wanafunzi walikumbuka maneno ya Daudi walipoona yale ambayo Yesu alifanya hekaluni. Hata hivyo, ni nini kilichofanya moyo wa Yesu uwake moto, na kumsukuma, au kumchochea kutenda kwa njia hiyo?

10. Neno “bidii” linamaanisha nini katika Biblia?

10 Neno “bidii” katika zaburi ya Daudi linatokana na neno la Kiebrania ambalo mara nyingi linatafsiriwa katika sehemu nyingine za Biblia kuwa “wivu” au “mwenye wivu.” Nyakati nyingine, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatafsiri neno hilo kuwa ‘kutaka watu wajitoe kikamili.’ (Soma Kutoka 20:5; 34:14; Yoshua 24:19.) Kamusi moja ya Biblia inasema hivi kuhusu neno hilo: “Mara nyingi neno hilo linatumiwa kuhusu uhusiano katika ndoa . . . Kama vile wivu wa mume au mke unavyomchochea kudai kwa nguvu haki fulani ya pekee, ndivyo Mungu anavyotetea na kudai haki Yake kutoka kwa wale ambao ni mali Yake ya pekee.” Kwa hiyo, katika Biblia, neno “bidii” halimaanishi tu shauku au uchangamfu wa kufuatia jambo fulani, kama vile watu wengi wanavyoonyesha katika mchezo wanaopenda. Daudi alionyesha bidii kwa kuwa na wivu unaofaa, yaani, kutovumilia ushindani au lawama, kuwa na hamu kubwa ya kulinda jina zuri au kurekebisha madhara.

11. Ni nini kilichomchochea Yesu ajitahidi kwa bidii?

11 Wanafunzi wa Yesu hawakukosea walipohusianisha maneno ya Daudi na yale ambayo waliona Yesu akifanya katika hekalu. Yesu alijitahidi sana si kwa sababu wakati wake ulikuwa na mwisho bali kwa sababu alikuwa mwenye bidii au mwenye wivu kwa ajili ya jina la Baba yake na kwa ajili ya ibada safi. Alipoona watu wakileta lawama na makufuru juu ya jina la Mungu, alikuwa na sababu nzuri ya kuwa mwenye bidii, au wivu, na alichukua hatua ya kurekebisha hali hiyo. Yesu alipoona watu wa hali ya chini wakikandamizwa na kutumiwa vibaya na viongozi wa kidini, bidii yake ilimchochea kuwapa watu kitulizo na pia kuwashutumu vikali viongozi wa kidini wenye kukandamiza.—Mt. 9:36; 23:2, 4, 27, 28, 33.

Uwe Mwenye Bidii kwa Ajili ya Ibada ya Kweli

12, 13. Viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wamefanya nini leo kuhusu (a) jina la Mungu? (b) Ufalme wa Mungu?

12 Mitazamo na matendo ya watu wanaodai kumwabudu Mungu leo inafanana na hata ni mibaya zaidi kuliko ilivyokuwa katika siku za Yesu. Kwa mfano, kumbuka kwamba kati ya mambo ambayo Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali, ni kuhusu jina la Mungu: “Jina lako na litakaswe.” (Mt. 6:9) Je, tunaona viongozi wa kidini, hasa makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, wakiwafundisha watu kumjua Mungu kwa jina lake na kulitakasa, au kuliheshimu jina hilo? Badala ya kufanya hivyo, wamemharibia Mungu sifa kwa kufundisha mafundisho ya uwongo kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi ya mwanadamu, na moto wa mateso, na hivyo kumfanya Mungu aonekane kuwa fumbo, asiyeeleweka, mkatili, na hata mtesaji. Pia, wamemletea Mungu suto kwa maovu wanayotenda na unafiki wao. (Soma Waroma 2:21-24.) Zaidi ya hayo, wamefanya yote wawezayo ili kuficha jina la Mungu, na hata wameliondoa katika tafsiri zao za Biblia. Kwa hiyo, wanawazuia watu wasimkaribie Mungu na kusitawisha uhusiano mzuri pamoja naye.—Yak. 4:7, 8.

13 Pia, Yesu aliwafundisha wafuasi wake kusali kuhusu Ufalme wa Mungu: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mt. 6:10) Hata ingawa viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wanarudia mara nyingi sala hiyo, wamewatia watu moyo kuunga mkono siasa na mashirika mengine ya kibinadamu. Zaidi ya hayo, wanawadharau wale wanaojitahidi kuhubiri na kutoa ushahidi kuhusu Ufalme huo. Matokeo ni kwamba watu wengi wanaodai kuwa Wakristo hawazungumzi kuhusu Ufalme wa Mungu, wala hawaamini Ufalme huo.

14. Makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wamepunguza jinsi gani uzito wa Neno la Mungu?

14 Katika sala kwa Mungu, Yesu alisema waziwazi hivi: “Neno lako ni kweli.” (Yoh. 17:17) Na kabla ya kuondoka duniani, Yesu alifunua kwamba angemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili awaandalie watu wake chakula cha kiroho. (Mt. 24:45) Ingawa wanadai kwamba wanawafundisha watu Neno la Mungu, je, makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wamethibitika kuwa waaminifu kwa kazi ambayo walikabidhiwa na Bwana? Hapana. Wana mwelekeo wa kusema kwamba mambo yaliyo katika Biblia ni hadithi tu. Badala ya kuwalisha kondoo wao chakula cha kiroho, na hivyo kuwaletea faraja na nuru ya kiroho, makasisi wamefurahisha masikio ya waamini wao kwa kuwafundisha falsafa za wanadamu. Zaidi ya hayo, wamepunguza uzito wa viwango vya Mungu kwa kuwafundisha yale yanayoitwa eti maadili mapya.—2 Tim. 4:3, 4.

15. Unahisi jinsi gani kuhusu mambo yote ambayo makasisi wamefanya katika jina la Mungu?

15 Kwa sababu ya mambo yote ambayo yamefanywa eti katika jina la Mungu wa Biblia, watu wengi wanyoofu wamekatishwa tamaa au wamepoteza kabisa imani katika Mungu na katika Biblia. Wamenaswa na Shetani na mfumo wake mwovu wa mambo. Unahisi namna gani unapoona na kusikia mambo kama hayo yakifanyika siku baada ya siku? Ukiwa mtumishi wa Yehova, unapoona suto na kusikia makufuru yanayosemwa kuhusu jina la Mungu, je, unachochewa kufanya yote unayoweza ili kusahihisha mambo? Unapoona watu wanyoofu wakidanganywa na kutumiwa vibaya, je, huchochewi kuzifariji nafsi hizo zilizokandamizwa? Yesu alipoona watu wa siku zake ‘wakichunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji,’ hakuwahurumia tu. ‘Alianza kuwafundisha mambo mengi.’ (Mt. 9:36; Marko 6:34) Tuna sababu nzuri za kuwa wenye bidii kwa ajili ya ibada ya kweli, kama Yesu.

16, 17. (a) Ni nini kinachopaswa kutuchochea tujitahidi sana katika huduma? (b) Tutachunguza nini katika habari inayofuata?

16 Tunapokuwa na maoni hayo kuhusu huduma yetu, maneno ya mtume Paulo katika 1 Timotheo 2:3, 4 yanakuwa na maana ya pekee. (Soma.) Tunafanya kazi ya kuhubiri kwa bidii si kwa sababu tunajua tu kwamba tunaishi katika siku za mwisho bali pia kwa sababu tunatambua kwamba ni mapenzi ya Mungu. Anataka watu wapate ujuzi wa kweli ili wao pia wajifunze kumwabudu na kumtumikia na hivyo wabarikiwe. Tunachochewa kujitahidi sana katika huduma, si kwa sababu tu wakati uliobaki ni mfupi, lakini kwa sababu tunataka kuliheshimu jina la Mungu na kuwasaidia watu wajue mapenzi yake. Tuna bidii kwa ajili ya ibada ya kweli.—1 Tim. 4:16.

17 Tukiwa watu wa Yehova, tumebarikiwa kupata ujuzi wa kweli kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu na dunia. Tunaweza kuwasaidia watu wapate furaha na tumaini hakika kwa ajili ya wakati ujao. Tunaweza kuwaonyesha jinsi ya kupata ulinzi wakati mfumo huu wa mambo wa Shetani utakapoharibiwa. (2 The. 1:7-9) Badala ya kukata tamaa au kuvunjika moyo kwa sababu tunaona kwamba siku ya Yehova inachelewa, tunapaswa kufurahi kwamba bado tuna wakati wa kuonyesha bidii kwa ajili ya ibada ya kweli. (Mika 7:7; Hab. 2:3) Tunaweza kusitawisha jinsi gani bidii hiyo? Tutachunguza jambo hilo katika habari inayofuata.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni nini kilichomchochea Yesu kuwa na bidii muda wote wa huduma yake?

• Neno “bidii” linamaanisha nini katika Biblia?

• Ni nini tunachoona leo ambacho kinapaswa kutuchochea kuwa wenye bidii kwa ajili ya ibada ya kweli?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Yesu alikazia fikira kufanya mapenzi ya Baba yake na kuwaonyesha upendo wanadamu wenzake

[Picha katika ukurasa wa 10]

Tuna sababu nzuri za kuwa wenye bidii kwa ajili ya ibada ya kweli