Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Wote Wanaalikwa!

Watu Wote Wanaalikwa!

Watu Wote Wanaalikwa!

WATU wote wanaalikwa wapi? Wanaalikwa kutembelea mojawapo ya ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova, ambazo kwa kawaida zinaitwa Betheli. Kuna ofisi za tawi 118 zilizo katika nchi mbalimbali. Mara nyingi wageni wanaeleza jinsi wanavyothamini kutoka moyoni kazi wanazoona zikifanywa Betheli.

Baada ya kuona wafanyakazi wengi wenye bidii wakimtumikia Yehova kwa furaha kwenye ofisi ya tawi huko Mexico, mwanafunzi mmoja wa Biblia ambaye ni kijana alivutiwa sana hivi kwamba akauliza: “Ninahitaji kufanya nini ili niishi hapa?” Akaambiwa: “Kwanza, ni lazima ubatizwe. Kisha, ni vizuri kutumikia ukiwa painia, yaani, mhubiri wa wakati wote wa Ufalme.” Mwanamume huyo kijana alifuata mapendekezo hayo, na miaka miwili baadaye akaalikwa kutumika katika Betheli ya Mexico, ambako amekuwa akitumikia kwa miaka 20 ambayo imepita.

Betheli Ni Nini?

Katika lugha ya Kiebrania, neno “Betheli” linamaanisha “Nyumba ya Mungu.” (Mwa. 28:19) Vifaa vilivyo katika ofisi mbalimbali za tawi vinatumiwa kuchapisha na kusambaza Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia na kuandaa msaada wa kiroho kwa makutaniko zaidi ya 100,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Wanabetheli karibu 20,000, wanaume kwa wanawake kutoka katika jamii na tamaduni mbalimbali, wanamtumikia Yehova bila uchoyo na pia ndugu na dada zao wa kiroho kwa wakati wote. Wale ambao wamefanya kazi hiyo ya Kikristo kwa miaka mingi wanatumika pamoja na vijana wenye nguvu. Wakati wa jioni na siku za mwisho-juma, washiriki wa familia za Betheli wanafurahia kushirikiana na makutaniko ya karibu ya Mashahidi wa Yehova katika mikutano na katika huduma ya Kikristo. Pia, wanatumia wakati wao wa ziada kujifunza Biblia, kufurahia tafrija, na kushughulikia mambo ya kibinafsi.

Washiriki wa familia ya Betheli wanapokea kiasi kidogo cha pesa kwa ajili ya mahitaji yao kila mwezi. Wanafurahia vyakula vitamu na vyenye kujenga mwili na kuishi katika vyumba safi, vyenye kustarehesha. Makao ya Betheli hayajengwi kwa ajili ya maisha ya anasa. Hata hivyo, ni majengo mazuri yanayofaa. Wageni hawavutiwi tu na majengo, bustani zinazotunzwa vizuri, na utaratibu mzuri wa kazi, bali pia na roho ya fadhili na ushirikiano wanayoona Betheli. Kila mtu anafanya kazi kwa bidii, hata hivyo, hakuna hata mmoja ambaye haonyeshi urafiki eti kwa sababu ana shughuli nyingi. Katika Betheli, hakuna ubaguzi wa kijamii wala mtu anayejiona kuwa bora kwa sababu ya mgawo wake. Kila mgawo ni wa maana, iwe ni mgawo wa kusafisha, kutunza bustani, kupika, au kufanya kazi ya kuchapisha au katika ofisi. Wanabetheli, kama wanavyojulikana wale wanaotumika Betheli, wanafanya kazi pamoja kama kikundi kimoja ili kutegemeza huduma ya Mashahidi wa Yehova.—Kol. 3:23.

Wafahamu Wanabetheli Fulani

Acheni tuwafahamu vizuri zaidi wale ambao ni washiriki wa familia hiyo ya kimataifa. Ni nini kilichowachochea kutaka kutumika Betheli? Fikiria mfano wa Mario. Alipobatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, Mario alikuwa na kazi nzuri sana katika kampuni kubwa ya magari huko Ujerumani naye alikuwa na nafasi ya kufanya maendeleo katika kazi hiyo. Muda mfupi baada ya kubatizwa, alijitolea kufanya kazi kwa juma moja katika Betheli ya nchi yake. Alipewa kazi ya kusaidia katika kiwanda cha kuchapisha. Mario aliona tofauti kubwa kati ya wafanyakazi wenzake Betheli na wale aliofanya kazi nao katika ulimwengu. Kwa hiyo, alijaza ombi la kuwa mtumishi wa wakati wote Betheli. Ingawa watu wake wengi wa ukoo na wafanyakazi wenzake hawakuelewa kwa nini alifanya uamuzi huo, sasa Mario anatumika kwa furaha katika Betheli ya Ujerumani.

Wengi wanaingia katika utumishi wa Betheli bila elimu yoyote ya pekee au bila ujuzi fulani wa kazi. Ndivyo ilivyokuwa kwa Abel, ambaye ametumika katika Betheli ya Mexico kwa miaka 15. Anasema hivi: “Betheli imekuwa shule halisi kwangu. Nimejifunza kuendesha mashini za kuchapisha ambazo zimetengenezwa kwa utata sana. Ninajua kwamba nikiwa na ujuzi huo, ningeweza kupata pesa nyingi sana nje ya Betheli, lakini singekuwa na maisha ninayofurahia hapa, yaani, maisha matulivu yenye kuridhisha bila mahangaiko na mashindano kama ilivyo katika kampuni nyingi za kibiashara. Ninahisi kwamba nimepata elimu bora zaidi ambayo mtu anaweza kupata, ambayo imenisaidia kukua kiroho na pia kiakili. Singeweza kupata faida hizo za kiroho hata katika chuo kikuu ambacho ni bora zaidi.”

Utajengwa Ukitembelea Betheli

Kutembelea tu Betheli kunaweza kumsaidia sana mtu kiroho. Ndivyo ilivyokuwa kwa Omar, huko Mexico. Mama yake alimfundisha kweli za Biblia. Lakini akiwa na umri wa miaka 17, Omar aliacha kuhudhuria mikutano ya Kikristo na pia kushiriki katika huduma ya hadharani. Mwishowe, alianza kuishi maisha mapotovu na ya kutafuta vitu vya kimwili. Baadaye, alipokuwa akifanya kazi katika kampuni moja ya mawasiliano, Omar alikuwa kati ya kikundi cha wafanyakazi wa kampuni hiyo ambao walitembelea Betheli huko Mexico ili kuonyesha jinsi mashini fulani inavyofanya kazi. Omar anasema hivi: “Baada ya onyesho hilo, wale waliotualika walitutembeza katika majengo hayo. Mambo niliyoona na fadhili nilizoonyeshwa zilinifanya nitafakari kuhusu maisha niliyokuwa nikiishi, nikiwa nimejitenga na Yehova. Mara moja, nilianza kuhudhuria mikutano tena na kujifunza Biblia. Miezi sita baada ya kutembelea Betheli, nilibatizwa. Ninamshukuru Yehova kwa sababu ya kichocheo nilichopata baada ya kutembelea Betheli.”

Masahiko, anayeishi huko Japani, pia alilelewa katika familia ya Mashahidi. Hata hivyo, alianza kufikiri kwamba maisha ya Kikristo yalimnyima uhuru kabisa. Alianza kushiriki katika utendaji mbalimbali shuleni na akaacha kuhudhuria mikutano na kuhubiri. Masahiko anakumbuka hivi: “Siku moja familia yetu iliamua kutembelea Betheli pamoja na marafiki wachache Wakristo. Nilienda kwa sababu familia yetu ilisisitiza kwamba ninapaswa kwenda pamoja nao. Nilipotembelea Betheli, nilihisi nimeburudishwa kuliko wakati mwingine wowote. Niliposafiri pamoja na Wakristo wengine, nilifurahia ushirika ambao sijawahi kamwe kufurahia nikiwa na marafiki wangu ambao si Mashahidi. Tamaa ya kuishi maisha ya Kikristo ilisitawi ndani yangu, nikaamua kuomba funzo la Biblia.” Masahiko anatumika sasa akiwa mhudumu wa wakati wote katika kutaniko la kwao.

Mwanamke mmoja Shahidi kutoka Ufaransa alihamia Moscow kufanya kazi. Akiwa huko, hakushirikiana na watu wa Yehova na hivyo akadhoofika kiroho. Alianza kufanya mambo machafu na mwishowe akaolewa na mtu ambaye si Shahidi. Kisha, dada mmoja Shahidi kutoka Ufaransa akaja kumtembelea, nao wakasafiri pamoja mpaka St. Petersburg, Urusi, ili kutembelea makao ya Betheli huko. Mwanamke huyo anaandika hivi: “Tulikaribishwa kwa uchangamfu Betheli, na hilo lilinigusa moyo. Kulikuwa na amani nyingi sana. Nilihisi roho ya Yehova. Mbona nilifanya kosa la kuacha tengenezo la Yehova? Baada ya kutembelea Betheli, nilisali ili Yehova anisaidie na nikaanza kuwafundisha watoto wangu Biblia nikiwa nimeazimia tena moyoni.” Mbali na msaada mwingine wa kiroho ambao huenda Shahidi huyo aliyekuwa dhaifu alipokea, alitiwa nguvu sana alipotembelea Betheli na baadaye akafanya maendeleo mazuri.

Kutembelea Betheli kunaweza kuwa na matokeo gani kwa wale ambao hawafahamu Mashahidi wa Yehova? Mwaka wa 1988, Alberto, ambaye alijihusisha sana na siasa, alitembelea Betheli huko Brazili. Alivutiwa sana na usafi, utaratibu, na hasa kuona kazi ikifanywa waziwazi. Muda mfupi kabla ya kutembelea Betheli, Alberto alikuwa ametembelea seminari fulani ambako ndugu-mkwe wake alitumikia akiwa kasisi. Alberto aliona tofauti kubwa. Alberto anasema hivi: “Kila kitu katika seminari kilifanywa kwa siri.” Muda mfupi baada ya kutembelea Betheli, alikubali kujifunza Biblia, akaachana na siasa, na sasa anatumikia akiwa mzee wa kutaniko.

Tunakukaribisha Utembelee Betheli!

Watu wengi wamejitahidi kwa njia ya pekee ili kutembelea ofisi ya tawi katika nchi yao. Kwa mfano, huko Brazili, Paulo na Eugenia waliweka pesa katika akiba kwa miaka minne ili waweze kusafiri umbali wa kilomita 3,000 kwa basi kwa muda wa siku mbili ili waone majengo ya Betheli katika nchi hiyo. Wanasema hivi: “Jitihada zetu zote hazikuwa za bure. Sasa tunaelewa kikamili zaidi tengenezo la Yehova. Tunapowaeleza wanafunzi wetu wa Biblia kazi inayofanywa Betheli, nyakati nyingine wanatuuliza hivi: ‘Je, umewahi kuwa huko?’ Sasa tunaweza kusema ndiyo.”

Je, kuna ofisi ya tawi na makao ya Betheli katika nchi yenu au katika nchi iliyo karibu? Tunakualika utembelee majengo hayo. Bila shaka, utakaribishwa kwa uchangamfu na kufaidika kabisa kiroho ukitembelea Betheli.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mario

[Picha katika ukurasa wa 18]

Abel

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ujerumani

[Picha katika ukurasa wa 18]

Japani

[Picha katika ukurasa wa 18]

Brazili