Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Harani—Kituo cha Kale Chenye Utendaji Mwingi

Harani—Kituo cha Kale Chenye Utendaji Mwingi

Harani—Kituo cha Kale Chenye Utendaji Mwingi

WATU ambao wamezoea kusoma Maandiko wanaposikia jina Harani, mara moja wanamkumbuka yule mzee wa ukoo mwaminifu, Abrahamu. Alipokuwa akitoka Uru kwenda nchi ya Kanaani, yeye pamoja na mke wake, Sara, na baba yake, Tera, na mpwa wake Loti walisimama huko Harani. Akiwa huko, Abrahamu alijikusanyia mali nyingi za kimwili. Baada ya baba yake kufa, Abrahamu aliendelea na safari yake kuelekea nchi ambayo Mungu wa kweli alikuwa amemwahidi. (Mwa. 11:31, 32; 12:4, 5; Mdo. 7:2-4) Baadaye, Abrahamu alimtuma mtumishi wake aliyekuwa na umri mkubwa zaidi huko Harani au kwenye eneo fulani la karibu ili amtafutie Isaka mke. Yakobo, mjukuu wa Abrahamu aliishi pia huko kwa miaka mingi.—Mwa. 24:1-4, 10; 27:42-45; 28:1, 2, 10.

Katika vitisho ambavyo Mfalme Senakeribu wa Ashuru alimtolea Mfalme Hezekia wa Yuda, alitaja Harani kati ya “mataifa” yaliyokuwa yameshindwa na wafalme wa Ashuru. Katika kisa hicho, “Harani” lilitia ndani jiji hilo pamoja na wilaya iliyolizunguka. (2 Fal. 19:11, 12) Unabii wa Ezekieli unataja kuwa jiji la Harani lilifanya biashara hasa na Tiro, na hilo linathibitisha kwamba jiji la Harani lilikuwa kituo cha maana sana cha kibiashara.—Eze. 27:1, 2, 23.

Leo, Harani ni mji mdogo tu ulio karibu na Şanlıurfa, mashariki mwa Uturuki. Lakini kwa kweli, wakati mmoja jiji la kale la Harani lilikuwa kituo chenye shughuli nyingi. Harani ni moja kati ya maeneo machache sana ya kale ambayo bado yana majina yaliyotumiwa nyakati za Biblia. Jina la Kiashuru la jiji hilo, Harranu, linaweza kumaanisha “Barabara” au “Barabara ya Magari ya Kukokotwa,” kuonyesha kwamba jiji la Harani lilikuwa kwenye njia kuu za kibiashara kati ya majiji mengine makubwa zaidi. Kulingana na maandishi yaliyochimbuliwa huko Harani, mama ya Mfalme Nabonido wa Babiloni alikuwa kuhani mkuu wa kike kwenye hekalu la Sin, mungu wa mwezi wa Harani. Inasemekana kwamba Nabonido alijenga upya hekalu hilo. Baada ya hapo, Harani lilitawaliwa na serikali mbalimbali kubwa.

Leo, mji wa Harani ni tofauti kabisa na jinsi ulivyokuwa zamani. Jiji la kale la Harani lilikuwa jiji la maana sana na lilikuwa limesitawi kwelikweli, hasa katika nyakati fulani. Lakini leo, Harani ni eneo lenye nyumba zenye paa za umbo la mviringo. Mji huo unazungukwa na magofu ya jiji la kale lililokuwa limesitawi. Katika ulimwengu mpya wa Mungu, watu wengi ambao wakati mmoja waliishi huko Harani, kama vile Abrahamu, Sara, na Loti, watafufuliwa. Inaelekea sana kwamba watatueleza mengi kuhusu Harani, kituo cha kale chenye shughuli nyingi.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Magofu ya Harani

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nyumba zenye paa za umbo la mviringo

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mandhari ya mji wa Harani leo