Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaacha Yehova Akuulize Maswali?

Je, Unaacha Yehova Akuulize Maswali?

Je, Unaacha Yehova Akuulize Maswali?

BIBLIA ina mamia ya maswali au maulizo ambayo yanapenya kabisa ndani ya moyo. Kwa kweli, Yehova Mungu mwenyewe anatumia maswali kufundisha kweli za maana sana. Kwa mfano, Yehova alitumia maswali fulani alipokuwa akimwonya Kaini arekebishe mwenendo wake wenye madhara. (Mwa. 4:6, 7) Nyakati nyingine, Yehova aliuliza swali moja tu ambalo lilimchochea mtu kuchukua hatua inayofaa. Baada ya kumsikia Yehova akiuliza: “Nitamtuma nani, na ni nani atakayeenda kwa ajili yetu?” nabii Isaya alijibu hivi: “Mimi hapa! Nitume mimi.”—Isa. 6:8.

Yesu, yule Mwalimu Mkuu, alitumia pia maswali kwa ustadi. Vitabu vya Injili vina maswali zaidi ya 280 ambayo yaliulizwa na Yesu. Ingawa nyakati nyingine alitumia maswali kuwanyamazisha wapinzani wake, mara nyingi aliyatumia ili kugusa mioyo ya wasikilizaji wake, na kuwachochea wafikirie hali yao ya kiroho. (Mt. 22:41-46; Yoh. 14:9, 10) Vivyo hivyo, mtume Paulo, ambaye aliandika vitabu 14 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, alitumia maswali kwa njia yenye kushawishi. (Rom. 10:13-15) Kwa mfano, barua yake kwa Waroma ina maswali mengi sana. Maswali ya Paulo yanawachochea wasomaji kuthamini “kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi.”—Rom. 11:33.

Ingawa maswali fulani yanahitaji kujibiwa kwa sauti, mengine yanakusudiwa kumchochea mtu atafakari kwa uzito. Vitabu vya Injili vinaonyesha kwamba Yesu alitumia sana maswali yaliyowachochea watu kutafakari kwa uzito. Pindi moja, Yesu aliwaonya hivi wanafunzi wake: “Jihadharini na chachu ya Mafarisayo na chachu ya Herode,” yaani, unafiki wao na mafundisho yao ya uwongo. (Marko 8:15; Mt. 16:12) Wanafunzi wa Yesu hawakuelewa alichomaanisha wakaanza kubishana kwa sababu walikuwa wamesahau kubeba mkate. Angalia jinsi Yesu alivyotumia maswali katika mazungumzo mafupi yaliyofuata. “Akawaambia: ‘Kwa nini mnabishana kwa sababu hamna mikate? Je, bado hamjaelewa wala kupata maana? Je, mioyo yenu ni mizito isiweze kuelewa? “Ijapokuwa mna macho, hamwoni; na ijapokuwa mna masikio, hamsikii?” . . . Je, bado hamjapata maana?’” Maswali ya Yesu yalikusudiwa kuwafanya wanafunzi wake wafikiri, na kuwachochea kutafakari kuhusu maana halisi ya maneno yake.—Marko 8:16-21.

“Acha Mimi Nikuulize Maswali”

Yehova Mungu alitumia maswali kurekebisha maoni ya mtumishi wake Ayubu. Kwa kutumia maswali mengi, Yehova alimfundisha Ayubu kwamba yeye ni duni sana akilinganishwa na Muumba wake. (Ayubu, sura ya 38-41) Je, Yehova alitaka Ayubu ajibu kila swali kwa sauti? Inaonekana kwamba hakutaka ajibu kwa sauti. Ni wazi kwamba swali kama vile “Ulikuwa wapi nilipoweka msingi wa dunia?” lilikusudiwa kuchochea fikira na hisia za Ayubu. Baada ya kuulizwa maswali mengi, Ayubu alinyamaza tu. Kisha akasema hivi: “Nitakujibu nini? Nimeuweka mkono wangu juu ya kinywa changu.” (Ayu. 38:4; 40:4) Ayubu alipata maana akajinyenyekeza. Hata hivyo, Yehova hakuwa akimfundisha Ayubu kuwa mnyenyekevu tu. Alirekebisha pia maoni ya Ayubu. Jinsi gani?

Ingawa Ayubu alikuwa “mtu asiye na lawama na mnyoofu,” nyakati nyingine maneno yake yalionyesha kwamba alikuwa na maoni yasiyofaa, na Elihu alifunua jambo hilo alipomkaripia Ayubu kwa sababu “aliitangaza nafsi yake mwenyewe kuwa adilifu badala ya Mungu.” (Ayu. 1:8; 32:2; 33:8-12) Kwa hiyo, maswali ya Yehova pia yalirekebisha uelewaji wa Ayubu. Akizungumza na Ayubu kutoka katika dhoruba ya upepo, Mungu alisema hivi: “Ni nani huyu anayefunika shauri kwa maneno yasiyo na ujuzi? Tafadhali jifunge viuno vyako, kama mwanamume, na acha mimi nikuulize maswali, nawe unijulishe.” (Ayu. 38:1-3) Kwa kutumia maswali, Yehova alikazia hekima na nguvu zake zisizo na mipaka ambazo zinaonyeshwa na kazi zake za ajabu. Ujuzi huo ulimsaidia Ayubu kuamini kabisa hukumu za Yehova na njia yake ya kufanya mambo. Kuulizwa maswali moja kwa moja na Mungu Mweza-Yote kulimchochea Ayubu amwogope na kumheshimu sana!

Jinsi Tunavyoweza Kuacha Yehova Atuulize Maswali

Namna gani sisi? Je, sisi pia tunaweza kufaidika kutokana na maswali yaliyoandikwa katika Biblia? Ndiyo, tunaweza! Tunaweza kupata thawabu nyingi sana za kiroho tukitua na kufikiria maswali hayo. Maswali yanayopenya ndani ya moyo yaliyo katika Neno la Mungu yanachangia nguvu za neno hilo. Kwa kweli, “neno la Mungu . . . lina nguvu . . . nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Ebr. 4:12) Hata hivyo, ili tufaidike kabisa tunahitaji kujiuliza maswali hayo, ni kana kwamba Yehova anatuuliza sisi binafsi. (Rom. 15:4) Acheni tuchunguze mifano michache.

“Je, Mwamuzi wa dunia yote hatafanya lililo sawa?” (Mwa. 18:25) Abrahamu alimuuliza Yehova swali hilo lisilohitaji jibu wakati Mungu alipokuwa akihukumu Sodoma na Gomora. Abrahamu aliona kwamba ni jambo lisilowaziwa kwa Yehova kutenda isivyo haki kwa kuwaangamiza watu waadilifu pamoja na waovu. Swali la Abrahamu linaonyesha kwamba alikuwa na imani yenye nguvu katika uadilifu wa Yehova.

Leo, huenda watu fulani wakakisia mambo fulani kuhusu hukumu za Yehova za wakati ujao, kama vile ni nani hasa watakaookoka Har–Magedoni au ni nani watakaofufuliwa. Badala ya kuhangaishwa na mawazo kama hayo, tunaweza kukumbuka swali la Abrahamu. Kujua kwamba Yehova ni Baba wa kimbingu mwenye kujali na kuwa na uhakika kabisa kama Abrahamu kwamba ni mwenye haki na rehema, kunatusaidia tusipoteze wakati na nguvu zetu kwa kuwa na wasiwasi usio na maana, kutokuwa na mashaka yanayodhoofisha, na kuepuka ubishi usio na maana.

“Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?” (Mt. 6:27) Yesu alipokuwa akihutubia umati mkubwa ambao ulitia ndani wanafunzi wake, alitumia swali hilo kukazia kwamba walihitaji kujitiisha chini ya mikono yenye upendo ya Yehova. Siku za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo zinasababisha mahangaiko mengi, lakini kukazia mahangaiko hayo hakuwezi kurefusha au kuboresha maisha yetu.

Kujikumbusha swali hilo la Yesu kunaweza kutusaidia kuwa na maoni yanayofaa wakati wowote tunapokuwa na mahangaiko kuhusu hali yetu au ya wapendwa wetu. Swali hilo linaweza kutusaidia tuache kuhangaika na kuwa na maoni yasiyofaa ambayo yanatudhoofisha kiakili, kihisia, na kimwili. Yesu alituhakikishia kwamba Baba yetu wa mbinguni, ambaye analisha ndege wa mbinguni na kuivika mimea ya shambani, anajua vizuri kabisa vitu tunavyohitaji.—Mt. 6:26-34.

“Je, mtu anaweza kukusanya moto kifuani pake na mavazi yake yasiungue?” (Met. 6:27) Sura tisa za kwanza za kitabu cha Methali zina hotuba fupi ambazo baba anatoa ili kumfundisha mwana wake kuwa na hekima. Swali ambalo limetajwa hapo juu linaonyesha maumivu yanayosababishwa na uzinzi. (Met. 6:29) Tukigundua kwamba tumekuwa tukiwachezea wengine kimapenzi au tumekuwa na tamaa isiyofaa ya kingono, swali hilo linapaswa kutuonya kuhusu hatari tunayokabili. Kanuni ya swali hilo inaweza pia kumsaidia mtu anayeshawishiwa kutenda kwa njia isiyo ya hekima. Swali hilo linakazia wazi kabisa kanuni hii yenye faida ya Biblia: ‘Unavuna unachopanda’!—Gal. 6:7.

“Wewe ni nani ili umhukumu mtumishi wa nyumbani wa mwingine?” (Rom. 14:4) Katika barua yake kwa Waroma, Paulo alizungumzia matatizo ambayo yalitokea katika kutaniko la karne ya kwanza. Wakristo fulani, wenye hali na malezi mbalimbali, walikuwa na mwelekeo wa kuhukumu maamuzi na matendo ya waamini wenzao. Swali la Paulo liliwakumbusha kwamba walipaswa kukaribishana na kumwachia Yehova kazi ya kuhukumu.

Vivyo hivyo leo, watu wa Yehova wana malezi na hali mbalimbali. Hata hivyo, Yehova ametuleta pamoja na kutuwezesha kuwa na umoja wenye thamani. Je, tunachangia umoja huo? Ikiwa tuna mwelekeo wa kushutumu haraka-haraka matendo ya ndugu fulani yanayotegemea dhamiri yake, ni jambo la hekima kama nini kujiuliza swali hilo la Paulo!

Maswali Yanatusaidia Kumkaribia Yehova Zaidi

Mifano hiyo michache inaonyesha kwamba maswali yaliyo katika Neno la Mungu yana nguvu sana. Kufikiria mistari inayozunguka kila swali kunaweza kutusaidia kutumia habari hiyo kulingana na hali zetu. Na tunaposoma Biblia, tutapata maswali mengine yenye faida.—Ona sanduku kwenye ukurasa wa 14.

Kuruhusu maswali yanayopenya yaliyo katika Neno la Mungu yaguse kabisa mioyo yetu kutatusaidia kupatanisha akili na mioyo yetu na njia za uadilifu za Yehova. Baada ya kuulizwa maswali na Yehova, Ayubu alikiri hivi: “Nimesikia habari zako kwa fununu, lakini sasa jicho langu mwenyewe linakuona wewe.” (Ayu. 42:5) Ndiyo, sasa Yehova alikuwa halisi zaidi kwa Ayubu, ni kana kwamba Ayubu alikuwa akimwona mbele yake. Baadaye mwanafunzi Yakobo alisema hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8) Acheni turuhusu kila sehemu ya Neno la Mungu, kutia ndani maswali yaliyomo, yatusaidie kukua kiroho na ‘kumwona’ Yehova kwa njia iliyo wazi zaidi!

[Sanduku katika ukurasa wa 14]

Kujiuliza maswali haya kunaweza kukusaidia jinsi gani kuona mambo kama Yehova anavyoyaona?

▪ “Je, Yehova hupendezwa sana na matoleo ya kuteketezwa na dhabihu kuliko kuitii sauti ya Yehova?”—1 Sam. 15:22.

▪ “Yule anayelifanya jicho, je, hawezi kutazama?”—Zab. 94:9.

▪ “Watu kujitafutia utukufu wao wenyewe, je, huo ni utukufu?”—Met. 25:27.

▪ “Je, umewaka hasira kwa haki?”—Yona 4:4.

▪ “Mtu atapata faida gani akiupata ulimwengu wote lakini aipoteze nafsi yake?”—Mt. 16:26.

▪ “Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo?”—Rom. 8:35.

▪ “Una nini ambacho hukupokea?”—1 Kor. 4:7.

▪ “Nuru ina ushirika gani na giza?”—2 Kor. 6:14.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ayubu alijifunza nini kutokana na maswali ya Yehova?