Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Waadilifu Watang’aa kwa Uangavu Kama Jua”

“Waadilifu Watang’aa kwa Uangavu Kama Jua”

“Waadilifu Watang’aa kwa Uangavu Kama Jua”

“Wakati huo waadilifu watang’aa kwa uangavu kama jua katika ufalme wa Baba yao.”—MT. 13:43.

1. Yesu alitumia mifano kueleza mambo gani mbalimbali ya Ufalme?

YESU KRISTO alitumia mifano mingi ili kueleza mambo mbalimbali ya Ufalme. ‘Aliuambia umati mambo kwa mifano. Kwa kweli, hakuwa akisema nao bila mfano.’ (Mt. 13:34) Katika mifano kuhusu kupanda mbegu ya kweli ya Ufalme, Yesu alikazia jinsi ambavyo hali ya moyo wa mtu inavyomchochea kukubali ujumbe huo, na pia daraka ambalo Yehova anatimiza katika kutokeza ukuzi wa kiroho. (Marko 4:3-9, 26-29) Yesu alitumia pia mfano ili kuonyesha ukuzi mkubwa wa kazi ya Ufalme hapa duniani, hata ingawa nyakati nyingine ukuzi huo hauonekani mwanzoni. (Mt. 13:31-33) Kwa kuongezea, alikazia kwamba si lazima watu wote wanaokubali ujumbe wa Ufalme wawe raia wanaostahili wa Ufalme huo.—Mt. 13:47-50. *

2. Katika mfano wa Yesu wa ngano na magugu, mbegu nzuri inafananisha nani?

2 Hata hivyo, mfano mmoja ambao Yesu alitoa unakazia kazi ya kuwakusanya wale watakaotawala pamoja naye katika Ufalme wake. Kwa kawaida, mfano huo unaitwa mfano wa ngano na magugu na unapatikana katika sura ya 13 ya kitabu cha Mathayo. Ingawa katika mfano mwingine Yesu anatuambia kwamba mbegu ambayo inapandwa ni “neno la ufalme,” katika mfano huu, anatuambia kwamba mbegu hiyo nzuri inafananisha jambo lingine tofauti, inafananisha “wana wa ufalme.” (Mt. 13:19, 38) Hao si raia wa Ufalme bali ni “wana,” au warithi wa Ufalme.—Rom. 8:14-17; soma Wagalatia 4:6, 7.

Mfano wa Ngano na Magugu

3. Mtu anayetajwa katika mfano huo anakabili tatizo gani na anaamua kulishughulikia jinsi gani?

3 Huu ndio mfano wa ngano na magugu: “Ufalme wa mbinguni umekuwa kama mtu aliyepanda mbegu nzuri katika shamba lake. Watu wakiwa wamelala usingizi, adui yake alikuja na kupanda magugu katikati ya ngano, naye akaondoka. Wakati jani lilipoota na kuzaa matunda, magugu yalionekana pia. Kwa hiyo watumwa wa mwenye nyumba wakaja na kumwambia, ‘Bwana, je, hukupanda mbegu nzuri katika shamba lako? Imekuwaje basi lina magugu?’ Akawaambia, ‘Adui, mtu fulani, alifanya hivyo.’ Wakamwambia, ‘Basi, je, unataka twende kuyakusanya?’ Akasema, ‘Hapana; ili, mnapoyakusanya magugu, msije mkang’oa ngano pamoja nayo. Acheni zikue pamoja mpaka wakati wa mavuno; na katika majira ya mavuno nitawaambia wavunaji, Kwanza kusanyeni magugu na kuyafunga matita-matita ili kuyateketeza motoni, ndipo nendeni mkusanye ngano ghalani mwangu.’”—Mt. 13:24-30.

4. (a) Mtu anayetajwa katika mfano huo ni nani? (b) Yesu alianza wakati gani na jinsi gani kupanda mbegu hiyo?

4 Mtu aliyepanda mbegu nzuri katika shamba lake ni nani? Yesu anajibu swali hilo baadaye anapowaeleza hivi wanafunzi wake: “Mpandaji wa mbegu nzuri ni Mwana wa binadamu.” (Mt. 13:37) Yesu, ambaye ni “Mwana wa binadamu,” alitayarisha shamba katika kipindi cha miaka mitatu na nusu ya huduma yake duniani ili apande mbegu. (Mt. 8:20; 25:31; 26:64) Kisha kuanzia Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. na kuendelea, alianza kupanda mbegu nzuri, yaani, “wana wa ufalme.” Inaonekana kwamba mbegu hiyo ilipandwa wakati Yesu, akiwa mwakilishi wa Yehova, alipoanza kuwamwagia wanafunzi wake roho takatifu, na hivyo akawatia mafuta ili wawe wana wa Mungu. * (Mdo. 2:33) Mbegu hiyo nzuri ilikomaa na kuwa ngano. Kwa hiyo, Yesu alipanda mbegu nzuri ili mwishowe akusanye hesabu kamili ya wale ambao wangekuwa warithi na watawala wenzake katika Ufalme wake.

5. Adui anayetajwa katika mfano huo ni nani, na magugu yanafananisha nani?

5 Adui ni nani, na magugu ni nani? Yesu anatuambia kwamba adui “ni Ibilisi.” Biblia inasema magugu ni “wana wa yule mwovu.” (Mt. 13:25, 38, 39) Kwa njia halisi, magugu ambayo Yesu alizungumzia huenda yalikuwa magugu fulani yenye sumu ambayo yanafanana sana na ngano ambayo haijakomaa. Mfano huo unawafaa sana Wakristo wa uwongo, wale wanaodai kuwa wana wa Ufalme lakini hawazai matunda yanayofaa! Wakristo hao wenye unafiki ambao wanadai kuwa wafuasi wa kweli wa Kristo kwa kweli wao ni sehemu ya “mbegu” ya Shetani Ibilisi.—Mwa. 3:15.

6. Magugu yalianza kutokea wakati gani, na watu walikuwa “wamelala usingizi” jinsi gani wakati huo?

6 Wakristo hao ambao ni kama magugu walitokea wakati gani? Yesu anasema hivi: “Watu wakiwa wamelala usingizi.” (Mt. 13:25) Ni wakati gani huo? Tunapata jibu katika maneno ambayo mtume Paulo aliwaambia wazee wa huko Efeso: “Ninajua kwamba baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wenye kukandamiza wataingia katikati yenu nao hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Mdo. 20:29, 30) Kisha akawahimiza wazee hao wakae macho kiroho. Mitume, ambao walikuwa kama “kizuizi” kwa uasi-imani, walipoanza kulala usingizi katika kifo, Wakristo wengi walilala usingizi wa kiroho. (Soma 2 Wathesalonike 2:3, 6-8.) Uasi-imani mkubwa ulianza wakati huo.

7. Je, ngano iligeuka na kuwa magugu? Eleza.

7 Yesu hakusema kwamba ngano ingegeuka na kuwa magugu, alisema kwamba magugu yangepandwa katikati ya ngano. Kwa hiyo, mfano huo haumaanishi kwamba Wakristo wa kweli wangeacha kweli. Badala yake, unaonyesha kwamba Shetani angejitahidi kwa makusudi kulipotosha kutaniko la Kikristo kwa kuingiza watu waovu ndani yake. Mtume wa mwisho, Yohana, alipokuwa amezeeka, uasi-imani huo ulikuwa unaonekana waziwazi.—2 Pet. 2:1-3; 1 Yoh. 2:18.

“Acheni Zikue Pamoja Mpaka Wakati wa Mavuno”

8, 9. (a) Kwa nini wasikilizaji wa Yesu waliona hekima ya maagizo ambayo Bwana aliwapa watumwa wake? (b) Ngano na magugu ya mfano yalikua pamoja jinsi gani?

8 Watumwa wanamwambia Bwana wao tatizo wanalokabili na kumuuliza hivi: “Basi, je, unataka twende kuyakusanya [magugu]?” (Mt. 13:27, 28) Huenda jibu lake likaonekana kuwa lenye kushangaza. Anawaambia waache ngano na magugu yakue pamoja mpaka wakati wa mavuno. Wanafunzi wa Yesu wangeona hekima ya kutii amri hiyo. Walijua kwamba ni vigumu kutofautisha ngano na yale magugu yenye sumu yanayofanana kabisa na ngano. Wanafunzi waliojua mambo ya ukulima walitambua pia kwamba kwa kawaida mizizi ya magugu hayo inaingia katikati ya mizizi ya ngano. * Ndiyo sababu Bwana wao anawaambia wangoje!

9 Vivyo hivyo, kwa karne nyingi, madhehebu mbalimbali ya dini zinazodai kuwa za Kikristo yamezaa magugu mengi sana, kwanza katika makanisa ya Kikatoliki na ya Kiothodoksi na baadaye katika vikundi vingi sana vya Kiprotestanti ambavyo vilisitawi. Wakati huohuo, mbegu chache za ngano halisi zilipandwa ulimwenguni. Katika mfano huo, mwenye nyumba alingoja kwa subira kwa muda mrefu ili ngano ikue mpaka wakati ambapo kipindi kifupi cha mavuno kingefika.

Wakati wa Mavuno Uliongojewa Sana

10, 11. (a) Kazi ya kuvuna inafanywa wakati gani? (b) Ngano ya mfano inakusanywa jinsi gani ndani ya ghala la Yehova?

10 Yesu anatuambia hivi: “Yale mavuno ni umalizio wa mfumo wa mambo, na wavunaji ni malaika.” (Mt. 13:39) Katika siku za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo, wana wa Ufalme wanakusanywa na kutenganishwa kutoka kwa watu wowote ambao ni kama magugu. Mtume Petro anatuambia hivi kuhusu jambo hilo: “Ni wakati uliowekwa wa hukumu kuanza na nyumba ya Mungu. Sasa ikiwa inaanza na sisi kwanza, basi mwisho wa wale wasioitii habari njema ya Mungu utakuwaje?”—1 Pet. 4:17.

11 Muda mfupi baada ya siku za mwisho au “umalizio wa mfumo wa mambo” kuanza, wale waliodai kuwa Wakristo wa kweli walianza kuhukumiwa ili kuamua ikiwa kwa kweli walikuwa “wana wa ufalme” au “wana wa yule mwovu.” “Kwanza” Babiloni Mkubwa alianguka, “ndipo” wana wa Ufalme wakakusanywa pamoja wakati kazi ya kuvuna ilipoanza. (Mt. 13:30) Lakini ngano ya mfano inakusanywa jinsi gani leo ndani ya depo au ghala la Yehova? Watu hao waliovunwa walijiunga na kutaniko la Kikristo ambalo limepangwa kitengenezo na ambalo linaendeleza ibada safi, ambamo wanakubaliwa na Mungu na kupata ulinzi wake, au walipata thawabu yao ya kwenda mbinguni.

12. Kazi ya kuvuna inaendelea kwa muda gani?

12 Hukumu inaendelea kwa muda gani? Yesu alisema kwamba kuna “majira” ya mavuno, kwa hiyo hukumu inaendelea kwa kipindi fulani. (Ufu. 14:15, 16) Hukumu ya watiwa-mafuta wakiwa mtu mmoja-mmoja inaendelea katika kipindi chote cha siku za mwisho. Itaendelea mpaka watiwe muhuri wa mwisho.—Ufu. 7:1-4.

13. Magugu yanasababisha kukwazika namna gani, nao wanaasi sheria jinsi gani?

13 Ni nani watakaokusanywa kutoka katika Ufalme, na wanasababisha jinsi gani kukwazika na kuasi sheria? (Mt. 13:41) Viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo ambao ni kama magugu wamepotosha mamilioni ya watu kwa karne nyingi. Wamefanya hivyo kwa kufundisha mafundisho ambayo hayamletei Mungu heshima, ‘mambo ambayo yanasababisha kukwazika,’ kama vile fundisho la watu kuadhibiwa milele katika moto wa mateso na fundisho la Utatu ambalo ni fumbo lisiloeleweka. Viongozi wengi wa kidini wamewawekea mfano mbaya sana kondoo wao kwa kufanya uzinzi pamoja na ulimwengu huu na nyakati nyingine wanatenda waziwazi mambo yaliyopotoka kimaadili. (Yak. 4:4) Kwa kuongezea, dini zinazodai kuwa za Kikristo zinawaruhusu washiriki wake waendelee kuwa na mwenendo mpotovu wa kingono. (Soma Yuda 4.) Hata ingawa wanatenda mambo hayo yote, wanaendelea kujionyesha kwa nje kuwa watakatifu na watu wanaomwogopa Mungu. Wana wa Ufalme wanafurahi kama nini kutengwa mbali na uvutano huo wa magugu na mafundisho yenye kupotosha ambayo yanawakwaza watu!

14. Watu ambao ni kama magugu wanalia na kusaga meno yao jinsi gani?

14 Watu ambao ni kama magugu wanalia na kusaga meno yao jinsi gani? (Mt. 13:42) “Wana wa yule mwovu” wanateseka kwa sababu “wana wa ufalme” wamefunua hali ya kiroho yenye sumu ya magugu hayo ya mfano. Pia, wanaomboleza kwa sababu washiriki wengi wa makanisa yao hawaungi tena mkono dini, hivyo wanapoteza mamlaka ya kuwaongoza.—Soma Isaya 65:13, 14.

15. Watu ambao ni kama magugu wanateketezwa kwa moto namna gani?

15 Ni katika maana gani magugu yanakusanywa na kuteketezwa kwa moto? (Mt. 13:40) Hilo linaonyesha jambo ambalo litayapata magugu hayo mwishowe. Kutupwa kwa magugu hayo kwa njia ya mfano ndani ya tanuru ya moto kunaonyesha kwamba yataharibiwa milele. (Ufu. 20:14; 21:8) Wakristo wa uwongo na wadanganyifu ambao ni kama magugu, wataharibiwa kabisa wakati wa “dhiki kuu.”—Mt. 24:21.

“Watang’aa kwa Uangavu Kama Jua”

16, 17. Malaki alitoa unabii gani kuhusu hekalu la Mungu, na ulianza kutimizwa jinsi gani?

16 Watu ambao ni kama ngano “watang’aa kwa uangavu kama jua” wakati gani? (Mt. 13:43) Malaki alitabiri hivi kuhusu kusafishwa kwa hekalu la Mungu: “‘Kwa ghafula Bwana wa kweli atakuja kwenye hekalu Lake, ambaye ninyi mnamtafuta, na mjumbe wa agano mnayependezwa naye. Tazama! Atakuja hakika,’ asema Yehova wa majeshi. ‘Lakini ni nani atakayeistahimili siku ya kuja kwake, naye ni nani atakayesimama wakati atakapoonekana? Kwa maana atakuwa kama moto wa msafishaji na kama sabuni ya wafuaji wa nguo. Naye ataketi kama msafishaji na mtakasaji wa fedha naye atawatakasa wana wa Lawi; naye atawasafisha kama dhahabu na kama fedha, nao watakuwa kwa Yehova watu wanaotoa toleo la zawadi katika uadilifu.’”—Mal. 3:1-3.

17 Katika nyakati zetu, ni wazi kwamba unabii huo ulianza kutimizwa mwaka wa 1918 wakati Yehova, pamoja na “mjumbe wa agano,” Yesu Kristo, walipokagua hekalu la kiroho. Malaki anatuambia jambo linalotukia wakati kazi hiyo ya kusafisha inapokamilika: “Nanyi mtaona tena tofauti kati ya mwadilifu na mwovu, kati ya mtu anayemtumikia Mungu na mtu ambaye hajamtumikia.” (Mal. 3:18) Kuongezeka kwa utendaji wa Wakristo wa kweli waliotendeshwa tena kunaonyesha kwamba mavuno yalianza wakati huo.

18. Ni nini ambacho Danieli alitabiri kwamba kingetukia katika siku zetu?

18 Nabii Danieli alitabiri hivi kuhusu siku zetu: “Wale walio na ufahamu watang’aa kama mwangaza wa anga; na wale wanaoleta wengi kwenye uadilifu, watang’aa mpaka wakati usio na kipimo, milele kama nyota.” (Dan. 12:3) Ni nani hao wanaong’aa kwa uangavu sana? Si wengine ila ni Wakristo watiwa-mafuta, ngano ya kweli ambayo Yesu alitaja katika mfano wake kuhusu ngano na magugu! Umati mkubwa unaoongezeka wa kondoo wa mfano umetambua waziwazi ‘kukusanywa’ kwa Wakristo wa uwongo ambao ni kama magugu. Washiriki wa umati huo mkubwa ambao wanatazamia kuwa raia wa Ufalme wanashikamana na mabaki ya Waisraeli wa kiroho na wao pia wanaacha nuru yao iangaze katika ulimwengu wenye giza.—Zek. 8:23; Mt. 5:14-16; Flp. 2:15.

19, 20. “Wana wa ufalme” wanangoja nini kwa hamu, na tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

19 Leo, “wana wa ufalme” wanangoja kwa hamu thawabu yao tukufu ya kimbingu. (Rom. 8:18, 19; 1 Kor. 15:53; Flp. 1:21-24) Hata hivyo, kabla ya wakati huo, ni lazima waendelee kuwa waaminifu, waendelee kuangaza kwa uangavu wakiwa tofauti kabisa na “wana wa yule mwovu.” (Mt. 13:38; Ufu. 2:10) Sote tunafurahi kama nini kwamba tumepata pendeleo la kuona matokeo ya kazi hiyo ya ‘kukusanya’ magugu kwa njia ya mfano katika nyakati zetu!

20 Lakini kuna uhusiano gani kati ya wana wa Ufalme na umati mkubwa unaozidi kuongezeka wa wale wanaotumaini kuishi milele duniani wakiwa raia wa Ufalme? Habari inayofuata itajibu swali hilo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Kwa maelezo zaidi kuhusu mifano hiyo, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2008 (15/7/2008), ukurasa wa 12-21.

^ fu. 4 Katika mfano huo, kazi ya kupanda mbegu haifananishi kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, ambayo ingewakusanya watu wapya ambao wangekuwa Wakristo watiwa-mafuta. Yesu alisema hivi kuhusu mbegu nzuri ambayo inapandwa katika shamba: “Hiyo ni [si kwamba “itakuwa”] wana wa ufalme.” Kupanda kunafananisha kuwatia mafuta wana hao wa Ufalme katika shamba la ulimwengu.

^ fu. 8 Mizizi ya magugu hayo yenye sumu inaingia kabisa katikati ya mizizi ya ngano, hivi kwamba mtu aking’oa magugu hayo kabla ya wakati wa kuvuna atang’oa pia ngano.—Ona Insight on the Scriptures, Buku la 1, ukurasa wa 1178 au Étude perspicace des Écritures, Buku la 1, ukurasa wa 836.

Je, Unakumbuka?

Katika mfano wa Yesu kuhusu ngano na magugu, mambo yafuatayo yanamaanisha nini?

• Mbegu nzuri

• Mtu aliyepanda mbegu

• Kupanda mbegu

• Adui

• Magugu

• Majira ya mavuno

• Ghala au depo

• Kulia na kusaga meno

• Tanuru ya moto

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mbegu nzuri ilianza kupandwa wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ngano ya mfano inakusanywa sasa ndani ya ghala la Yehova

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.