Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msimamizi-nyumba Mwaminifu na Baraza Lake Linaloongoza

Msimamizi-nyumba Mwaminifu na Baraza Lake Linaloongoza

Msimamizi-nyumba Mwaminifu na Baraza Lake Linaloongoza

“Ni nani kwa kweli aliye msimamizi-nyumba mwaminifu, mwenye busara, ambaye bwana wake atamweka rasmi juu ya watumishi wake kuendelea kuwapa kipimo chao cha chakula katika wakati unaofaa?”—LUKA 12:42.

1, 2. Ni swali gani la maana ambalo Yesu aliuliza alipokuwa akitoa ishara yenye matukio mengi ya siku za mwisho?

ALIPOKUWA akitoa ishara yenye matukio mengi ya siku za mwisho, Yesu aliuliza swali hili: “Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa?” Kisha Yesu akasema kwamba kwa sababu ya kuwa mwaminifu, mtumwa huyo atapewa thawabu kwa kuwekwa juu ya mali zote za Bwana wake.—Mt. 24:45-47.

2 Miezi fulani mapema, Yesu alikuwa ameuliza swali kama hilo. (Soma Luka 12:42-44.) Alimwita mtumwa huyo “msimamizi-nyumba” na akatumia neno “watumishi” kuwahusu “watumishi wake wa nyumbani.” Msimamizi-nyumba ni mwangalizi wa nyumba anayepewa daraka la kuwasimamia watumishi. Hata hivyo, msimamizi-nyumba huyo ni mtumishi pia. Mtumwa, au msimamizi-nyumba huyo ni nani, naye anatoa jinsi gani ‘chakula kwa wakati unaofaa’? Ni jambo la maana kwetu sote kutambua njia ambayo inatumiwa kutoa chakula hicho cha kiroho.

3. (a) Wasomi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wanasema maneno ya Yesu kuhusu yule “mtumwa” yanawahusu nani? (b) Yule “msimamizi-nyumba,” au “mtumwa” ni nani, na “watumishi,” au ‘watumishi wa nyumbani’ ni nani?

3 Mara nyingi wasomi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wanafikiri kwamba maneno hayo ya Yesu yanawahusu wale ambao wana vyeo vya madaraka kati ya wale wanaodai kuwa Wakristo. Lakini Yesu, ambaye ni “bwana” katika mfano huo, hakusema kwamba kungekuwa na watumwa wengi waliotawanyika katika madhehebu au dini mbalimbali zinazodai kuwa za Kikristo. Badala yake, alisema waziwazi kwamba kungekuwa na “msimamizi-nyumba” au “mtumwa” mmoja tu, ambaye Yesu angemweka juu ya mali zake zote. Kwa hiyo, kama vile ambavyo gazeti hili limeeleza mara nyingi, msimamizi-nyumba huyo anawakilisha “kundi dogo” la wanafunzi watiwa-mafuta wakiwa kikundi. Katika mistari mingine ya Injili ya Luka, Yesu alikuwa amezungumza kuhusu wanafunzi hao. (Luka 12:32) Maneno “watumishi,” au ‘watumishi wa nyumbani’ yanahusu kikundi hichohicho lakini yanakazia daraka lao wakiwa mtu mmoja-mmoja. Swali lenye kuvutia fikira linatokea, Je, mshiriki mmoja-mmoja wa jamii hiyo ya mtumwa anashiriki katika kutayarisha chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa? Tunaweza kupata jibu kwa kuchunguza kwa makini yale ambayo Maandiko yanasema.

Watumishi wa Yehova Katika Nyakati za Kale

4. Yehova alitumia maneno gani kuhusu taifa la kale la Israeli, na tunapaswa kukumbuka jambo gani la maana kuhusu taifa hilo?

4 Yehova aliwaita watu wake, taifa la kale la Israeli, kwa ujumla kuwa mtumishi wake. “‘Ninyi [kwa wingi] ni mashahidi wangu [kwa wingi],’ asema Yehova, ‘mtumishi wangu [kwa umoja] ambaye nimemchagua.’” (Isa. 43:10) Washiriki wote wa taifa hilo walitiwa ndani ya jamii hiyo moja ya mtumishi. Hata hivyo, ni jambo la maana kukumbuka kwamba ni makuhani tu pamoja na Walawi wasio makuhani ndio waliokuwa na daraka la kulifundisha taifa hilo.—2 Nya. 35:3; Mal. 2:7.

5. Yesu alisema kungekuwa na badiliko gani kubwa?

5 Je, taifa la Israeli ndilo lililokuwa mtumwa ambaye Yesu alizungumza kumhusu? Hapana. Tunajua si taifa hilo kwa sababu ya maneno haya ambayo Yesu aliwaambia Wayahudi wa siku zake: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” (Mt. 21:43) Ni wazi kwamba kungekuwa na badiliko. Yehova angetumia taifa jipya. Hata hivyo, inapohusu mafundisho ya kiroho, mtumwa anayetajwa katika mfano wa Yesu anatimiza daraka kama lile ambalo lilitimizwa na “mtumishi” wa Mungu katika Israeli la kale.

Mtumwa Mwaminifu Anatokea

6. Ni taifa gani jipya lililoanza wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., na ni nani waliokuwa washiriki wa taifa hilo?

6 Taifa hilo jipya ni “Israeli wa Mungu,” na washiriki wake ni Waisraeli wa kiroho. (Gal. 6:16; Rom. 2:28, 29; 9:6) Taifa hilo lilianza wakati roho ya Mungu ilipomwagwa juu yao wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Kisha, Wakristo wote waliotiwa mafuta kwa roho wakawa washiriki wa taifa hilo ambalo sasa lilitumika likiwa jamii ya mtumwa iliyowekwa rasmi na Bwana, Yesu Kristo. Kila mshiriki wa taifa hilo alipewa daraka la kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Lakini je, kila mshiriki wa kikundi hicho angeshiriki katika kutayarisha chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa? Acheni tuone jinsi Maandiko yanavyojibu swali hilo.

7. Mwanzoni, kazi kuu ya mitume ilikuwa nini, na baadaye kazi hiyo ilipanuka jinsi gani?

7 Yesu alipowachagua wale mitume wake 12, kazi yao kuu ilitia ndani kutumwa kuwahubiria wengine habari njema. (Soma Marko 3:13-15.) Mgawo huo ulipatana na maana ya msingi ya neno apostolos la Kigiriki, ambalo linatokana na kitenzi kinachomaanisha “kumtuma mtu.” Hata hivyo, kadiri wakati ulivyopita na kutaniko la Kikristo lilipokuwa karibu kuanzishwa, daraka la mitume likawa ‘cheo cha uangalizi.’—Mdo. 1:20-26.

8, 9. (a) Hangaiko kuu la wale mitume 12 lilikuwa nini? (b) Kama ilivyothibitishwa na baraza linaloongoza, ni nani wengine walikabidhiwa madaraka ya ziada?

8 Hangaiko kuu la wale mitume 12 lilikuwa nini? Mambo yaliyotukia baada ya siku ya Pentekoste yanajibu swali hilo. Ubishi ulipotokea kuhusu ugawaji wa kila siku wa chakula kwa wajane, wale mitume 12 waliwakusanya wanafunzi na kusema hivi: “Si vyema sisi kuliacha neno la Mungu ili kugawa chakula mezani.” (Soma Matendo 6:1-6.) Kisha, mitume waliwaweka rasmi ndugu wengine wanaostahili kiroho ili kushughulikia ‘kazi hiyo ya lazima’ ili mitume wajitoe “kwa huduma ya neno.” Mpango huo ulibarikiwa na Yehova kwa sababu ‘neno la Mungu liliendelea kukua, na hesabu ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana katika Yerusalemu.’ (Mdo. 6:7) Kwa hiyo, mitume ndio waliokuwa na daraka kuu la kutayarisha chakula cha kiroho.—Mdo. 2:42.

9 Baadaye, wengine walikabidhiwa madaraka mazito. Chini ya mwongozo wa roho takatifu, Paulo na Barnaba walitumwa na kutaniko la Antiokia kuwa wamishonari. Walijulikana pia kuwa mitume, hata ingawa hawakuwa kati ya wale mitume wa kwanza 12. (Mdo. 13:1-3; 14:14; Gal. 1:19) Baraza linaloongoza huko Yerusalemu lilithibitisha kuwekwa rasmi kwao. (Gal. 2:7-10) Muda mfupi baadaye, Paulo alishiriki katika kutoa chakula cha kiroho. Aliandika barua yake ya kwanza iliyoongozwa na roho takatifu.

10. Je, Wakristo wote waliotiwa mafuta kwa roho walishiriki katika kutayarisha chakula cha kiroho katika karne ya kwanza? Eleza.

10 Hata hivyo, je, ni Wakristo wote waliotiwa mafuta kwa roho ambao walihusika katika kusimamia kazi ya kuhubiri na kutayarisha chakula cha kiroho? Hapana. Mtume Paulo anatuambia hivi: “Je, wote ni mitume? Je, wote ni manabii? Je, wote ni walimu? Je, wote hufanya matendo yenye nguvu?” (1 Kor. 12:29) Ingawa Wakristo wote waliozaliwa kwa roho walishiriki katika kazi ya kuhubiri, ni wachache tu, yaani, wanaume wanane, ndio waliotumiwa kuandika vile vitabu 27 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

Mtumwa Mwaminifu Katika Siku Zetu

11. Mtumwa aliwekwa rasmi juu ya “mali” gani?

11 Maneno ya Yesu katika Mathayo 24:45 yanaonyesha wazi kwamba bado kungekuwa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara duniani katika siku za mwisho. Andiko la Ufunuo 12:17 linawaita watu hao kuwa “waliobaki” wa uzao wa mwanamke. Wakiwa kikundi, mabaki hao wamewekwa rasmi juu ya mali zote za Kristo hapa duniani. “Mali” ambazo msimamizi-nyumba mwaminifu amewekwa rasmi kutunza ni mambo yote ya Bwana huyo yanayohusu Ufalme duniani. Mali hizo zinatia ndani raia wa kidunia wa Ufalme huo na vifaa na majengo yanayotumiwa katika kazi ya kuhubiri habari njema.

12, 13. Mkristo anajua namna gani kwamba ana mwito wa kwenda mbinguni?

12 Mkristo anajua namna gani kwamba ana tumaini la kwenda mbinguni na ikiwa ni mmoja wa mabaki ya Waisraeli wa kiroho? Mtume Paulo anajibu swali hilo katika maneno aliyowaambia wale ambao walikuwa na tumaini la kwenda mbinguni kama yeye: “Wote wanaoongozwa na roho ya Mungu, hao ndio wana wa Mungu. Kwa maana hamkupokea roho ya utumwa inayosababisha woga tena, bali mlipokea roho ya kufanywa kuwa wana, roho ambayo kupitia hiyo tunapaaza sauti: ‘Abba, Baba!’ Roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu. Basi, ikiwa sisi ni watoto, sisi pia ni warithi: warithi wa Mungu kwelikweli, lakini warithi pamoja na Kristo, mradi tu tunateseka pamoja ili pia tutukuzwe pamoja.”—Rom. 8:14-17.

13 Kwa ufupi, watu hao wametiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu nao wanapokea “mwito,” au mwaliko wa kwenda mbinguni. (Ebr. 3:1) Mungu ndiye anayewaalika kibinafsi. Na bila kusitasita, bila kuwa na shaka au woga wowote, wanakubali mara moja kuzaliwa wakiwa wana wa Mungu. (Soma 1 Yohana 2:20, 21.) Kwa hiyo, hawajichagulii wenyewe tumaini hilo, lakini Yehova anatia muhuri wake, au roho yake takatifu, juu yao.—2 Kor. 1:21, 22; 1 Pet. 1:3, 4.

Maoni Yanayofaa

14. Watiwa-mafuta wana maoni gani kuhusu mwito wao?

14 Watiwa-mafuta hao wanapaswa kuwa na maoni gani kujihusu wanapongojea thawabu yao ya kwenda mbinguni? Wanatambua kwamba ingawa wamepewa mwaliko mzuri ajabu, huo ni mwaliko tu. Ni lazima waendelee kuwa waaminifu mpaka kifo ili wapate zawadi hiyo. Kwa unyenyekevu, wanahisi kama Paulo aliyesema hivi: “Akina ndugu, bado mimi mwenyewe sijioni kwamba nimekwisha kulishika hilo; lakini kuna jambo moja kulihusu: Nayasahau mambo ya nyuma na kujinyoosha kwenda mbele kuelekea mambo yaliyo mbele, ninafuatilia kuelekea ule mradi kwa ajili ya tuzo la mwito wa Mungu wa kwenda juu kwa njia ya Kristo Yesu.” (Flp. 3:13, 14) Ni lazima mabaki watiwa-mafuta wafanye yote wanayoweza ili ‘watembee kwa kuustahili mwito walioitiwa, wakiwa na unyenyekevu kamili wa akili,’ na kufanya hivyo “kwa kuogopa na kutetemeka.”—Efe. 4:1, 2; Flp. 2:12; 1 The. 2:12.

15. Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani kuwahusu wale wanaokula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho, na watiwa-mafuta wana maoni gani kujihusu?

15 Kwa upande mwingine, Wakristo wengine wanapaswa kuwa na maoni gani kumhusu mtu ambaye anadai kwamba ametiwa-mafuta na hivyo anaanza kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho? Hawapaswi kumhukumu mtu huyo. Jambo hilo ni kati yake na Yehova. (Rom. 14:12) Hata hivyo, Wakristo ambao ni watiwa-mafuta wa kweli hawadai wengine wawatendee kwa njia ya pekee. Hawaamini kwamba kwa sababu wametiwa mafuta wana ufahamu wa pekee kuliko hata washiriki fulani wenye uzoefu wa “umati mkubwa.” (Ufu. 7:9) Hawaamini kwamba wana roho takatifu nyingi zaidi kuliko Wakristo wenzao ambao ni washiriki wa “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Hawatazamii kutendewa kwa njia ya pekee; wala hawadai kwamba kula mkate na kunywa divai ya Ukumbusho kunawafanya wawe juu ya wazee waliowekwa rasmi kutanikoni.

16-18. (a) Je, watiwa-mafuta wote wanashiriki katika kutoa kweli mpya za kiroho? Toa mfano. (b) Kwa nini hakuna haja ya Baraza Linaloongoza kuwasiliana na wote wanaodai kwamba ni watiwa-mafuta?

16 Je, watiwa-mafuta wote duniani ni washiriki wa kikundi fulani cha duniani pote ambacho kinashirikiana kwa njia fulani katika kufunua kweli mpya za kiroho? Hapana. Ingawa jamii ya mtumwa ikiwa kikundi ina daraka la kuwalisha kiroho wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo, si kila mshiriki wa jamii ya mtumwa ana madaraka au migawo ileile. (Soma 1 Wakorintho 12:14-18.) Kama ilivyotajwa mwanzoni, katika karne ya kwanza, wote walishiriki katika kazi ya maana sana ya kuhubiri. Lakini ni washiriki wachache tu ndio waliotumiwa kuandika vitabu vya Biblia na kusimamia kutaniko la Kikristo.

17 Kwa mfano: Nyakati nyingine, Maandiko yanasema kwamba “kutaniko” linachukua hatua fulani katika kushughulikia mambo ya kihukumu. (Mt. 18:17) Hata hivyo, ukweli ni kwamba ni wazee tu wanaochukua hatua hiyo wakiwa wawakilishi wa kutaniko. Wazee hawazungumzi na washiriki wote wa kutaniko na kuwauliza maoni yao kabla ya kufanya uamuzi. Kulingana na mpango wa kitheokrasi, wanatimiza daraka ambalo wamegawiwa; wanatenda kwa niaba ya kutaniko lote.

18 Vivyo hivyo leo, kuna hesabu ndogo ya wanaume watiwa-mafuta ambao wana daraka la kuiwakilisha jamii ya mtumwa. Wanaume hao ndio washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Wanaume hao waliotiwa mafuta kwa roho wanasimamia kazi ya Ufalme na programu ya kutayarisha chakula cha kiroho. Hata hivyo, kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, Baraza Linaloongoza haliwasiliani na kila mshiriki wa jamii ya mtumwa kabla ya kufanya maamuzi. (Soma Matendo 16:4, 5.) Lakini, Mashahidi wote watiwa-mafuta wanashiriki kikamili katika kazi ya maana sana ya kuvuna ambayo inaendelea leo. Wakiwa jamii, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ni mwili mmoja, lakini wakiwa mtu mmoja-mmoja wana migawo mbalimbali.—1 Kor. 12:19-26.

19, 20. Washiriki wa umati mkubwa wana maoni gani yenye usawaziko kuhusu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na Baraza lake Linaloongoza?

19 Mambo hayo ya hakika yanapaswa kuwachochea jinsi gani washiriki wa umati mkubwa ambao wanatumaini kuishi milele duniani? Wakiwa sehemu ya mali za Mfalme, wanafurahi kuunga mkono kikamili mipango inayofanywa na Baraza Linaloongoza, ambalo linamwakilisha “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Washiriki wa umati mkubwa wanathamini chakula cha kiroho kinachotayarishwa chini ya mwongozo wa Baraza Linaloongoza. Lakini wakati uleule, ingawa washiriki wa umati mkubwa wanaiheshimu jamii ya mtumwa, wanakuwa waangalifu ili wasimtukuze mtu yeyote yule anayedai kuwa mshiriki wa jamii ya mtumwa huyo. Hakuna Mkristo yeyote ambaye kwa kweli alitiwa mafuta kwa roho ya Mungu angetaka au kutazamia atendewe kwa njia hiyo.—Mdo. 10:25, 26; 14:14, 15.

20 Iwe sisi ni ‘watumishi wa nyumbani’ mwake, ambao ni washiriki wa mabaki ya watiwa-mafuta, au sisi ni washiriki wa umati mkubwa, acheni tuazimie kushirikiana kikamili na msimamizi-nyumba mwaminifu na Baraza lake Linaloongoza. Acheni sote ‘tukeshe’ na kubaki waaminifu mpaka mwisho.—Mt. 24:13, 42.

Je, Unakumbuka?

• “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ni nani, na watumishi wa nyumbani mwake ni nani?

• Mtu anajua namna gani kwamba ana mwito wa kwenda mbinguni?

• Ni nani aliye na daraka kuu la kutayarisha chakula kipya cha kiroho?

• Mtiwa-mafuta anapaswa kuwa na maoni gani kujihusu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Leo, Baraza Linaloongoza linaiwakilisha jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Kulikuwa na mpango kama huo katika karne ya kwanza