Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kuvumilia Jinsi Gani Katika Huduma?

Unaweza Kuvumilia Jinsi Gani Katika Huduma?

Unaweza Kuvumilia Jinsi Gani Katika Huduma?

JE, UMEWAHI kuhisi umechoka kabisa hivi kwamba unataka kuacha kazi ya kuhubiri? Uvumilivu wetu unaweza kujaribiwa na upinzani mkali, mahangaiko, afya mbaya, shinikizo kutoka kwa wengine, au kutopata matokeo mazuri katika huduma. Hata hivyo, fikiria mfano wa Yesu. Alivumilia jaribu kali zaidi kuliko majaribu yote “kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake.” (Ebr. 12:2) Alijua kwamba kwa kuthibitisha kuwa mashtaka yaliyotolewa kumhusu Mungu hayakuwa na msingi wowote, alikuwa akiufanya moyo wa Yehova ushangilie.—Met. 27:11.

Ukivumilia katika huduma, wewe pia unaweza kuufanya moyo wa Yehova ushangilie. Hata hivyo, namna gani ikiwa matatizo fulani yanakufanya ukose nguvu za kiroho? Krystyna, ambaye ni mzee kwa umri na ambaye ana afya mbaya, anakubali hivi: “Ni jambo la kawaida kuhisi nimechoka na kuvunjika moyo. Matatizo yangu ya uzee, kama vile afya mbaya na mahangaiko kuhusu maisha ya kila siku yanapunguza bidii yangu mara kwa mara.” Unaweza kuvumilia jinsi gani katika huduma hata ukikabili matatizo hayo?

Waige Manabii

Ili wahubiri waaminifu wa Ufalme wavumilie katika kazi ya kuhubiri, wanaweza kujitahidi kuwa na mtazamo wa akili kama ule wa manabii wa zamani. Kwa mfano, mfikirie Yeremia. Alipoitwa ili atumikie akiwa nabii, mwanzoni alisitasita. Hata hivyo, Yeremia aliweza kuvumilia katika mgawo wake mgumu kwa miaka zaidi ya 40 kwa sababu alijifunza kumtegemea kabisa Mungu.—Yer. 1:6; 20:7-11.

Henryk anapata nguvu kwa kufikiria mfano wa Yeremia. Anasema hivi: “Katika miaka zaidi ya 70 ambayo nimekuwa nikihubiri, nyakati nyingine nimevunjika moyo kwa sababu ya itikio la watu—ukali wao au kutopendezwa kwao. Nyakati kama hizo, ninajikumbusha mfano wa Yeremia. Upendo wake kwa Yehova na uhusiano wake mzuri pamoja naye ulimtia nguvu kuendelea kutoa unabii.” (Yer. 1:17) Rafał pia amechochewa sana na mfano wa Yeremia. Anasema: “Badala ya kujifikiria tu na kuhangaikia hisia zake mwenyewe, Yeremia alimtegemea Mungu. Aliendelea bila woga hata ingawa alichukiwa na watu wengi. Ninajitahidi kukumbuka mfano wake.”

Nabii mwingine aliyeweka mfano unaowasaidia wengi kuvumilia katika huduma ni Isaya. Mungu alimwambia kwamba wananchi wenzake hawangemsikiliza. Yehova alisema hivi: “Fanya moyo wa watu hawa kuwa mgumu, na uyafanye masikio yao kuwa magumu.” Je, Isaya angeshindwa? Mungu hakuona hivyo! Isaya alipopewa mgawo wa kuwa nabii, alisema hivi: “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isa. 6:8-10) Isaya alishikamana na mgawo wake. Je, hivyo ndivyo unavyoitikia amri ya kuhubiri?

Ili tuvumilie katika huduma kama Isaya, hata watu wasipopendezwa, tunahitaji kuepuka kukazia fikira itikio baya la watu. Rafał anaeleza jinsi anavyopambana na hali ya kuvunjika moyo: “Ninajitahidi kuepuka kufikiria sana maneno mabaya ninayoambiwa. Watu katika eneo langu wana haki ya kuitikia kwa njia yoyote wanayotaka.” Anna anaongezea hivi: “Ninajitahidi kutokazia fikira sana jambo lolote lisilofaa au lenye kuvunja moyo. Kusali na kuchunguza andiko la kila siku kabla ya kwenda katika utumishi wa shambani kunanisaidia katika jambo hilo. Maoni yoyote yasiyofaa yanaondoka haraka akilini.”

Nabii Ezekieli alitumika katikati ya Wayahudi wakaidi waliokuwa uhamishoni huko Babiloni. (Eze. 2:6) Ikiwa nabii Ezekieli angekosa kuwaambia watu maneno ya Mungu kisha mtu yeyote mwovu afe bila kupata onyo, Ezekieli angekuwa na hatia. Yehova alimwambia Ezekieli hivi: “Damu yake nitaidai kutoka katika mkono wako mwenyewe.”—Ezek. 3:17, 18.

Henryk anajitahidi kuwa na mtazamo kama wa Ezekieli: “Ninataka kuwa safi kutokana na damu ya watu wote. Uhai wenye thamani wa wanadamu uko hatarini.” (Mdo. 20:26, 27) Zbigniew anahisi vivyo hivyo: “Ezekieli alihitaji kuendelea bila kujali maoni ya wengine. Hilo linanisaidia kuiona kazi ya kuhubiri kama Muumba anavyoiona.”

Hujaachwa Peke Yako

Huachwi peke yako unaposhiriki katika kazi ya kuhubiri. Kama mtume Paulo, tunaweza kusema hivi: “Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:9) Krystyna, ambaye anakubali kwamba nyakati nyingine anavunjika moyo, anasema hivi: “Ndiyo sababu ninamsihi sikuzote Yehova anipe nguvu. Hakosi kamwe kunipa nguvu ninapomwomba.” Ndiyo, tunahitaji roho ya Mungu ili itutegemeze katika huduma yetu!—Zek. 4:6.

Tunaposhiriki katika utumishi wa shambani, roho takatifu inatusaidia pia kuonyesha sifa za “matunda ya roho.” (Gal. 5:22, 23) Na sifa hizo zinatusaidia kuvumilia katika kazi ya kuhubiri, hata tukikabili hali gani. Henryk anasema: “Kushiriki katika utumishi wa shambani kunanisaidia kuboresha utu wangu. Ninajifunza kuwa mwenye subira na mwenye kujali na kutokuwa mwepesi wa kukata tamaa.” Kuvumilia katika huduma hata unapokabili matatizo mbalimbali kunaweza kukusaidia kusitawisha matunda ya roho kwa wingi hata zaidi.

Yehova anawatumia malaika wake kuongoza kazi hii ya pekee. (Ufu. 14:6) Biblia inafunua kwamba kuna “makumi ya maelfu ya makumi ya maelfu na maelfu ya maelfu” ya viumbe hao wa roho. (Ufu. 5:11) Chini ya mwongozo wa Yesu, malaika hao wanawategemeza watumishi wa Mungu duniani. Je, unakumbuka hilo kila wakati unapokuwa katika utumishi?

Anna anasema: “Kutafakari kuhusu uhakika wa kwamba malaika wako pamoja nasi katika huduma kunanitia moyo sana. Ninathamini msaada ambao wanatupa chini ya mwongozo wa Yehova na Yesu.” Ni pendeleo kubwa kama nini kufanya kazi pamoja na malaika waaminifu!

Namna gani wahubiri wenzetu wa Ufalme? Tumebarikiwa sana kwa sababu tunashirikiana na kundi kubwa la Mashahidi waaminifu. Bila shaka umejionea ukweli wa methali hii ya Biblia: “Chuma hunolewa kwa chuma. Ndivyo mtu anavyounoa uso wa mwingine.”—Met. 27:17.

Kushiriki pamoja na wengine katika huduma kunatupa nafasi nzuri sana ya kujifunza mbinu za kuhubiri ambazo huenda ni mpya kwetu. Elżbieta anasema hivi: “Kuhubiri pamoja na wahubiri mbalimbali kunanipa nafasi za kuwaonyesha upendo waamini wenzangu na pia watu tunaowahubiria.” Jitahidi kuhubiri pamoja na wahubiri mbalimbali. Ukifanya hivyo, huduma yako itapendeza sana.

Jitunze Vizuri

Ili tuendelee kuwa na shauku katika huduma, ni lazima tufanye mipango mizuri, tuwe na mazoea mazuri ya kujifunza kibinafsi, na tupumzike vya kutosha. Yaani, ni lazima tujitunze kiroho na kimwili.

Biblia inasema hivi: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida.” (Met. 21:5) Zygmunt, ambaye sasa ana umri wa miaka 88, anasema hivi: “Kuwa na ratiba nzuri ya utumishi kunanisaidia kutimiza miradi fulani. Ninapanga wakati wangu kwa uangalifu ili niwe na wakati wa kutosha wa kuhubiri.”

Tunapoyajua Maandiko kwa undani tunakuwa na nguvu na uwezo wa kushiriki katika huduma yetu. Kama vile tunavyohitaji kula chakula cha kimwili ili tuendelee kuwa hai, ni lazima tule chakula cha kiroho kwa ukawaida ili tuendelee kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Kujilisha Neno la Mungu kila siku na kula ‘chakula cha wakati unaofaa’ kunaweza kututia nguvu za kushiriki katika huduma.—Mt. 24:45-47.

Elżbieta alibadili kabisa mtindo wake wa maisha ili aboreshe huduma yake. Anasema hivi: “Nimepunguza sana wakati ninaotumia kutazama televisheni ili niwe na wakati zaidi wa kujitayarisha kwa ajili ya huduma. Ninaposoma Biblia kila jioni, ninawafikiria watu niliokutana nao katika eneo. Ninatafuta maandiko na habari ambazo zinaweza kuwasaidia.”

Kupumzika vya kutosha kutakusaidia uwe na nguvu zaidi na kutakuwezesha kushiriki kikamili katika huduma. Lakini tafrija inayopita kiasi inaweza kuwa na matokeo mabaya kwa kazi yako. Andrzej, ambaye ni mhubiri mwenye bidii anasema: “Kutopumzika kunamfanya mtu achoke sana, na mtu kama huyo anakabili hatari ya kushuka moyo. Ninafanya yote ninayoweza kuepuka hali hiyo.”—Mhu. 4:6.

Ingawa tunahubiri kwa bidii, ni watu wachache tu wanaokubali habari njema. Hata hivyo, Yehova hatasahau kamwe kazi yetu. (Ebr. 6:10) Hata ikiwa wengi hawataki kuzungumza nasi, huenda wakazungumza kuhusu ziara yetu baada ya sisi kuondoka. Matokeo yanaweza kuwa kama yale tunayosoma kumhusu Ezekieli: Watu kwa “hakika watajua pia kwamba nabii alikuwako katikati yao.” (Eze. 2:5) Bila shaka, huduma yetu si rahisi, lakini tunapata faida nyingi kutokana nayo na watu wanaotusikiliza watapata faida pia.

Zygmunt anasema: “Kushiriki katika huduma kunatusaidia kuvaa utu mpya na kuonyesha kwamba tunampenda Mungu na majirani wetu.” Andrzej anaongezea hivi: “Ni pendeleo kushiriki katika kazi hii inayookoa uhai. Haitarudiwa kamwe kwa kadiri na chini ya hali kama za leo.” Wewe pia unaweza kupata baraka nyingi sana kwa kuvumilia katika huduma leo.—2 Kor. 4:1, 2.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kujitunza kiroho na kimwili kunatusaidia kuvumilia katika huduma