Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unasali Kupatana na Maneno ya Yesu?

Je, Unasali Kupatana na Maneno ya Yesu?

Je, Unasali Kupatana na Maneno ya Yesu?

“Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, umati ukashangazwa na njia yake ya kufundisha.”—MT. 7:28.

1, 2. Kwa nini umati ulishangazwa na njia ya Yesu ya kufundisha?

TUNAPASWA kukubali maneno ya Yesu Kristo, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, na kuyatumia katika maisha yetu. Bila shaka, hakuna mtu mwingine yeyote aliyesema kama yeye. Si ajabu kwamba watu walishangazwa na njia yake ya kufundisha katika yale Mahubiri ya Mlimani!—Soma Mathayo 7:28, 29.

2 Mwana wa Yehova hakufundisha kama waandishi, ambao walitoa hotuba ndefu-ndefu zilizotegemea mafundisho ya wanadamu wasio wakamilifu. Kristo alifundisha “kama mtu mwenye mamlaka” kwa sababu mambo aliyosema yalitoka kwa Mungu. (Yoh. 12:50) Kwa hiyo, acheni tuone jinsi tunavyoweza na tunavyopaswa kusali kupatana na maneno ya Yesu katika yale Mahubiri ya Mlimani.

Usisali Kamwe Kama Wanafiki Wanavyosali

3. Eleza kwa ufupi maneno ya Yesu katika Mathayo 6:5.

3 Sala ni sehemu ya maana sana ya ibada ya kweli, na tunapaswa kusali kwa Yehova kwa ukawaida. Lakini tunapaswa kusali kupatana na maneno ambayo Yesu alisema katika Mahubiri ya Mlimani. Alisema hivi: “Wakati mnaposali, msiwe kama wanafiki; kwa sababu wanapenda kusali wakiwa wamesimama katika masinagogi na kwenye pembe za njia pana ili waonekane na watu. Kwa kweli ninawaambia ninyi, Wanapata thawabu yao kwa ukamili.”Mt. 6:5.

4-6. (a) Kwa nini Mafarisayo walipenda kusali “wakiwa wamesimama katika masinagogi na kwenye pembe za njia pana”? (b) Wanafiki hao walipata jinsi gani “thawabu yao kwa ukamili”?

4 Wakati wa kusali, wanafunzi wa Yesu hawakupaswa kuiga “wanafiki” kama Mafarisayo waliojiona kuwa waadilifu, na ambao walijaribu kuwadanganya watu kwa kujifanya watakatifu. (Mt. 23:13-32) Wanafiki hao walipenda kusali “wakiwa wamesimama katika masinagogi na kwenye pembe za njia pana.” Kwa nini? Ili “waonekane na watu.” Wayahudi wa karne ya kwanza walikuwa na desturi ya kusali pamoja wakiwa kutaniko wakati wa matoleo ya kuteketezwa katika hekalu (karibu saa tatu asubuhi na saa tisa alasiri). Wakaaji wengi wa Yerusalemu walisali pamoja na umati wa waabudu katika eneo la hekalu. Kwa kawaida, Wayahudi waliomwogopa Mungu walisali mara mbili kwa siku nje ya jiji wakiwa “wamesimama katika masinagogi.”—Linganisha na Luka 18:11, 13.

5 Kwa kuwa watu wengi hawakuwa karibu na hekalu au sinagogi wakati wa sala hizo zilizotajwa, wangeweza kusali mahali popote walipokuwa saa hizo. Wengine walihakikisha kwamba wakati wa sala walikuwa “kwenye pembe za njia pana.” Walitaka “waonekane na watu” ambao walikuwa wakipita kwenye makutano ya barabara. Wanafiki hao waliojifanya watakatifu walikuwa ‘wakitoa sala ndefu kwa kisingizio’ ili wawavutie watazamaji. (Luka 20:47) Hatupaswi kuwa na mtazamo kama huo.

6 Yesu alitangaza kwamba wanafiki hao walikuwa ‘wakipata thawabu yao kwa ukamili.’ Walitamani sana kutambuliwa na kusifiwa na wanadamu wenzao, na hiyo ndiyo thawabu pekee waliyopata. Ingekuwa thawabu kamili, kwa kuwa Yehova hangejibu sala zao za kinafiki. Hata hivyo, Mungu angejibu sala za wafuasi wa kweli wa Kristo, kama maneno yafuatayo ya Yesu yanavyoonyesha.

7. Shauri kuhusu kusali katika ‘chumba chetu cha faragha’ linamaanisha nini?

7 “Lakini wewe unaposali, ingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako aliye mahali pa siri; ndipo Baba yako anayetazama akiwa mahali pa siri atakulipa.” (Mt. 6:6) Yesu alipotoa shauri kuhusu kusali katika chumba cha faragha baada ya kufunga mlango, hakumaanisha kwamba mtu hawezi kuliwakilisha kutaniko katika sala. Alikuwa akiwashutumu wale waliosali mbele ya watu ili watambuliwe na kusifiwa na wengine. Tunapaswa kukumbuka jambo hilo tunapopata pendeleo la kuwakilisha watu wa Mungu katika sala ya watu wote. Acheni tufuate pia shauri lifuatalo la Yesu kuhusu sala.

8. Kulingana na Mathayo 6:7, tunapaswa kuepuka njia gani isiyofaa ya kusali?

8 “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa wanavyofanya, kwa maana wao huwaza watasikiwa kwa kutumia maneno mengi.” (Mt. 6:7) Hivyo, Yesu alitaja njia nyingine isiyofaa ya kusali—kurudia-rudia. Hakumaanisha kwamba hatupaswi kamwe kurudia sihi za kutoka moyoni na maneno ya shukrani tunaposali. Katika bustani ya Gethsemane usiku uliotangulia kifo chake, Yesu alirudia-rudia ‘neno lilelile’ katika sala.—Marko 14:32-39.

9, 10. Ni katika maana gani hatupaswi kurudia-rudia sala?

9 Ni kosa kwetu kuiga sala za kurudiwa-rudiwa za “watu wa mataifa.” Wanarudia “tena na tena” mambo waliyoweka akilini na maneno mengi yasiyo na maana. Waabudu wa Baali hawakupata faida yoyote kwa kuliitia jina la mungu huyo wa uwongo “kutoka asubuhi mpaka katikati ya mchana, wakisema: ‘Ee Baali, tupe jibu!’” (1 Fal. 18:26) Mamilioni ya watu leo wanatoa sala zenye maneno mengi yanayorudiwa-rudiwa, huku wakifikiri kimakosa kwamba “watasikiwa.” Lakini Yesu anatusaidia kuelewa kwamba “kutumia maneno mengi” katika sala ndefu za kurudia-rudia hakuna maana yoyote mbele za Yehova. Yesu alisema pia hivi:

10 “Kwa hiyo, msijifanye kama wao, kwa maana Mungu Baba yenu anajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla hamjamwomba.” (Mt. 6:8) Viongozi wengi wa dini ya Kiyahudi walijifanya kama Watu wa Mataifa kwa kutoa sala zenye maneno mengi sana. Sala inayotoka moyoni ambayo inatia ndani maneno ya sifa, shukrani, na maombi ni sehemu ya maana ya ibada ya kweli. (Flp. 4:6) Hata hivyo, ni kosa kwetu kusema maneno yaleyale tena na tena tukifikiri kwamba ni lazima turudie-rudie ili Mungu ajue mahitaji yetu. Tunaposali, tunapaswa kukumbuka kwamba tunawasiliana na Mungu ‘ambaye anajua ni vitu gani tunavyohitaji hata kabla hatujamwomba.’

11. Tunapaswa kukumbuka nini ikiwa tuna pendeleo la kusali mbele ya watu?

11 Maneno ya Yesu kuhusu sala zisizokubalika yanapaswa kutukumbusha kwamba Mungu havutiwi na maneno yenye madoido na yanayopita kiasi. Tunapaswa kukumbuka pia kwamba kusali mbele ya watu si nafasi ya kujaribu kuwavutia wasikilizaji au kuwafanya wajiulize sala itamalizika wakati gani ili waseme “Amina.” Kutoa matangazo au kuwashauri wasikilizaji kupitia sala hakupatani hata kidogo na maneno ya Yesu katika Mahubiri ya Mlimani.

Yesu Anatufundisha Jinsi ya Kusali

12. Eleza maana ya ombi hili, “jina lako na litakaswe.”

12 Ingawa Yesu aliwaonya wanafunzi wake wasitumie isivyofaa pendeleo la pekee sana la kusali, aliwafundisha jinsi ya kusali. (Soma Mathayo 6:9-13.) Ile sala ya kielelezo haipaswi kurudiwa-rudiwa kutoka akilini. Badala yake, inatuwekea kielelezo cha jinsi ya kusali. Kwa mfano, Yesu alimtanguliza Mungu katika maneno haya ya kwanza: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mt. 6:9) Ni vizuri kumuita Yehova “Baba yetu” kwa sababu ni Muumba wetu, ambaye anakaa “mbinguni,” juu zaidi ya dunia. (Kum. 32:6; 2 Nya. 6:21; Mdo. 17:24, 28) Neno “yetu” linapaswa kutukumbusha kwamba waamini wenzetu pia wana uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Maneno “jina lako na litakaswe” ni ombi kwa Yehova ili achukue hatua ya kujitakasa kwa kuondoa lawama yote ambayo imeletwa juu ya jina hilo tangu uasi katika Edeni. Yehova atajibu sala hiyo kwa kuondoa uovu duniani, na kujitakasa mwenyewe.—Eze. 36:23.

13. (a) Ombi, “ufalme wako na uje” litatimizwa jinsi gani? (b) Kutendeka kwa mapenzi ya Mungu duniani kutatia ndani nini?

13 “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mt. 6:10) Ombi hilo ambalo Yesu alitaja katika sala ya kielelezo linapaswa kutukumbusha kwamba “ufalme” ni serikali ya mbinguni ya Kimasihi ambayo iko mikononi mwa Kristo na “watakatifu” wanaofufuliwa ili washirikiane naye. (Dan. 7:13, 14, 18; Isa. 9:6, 7) Tunaposali Ufalme wa Mungu “uje” tunaomba uje kuwaangamiza wote wanaopinga utawala wa Mungu duniani. Hilo litatukia hivi karibuni, kisha dunia itakuwa paradiso yenye uadilifu, amani, na ufanisi. (Zab. 72:1-15; Dan. 2:44; 2 Pet. 3:13) Mapenzi ya Yehova yanatendeka mbinguni, na tunaposali yatendeke duniani tunaomba ili Mungu atimize makusudi yake kuhusu dunia yetu, na kuangamiza wale wanaompinga leo kama alivyowaangamiza wale waliompinga zamani.—Soma Zaburi 83:1, 2, 13-18.

14. Kwa nini inafaa kuomba “mkate wetu kwa ajili ya siku hii”?

14 “Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii.” (Mt. 6:11; Luka 11:3) Tunaposali hivyo, tunamwomba Mungu atupe chakula tunachohitaji “kwa ajili ya siku hii.” Hilo linaonyesha tuna imani kwamba Yehova ana uwezo wa kutimiza mahitaji yetu siku kwa siku. Hatusali ili atupe mahitaji ya ziada. Huenda ombi hilo kuhusu mahitaji yetu ya kila siku likatukumbusha kwamba Mungu aliwaamuru Waisraeli wakusanye mana “kila mtu kiasi chake siku baada ya siku.”—Kut. 16:4.

15. Eleza maana ya ombi hili: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.”

15 Ombi linalofuata katika sala ya kielelezo linatukumbusha jambo ambalo tunahitaji kufanya. Yesu alisema: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.” (Mt. 6:12) Injili ya Luka inaonyesha kwamba “madeni” hayo ni “dhambi.” (Luka 11:4) Tunaweza kumtarajia Yehova atusamehe ikiwa tu tayari “tumewasamehe” wale wanaotukosea. (Soma Mathayo 6:14, 15.) Tunapaswa kuwasamehe wengine kutoka moyoni.—Efe. 4:32; Kol. 3:13.

16. Tuelewe jinsi gani maombi mawili kuhusu majaribu na kukombolewa kutokana na yule mwovu?

16 “Usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.” (Mt. 6:13) Tuelewe jinsi gani maombi hayo mawili yanayohusiana katika sala ya Yesu ya kielelezo? Tunajua kwa hakika jambo hili: Yehova hatujaribu ili tutende dhambi. (Soma Yakobo 1:13.) Kwa kweli, Shetani, “yule mwovu,” ndiye “Mjaribu.” (Mt. 4:3) Hata hivyo, Mungu anaporuhusu mambo fulani yatukie, Biblia husema kwamba anayafanya. (Rut. 1:20, 21; Mhu. 11:5) Kwa hiyo, tunaposali “usituingize katika jaribu” tunaomba ili Yehova asituruhusu tuanguke tunapopata jaribu la kutomtii. Mwishowe, tunaposali “utukomboe kutokana na yule mwovu” tunaomba ili Yehova asimruhusu Shetani atushinde. Na tunaweza kuwa na hakika kwamba ‘Mungu hataacha tujaribiwe kupita tunavyoweza kuhimili.’—Soma 1 Wakorintho 10:13.

‘Endeleeni Kuomba, Kutafuta, Kupiga Hodi’

17, 18. Ni nini maana ya ‘kuendelea kuomba, kutafuta, na kupiga hodi’?

17 Mtume Paulo aliwahimiza hivi waamini wenzake: “Dumuni katika sala.” (Rom. 12:12) Yesu alitoa amri kama hiyo aliposema hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa. Kwa maana kila mtu anayeomba hupokea, na kila mtu anayetafuta hupata, na kila mtu anayepiga hodi atafunguliwa.” (Mt. 7:7, 8) Ni vizuri ‘kuendelea kuomba’ jambo lolote ambalo linapatana na mapenzi ya Mungu. Mtume Yohana aliandika hivi kupatana na maneno hayo ya Yesu: “Huu ndio uhakika ambao tunao [kumhusu Mungu], kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”—1 Yoh. 5:14.

18 Shauri la Yesu la ‘kuendelea kuomba na kutafuta’ linamaanisha kwamba tunapaswa kusali kwa bidii bila kukata tamaa. Ni jambo la maana kwetu pia ‘kuendelea kupiga hodi’ ili tuingie katika Ufalme na kufurahia baraka, faida, na thawabu za Ufalme. Lakini je, tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atajibu sala zetu? Ndiyo, tunaweza ikiwa sisi ni waaminifu kwa Yehova, kwa kuwa Kristo alisema hivi: “Kila mtu anayeomba hupokea, na kila mtu anayetafuta hupata, na kila mtu anayepiga hodi atafunguliwa.” Mambo mengi ambayo watumishi wa Yehova wamejionea yanathibitisha kwamba kwa kweli Mungu ni “Msikiaji wa sala.”—Zab. 65:2.

19, 20. Kulingana na maneno ya Yesu katika Mathayo 7:9-11, Yehova ni kama baba mwenye upendo namna gani?

19 Yesu alimfananisha Mungu na baba mwenye upendo ambaye anampa mwana wake vitu vyema. Hebu jiwazie ukisikiliza Mahubiri ya Mlimani na kumsikia Yesu akisema hivi: “Ni nani kati yenu ambaye mwana wake akimwomba mkateje, atampa jiwe? Au, labda, akiomba samakije, atampa nyoka? Kwa hiyo, ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo nzuri, je, Baba yenu aliye mbinguni hatawapa hata zaidi vitu vyema wale wanaomwomba?”Mt. 7:9-11.

20 Ingawa baba wa kibinadamu akilinganishwa na Yehova ni ‘mwovu’ kwa sababu ya dhambi ambayo amerithi, anampenda kiasili mwana wake. Hawezi kumdanganya mwana wake, badala yake anajitahidi kumpa “zawadi zilizo njema.” Akiwa na mtazamo huo wa baba kutuelekea, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anatupa “vitu vyema,” kama vile roho yake takatifu. (Luka 11:13) Inaweza kututia nguvu ili tutoe utumishi unaokubalika kwa Yehova, Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.”—Yak. 1:17.

Endelea Kufaidika na Maneno ya Yesu

21, 22. Kwa nini Mahubiri ya Mlimani ni ya pekee, na unahisi namna gani kuhusu maneno hayo ya Yesu?

21 Kwa kweli, Mahubiri ya Mlimani ni hotuba bora zaidi iliyowahi kutolewa duniani. Ni ya pekee kwa sababu ya mafundisho yake ya wazi kumhusu Mungu. Kama mambo tuliyojifunza katika mfululizo huu wa makala yanavyoonyesha, tunaweza kufaidika sana tukitumia mashauri yaliyo katika mahubiri hayo. Maneno ya Yesu yanaweza kuboresha maisha yetu sasa na kutuwezesha kuwa na tumaini la wakati ujao wenye furaha.

22 Katika makala hizi, tumechunguza hazina chache tu za kiroho katika Mahubiri ya Yesu ya Mlimani. Si ajabu kwamba wale waliosikiliza hotuba yake ‘walishangazwa na njia yake ya kufundisha.’ (Mt. 7:28) Bila shaka, hata sisi tutaitikia vivyo hivyo tukijaza katika akili na mioyo yetu maneno hayo na mengine yenye thamani ya yule Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo.

Ungesema Nini?

• Yesu alisema nini kuhusu sala za kinafiki?

• Kwa nini tunapaswa kuepuka kurudia maneno yaleyale tunaposali?

• Sala ya Yesu ya kielelezo ina maombi gani?

• Tunaweza jinsi gani ‘kuendelea kuomba, kutafuta, na kupiga hodi’?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yesu aliwashutumu wanafiki ambao walisali ili waonekane tu na kusikiwa

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je, unajua kwa nini tunapaswa kusali kwa ajili ya mkate wetu wa siku hii?