Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pata Shangwe Katika Kazi ya Kufanya Wanafunzi

Pata Shangwe Katika Kazi ya Kufanya Wanafunzi

Pata Shangwe Katika Kazi ya Kufanya Wanafunzi

“Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.”—MT. 28:19.

1-3. (a) Wengi wanahisi jinsi gani kuhusu kuongoza mafunzo ya Biblia? (b) Tutachunguza maswali gani?

“NIMEKUWA nikijifunza na familia moja kutoka Pakistan kwa majuma 11 yaliyopita,” aliandika dada mmoja aliye katika kikundi cha lugha ya Kihindi huko Marekani. Anaendelea kusema: “Tumekuwa marafiki. Ninabubujikwa na machozi ninapofikiria kwamba familia hiyo itarudi huko Pakistan hivi karibuni. Ninalia kwa sababu ya huzuni ninayohisi kwa kupoteza ushirika wao, na hasa kwa sababu ya shangwe ambayo nimepata kwa kuwafundisha kumhusu Yehova.”

2 Kama dada huyo, je, umewahi kupata shangwe inayotokana na kujifunza Biblia na mtu fulani? Yesu na wanafunzi wake wa karne ya kwanza walipata shangwe kubwa katika kazi ya kufanya wanafunzi. Wanafunzi 70 ambao Yesu alikuwa amezoeza waliporudi wakiwa na shangwe, Yesu mwenyewe alipata “shangwe sana katika roho takatifu.” (Luka 10:17-21) Vivyo hivyo, wengi leo wanapata shangwe nyingi katika kazi ya kufanya wanafunzi. Kwa kweli, katika mwaka wa 2007, wahubiri wenye bidii na wenye furaha, waliongoza kwa wastani mafunzo ya Biblia milioni sita na nusu kila mwezi!

3 Hata hivyo, wahubiri fulani hawajawahi kupata shangwe ya kuongoza funzo la Biblia. Huenda wengine hawajaongoza funzo katika miaka ya hivi karibuni. Ni matatizo gani tunayoweza kukabili tunapojitahidi kuongoza funzo la Biblia? Tunaweza kuyashinda jinsi gani? Na ni thawabu gani tunazopata tunapofanya yote tunayoweza ili kutii amri hii ya Yesu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi”?—Mt. 28:19.

Matatizo Yanayoweza Kutupotezea Shangwe

4, 5. (a) Watu wengi wanaitikia jinsi gani katika sehemu fulani za ulimwengu? (b) Ni matatizo gani ambayo wahubiri wanakabili mahali pengine?

4 Katika sehemu fulani za ulimwengu, watu wanakubali kwa hamu vichapo vyetu na wanataka sana kujifunza Biblia pamoja nasi. Wenzi wawili wa ndoa kutoka Australia ambao walikuwa wakitumika kwa muda huko Zambia waliandika hivi: “Habari hizi ni za kweli. Zambia ni eneo lenye matokeo sana. Mahubiri ya barabarani ni mazuri ajabu! Watu wanatujia, na hata wengine wanaomba makala hususa za magazeti fulani.” Katika mwaka wa hivi karibuni, ndugu na dada wa Zambia waliongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya 200,000, yaani, kwa wastani, zaidi ya funzo moja la Biblia kwa kila mhubiri.

5 Hata hivyo, mahali pengine, inaweza kuwa vigumu kwa wahubiri kuwapa watu vichapo na kuongoza mafunzo ya Biblia kwa ukawaida. Kwa nini? Mara nyingi, watu hawapatikani nyumbani, au wale wanaopatikana nyumbani huenda hawapendezwi na mambo ya dini. Pengine wamelelewa katika familia ambazo hazipendezwi na mambo ya dini au huenda wanachukizwa na unafiki wa dini. Watu wengi wameumizwa kiroho, wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku na wachungaji wa uwongo. (Mt. 9:36) Inaeleweka kwa nini huenda watu hao wakasita kuzungumzia Biblia.

6. Huenda wahubiri fulani wakawa na matatizo gani?

6 Wahubiri fulani waaminifu wanakabili tatizo tofauti ambalo linaweza kuwafanya wapoteze shangwe. Ingawa zamani walikuwa wenye bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi, sasa hawawezi kutimiza mengi kwa sababu ya ugonjwa au uzee. Pia, fikiria tatizo fulani ambalo huenda tukajiletea wenyewe. Kwa mfano, je, unahisi kwamba huna uwezo wa kuongoza funzo la Biblia? Huenda ukahisi kama alivyohisi Musa wakati Yehova alipomtuma azungumze na Farao. Musa alisema: “Nakuomba radhi, Yehova, lakini mimi si msemaji mzuri, tangu jana wala tangu kabla ya hapo.” (Kut. 4:10) Kwa kawaida, mtu anapoogopa kwamba atashindwa, anahisi hafai. Huenda tukawa na wasiwasi kwamba mtu fulani hatakuwa mwanafunzi eti kwa sababu sisi si walimu bora. Hivyo, ili kuepuka jambo hilo, huenda tukaamua kutoongoza funzo. Tunaweza kushinda jinsi gani matatizo yanayotajwa hapo juu?

Tayarisha Moyo Wako

7. Ni nini kilichomchochea Yesu katika huduma yake?

7 Hatua ya kwanza ni kutayarisha moyo wako. Yesu alisema: ‘Kutokana na wingi wa moyo kinywa husema.’ (Luka 6:45) Kuhangaikia kwa unyoofu hali ya wengine kulimchochea Yesu katika huduma yake. Kwa mfano, alipoona hali mbaya ya kiroho ya Wayahudi wenzake, ‘aliwasikitikia.’ Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mavuno ni mengi . . . Mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.”—Mt. 9:36-38.

8. (a) Tunapaswa kufikiria nini? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na maelezo ya mwanafunzi mmoja wa Biblia?

8 Tunaposhiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi, tunapaswa kufikiria kwa uzito jinsi ambavyo tumefaidika kwa sababu mtu fulani alikubali kujifunza Biblia pamoja nasi. Pia, fikiria watu tutakaokutana nao katika huduma na jinsi watakavyofaidika wanaposikiliza ujumbe wetu. Mwanamke mmoja aliandikia ofisi ya tawi ya nchi anakoishi: “Ningependa kuwaambia kwamba ninawathamini sana Mashahidi ambao wananifundisha nyumbani kwangu. Ninajua kwamba nyakati nyingine huenda ninawasumbua kwa sababu nina maswali mengi sana na sikuzote wanalazimika kubaki kwa muda mrefu zaidi. Lakini wana subira na wana hamu ya kunifundisha mambo ambayo wamejifunza. Ninamshukuru Yehova na Yesu kwamba nimewajua watu hao.”

9. Yesu alikazia fikira nini, na tunaweza kumwiga jinsi gani?

9 Bila shaka, si kila mtu aliyeyakubali mafundisho ya Yesu. (Mt. 23:37) Wengine walimfuata kwa muda mfupi tu lakini baadaye wakapinga mafundisho yake na hivyo wakawa “hawatembei tena pamoja naye.” (Yoh. 6:66) Hata hivyo, Yesu hakuruhusu kutopendezwa kwa watu fulani kumfanye ahisi kwamba ujumbe wake hauna thamani. Ingawa mbegu nyingi alizopanda hazikuzaa matunda, Yesu alikazia fikira mambo mazuri aliyokuwa akifanya. Aliona kwamba mashamba yalikuwa meupe kwa ajili ya mavuno na alipata shangwe nyingi kwa kusaidia katika kazi hiyo ya mavuno. (Soma Yohana 4:35, 36.) Badala ya kuona tu udongo ambao hauzai, je, tunaweza kukazia fikira mavuno mazuri tunayoweza kupata katika eneo tulilogawiwa? Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kudumisha mtazamo huo mzuri.

Panda Mbegu Ukitazamia Kuvuna

10, 11. Unaweza kufanya nini ili kudumisha shangwe yako?

10 Mkulima anapanda mbegu huku akitazamia kuvuna. Vivyo hivyo, tunapaswa kuhubiri tukiwa na kusudi la kuanzisha mafunzo ya Biblia. Hata hivyo, namna gani ikiwa unahubiri kwa ukawaida lakini unapata watu wachache sana nyumbani kwao au inaonekana huwapati watu ambao uliahidi kuwarudia? Hilo linaweza kuvunja moyo. Je, uache kuhubiri nyumba kwa nyumba? Hapana! Bado watu wengi wanahubiriwa kwa mara ya kwanza kupitia mahubiri ya nyumba kwa nyumba, ambayo yamekuwa na matokeo kwa miaka mingi.

11 Hata hivyo, ili kudumisha shangwe yako, je, unaweza kupanua njia zako za kuhubiri, labda kwa kutumia njia nyingine za kuwafikia watu? Kwa mfano, je, umewahi kuwahubiria watu barabarani au mahali pao pa kazi? Je, unaweza kuwasiliana na watu kwenye simu au kupata namba za wale ambao tayari umezungumza nao kuhusu ujumbe wa Ufalme ili uendeleze mazungumzo nao? Kwa kuonyesha uvumilivu na kubadilika kulingana na hali katika huduma yako, utakuwa na shangwe ya kuwapata watu ambao watakubali ujumbe wa Ufalme.

Kuvumilia Hali ya Kutopendezwa

12. Tunaweza kufanya nini ikiwa watu wengi katika eneo letu wanaonekana hawapendezwi?

12 Namna gani ikiwa watu wengi katika eneo lenu hawapendezwi na mambo ya dini? Je, unaweza kuanza mazungumzo yako kwa kutaja jambo ambalo litawavutia? Mtume Paulo aliwaandikia hivi waamini wenzake huko Korintho: “Kwa Wayahudi nilikuwa kama Myahudi . . . Kwa wale wasio na sheria nilikuwa kama asiye na sheria, ijapokuwa mimi siko bila sheria kwa Mungu.” Paulo alikuwa na kusudi gani? Alisema hivi: “Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili kwa vyovyote niwaokoe wengine.” (1 Kor. 9:20-22) Je, wewe pia unaweza kupata habari zitakazowapendeza watu wa eneo lenu? Watu wengi ambao hawafuati dini wanataka sana kuboresha hali ya familia zao. Huenda pia wanataka maisha yao yawe yenye kusudi. Je, tunaweza kuwaeleza ujumbe wa Ufalme kwa njia ambayo itawavutia?

13, 14. Tunaweza kufanya nini ili kupata shangwe nyingi zaidi katika kazi ya kufanya wanafunzi?

13 Wahubiri wengi wameongeza shangwe ambayo wanapata katika kazi ya kufanya wanafunzi, hata katika maeneo ambako watu wengi wanaonekana hawapendezwi. Jinsi gani? Kwa kujifunza lugha ya kigeni. Wenzi wawili wa ndoa wenye umri wa zaidi ya miaka 60 walitambua kwamba maelfu ya wanafunzi Wachina na familia zao walikuwa wakiishi katika eneo la kutaniko lao. Mume anasema hivi: “Hilo lilituchochea kujifunza Kichina. Ingawa hilo lilimaanisha kutumia wakati kila siku kujifunza lugha hiyo, tulianza kuongoza mafunzo mengi ya Biblia na Wachina walioishi katika eneo letu.”

14 Hata ikiwa huwezi kujifunza lugha ya kigeni, unaweza kutumia vizuri kijitabu Good News for People of All Nations (Une bonne nouvelle pour des gens de toutes nations) unapokutana na wale wanaozungumza lugha nyingine. Pia, kwa kawaida unaweza kupata vichapo katika lugha ya watu ambao unakutana nao. Hivyo, unahitaji wakati na jitihada nyingi ili kuzungumza na watu wa lugha na utamaduni mwingine. Lakini kumbuka kanuni hii katika Neno la Mungu: “Yeye anayepanda kwa wingi atavuna pia kwa wingi.”—2 Kor. 9:6.

Kutaniko Lote Linahusika

15, 16. (a) Kwa nini kutaniko lote linahusika katika kazi ya kufanya wanafunzi? (b) Waliozeeka wanatimiza sehemu gani?

15 Hata hivyo, kazi ya kufanya wanafunzi haitegemei jitihada za mtu mmoja tu. Badala yake, ni jitihada za kutaniko lote. Kwa nini? Yesu alisema hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:35) Na kwa kweli, wanafunzi wa Biblia wanapohudhuria mikutano, mara nyingi wanavutiwa na upendo unaoonyeshwa katika mikutano na makusanyiko yetu. Mwanafunzi mmoja wa Biblia aliandika: “Ninafurahia sana kuhudhuria mikutano. Watu wanakukaribisha kwa uchangamfu!” Yesu alisema kwamba wale wanaokuwa wafuasi wake huenda wakapingwa na familia zao. (Soma Mathayo 10:35-37.) Hata hivyo, aliahidi kwamba katika kutaniko, wangepata “ndugu na dada na mama na watoto” wengi wa kiroho.—Marko 10:30.

16 Ndugu na dada zetu waliozeeka hasa wanatimiza sehemu ya maana sana katika kuwasaidia wanafunzi wa Biblia wafanye maendeleo. Jinsi gani? Hata ikiwa wengine kati ya waliozeeka hawawezi kuongoza funzo la Biblia, maelezo yao yenye kujenga kwenye mikutano ya kutaniko yanatia nguvu imani ya wote ambao wanayasikia. Kutembea kwao kwa miaka mingi “katika njia ya uadilifu” kunaongeza uzuri wa kutaniko na kunawavutia watu wanyoofu kwenye tengenezo la Mungu.—Met. 16:31.

Kushinda Woga

17. Tunaweza kufanya nini ikiwa tunahisi kwamba hatuna uwezo wa kuongoza funzo la Biblia?

17 Unaweza kufanya nini ikiwa unahisi kwamba huna uwezo wa kuongoza funzo la Biblia? Kumbuka kwamba Yehova alimsaidia Musa kwa kumpa roho takatifu na mtu wa kumsaidia, ndugu yake, Haruni. (Kut. 4:10-17) Yesu aliahidi kwamba roho ya Mungu ingetusaidia katika kazi yetu ya kuhubiri. (Mdo. 1:8) Zaidi ya hayo, Yesu aliwatuma wanafunzi kuhubiri wakiwa wawili-wawili. (Luka 10:1) Hivyo, ikiwa unaona ni vigumu kuongoza funzo la Biblia, sali ili roho ya Mungu ikupe hekima, kisha uhubiri pamoja na mtu mwingine ambaye anaweza kukusaidia uwe na uhakika na ambaye uzoefu wake unaweza kukusaidia. Imani yetu inatiwa nguvu tunapokumbuka kwamba Yehova aliamua kutumia watu wa kawaida, yaani, “vitu dhaifu vya ulimwengu” ili kutimiza kazi hii ya pekee sana.—1 Kor. 1:26-29.

18. Tunaweza kufanya nini ikiwa tunahisi kwamba hatuwezi kumsaidia mwanafunzi wa Biblia?

18 Tunaweza kufanya nini ikiwa tunahisi kwamba hatuna uwezo wa kumsaidia mwanafunzi wa Biblia? Tunapaswa kukumbuka kwamba kumfanya mtu kuwa mwanafunzi si kama kazi ya kupika chakula ambayo inaweza kufaulu au kutofaulu ikitegemea hasa mtu mmoja, yaani, mpishi. Badala yake, kumfanya mtu kuwa mwanafunzi kunategemea ushirikiano wa angalau watu watatu. Yehova ndiye anayetimiza sehemu ya maana zaidi, ni yeye anayewavuta watu. (Yoh. 6:44) Sisi na wengine katika kutaniko tunafanya yote tunayoweza kutumia ufundi wa kufundisha ili kumsaidia mwanafunzi afanye maendeleo. (Soma 2 Timotheo 2:15.) Na mwanafunzi anahitaji kutenda kulingana na mambo anayojifunza. (Mt. 7:24-27) Mtu akiacha kujifunza Biblia, huenda tukavunjika moyo. Tunatumaini kwamba wanafunzi wa Biblia watafanya uamuzi mzuri, lakini kila mtu atalazimika ‘kutoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.’—Rom. 14:12.

Tutapata Thawabu Gani?

19-21. (a) Tunapata faida gani kwa kuongoza mafunzo ya Biblia? (b) Yehova anawaona jinsi gani wote wanaoshiriki katika kazi ya kuhubiri?

19 Kuongoza mafunzo ya Biblia kunatusaidia kuendelea kutafuta kwanza Ufalme. Pia, kunakazia kweli za Neno la Mungu ndani ya akili na mioyo yetu. Kwa nini? Painia mmoja anayeitwa Barak anaeleza: “Ili uongoze mafunzo ya Biblia unahitaji kuwa mwanafunzi mzuri zaidi wa Neno la Mungu. Nimetambua kwamba ili nimfundishe vizuri mtu mwingine ninapaswa kwanza kuitia nguvu imani yangu.”

20 Ikiwa huongozi funzo la Biblia, je, hilo linamaanisha kwamba Mungu haoni utumishi wako kuwa wenye thamani? Hapana! Yehova anathamini sana jitihada zetu za kumsifu. Wote ambao wanashiriki katika kazi ya kuhubiri ni “wafanyakazi wenzi wa Mungu.” Hata hivyo, kuongoza funzo la Biblia kunatuletea shangwe zaidi tunapoona jinsi Mungu anavyoikuza mbegu tuliyopanda. (1 Kor. 3:6, 9) Painia mmoja anayeitwa Amy anasema hivi: “Unapomwona mwanafunzi wa Biblia akiendelea kufanya maendeleo, unamshukuru sana Yehova kwa kukutumia kumpa mtu huyo zawadi nzuri ajabu, yaani, nafasi ya kumjua Yehova na ya kupata uzima wa milele.”

21 Kufanya yote tunayoweza kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia kutatusaidia kuendelea kukaza fikira juu ya kumtumikia Mungu sasa na kutatia nguvu tumaini letu la kuokoka na kuingia katika ulimwengu mpya. Kwa msaada wa Yehova, tunaweza pia kuwasaidia wale wanaotusikiliza waokolewe. (Soma 1 Timotheo 4:16.) Hilo litatuletea shangwe nyingi kama nini!

Je, Unakumbuka?

• Ni matatizo gani ambayo huenda yakawazuia wahubiri fulani wasiongoze mafunzo ya Biblia?

• Tunaweza kufanya nini ikiwa watu wengi katika eneo letu wanaonekana hawapendezwi?

• Tunapata thawabu gani tukiongoza funzo la Biblia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, unapanua njia zako za kuhubiri ili uwapate watu wenye mioyo minyoofu?