Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushinda Magumu ili Kupeleka Habari Njema

Kushinda Magumu ili Kupeleka Habari Njema

Kushinda Magumu ili Kupeleka Habari Njema

LORI letu linafika katika kituo cha ukaguzi kinachosimamiwa na wanaume, wanawake, na vijana 60 hivi wenye silaha. Baadhi yao wamevaa mavazi ya kijeshi; wengine wamevaa nguo za raia. Wengi wao wana silaha za hali ya juu sana. Ni kana kwamba wanatungoja. Kuna msukosuko wa kijamii.

Tumekuwa tukisafiri kwa siku nne, tukiwa tumebeba tani kumi za vichapo vya Biblia. Hatujui ikiwa wataturuhusu tupite. Je, watataka tuwape pesa? Itachukua muda gani kuwasadikisha kwamba kazi yetu ni ya amani?

Mtu mmoja anayependa kufyatua risasi bila sababu, anafyatua risasi hewani ili kutuonyesha kwamba ndiye kiongozi. Anaona simu zetu za mkononi na kutuagiza tumpe simu hizo. Tunapositasita, anatuonyesha kwa ishara kwamba atatukata shingo tusipompa. Tunampa simu zetu.

Kwa ghafula, mwanamke mmoja mwenye mavazi ya kijeshi anachukua bunduki yake na kuja tulipo. Yeye ndiye “mwandishi,” na anataka tumpe kitu fulani pia. Maisha ni magumu, kwa hiyo anataka tumpe kitu chochote ambacho kitamfaa. Kisha askari mwingine anafunua kifuniko cha tangi la mafuta la lori letu na kuanza kujaza chombo chake. Anapuuza malalamiko yetu huku akidai kwamba anafuata tu maagizo aliyopewa. Hatuwezi kufanya chochote. Tunatumaini tu kwamba wengine hawatafanya hivyo pia.

Mwishowe, kizuizi kinaondolewa, nasi tunaendelea na safari yetu. Wasiwasi ambao mimi na mwenzangu tulikuwa nao unapungua. Tulikuwa tukiogopa sana, lakini sasa tumezoea vituo hivyo vya ukaguzi vyenye kuogopesha. Kati ya Aprili (Mwezi wa 4) 2002 na Januari (Mwezi wa 1) 2004, tumesafiri mara 18 kutoka katika bandari ya Douala, Kamerun, mpaka Bangui, mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati. Kwa kawaida, safari hiyo ya umbali wa kilomita 1,600 ina hatari nyingi na mambo mengi yasiyotazamiwa. *

Joseph na Emmanuel, madereva ambao wamekuwa wakifunga safari hizo kwa ukawaida wanasema: “Safari hizo zimetufundisha mambo mengi. Ni jambo la hekima kutoa sala nyingi za kimyakimya kisha kutulia. Mtunga-zaburi aliandika hivi: ‘Nimeweka tegemeo langu katika Mungu. Sitaogopa. Mtu wa udongo anaweza kunitenda nini?’ Tunajaribu kuwa na mtazamo huohuo. Tuna hakika kwamba Yehova anajua safari yetu ni ya kupeleka ujumbe wa tumaini ambao unahitajiwa sana.”—Zaburi 56:11.

Jitihada za Ulimwenguni Pote za Kuandaa Chakula cha Kiroho

Watu wengi katika sehemu hii ya Afrika wanapenda kusikia habari njema ya Ufalme wa Mungu. Vichapo ambavyo tunasafirisha vimekusudiwa kuwasaidia kutosheleza mahitaji yao ya kiroho. (Mathayo 5:3; 24:14) Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Kamerun ambayo iko Douala, inasambaza kwa ukawaida vichapo kwa wahubiri zaidi ya 30,000 wa Ufalme na kwa watu wanaopendezwa wanaoishi nchini Kamerun na katika nchi nyingine nne za karibu.

Tayari vichapo hivyo vimesafirishwa kutoka mbali sana. Vingi vilichapishiwa nchini Hispania, Italia, Ufini, Uingereza, na Ujerumani. Halafu vikasafirishwa kwa meli kutoka Ufaransa. Kwa kawaida, kontena yenye vichapo vya Biblia inafika katika bandari ya Douala baada ya kila majuma mawili.

Kontena hiyo inawekwa kwenye lori ambalo linaipeleka kwenye ofisi ya tawi. Wafanyakazi wa Idara ya Upakizi na Usafirishaji wanapanga vichapo hivyo ikitegemea sehemu ambako vitapelekwa. Si rahisi kuvipeleka vichapo hivyo sehemu za mbali sana za mashambani. Lakini hiyo ni sehemu ya kazi ya kupeleka habari njema “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Ofisi inategemea wajitoleaji wenye kujidhabihu ambao kwa kupenda wanafunga safari hizo hatari. Hivyo, vichapo vya Biblia vinasambazwa kwa ukawaida kwa mamilioni ya watu katika sehemu ya katikati ya Afrika.

Safari ya Kawaida

Vichapo vinapelekwa kwa lori mpaka Chad, Gabon, Guinea ya Ikweta, Jamhuri ya Afrika ya Kati, na Kamerun. Acheni tusafiri pamoja na madereva wa lori moja. Jiwazie ukiwa umeketi pamoja na madereva, na ujitayarishe kwa ajili ya safari hatari ambayo itachukua siku kumi au zaidi.

Madereva sita wanasaidiana katika safari hii. Ni lazima wawe wenye nguvu, ustadi, subira, na wavalie vizuri. Wanavaa nguo za Kiafrika au shati na tai. Wakati fulani, maofisa wa forodha walisema hivi: “Angalia lori hili safi lenye madereva walio safi, ni kama tu wanavyoonekana katika picha zilizo katika vichapo vyao.” Jambo la maana hata zaidi kuliko mavazi ya madereva hao ni utayari wao wa kwenda popote ili kuwatumikia wengine.—Zaburi 110:3.

Tunaondoka Douala karibu saa 12 asubuhi, baada tu ya jua kuchomoza ili tuepuke msongamano mkubwa wa magari katika jiji hili kubwa. Baada ya kuvuka daraja karibu na ofisi ya tawi na kupita katika jiji hilo lenye shughuli nyingi, tunaelekea kituo chetu cha kwanza upande wa mashariki huko Yaoundé, mji mkuu wa Kamerun.

Madereva wote sita watakwambia jinsi ilivyo vigumu kuendesha lori lenye vitabu vyenye uzito wa tani kumi. Siku tatu za kwanza hatupati matatizo mengi kwa sababu barabara ni ya lami. Hata hivyo, lazima dereva awe makini sana. Kwa ghafula, mvua kubwa inaanza kunyesha. Kuanzia hapa barabara haina lami. Hatuoni vizuri, barabara inateleza, na tunalazimika kwenda polepole kwa sababu barabara si nzuri. Giza linaanza kuingia. Ni wakati wa kusimamisha lori ili tule na kujaribu kulala huku tukiwa tumewekelea miguu yetu kwenye sehemu ya mbele ya lori (dashibodi). Hivyo ndivyo maisha yalivyo katika safari hizi!

Tunaendelea na safari yetu asubuhi na mapema siku inayofuata. Dereva mmoja anasaidia kwa kuangalia kwa makini hali za barabara. Anatoa onyo mara moja tunapokaribia sana mtaro ulio kando ya barabara. Madereva wanajua vizuri kwamba gari likiteleza na kuingia katika mtaro, itawachukua siku nyingi kutoka humo. Barabara ingali mbovu tunapovuka mpaka na kuingia katika Jamhuri ya Afrika ya Kati. Sasa tunasafiri umbali wa kilomita 650 kupitia maeneo yenye kuvutia ya mashambani yenye milima na rangi ya kijani kibichi. Watoto, wazee, na akina mama wenye watoto mgongoni wanatupungia mikono tunapopita polepole katika vijiji vyao. Kwa sababu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, kuna magari machache barabarani, kwa hiyo watu wanatuangalia kwa mshangao.

Mambo Yenye Kufurahisha

Janvier, mmoja wa madereva wetu, anatuambia kwamba ingawa hawana wakati wa ziada, mara nyingi wanasimama katika vijiji vidogo ili kupumzika kidogo na kugawanya vichapo vya Biblia. Anakumbuka hivi: “Kila mara tulipofika Baboua, tulijitahidi kuzungumza na mhudumu fulani wa hospitali ambaye alipendezwa sana na ujumbe wa Ufalme, na tulikuwa tukijifunza naye Biblia kwa muda mfupi. Siku moja hata tulimwonyesha yeye na familia yake video ya Noa. Marafiki na majirani walikuja, na muda si muda, nyumba yake ikajaa watu wengi wenye msisimko. Kila mmoja alikuwa amesikia kumhusu Noa, na sasa wangeweza kufuata simulizi lake kwenye video. Tuliguswa moyo sana kuona jinsi walivyothamini. Baadaye, walipanga kuandaa chakula cha pekee ili kutushukuru, na walituhimiza tulale hapo usiku huo. Lakini ilitubidi kuondoka mara moja na kuendelea na safari yetu ndefu, lakini tulifurahi kwamba tuliweza kuwahubiria habari njema watu hao wanyenyekevu.”

Dereva mwingine anayeitwa Israel, anakumbuka mambo fulani yaliyotukia pindi moja walipokuwa wakienda Bangui, ambako tunaelekea. Anasema: “Kadiri tulivyokaribia Bangui ndivyo vizuizi vya barabarani vilivyoongezeka. Jambo zuri ni kwamba askari wengi walikuwa wenye urafiki na walikumbuka lori letu kwa sababu ya safari zetu za awali. Walitualika tuketi nao, nao walikubali kwa furaha vichapo vya Biblia. Wanathamini sana vitabu, kwa hiyo wanaandika majina yao ndani ya vitabu, kutia ndani tarehe na jina la mtu ambaye aliwapa vitabu hivyo. Baadhi ya askari-jeshi walikuwa na watu wa ukoo ambao ni Mashahidi, na hiyo ni sababu nyingine iliyowafanya wawe wenye urafiki.”

Joseph, dereva mwenye uzoefu zaidi, anasimulia lile analoona kuwa jambo kuu katika safari hizo, yaani, kufika mwisho wa safari. Anakumbuka hivi kuhusu safari moja: “Tukiwa umbali wa kilomita chache tu kutoka Bangui, tuliwapigia simu ndugu zetu ili kuwajulisha kwamba tungefika baada ya muda mfupi. Walifuatana nasi tulipokuwa tukipita jijini na kutusaidia kupata vibali vya kisheria. Tulipofika, watu wote katika ofisi ya tawi walikuja kutusalimu wakitukumbatia kwa uchangamfu. Washiriki wa kutoka makutaniko ya karibu walikuja kutusaidia na baada ya saa chache, mamia ya makatoni yenye Biblia, vitabu, vijitabu, na magazeti yalikuwa yamepakuliwa na kupangwa ndani ya depo.”

“Nyakati nyingine,” anaongezea Joseph, “tulibeba nguo za misaada, viatu, na vitu vya watoto ambavyo vilipaswa kupelekwa katika nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Ilifurahisha kama nini kuona tabasamu za akina ndugu wenye uthamini!”

Baada ya kupumzika kwa siku moja, tunatayarisha lori letu na kurudi kwa njia tuliyopitia tukija. Tutapata matatizo njiani, lakini matatizo hayo yote hayawezi kamwe kulinganishwa na mambo yenye kufurahisha tuliyopata.

Safari ndefu, mvua kubwa, barabara mbovu, magurudumu kutoboka, na lori kuharibika ni mambo yanayoweza kuvunja moyo. Askari-jeshi wakaidi wanasumbua mara nyingi. Hata hivyo, hakuna jambo linalowaletea uradhi madereva hao kama kupeleka habari njema ya Ufalme katika sehemu za mbali sana za Afrika na kuona ujumbe huo ukibadili maisha ya watu wanaoupokea.

Kwa mfano, kwa sababu ya safari hizo, mwanakijiji mmoja katika eneo la mashambani katika Jamhuri ya Afrika ya Kati, karibu na mpaka wa Sudan, sasa anasoma tafsiri ya kisasa ya Biblia. Mke wake anajifunza magazeti ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi, na watoto wao wanafaidika kwa kusoma kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. * Watu hao na wengine wengi katika jamii hizo za mashambani wanapokea chakula cha kiroho kama ndugu zao Wakristo katika majiji mengi makubwa. Kwa kweli hilo ni jambo linaloleta uradhi mkubwa!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Tangu wakati huo, mengi yamefanywa ili kuboresha hali ya usalama katika barabara kati ya Douala na Bangui.

^ fu. 25 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Ramani/ Picha katika ukurasa wa 9]

 

KAMERUN

Douala

JAMHURI YA AFRIKA YA KATI

Bangui

[Picha katika ukurasa wa 9]

Joseph

[Picha katika ukurasa wa 9]

Emmanuel

[Picha katika ukurasa wa 10]

Ofisi ya tawi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati huko Bangui

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kupakua vichapo kutoka katika lori huko Bangui