Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa kuwa Wayahudi waliamriwa wasiwe na “kitu chochote kilicho na chachu” wakati wa Pasaka, kwa nini Yesu alitumia divai, inayotengezwa kwa kuchachusha, alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake?—Kutoka 12:20; Luka 22:7, 8, 14-20.

Maadhimisho ya Pasaka, ambayo yalitia alama kule kutoka kwa wana wa Israeli nchini Misri, yalianzishwa mwaka wa 1513 K.W.K. Akitoa maagizo kuhusu kuadhimisha pasaka, Yehova alisema hivi: “Hamtakula kitu chochote kilicho na chachu. Katika makao yenu yote mtakula keki zisizo na chachu.” (Kutoka 12:11, 20) Katazo hilo kutoka kwa Mungu lilihusu tu aina fulani ya mkate uliopaswa kuliwa wakati wa Pasaka. Divai haikutajwa popote.

Katazo kuhusu chachu lilitolewa hasa kwa sababu Waisraeli walipaswa kuondoka Misri haraka-haraka. “Basi watu wakachukua unga wao wa kukandwa kabla haujachacha,” linasema andiko la Kutoka 12:34, “pamoja na vikandio vyao vikiwa vimefungwa katika nguo zao za kujitanda begani mwao.” Kukosekana kwa chachu katika maadhimisho yaliyofuata ya Pasaka kungevikumbusha vizazi vilivyofuata jambo hilo muhimu.

Baada ya muda, chachu ilionwa mara nyingi kuwa inafananisha dhambi au uharibifu. Kwa mfano, akizungumza kumhusu mtu fulani mwenye maadili mapotovu aliyekuwa katika kutaniko la Kikristo, mtume Paulo aliuliza hivi: “Je, hamjui kwamba chachu kidogo huchachisha donge lote?” Kisha akasema: “Ondoleeni mbali chachu ya zamani, ili muwe donge jipya kulingana na mlivyo bila chachu. Kwa maana, kwa kweli, Kristo pasaka yetu ametolewa dhabihu. Kwa hiyo na tufanye sherehe, si kwa chachu ya zamani, wala si kwa chachu ya ubaya na uovu, bali kwa keki zisizo na chachu za unyoofu na kweli.” (1 Wakorintho 5:6-8) Mkate usio na chachu tu ndio ungeweza kutumiwa kama mfano wa mwili wa Yesu wa kibinadamu usio na dhambi.—Waebrania 7:26.

Matumizi ya divai katika maadhimisho ya Pasaka ni jambo lililoongezwa baadaye na Wayahudi. Inawezekana kwamba, liliongezwa baada ya wao kurudi kutoka uhamishoni huko Babiloni. Biblia haina habari yoyote inayopinga jambo hilo lililoongezwa. Hivyo kwa kufaa, Yesu angeweza kutumia divai katika mlo wa Pasaka. Bila shaka, kuchacha kiasili kwa divai iliyotumiwa nyakati za zamani kulitofautiana na kutia chachu kwenye mikate. Chachu au hamira ilihitaji kuongezwa kwenye unga ili uchache. Divai iliyotengenezwa kwa zabibu haikuhitaji kuongezwa vitu hivyo. Tayari zabibu zilikuwa na vitu vya kuifanya divai ichache. Maji ya zabibu ambayo hayakuwa na chachu hayangepatikana wakati wa Pasaka kwa kuwa hayangeweza kubaki bila kuchacha tangu wakati wa mavuno, yaani, Agosti na Septemba (Mwezi wa 8 na wa 9) mpaka wakati wa Pasaka, yaani, Aprili au Mei (Mwezi wa 4 au wa 5).

Hivyo, tendo la Yesu la kutumia divai kama mfano katika Ukumbusho halipingani kwa njia yoyote na maagizo ya Pasaka kuhusu chachu. Divai yoyote nyekundu ambayo haijatiwa sukari, haijachanganywa na vinywaji vikali, au kukolezwa inafaa kutumiwa kama mfano wa “damu yenye thamani” ya Kristo.—1 Petro 1:19.