Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupeperushwa na Maadili Yanayobadilika

Kupeperushwa na Maadili Yanayobadilika

Kupeperushwa na Maadili Yanayobadilika

HADITHI moja inayopendwa na watu wengi inasema kwamba Diogenes, anayejulikana kuwa mwanafalsafa aliyeishi huko Athene katika karne ya nne K.W.K., alitembea mchana akiwa na taa kwa kusudi la kumtafuta mtu aliye safi kiadili, lakini hakumpata.

Ni vigumu kuthibitisha ikiwa hadithi hiyo ni sahihi. Hata hivyo, ikiwa Diogenes angekuwa hai leo, haingeshangaza kumwona akijitahidi hata zaidi kupata watu walio na maadili safi. Inaelekea kuwa watu wengi wanakataa kuamini wazo la kwamba watu wanapaswa kukubali maadili yoyote yaliyowekwa. Mara nyingi, vyombo vya habari vinazungumza kuhusu upotovu wa maadili faraghani, serikalini, kazini, katika michezo, katika biashara, na katika mambo mengine. Viwango vingi vya maadili ambavyo vilipendwa zamani haviheshimiwi tena. Viwango vilivyowekwa zamani vinachunguzwa upya na mara nyingi vinakataliwa. Watu wanakubali maadili mengine kwa maneno tu lakini hawayafuati.

Alan Wolfe, mtaalamu wa jamii na dini, anasema hivi: “Siku za kufuata viwango vya maadili vilivyokubaliwa na wengi zimepita.” Pia, alisema hivi: “Katika historia watu hawajapata kamwe kuwa na maoni ya kwamba hawawezi kutegemea mila na mashirika ili kuwaongoza kiadili, kama ilivyo leo.” Kuhusu miaka 100 iliyopita, gazeti moja (Los Angeles Times) linaeleza kuhusu maoni ya mwanafalsafa Jonathan Glover ya kwamba kuzorota kwa dini na sheria za maadili za ulimwengu wote kumechangia sana jeuri duniani.

Hata hivyo, mvurugo huo kuhusu maadili yanayokubaliwa, haujawazuia baadhi ya watu kutafuta mwongozo wa maadili. Miaka michache iliyopita, Federico Mayor, aliyekuwa mkurugenzi-mkuu wa UNESCO, alisema kwamba “kuliko wakati mwingine wowote, watu ulimwenguni pote wanahangaika sana kutafuta mwongozo wa maadili.” Lakini hata ikiwa watu ulimwenguni wameshindwa kufuata viwango vizuri vya maadili, hilo halimaanishi kwamba hakuna viwango vizuri vya maadili ambavyo vinaweza na vinapaswa kufuatwa.

Hata hivyo, je, watu wote wanaweza kukubaliana kuhusu viwango vinavyopaswa kufuatwa? Bila shaka hapana. Na ikiwa watu hawakubaliani kuhusu viwango vilivyo sawa na visivyo sawa, mtu anaweza kuchunguza maadili yoyote jinsi gani? Leo maoni ya kwamba maadili yanategemea mapendezi ya mtu binafsi yanapendwa sana na watu wengi. Hata hivyo, unaweza kuona kwamba kwa ujumla mtazamo huo haujafanya maadili yawe bora.

Paul Johnson, mwanahistoria Mwingereza, anaamini kuwa maoni hayo ya kwamba maadili yanategemea mapendezi ya mtu binafsi yamechangia “kudhoofisha . . . hisi ya mtu iliyositawishwa ya kuwa na wajibu na jukumu kuelekea kanuni za kweli zilizowekwa na zinazofaa za maadili,” hisi ambayo ilienea sana kabla ya mwanzo wa karne ya 20.

Hivyo basi, je, inawezekana kupata “kanuni za kweli zilizowekwa na zinazofaa za maadili” au kuishi kupatana na “sheria za maadili za ulimwengu wote”? Je, kuna chanzo kinachoweza kutoa viwango vyenye kudumu na visivyobadilika ambavyo vinaweza kuimarisha maisha yetu na kutupa tumaini la wakati ujao? Habari inayofuata itajibu maswali hayo.