Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunaazimia Kutimiza Huduma Yetu

Tunaazimia Kutimiza Huduma Yetu

Simulizi la Maisha

Tunaazimia Kutimiza Huduma Yetu

Kama lilivyosimuliwa na Lena Davison

“Ninapoteza uwezo wangu wa kuona. Siwezi kuona,” akasema rubani wetu kwa sauti isiyosikika vizuri. Muda mfupi baadaye, aliacha kushikilia usukani wa ndege ndogo tuliyokuwa tukisafiria, akazimia kwenye kiti chake. Mume wangu ambaye hakujua kuendesha ndege, alijaribu awezavyo kumwamsha. Kabla sijawaeleza jinsi tulivyoponea chupuchupu, acheni nieleze kilichofanya tusafiri kwa ndege hiyo iliyokuwa katika anga la Papua New Guinea, mojawapo ya sehemu za mbali zaidi za dunia.

NILIZALIWA nchini Australia mwaka wa 1929 na nikalelewa katika jiji la Sydney, mji mkuu wa jimbo la New South Wales. Baba yangu, Bill Muscat, alikuwa Mkomunisti ambaye, kwa kushangaza sana aliamini kwamba kuna Mungu. Mwaka wa 1938, alikubali hata kutia sahihi ombi la kitaifa la kumruhusu Joseph F. Rutherford, wa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova ahubiri katika Jumba la Jiji la Sydney.

Baba alituambia hivi wakati huo: “Bila shaka ana jambo la maana ambalo anataka kusema.” Miaka minane baadaye, tulijifunza mambo mengi kuhusu ujumbe wake. Baba alimkaribisha Shahidi wa Yehova aliyeitwa Norman Bellotti nyumbani kwetu ili wazungumze kuhusu Biblia. Shahidi huyo alikuwa mhudumu painia wa wakati wote. Familia yetu ilikubali kweli ya Biblia haraka na muda mfupi baadaye tukawa wenye bidii sana katika huduma ya Kikristo.

Katikati ya miaka ya 1940, niliacha shule ili kumsaidia mama yangu ambaye alikuwa mgonjwa sana. Pia nilifanya kazi ya kushona nguo ili kupata riziki. Jumamosi (Siku ya Posho) usiku, mimi na dada yangu Rose, tulienda kuhubiri na mapainia fulani barabarani nje ya Jumba la Jiji la Sydney. Mwaka wa 1952, ndugu yangu mkubwa, John, alihitimu katika shule ya wamishonari ya Gileadi huko Marekani na akapewa mgawo wa kwenda Pakistan. Mimi pia nilipenda huduma na nilitaka kufuata mfano wake. Hivyo, mwaka uliofuata nikawa painia wa kawaida.

Ndoa na Kazi ya Umishonari

Muda mfupi baadaye, nilikutana na John Davison ambaye alikuwa akifanya kazi katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Australia. Unyenyekevu wake, azimio lake la moyoni, na utu wake imara ulinivutia. Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, alifungwa mara tatu kwa sababu ya kudumisha msimamo wake wa Kikristo wa kutokuwamo. Tuliamua pamoja kufanya huduma ya Kikristo iwe kazi yetu ya maisha.

Mimi na John tulifunga ndoa Juni (Mwezi wa 6) 1955. Tulinunua basi tukiwa na nia ya kulibadili ili liwe nyumba. Kusudi letu lilikuwa kulitumia basi hilo ili kuhubiri maeneo ya mbali ya Australia. Mwaka uliofuata, ombi lilitolewa ili Mashahidi wahamie New Guinea, sehemu ya kaskazini-mashariki ya kisiwa kikubwa kilicho kaskazini ya Australia. * Ujumbe wa Ufalme haukuwa umehubiriwa katika sehemu hiyo ya ulimwengu. Tulijitolea mara moja kwenda huko.

Wakati huo, njia pekee ya kuingia New Guinea ilikuwa kupata kazi ya wakati wote. Hivyo, John alianza kutafuta kazi. Muda si muda, akapata kazi katika kiwanda cha mbao huko New Britain, kisiwa kidogo zaidi ambacho ni sehemu ya New Guinea. Majuma kadhaa baadaye, tulifunga safari ya kwenda kwenye mgawo wetu mpya. Tulifika Rabaul, New Britain, mnamo Julai 1956. Tulikaa huko siku sita tukingoja mashua ambayo ingetupeleka Waterfall Bay.

Huduma Yetu Huko Waterfall Bay

Baada ya siku kadhaa za safari hatari ya mashua, tulifika Waterfall Bay, ghuba kubwa iliyo kilomita 240 hivi kusini mwa Rabaul. Huko, kulikuwa na kiwanda kikubwa cha mbao katika uwanja fulani msituni. Jioni hiyo wafanyakazi wote walipokuwa wameketi kuzunguka meza ya chakula, msimamizi alisema hivi: “Bwana na Bibi Davison, ni sheria ya kampuni hii kwa wafanyakazi wote kusema wao ni wa dini gani.”

Tulikuwa na hakika kabisa kwamba hakukuwa na sheria kama hiyo, lakini kwa kuwa tulikuwa tumekataa kuvuta sigara, walikuwa na mashaka kutuelekea. Kwa vyovyote vile, John alisema: “Sisi ni Mashahidi wa Yehova.” Kisha, kukawa na kimya cha ajabu. Wanaume hao walikuwa wamepigana Vita vya Pili vya Ulimwengu na waliwachukia Mashahidi kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo wakati wa vita hivyo. Tangu hapo na kuendelea, walitafuta nafasi za kutuletea matatizo.

Mwanzoni msimamizi alikataa kutupa friji na jiko, ijapokuwa tulikuwa na haki ya kupewa vitu hivyo. Vyakula fulani tulivyokuwa navyo viliharibika haraka, nasi tulilazimika kupika chakula kwa kutumia jiko bovu tulilopata msituni. Baadaye, wanakijiji walikatazwa kutuuzia vyakula walivyotoka kuvuna, kwa hiyo, tulikula tu mboga tulizopata. Pia, walituita wapelelezi na walichunguza ikiwa tulikuwa tunamfundisha mtu yeyote Biblia. Kisha nikapata malaria.

Hata hivyo, tuliazimia kutimiza huduma yetu. Kwa hiyo, tuliwaomba vijana wawili wenyeji waliokuwa wakifanya kazi katika kiwanda hicho cha mbao ambao walijua Kiingereza watufundishe lugha ya Pijini ya Melanesia, ambayo ni lugha ya taifa. Na sisi tuliwafundisha Biblia. Mwishoni mwa juma tulikuwa tukifunga safari nyingi za kitalii ili “kujionea” nchi. Tukiwa safarini, tuliwahubiria kwa busara wanavijiji ambao tulikutana nao. Tulitumia wanafunzi wetu wa Biblia kama watafsiri wetu. Tulivuka mito yenye maji yanayotiririka kwa nguvu na pembeni kulikuwa na mamba wengi waliokuwa wakiota jua. Ijapokuwa pindi moja tuliponea chupuchupu, kwa kawaida hatukusumbuliwa na wanyama hao hatari.

Kutengeneza Vifaa vya Kufundishia

Kadiri huduma yetu ilivyopanuka, tuliamua kuchapisha ujumbe mfupi wa Biblia ili tuwape watu waliopendezwa. Wanafunzi wetu wa Biblia waliofanya kazi kiwandani walitusaidia kutafsiri ujumbe wa kwanza wa aina hiyo. Kwa siku nyingi, tulichapisha mamia ya trakti wakati wa usiku na kuzisambaza kwa wanavijiji na wafanyakazi wa mashua ambazo zilikuwa zikipita.

Mwaka wa 1957, John Cutforth, mhudumu anayesafiri mwenye uzoefu, alitutembelea na kututia moyo. * Alisema kwamba huenda kutumia picha kukawa njia yenye matokeo ya kuwafundisha kweli za Biblia watu ambao hawakujua kusoma. Yeye na mume wangu walichora, au kubandika picha fulani rahisi ili kueleza mafundisho ya msingi ya Biblia. Baadaye, tulitumia saa nyingi sana kuchora kwenye vitabu picha hizo ambazo tulitumia katika mahubiri. Kila mwanafunzi wa Biblia alipata nakala ambayo aliitumia kuwahubiria watu wengine. Mwishowe, njia hiyo ya kufundisha ilitumiwa nchini kote.

Baada ya kukaa huko Waterfall Bay kwa miaka miwili na nusu, tulikamilisha muda wetu wa kufanya kazi na tukakubaliwa kukaa nchini. Hivyo, tulipoombwa tuwe mapainia wa pekee tulikubali.

Tunarudi Rabaul

Tulipokuwa tukisafiri kaskazini kwenda Rabaul, mashua yetu ilisimama usiku wote huko Wide Bay karibu na shamba la minazi na kakao. Wenzi wa ndoa wazee ambao walimiliki shamba hilo, walitaka kustaafu na kuhamia Australia, nao walimwomba John asimamie shamba hilo. Kazi hiyo ilivutia sana, lakini tulipozungumzia jambo hilo usiku huo, tulikubaliana kwamba hatukuja New Guinea kutafuta mali za kimwili. Tuliazimia kutimiza huduma yetu tukiwa mapainia. Hivyo, siku iliyofuata tuliwajulisha wenzi hao wa ndoa uamuzi wetu na tukapanda tena mashua yetu.

Baada ya kufika Rabaul, tulijiunga na kikundi kidogo cha Mashahidi kutoka nchi nyingine waliokuwa wamehamia eneo hilo. Watu wa eneo hilo walipendezwa sana na ujumbe wa Ufalme, nasi tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia. Wakati huohuo, tulifanya mikutano ya Kikristo katika jumba la kukodi, na watu 150 hivi walihudhuria. Wengi wao walikubali kweli na wakasaidia kueneza habari njema ya Ufalme wa Mungu katika sehemu nyingine nchini.—Mathayo 24:14.

Pia, tulitembelea Vunabal, kijiji kidogo kilicho kilomita 50 kutoka Rabaul. Watu kadhaa katika kijiji hicho walipendezwa sana na kweli ya Biblia. Muda si muda, Mkatoliki fulani mashuhuri alitambua jambo hilo. Akiwa pamoja na marafiki wake wa kanisani, alivunja funzo letu la Biblia la kila juma na kutufukuza katika kijiji hicho. Tulipojua kwamba kungekuwa na matatizo zaidi juma lililofuata, tuliwaomba polisi watusindikize.

Siku hiyo Wakatoliki wenye dhihaka walisimama kando ya barabara kwa umbali wa kilomita kadhaa. Wengi wao walikuwa tayari kutupiga kwa mawe. Wakati huo, kasisi mmoja alikuwa amekusanya kijijini mamia ya wanaume wa kabila fulani. Polisi walituhakikishia kwamba tulikuwa na haki ya kufanya mkutano wetu, hivyo waliwatawanya watu ili tuweze kupita. Hata hivyo, punde tu tulipoanza mkutano wetu, yule kasisi aliwachochea watu waanze fujo. Polisi walishindwa kuuzuia umati huo wa watu; hivyo, mkuu wa polisi akatusihi tuondoke na akatupeleka haraka kwenye gari letu.

Watu hao walituzunguka, wakitutukana, kututemea mate, na kutikisa ngumi zao huku kasisi akiwa amesimama, amekunja mikono yake, na kutabasamu. Baada ya sisi kukimbia, mkuu wa polisi alisema kwamba hajawahi kamwe kuona tukio baya kama hilo. Ingawa watu wengi huko Vunabal waliogopa kujifunza kweli kwa sababu ya jeuri ya umati huo, mwanafunzi mmoja wa Biblia alikubali kwa ujasiri kweli ya Ufalme. Tangu wakati huo, mamia ya watu wengine kotekote katika New Britain wamechukua msimamo wao upande wa kweli.

Eneo la New Guinea Linafunguka

Mnamo Novemba (Mwezi wa 11) 1960, tulitumwa Madang, mji mkubwa ulio katika pwani ya kaskazini ya New Guinea, ambacho ndicho kisiwa kikuu. Katika mji huo, mimi na John tulipewa nafasi nyingi sana za kuajiriwa kazi ya muda wote. Kampuni moja iliniomba nisimamie duka la nguo. Kampuni nyingine ilitaka nifanye kazi ya kurekebisha nguo. Wanawake fulani wa kigeni walijitolea kunisaidia kufungua duka langu mwenyewe la kushona nguo. Kwa kuwa tuliendelea kukumbuka mradi wetu, tulikataa kwa fadhili nafasi hizo na nyinginezo.—2 Timotheo 2:4.

Eneo la Madang lilikuwa na matokeo mazuri, na muda si muda kutaniko lenye kusitawi likaanzishwa. Tulisafiri kwa miguu na kwa pikipiki ili kuhubiri kwa siku kadhaa katika vijiji vilivyokuwa kandokando ya mji huo. Tulilala katika nyumba za misonge zilizohamwa, nasi tulilalia marundo ya nyasi tulizokata porini. Tulibeba tu chakula cha mikebe, biskuti, na chandarua ili kujikinga na mbu.

Pindi moja, tulitembelea kikundi cha watu waliopendezwa huko Talidig, kijiji kilicho kilomita 50 hivi kaskazini mwa Madang. Kwa kuwa watu hao walikuwa wakifanya maendeleo ya kiroho, mwalimu mkuu wa shule ya eneo hilo aliwakataza wasijifunzie Biblia tena kwenye uwanja wa watu wote. Baadaye, alichochea polisi waharibu nyumba za watu hao na kuwafukuza waishi porini. Hata hivyo, chifu wa eneo jirani alikubali watu hao waishi katika eneo lake. Baada ya muda, chifu huyo mwenye fadhili alikubali kweli ya Biblia, na Jumba jipya la Ufalme likajengwa katika eneo hilo.

Kazi ya Kutafsiri na ya Kusafiri

Miaka miwili tu baada ya kufika New Britain mwaka wa 1956, mimi na John tuliombwa tutafsiri vichapo mbalimbali vya Biblia katika lugha ya Pijini ya Melanesia. Tulifanya kazi hiyo kwa miaka mingi. Kisha mwaka wa 1970, tulialikwa katika ofisi ya tawi ya Port Moresby, mji mkuu wa Papua New Guinea, ili tufanye kazi ya wakati wote ya kutafsiri. Pia tuliwafundisha wengine lugha.

Mwaka wa 1975 tulirudi huko New Britain ili kufanya kazi ya kusafiri. Kwa miaka 13 iliyofuata, tulisafiri kwa ndege, mashua, gari, au miguu kwenda karibu kila sehemu ya nchi. Tulikabili hatari nyingi njiani, kutia ndani lile tukio lililotajwa mwanzoni mwa simulizi hili. Wakati huo, tulipokuwa tukikaribia uwanja mdogo wa ndege wa Kandrian huko New Britain, rubani alizimia kwa sababu ya vidonda vibaya sana vya tumbo. Tulizunguka juu ya jangwa huku ndege ikiwa katika mfumo wa kujiendesha yenyewe, naye John alikuwa akijaribu sana kumwamsha rubani aliyezimia. Mwishowe, rubani alirudiwa na fahamu, naye akaona vizuri kidogo na hivyo akaweza kutua, lakini alitua kwa shida. Kisha akazimia tena.

Mlango Mwingine wa Utendaji Unafunguka

Mwaka wa 1988, tulipewa mgawo wa kurudi tena Port Moresby ili kusaidia katika kazi ya kutafsiri iliyokuwa ikiongezeka kwenye ofisi ya tawi. Tukiwa watu 50 hivi tuliishi na kufanya kazi kama familia katika ofisi ya tawi, na pia tuliwazoeza watafsiri wapya. Sote tuliishi katika nyumba yenye vyumba vingi vidogo. Mimi na John tuliamua kuacha mlango wa chumba chetu ukiwa wazi ili kuwatia moyo washiriki wa familia yetu na wageni wengine waingie na kufahamiana nasi. Hivyo, tukawa na uhusiano wa karibu sana pamoja na familia yetu, tulipendana na kutegemezana sana.

Mwaka wa 1993, John alikufa kutokana na mshtuko wa moyo. Nilihisi kana kwamba sehemu fulani ya mwili wangu ilikuwa imekufa pia. Tuliishi pamoja katika ndoa kwa miaka 38 na tulitumia wakati huo wote pamoja katika huduma. Bado niliazimia kuendelea kwa nguvu za Yehova. (2 Wakorintho 4:7) Mlango wa chumba changu ulibaki wazi, na vijana waliendelea kunitembelea. Ushirika huo mzuri ulinisaidia kudumisha mtazamo mzuri.

Mwaka wa 2003, nilipewa mgawo mpya wa kwenda kutumika katika ofisi ya tawi ya Sydney, Australia, kwa sababu ya matatizo ya afya. Leo, nina umri wa miaka 77, nami bado ninafanya kazi ya wakati wote katika Idara ya Tafsiri, na pia nina bidii katika kazi ya kuhubiri. Marafiki wangu, watoto na wajukuu wangu wa kiroho wananiletea shangwe sikuzote.

Bado mlango wa chumba changu cha Betheli uko wazi, nami ninatembelewa na wageni karibu kila siku. Kwa kweli, mlango wa chumba changu unapofungwa, mara nyingi watu wanagonga ili wajue ikiwa kuna tatizo. Maadamu ningali hai, nitaendelea kuazimia kutimiza huduma yangu na kumtumikia Mungu wangu, Yehova.—2 Timotheo 4:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Wakati huo, sehemu ya mashariki ya kisiwa hicho ilikuwa imegawanywa mara mbili. Sehemu ya kusini ilikuwa Papua na ya kaskazini ilikuwa New Guinea. Leo, sehemu ya magharibi ya kisiwa hicho inaitwa Papua, nayo ni sehemu ya Indonesia, na sehemu ya mashariki inaitwa Papua New Guinea.

^ fu. 19 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1958 (1/6/1958), ukurasa wa 333-336, simulizi la maisha la John Cutforth.

[Ramani katika ukurasa wa 18]

 

NEW GUINEA

AUSTRALIA

Sydney

INDONESIA

PAPUA NEW GUINEA

Talidig

Madang

PORT MORESBY

NEW BRITAIN

Rabaul

Vunabal

Wide Bay

Waterfall Bay

[Hisani]

Map and globe: Based on NASA/Visible Earth imagery

[Picha katika ukurasa wa 17]

Nikiwa na John katika kusanyiko huko Lae, New Guinea, 1973

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa katika ofisi ya tawi huko Papua New Guinea, 2002