Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Chanzo cha Uovu Kinafunuliwa!

Chanzo cha Uovu Kinafunuliwa!

Chanzo cha Uovu Kinafunuliwa!

KATIKA karne ya kwanza, Wayahudi wengi walikuwa wakingojea kuja kwa Masihi aliyeahidiwa. (Yohana 6:14) Yesu alipotokea, aliwafariji watu na kuwapa ujuzi zaidi wa neno la Mungu. Aliponya wagonjwa, akalisha wenye njaa, akatuliza hali mbaya ya hewa, na hata akafufua wafu. (Mathayo 8:26; 14:14-21; 15:30, 31; Marko 5:38-43) Pia, alisema maneno ya Yehova na kuwapa watu ahadi ya uzima wa milele. (Yohana 3:34) Kupitia maneno na matendo yake, Yesu alionyesha wazi kabisa kwamba alikuwa Masihi, yule ambaye angewakomboa wanadamu kutoka katika dhambi na matokeo yake yote maovu.

Kupatana na hilo, viongozi wa kidini Wayahudi walipaswa kuwa wa kwanza kumkaribisha Yesu, kumsikiliza, na kukubali mwelekezo wake kwa shangwe. Lakini hawakufanya hivyo. Badala yake, walimchukia, wakamtesa, na kupanga njama ya kumuua!—Marko 14:1; 15:1-3, 10-15.

Kwa kufaa, Yesu aliwashutumu wanaume hao wenye kulaumika. (Mathayo 23:33-35) Hata hivyo, alitambua kwamba kuna mtu mwingine anayepaswa pia kulaumiwa kwa sababu ya mawazo na matendo maovu ya watu hao. Aliwaambia hivi: “Ninyi mmetoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi mnataka kufanya tamaa za baba yenu. Huyo alikuwa muuaji alipoanza, naye hakusimama imara katika kweli, kwa sababu kweli haimo ndani yake. Anaposema uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.” (Yohana 8:44) Ingawa Yesu alikubali kwamba wanadamu wana uwezo wa kutenda maovu, alionyesha ni nani hasa aliye chanzo cha uovu, yaani, Shetani Ibilisi.

Kwa kusema kwamba Shetani “hakusimama imara katika kweli,” Yesu alifunua kwamba wakati mmoja kiumbe huyo wa roho alikuwa mtumishi mwaminifu wa Mungu lakini akapotoka kutoka katika njia hiyo iliyo sawa. Kwa nini Shetani alimwasi Yehova? Ni kwa sababu alijiona kuwa mtu wa maana sana hivi kwamba akatamani ibada ambayo Mungu tu ndiye anayestahili kupewa. *Mathayo 4:8, 9.

Uasi wa Shetani ulifunuliwa katika bustani ya Edeni alipomdanganya Hawa ale tunda walilokatazwa. Kwa kusema uwongo wa kwanza kabisa na kwa kumchongea Yehova, Shetani alijifanya mwenyewe kuwa “baba ya uwongo.” Zaidi ya hilo, kwa kuwashawishi Adamu na Hawa wasitii, alifanya dhambi iwatawale, na hivyo kuwaongoza wao pamoja na wazao wao kwenye kifo. Kwa sababu hiyo, Shetani pia alijifanya mwenyewe kuwa “muuaji,” naye kwa kweli ndiye muuaji mkatili zaidi katika historia yote!—Mwanzo 3:1-6; Waroma 5:12.

Uvutano mwovu wa Shetani ulifika hata katika makao ya roho ambako aliwashawishi malaika wengine wajiunge naye katika uasi wake. (2 Petro 2:4) Kama Shetani, roho hao waovu walipendezwa na wanadamu kwa njia isiyofaa. Walivutiwa hasa na mahusiano mapotovu ya ngono, na hilo likawa na matokeo mabaya sana na yaliyo maovu.

Uovu Unajaa Duniani

Biblia inatuambia hivi: “Hesabu ya wanadamu ilipoanza kuongezeka . . . nao wakazaa mabinti, ndipo wana wa Mungu wa kweli wakaanza kuwaona mabinti wa wanadamu, kwamba ni wenye sura ya kupendeza; nao wakajichukulia wake, yaani, wote waliowachagua.” (Mwanzo 6:1, 2) Hao “wana wa Mungu wa kweli” walikuwa nani? Hawakuwa wanadamu bali walikuwa viumbe wa roho. (Ayubu 1:6; 2:1) Tunajua hilo jinsi gani? Kwanza, zoea la kufunga ndoa kati ya wanadamu lilianza miaka 1,500 hivi iliyotangulia, na hivyo hapakuwa na uhitaji wa pekee wa kutaja jambo hilo. Hivyo, kwa kutaja mahusiano ya ngono kati ya “wana wa Mungu wa kweli” waliovaa miili ya kibinadamu na “mabinti wa wanadamu,” kwa wazi masimulizi hayo yanazungumzia jambo fulani ambalo halikuwako na halikuwa la kawaida.

Kwa kuwa aina ya wazao waliotokana na mahusiano hayo haikuwa ya kawaida, ni wazi kwamba mahusiano hayo hayakuwa ya kawaida. Wazao hao walioitwa Wanefili, walikua na kuwa majitu. Pia, walikuwa wachokozi na wakatili. Kwa kweli, neno “Wanefili” linamaanisha “Waangushaji,” au “wale wanaofanya wengine waanguke.” Ilisemekana kwamba wakatili hao walikuwa “watu wenye nguvu wa kale, wanaume wenye sifa.”—Mwanzo 6:4.

Wanefili na baba zao walitenda maovu kwa njia isiyowazika. Andiko la Mwanzo 6:11 linasema: “Dunia ikaharibika machoni pa Mungu wa kweli, dunia ikajaa jeuri.” Ndiyo, wanadamu waliiga njia zenye jeuri na zilizopotoka za viumbe hao wapya walioishi kati yao.

Wanefili na baba zao waliweza jinsi gani kuwa na uvutano mkubwa hivyo na wenye uovu juu ya wanadamu? Kwa kuchochea tamaa na mielekeo ya wanadamu yenye dhambi. Matokeo yakawa nini? ‘Kila mwenye mwili akaharibu njia yake duniani.’ Mwishowe, Yehova aliharibu ulimwengu huo katika Gharika ya dunia nzima, na kumwokoa Noa mwadilifu na familia yake tu. (Mwanzo 6:5, 12-22) Lakini, malaika waliokuwa wamevaa miili ya kibinadamu walirudi kwenye makao ya roho wakiwa wameaibishwa. Wakiwa roho waovu waliong’olewa kutoka katika vyeo vyao, waliendelea kumpinga Mungu na familia yake ya malaika washikamanifu. Inaonekana kwamba tangu wakati huo, Mungu aliwazuia roho hao waovu kuvaa miili ya kibinadamu. (Yuda 6) Hata hivyo, wameendelea kuwa na uvutano mkubwa juu ya shughuli za wanadamu.

Yule Mwovu Anafunuliwa Waziwazi!

Andiko la 1 Yohana 5:19 linaonyesha jinsi ambavyo uvutano mwovu wa Shetani umeenea. Linasema hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” Ibilisi anaongoza wanadamu kwenye misiba mibaya zaidi na zaidi. Kwa kweli, ameazimia kuliko wakati mwingine wowote kusababisha madhara. Kwa nini? Kwa sababu baada ya Ufalme wa Mungu kusimamishwa mwaka wa 1914, alifukuzwa mbinguni pamoja na roho waovu. Biblia ilitabiri hivi kuhusu kufukuzwa huko: “Ole wa dunia . . . , kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:7-12) Hivyo basi, leo Shetani anatumia jinsi gani uvutano wake juu ya wanadamu?

Shetani anafanya hivyo hasa kwa kuchochea roho inayoongoza mawazo na matendo ya watu. Kwa sababu hiyo, andiko la Waefeso 2:2 linamwita Ibilisi “mtawala wa mamlaka ya hewa, roho [au, mwelekeo mkuu] ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” Badala ya kuwachochea watu wamwogope Mungu na kuwa wema, “hewa” hiyo ya kiibilisi inawafanya wamwasi Mungu na viwango vyake. Hivyo, Shetani na roho wake waovu wanaendeleza na kuchochea zaidi uovu unaotendwa na wanadamu.

“Linda Moyo Wako”

Kuenea kwa ponografia (picha au habari za ngono) ni mojawapo ya njia ambazo zinaonyesha “hewa” hiyo. Ponografia inawachochea watu kuwa na tamaa zisizofaa za ngono na inafanya tabia zisizo za kawaida zivutie. (1 Wathesalonike 4:3-5) Kulala watu kinguvu, ukatili, magenge yanayolala watu kinguvu, kufanya ngono na wanyama, na kutendea watoto vibaya kingono ni kati ya mambo yanayoonyeshwa katika ponografia ili kuwaburudisha watu. Hata ponografia ambayo haina mambo machafu kadiri hiyo inadhuru wale wanaoitazama au kuisoma kwa sababu inawafanya watamani habari au picha hizo zaidi na zaidi na kuwa na mazoea ya kujisisimua kingono kwa kuzitazama. * Huo ni uovu ambao unaharibu uhusiano wa mtu pamoja na wengine na pia uhusiano wake pamoja na Mungu. Ponografia inaonyesha upotovu wa kiakili wa roho waovu ambao wanaendeleza mazoea hayo. Roho waovu ni waasi ambao walianza kuwa na tamaa potovu ya ngono kabla ya Gharika ya siku za Noa.

Sulemani, mwanamume mwenye hekima, alikuwa na sababu nzuri ya kutoa himizo hili: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa, kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.” (Methali 4:23) Kutii himizo hilo na kuulinda moyo wako kutokana na mtego wa ponografia kunaweza kumaanisha kubadili kituo cha televisheni au kuzima kompyuta picha chafu zinapotokea, na ni muhimu kuchukua hatua thabiti haraka! Wazia kwamba wewe ni askari-jeshi na unajaribu kuzuia mshale uliolengwa kuelekea moyo wako. Shetani analenga na kujaribu kuharibu moyo wako wa mfano ambao unachochea tamaa na nia yako.

Pia, unahitaji kuulinda moyo wako ili usipende jeuri, kwa kuwa Ibilisi anajua kwamba “yeyote anayependa jeuri [Yehova] hakika anamchukia.” (Zaburi 11:5) Shetani hahitaji kukufanya utende matendo ya jeuri ili uwe adui ya Mungu; anachohitaji kufanya tu ni kukuchochea usitawishe tabia ya kupenda jeuri. Hivyo, haishangazi kwamba vyombo vya habari vinavyopendwa vina habari nyingi sana za jeuri, ambazo mara nyingi zinahusiana na uchawi. Wanefili walikufa na kutoweka, lakini tabia na sifa zao mbaya zimeenea sana! Je, uchaguzi wako wa burudani unaonyesha kwamba unapinga mbinu za Shetani?—2 Wakorintho 2:11.

Jinsi ya Kupinga Uvutano Mwovu wa Shetani

Huenda ikaonekana kwamba nguvu za uovu haziwezi kushindwa. Biblia inasema kwamba wale wanaojitahidi kumpendeza Mungu ‘wana kushindana mweleka juu ya majeshi ya roho waovu.’ Wanashindana pia na mwili wao wenyewe usio mkamilifu. Ili kushinda pambano hilo na kupata kibali cha Mungu, tunahitaji kutumia vizuri maandalizi mengi ambayo yametoka kwa Mungu.—Waefeso 6:12; Waroma 7:21-25.

Maandalizi hayo yanatia ndani roho takatifu ya Mungu, nguvu iliyo na uwezo mkubwa zaidi katika ulimwengu wote. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa karne ya kwanza: “Tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu.” (1 Wakorintho 2:12) Wale wanaoongozwa na roho ya Mungu wanasitawisha upendo kuelekea mambo ambayo Mungu anapenda na kuchukia yale ambayo anachukia. (Amosi 5:15) Mtu anaweza kupata roho takatifu jinsi gani? Hasa kwa kusali, kwa kujifunza Biblia ambayo imetokana na roho takatifu, na kwa kushirikiana na watu ambao kwa kweli wanampenda Mungu.—Luka 11:13; 2 Timotheo 3:16; Waebrania 10:24, 25.

Kwa kutumia maandalizi hayo kutoka kwa Mungu, unaanza kuvaa “mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu,” ambayo ndiyo ulinzi pekee wa hakika kutokana na “hila za Ibilisi.” (Waefeso 6:11-18) Kutumia maandalizi hayo kabisa ni jambo muhimu zaidi sasa kuliko wakati mwingine wowote. Kwa nini?

Mwisho wa Uovu Umekaribia!

“Wakati waovu wanapochipuka kama majani na wote wanaotenda mambo yenye kuumiza wanapochanuka, ni ili wao wapate kuangamizwa milele,” anasema mtunga-zaburi. (Zaburi 92:7) Ndiyo, kama ilivyokuwa katika siku za Noa, kuenea kwa uovu leo kunathibitisha kwamba hivi karibuni Mungu atahukumu si wanadamu waovu tu, bali pia Shetani na roho wake waovu, ambao watatupwa ndani ya abiso, yaani, hali ya kutotenda, na mwishowe wataharibiwa kabisa. (2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 20:1-3, 7-10) Ni nani atakayetekeleza hukumu hiyo? Si mwingine ila Yesu Kristo, ambaye tunasoma hivi juu yake: “Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alifunuliwa, yaani, ili azivunje kazi za Ibilisi.”—1 Yohana 3:8.

Je, unatamani sana kuona uovu ukikomeshwa? Ikiwa ndivyo, unaweza kufarijiwa na ahadi za Biblia. Hakuna kitabu kingine kinachofunua chanzo cha uovu, yaani, Shetani, na hakuna kitabu kingine kinachoonyesha jinsi atakavyoharibiwa mwishowe pamoja na kazi zake zote mbovu. Tunakutia moyo upate ujuzi sahihi wa Biblia ili ujilinde mwenyewe na uvutano mwovu wa Shetani sasa na uwe na tumaini hakika la kuishi katika ulimwengu usio na uovu.—Zaburi 37:9, 10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Jina la awali la malaika huyo aliyekuja kuwa Shetani halijulikani. Majina “Shetani” na “Ibilisi” yanamaanisha “Mpinzani” na “Mchongezi.” Kwa njia fulani, Shetani alitenda kama mfalme wa zamani wa Tiro. (Ezekieli 28:12-19) Wote wawili walikuwa na mwanzo mzuri lakini wakashawishiwa na kiburi chao wenyewe.

^ fu. 17 Ona makala ya mfululizo “Ponografia Inadhuru au Haidhuru?” katika gazeti la Amkeni! la Julai 22, 2003 (22/7/2003), lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/ Picha katika ukurasa wa 6]

Hadithi Zilizo na Mambo Machache ya Kweli

Masimulizi kuhusu miungu iliyokuwa nusu mungu na nusu mtu, majitu, na gharika iliyoleta uharibifu mkubwa yanapatikana katika hadithi za kale ulimwenguni pote. Kwa mfano, Maandishi ya Kiakadi ya Gilgameshi yanataja gharika, meli, na waokokaji. Inasemekana kwamba Gilgameshi mwenyewe alikuwa nusu mungu na nusu mtu, alikuwa mjeuri, na mwenye tamaa kubwa sana ya ngono. Hadithi za Waazteki zinaeleza kuhusu ulimwengu wa kale uliomilikiwa na majitu na pia zinataja gharika kubwa. Hadithi za watu wa Norway zinaeleza kuhusu majitu na mwanamume mmoja mwenye hekima aliyeitwa Bergelmir ambaye alijenga mashua kubwa na kujiokoa yeye pamoja na mke wake. Ushuhuda wa hadithi hizo zote unaunga mkono ushuhuda wa Biblia kwamba wanadamu wote ni wazao wa watu waliookoka gharika iliyoharibu ulimwengu mbovu wa kale.

[Picha]

Bamba lenye Maandishi ya Gilgameshi

[Hisani]

The University Museum, University of Pennsylvania (neg. # 22065)

[Picha katika ukurasa wa 5]

Leo watu wanaonyesha tabia za Wanefili

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ujuzi sahihi unatupa nguvu za kushinda uvutano mwovu