Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Tunaweza Kumjua Mungu?

Je, Kweli Tunaweza Kumjua Mungu?

Je, Kweli Tunaweza Kumjua Mungu?

“Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako . . . Mungu wa pekee wa kweli.“—Yohana 17:3.

“LO! JINSI kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi!” akasema mtume Paulo. Kisha akaongeza hivi: “Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika!” (Waroma 11:33) Je, maneno hayo yanamaanisha kwamba wanadamu hawawezi kupata hekima na ujuzi kumhusu Mungu, na hivyo hawawezi kumjua wala kujua makusudi yake?

Wanafalsafa fulani wa kidini wanaamini kwamba hatuwezi kumjua Mungu. Kitabu kimoja (The Encyclopedia of Religion) kinasema hivi kuhusu falsafa hiyo: “Mambo ya Mungu hayawezi kamwe kujulikana. . . . Mungu hawezi kupewa jina au kufafanuliwa. Jina au ufafanuzi wowote una mipaka, na Mungu . . . hana mipaka. . . . Hajulikani, kwa sababu hawezi kujulikana.” *

Kulingana na gazeti moja (Newsweek), watu wengi katika ulimwengu wanapendelea “imani mpya” ya kwamba, kuna “kweli moja tu, na kweli hiyo ni kwamba hakuna kweli.”

Hata hivyo, watu wengi hawapati majibu ya maswali yao kuhusu kusudi la uhai hayajibiwi. Wanaona matatizo yenye kuvunja moyo ya umaskini, ugonjwa, na jeuri. Nao hufadhaika sana kwa sababu ya kutokuwa na uhakika maishani. Huenda wakatamani kupata majibu, lakini wasipoyapata wanaweza kukata kauli kwamba maswali yao hayawezi kujibiwa. Hivyo, watu wengi kama hao wamejitenga na dini, na ikiwa bado wanaamini kwamba kuna Mungu, wao hutafuta njia yao wenyewe ya kumfikia.

Maoni ya Biblia

Wale wanaoikubali Biblia na ambao wako tayari kumkubali Yesu Kristo kuwa Msemaji wa Mungu, wanapaswa kupendezwa kujua maoni ya Biblia. Labda unakumbuka kwamba pindi moja Yesu alizungumza kuhusu barabara mbili, barabara “pana na kubwa . . . inayoongoza kwenye uharibifu” na barabara yenye “nafasi ndogo . . . inayoongoza kwenye uzima.” Alieleza jinsi ya kuwatambua wale walio katika kila barabara, kwa kusema hivi: “Kwa matunda yao mtawatambua watu hao.” Kwa matunda ya aina gani? Si kwa yale wanayosema bali kwa yale wanayotenda, kama Yesu alivyoeleza: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia.” Haitoshi tu kudai kwamba tunamwamini Mungu. Ni lazima tufanye mapenzi yake. Ni wazi kwamba tunapaswa kwanza kuwa na ujuzi sahihi kuhusu mapenzi ya Mungu.—Mathayo 7:13-23.

Yesu alionyesha wazi kwamba wanadamu wanaweza kupata ujuzi juu ya Mungu. Alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Hapana shaka kwamba tunaweza kupata hekima na ujuzi ambao Mungu hufunua, lakini ikiwa tu tutajitahidi kutafuta hekima na ujuzi huo. Jitihada hizo si za bure kwa sababu Mungu atawapa zawadi ya uzima wa milele wale wanaofanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Dini za Mashariki kama vile Uhindu, Utao, na Ubudha, zina maoni kama hayo.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Yesu alisema kwamba barabara yenye nafasi ndogo inaongoza kwenye uzima