Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtumaini Yehova na Uwe Hodari

Mtumaini Yehova na Uwe Hodari

Mtumaini Yehova na Uwe Hodari

“Mtumaini Yehova; uwe hodari na moyo wako uwe na nguvu. Naam, mtumaini Yehova.”—ZABURI 27:14.

1. Tumaini ni muhimu kadiri gani, na neno hilo linatumiwaje katika Maandiko?

TUMAINI la kweli ni kama mwangaza mwingi. Linatusaidia kuvumilia majaribu na kutazamia wakati ujao tukiwa na uhodari na shangwe. Ni Yehova peke yake anayeweza kutupa tumaini hakika, na anafanya hivyo kupitia Neno lake lililoongozwa kwa roho. (2 Timotheo 3:16) Neno “tumaini” linapatikana mara nyingi katika Biblia nalo linarejelea kutazamia jambo zuri kwa hamu na uhakika na vilevile kusudi la tazamio hilo. * Tumaini hilo si tamaa tu ambayo haina msingi wala uwezekano wa kutimizwa.

2. Tumaini lilikuwa na umuhimu gani katika maisha ya Yesu?

2 Yesu alipokabili majaribu na matatizo, alifikiria wakati ujao naye akamtumaini Yehova. “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake, yeye alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu, naye ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.” (Waebrania 12:2) Kwa kuwa alikazia fikira tazamio la kutetea enzi kuu ya Yehova na kulitakasa jina Lake, Yesu hakuacha kamwe kumtii Mungu licha ya mambo ambayo alikabili.

3. Tumaini lina umuhimu gani katika maisha ya watumishi wa Mungu?

3 Mfalme Daudi anataja uhusiano kati ya tumaini na uhodari, akisema: “Mtumaini Yehova; uwe hodari na moyo wako uwe na nguvu. Naam, mtumaini Yehova.” (Zaburi 27:14) Ikiwa tunataka moyo wetu uwe na nguvu, hatupaswi kamwe kuacha tumaini letu liwe hafifu bali tunapaswa kuendelea kulifanya liwe wazi akilini na kulithamini sana. Kufanya hivyo kutatusaidia kumwiga Yesu katika kuonyesha uhodari na bidii tunapofanya kazi ambayo aliwapa wanafunzi wake. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kwa kweli, tumaini linatajwa pamoja na imani na upendo likiwa sifa muhimu ya watumishi wa Mungu ambayo huwasaidia kuvumilia.—1 Wakorintho 13:13.

Je, ‘Unazidi Katika Tumaini’?

4. Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao wa “kondoo wengine” wanatazamia nini kwa hamu?

4 Watu wa Mungu wana wakati ujao mzuri. Wakristo watiwa-mafuta wanangoja kwa hamu kutumikia pamoja na Kristo mbinguni, na “kondoo wengine” wanatumaini ‘kuwekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu’ wa kidunia. (Yohana 10:16; Waroma 8:19-21; Wafilipi 3:20) ‘Uhuru huo wenye utukufu’ unatia ndani kukombolewa kutoka katika dhambi na matokeo yake mabaya. Naam, Yehova ambaye ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu” atawapa washikamanifu wake zawadi bora zaidi.—Yakobo 1:17; Isaya 25:8.

5. ‘Tunazidije katika tumaini’?

5 Tumaini la Kikristo linapaswa kuwa muhimu kadiri gani maishani mwetu? Tunasoma hivi kwenye Waroma 15:13: “Mungu anayetoa tumaini na awajaze ninyi shangwe yote na amani kwa kuamini kwenu, ili mzidi katika tumaini kwa nguvu za roho takatifu.” Naam, tumaini haliwezi kulinganishwa na mshumaa ulio gizani, bali linaweza kulinganishwa na miale miangavu ya jua la asubuhi, likifanya maisha ya mtu kuwa na amani, furaha, kusudi, na uhodari. Ona kwamba ‘tunazidi katika tumaini’ tunapoamini Neno la Mungu lililoandikwa na kupokea roho yake takatifu. Andiko la Waroma 15:4 linasema hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” Basi jiulize hivi: ‘Je, mimi hudumisha tumaini langu kwa kujifunza Biblia kwa bidii, kwa kuisoma kila siku? Je, mimi husali mara nyingi ili kupata roho ya Mungu?’—Luka 11:13.

6. Ili tudumishe tumaini letu, tunapaswa kujilinda dhidi ya nini?

6 Yesu, Kielelezo chetu, aliimarishwa na Neno la Mungu. Tunapomfikiria sana, tunaepuka ‘kuchoka na kuzimia katika nafsi zetu.’ (Waebrania 12:3) Tumaini letu kutoka kwa Mungu likififia akilini na moyoni mwetu au tukikengeushwa, labda na vitu vya kimwili au miradi ya kilimwengu, huenda tukachoka kiroho, na hatimaye kukosa nguvu na uhodari wa kudumisha maadili. Tukiwa na mtazamo huo, hata ‘imani yetu inaweza kuvunjika.’ (1 Timotheo 1:19) Kwa upande mwingine, tumaini la kweli huimarisha imani yetu.

Tumaini Ni Muhimu kwa Imani

7. Ni kwa njia gani tumaini ni muhimu kwa imani?

7 Biblia inasema hivi: “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Hivyo, tumaini si sifa inayoongeza tu imani; bali ni sehemu muhimu ya imani. Fikiria Abrahamu. Kwa maoni ya kibinadamu, yeye na mke wake Sara, walikuwa wamepita umri wa kupata watoto wakati Yehova alipowaahidi mrithi. (Mwanzo 17:15-17) Abrahamu alitendaje? “Ijapokuwa alikuwa amepita hali ya kuwa na tumaini, bado kwa kutegemea tumaini alikuwa na imani, ili awe baba ya mataifa mengi.” (Waroma 4:18) Naam, tumaini ambalo Abrahamu alipata kutoka kwa Mungu lilifanya imani yake ya kupata mzao iwe na msingi imara. Hivyo, imani yake iliimarisha tumaini lake na kulifanya liwe hakika. Abrahamu na Sara hata walikuwa na uhodari wa kuondoka nyumbani kwao na kuacha watu wao wa ukoo na kuishi miaka ya mwisho ya maisha yao katika mahema ugenini!

8. Kuvumilia kwa uaminifu huimarishaje tumaini?

8 Abrahamu alidumisha tumaini lake kwa kumtii Yehova kabisa hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. (Mwanzo 22:2, 12) Vivyo hivyo, kwa kutii na kuvumilia katika utumishi wa Yehova, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutapata thawabu yetu. Paulo aliandika kwamba matokeo ya “uvumilivu,” ni “hali yenye kukubaliwa,” ambayo hutokeza tumaini, “nalo tumaini halikatishi tamaa.” (Waroma 5:4, 5) Hiyo ndiyo sababu Paulo aliandika hivi pia: “Tunatamani kila mmoja wenu aonyeshe bidii ileile ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho.” (Waebrania 6:11) Mtazamo huo unaofaa ambao unategemea uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, unaweza kutusaidia kukabili tatizo lolote kwa uhodari, hata kwa shangwe.

“Shangilieni Katika Tumaini”

9. Tunapaswa kufanya nini kwa ukawaida ili ‘tushangilie katika tumaini’?

9 Tumaini letu tulilopewa na Mungu ni muhimu zaidi kuliko chochote ambacho ulimwengu unaweza kutoa. Andiko la Zaburi 37:34 linasema hivi: “Mtumaini Yehova na kuishika njia yake, naye atakuinua uimiliki dunia. Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.” Naam, tuna kila sababu ya ‘kushangilia katika tumaini.’ (Waroma 12:12) Hata hivyo, ili tufanye hivyo, ni lazima tuendelee kufikiria tumaini letu. Je, wewe hufikiria kwa ukawaida tumaini lako ulilopewa na Mungu? Je, unaweza kuwazia ukiwa katika Paradiso, ukiwa na afya nzuri, bila wasiwasi, ukizungukwa na wapendwa wako, na ukifanya kazi yenye kuridhisha? Je, wewe hutafakari kuhusu picha za Paradiso zinazoonyeshwa katika vichapo vyetu? Kutafakari hivyo kwa ukawaida ni kama kusafisha dirisha ili kuweza kuona mandhari yenye kupendeza. Tukipuuza kusafisha dirisha hilo, baada ya muda mfupi litapata uchafu ambao utatuzuia tusione waziwazi mandhari hiyo na kuvutiwa nayo. Kisha, tutavutiwa na mambo mengine. Tusiruhusu kamwe hilo litukie!

10. Kwa nini kutazamia thawabu kunaonyesha kwamba tuna uhusiano mzuri pamoja na Yehova?

10 Bila shaka, sababu yetu kuu ya kumtumikia Yehova ni kwamba tunampenda. (Marko 12:30) Hata hivyo, tunapaswa kutazamia kwa hamu thawabu. Kwa kweli, Yehova anatutazamia tufanye hivyo! Andiko la Waebrania 11:6 linasema hivi: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” Kwa nini Yehova anataka tumwone kuwa Mthawabishaji? Kwa sababu tunapofanya hivyo, tunaonyesha tunamjua vizuri Baba yetu wa mbinguni. Yeye ni mkarimu na anawapenda watoto wake. Fikiria jinsi ambavyo tungehuzunika na kuvunjika moyo kwa urahisi ikiwa hatungekuwa na “wakati ujao na tumaini.”—Yeremia 29:11.

11. Tumaini ambalo Musa alipewa na Mungu lilimsaidiaje kufanya maamuzi kwa hekima?

11 Musa ni kielelezo kizuri cha mtu ambaye alikazia fikira tumaini lake alilopewa na Mungu. Akiwa “mwana wa binti ya Farao” Musa angeweza kupata mamlaka, umashuhuri, na utajiri wa Misri. Je, angefuatilia mambo hayo au angemtumikia Yehova? Kwa uhodari, Musa aliamua kumtumikia Yehova. Kwa nini? Kwa sababu “alikaza macho kwenye malipo ya thawabu.” (Waebrania 11:24-26) Naam, Musa hakupuuza tumaini ambalo Yehova alikuwa ameweka mbele yake.

12. Kwa nini tumaini la Kikristo ni kama kofia ya chuma?

12 Mtume Paulo alilinganisha tumaini na kofia ya chuma. Kofia yetu ya chuma ya mfano hulinda nguvu zetu za kufikiri, linatuwezesha kufanya maamuzi kwa hekima, kutanguliza mambo yanayofaa, na kudumisha utimilifu. (1 Wathesalonike 5:8) Je, wewe huvaa kofia yako ya chuma ya mfano kila wakati? Ikiwa ndivyo, basi, kama Musa na Paulo, utaweka tumaini lako “si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie.” Ni kweli kwamba uhodari unahitajiwa ili kukataa kufuata mambo ya ubinafsi yanayopendwa sana, lakini kuna faida kubwa kufanya hivyo! Kwa nini ukubali kitu chochote chenye thamani ndogo kuliko “uzima ulio wa kweli,” ambao wale wanaomtumaini na kumpenda Yehova watapata?—1 Timotheo 6:17, 19.

‘Sitakuacha Hata Kidogo’

13. Yehova anawapa watumishi wake washikamanifu uhakikisho gani?

13 Watu wanaoweka tumaini lao katika mfumo wa mambo wa sasa hufikiria sana mambo mabaya ambayo wanakabili huku ulimwengu ukizidi kupatwa na “maumivu ya taabu.” (Mathayo 24:8) Lakini wale wanaomtumaini Yehova hawaogopeshwi na mambo hayo. Wataendelea ‘kukaa salama wala hawatasumbuliwa na hofu ya msiba.’ (Methali 1:33) Kwa sababu hawaweki tumaini lao katika mfumo huu wa mambo, wanatii kwa shangwe shauri hili la Paulo: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana yeye amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’”—Waebrania 13:5.

14. Kwa nini Wakristo hawapaswi kuhangaikia sana mahitaji yao ya kimwili?

14 Maneno hayo ya mkazo “hata kidogo” yanathibitisha kabisa kwamba Mungu atatutunza. Yesu pia alituhakikishia kwamba Mungu anatuhangaikia kwa upendo, aliposema: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote [vitu vya lazima maishani]. Kwa hiyo, msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.” (Mathayo 6:33, 34) Yehova anajua kwamba ni vigumu kwetu kuwa na bidii kwa ajili ya Ufalme wake na wakati huohuo kutimiza daraka la kujiandalia mahitaji ya kimwili. Basi, acheni tuwe na uhakika kabisa kwamba anaweza na anatamani kutosheleza mahitaji yetu.—Mathayo 6:25-32; 11:28-30.

15. Wakristo hudumishaje ‘jicho rahisi’?

15 Tunaonyesha kwamba tunamtegemea Yehova kwa kuwa na ‘jicho rahisi.’ (Mathayo 6:22, 23) Jicho rahisi ni nyoofu, lina nia nzuri, na halina pupa wala ubinafsi wa kutaka makuu. Kuwa na jicho rahisi hakumaanishi kuwa maskini au kupuuza madaraka yetu ya Kikristo. Badala yake, kunamaanisha kuwa na “utimamu wa akili” tunapoendelea kutanguliza utumishi wa Yehova.—2 Timotheo 1:7.

16. Kwa nini tunahitaji imani na uhodari ili kuwa na jicho rahisi?

16 Tunahitaji imani na uhodari ili kudumisha jicho rahisi. Kwa mfano, ikiwa mwajiri wako anasisitiza kwamba ufanye kazi kwa ukawaida wakati wa mikutano ya Kikristo, je, utatanguliza mambo ya kiroho kwa uhodari? Ikiwa mtu ana shaka kwamba Yehova atatimiza ahadi Yake ya kuwatunza watumishi Wake, basi Shetani akizidisha mkazo, mtu huyo anaweza kuacha kabisa kuhudhuria mikutano. Naam, tukikosa imani tunaweza kumruhusu Shetani atuongoze na kutuonyesha mambo ya kutanguliza badala ya kumwacha Yehova afanye hivyo. Huo utakuwa msiba ulioje!—2 Wakorintho 13:5.

“Mtumaini Yehova”

17. Wale wanaomtumaini Yehova wanabarikiwaje hata sasa?

17 Maandiko yanaonyesha tena na tena kwamba wale wanamtumaini na kumtegemea Yehova hawashindwi kamwe. (Methali 3:5, 6; Yeremia 17:7) Ni kweli kwamba kuna wakati ambapo huenda wakahitaji kutosheka na vitu vichache, lakini wanaona hilo kuwa dhabihu ndogo ikilinganishwa na baraka zilizo mbele yao. Hivyo, wanaonyesha kwamba ‘wanamtumaini Yehova’ na wana uhakika kwamba mwishowe atatosheleza tamaa zote za uadilifu za moyo wa washikamanifu wake. (Zaburi 37:4, 34) Hivyo, wana furaha nyingi hata sasa. “Tarajio la waadilifu ni kushangilia, lakini tumaini lenyewe la waovu litapotea.”—Methali 10:28.

18, 19. (a) Yehova anatupa uhakikisho gani wenye upendo? (b) Tunamwekaje Yehova kwenye ‘mkono wetu wa kuume’?

18 Mvulana mdogo anapotembea huku akiwa ameshikwa mkono na baba yake, yeye huhisi kwamba yuko salama salimini. Sisi pia huhisi hivyo tunapotembea pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Yehova aliliambia hivi taifa la Israeli: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. . . . Nitakusaidia kwelikweli. . . . Kwa maana mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”—Isaya 41:10, 13.

19 Maneno hayo yanaonyesha jambo lenye kuvutia, yaani, Yehova akiushika mkono wa mtu! Daudi aliandika hivi: “Nimemweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yuko upande wa mkono wangu wa kuume, sitatikiswa.” (Zaburi 16:8) Tunamwekaje Yehova kwenye ‘mkono wetu wa kuume’? Tunafanya hivyo angalau kwa njia mbili. Kwanza, tunaacha Neno lake lituongoze katika sehemu zote za maisha yetu; na pili, tunatazamia zawadi tukufu ambayo Yehova ameweka mbele yetu. Mtunga-zaburi Asafu aliimba hivi: “Niko pamoja nawe daima; umeushika mkono wangu wa kuume. Utaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanipeleka kwenye utukufu.” (Zaburi 73:23, 24) Tukiwa na uhakikisho huo, tunaweza kutazamia wakati ujao kwa uhakika.

“Ukombozi Wenu Unakaribia”

20, 21. Wale wanaomtumaini Yehova wanatazamia wakati ujao wa aina gani?

20 Kila siku inapopita, inakuwa muhimu zaidi tumweke Yehova kwenye mkono wetu wa kuume. Hivi karibuni, kuanzia na kuharibiwa kwa dini ya uwongo, ulimwengu wa Shetani utapatwa na dhiki ambayo haijawahi kutukia kamwe. (Mathayo 24:21) Wanadamu wasio na imani wataogopa. Hata hivyo, wakati huo wenye msukosuko, watumishi wa Yehova wenye uhodari watashangilia katika tumaini lao! Yesu alisema hivi: “Mambo haya yanapoanza kutukia, simameni wima na kuinua vichwa vyenu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.”—Luka 21:28.

21 Basi, acheni tushangilie katika tumaini ambalo tumepewa na Mungu na tusidanganywe wala kushawishiwa na hila za Shetani za kutukengeusha. Wakati huohuo, acheni tujitahidi kusitawisha imani, upendo, na kumwogopa Mungu. Tukifanya hivyo, tutakuwa na uhodari wa kumtii Yehova chini ya hali zote na kumpinga Ibilisi. (Yakobo 4:7, 8) Naam, “iweni hodari, nayo mioyo yenu na iwe na nguvu, ninyi nyote mnaomngojea Yehova.”—Zaburi 31:24.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Ingawa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo neno “tumaini” linatumiwa mara nyingi kurejelea thawabu ambayo Wakristo watiwa-mafuta watapata mbinguni, katika makala hii, neno tumaini litazungumziwa katika maana ya ujumla.

Je, Unaweza Kujibu?

• Ni kwa njia gani tumaini la Yesu lilimwezesha kuwa hodari?

• Kuna uhusiano gani kati ya imani na tumaini?

• Tumaini na imani zinawezaje kumpa Mkristo uhodari ili atangulize mambo yanayofaa maishani?

• Kwa nini wale ‘wanaomtumaini Yehova’ wanaweza kutazamia wakati ujao kwa uhakika?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Uwe kijana au mzee, je, unaweza kujiona ukiwa katika Paradiso?